Home About Articles Ask the Sheikh
null

Jibu la Swali

June 21, 2004
55

Ni nini kinachokusudiwa na sentensi iliyo mwishoni mwa Kifungu cha (10):

وَعَلَى الدَّوْلَةِ أَنْ تَمْنَعَ كُلَّ مَا يُشْعِرُ بِوُجُودِهِمْ مِنَ الْمُسْلِمِينَ

"...na ni wajibu kwa Dola kuzuia kila kitu kinachoashiria kuwepo kwao [kama tabaka tofauti] miongoni mwa Waislamu"

Je, hii inamaanisha kuwa itatolewa amri ya kuwakataza mashekhe na maimamu wa misikiti kuvaa mavazi rasmi (tarbushi, kilemba, na joho)?

Jibu: Sivyo hivyo. Kile ambacho Dola itakiondoa ni dhana ya viongozi wa kidini (men of religion) iliyopo kwa Wakristo. Wao wana mavazi maalumu (kwa ajili ya viongozi wa kidini) yanayowapa mamlaka ya kuhalalisha na kuharamisha peke yao bila wengine. Kisha ikatokea dhana inayofungamana na hilo baada ya kuibuka kwa Ubepari, ambapo mamlaka ya kiroho yawe yamefungika kwa "viongozi wa kidini" kupitia mavazi yao maalumu waliyopewa wao pekee, na mamlaka ya kitempola (kidunia) yawe kwa wasekula (viongozi wa dola). Kwa hivyo, haijuzu kwa kiongozi wa utawala kwao, kwa mujibu wa misingi ya Kibepari, kuvaa mavazi ya "viongozi wa kidini". Yaani, kuna utenganishaji wa dini na dola unaofungamana na Ubepari kwao.

Sisi katika Uislamu hatuna watu maalumu waliohusika pekee na tafsiri ya dini, kuhalalisha, na kuharamisha. Vilevile, kwetu hakuna utenganishaji wa dini na dola; hivyo hakuna mamlaka ya kiroho wala mamlaka ya kidunia yaliyotengana. Dhana hii na kila kinachoashiria hiyo ndicho kinachopaswa kufutwa.

Ama kuhusu kufanya uhalalishaji na uharamishaji kuwa ni haki ya watu maalumu wenye mavazi fulani, dhana hii haipo kwa Waislamu wengi. Harakati zilizofanywa na Hizb katika suala hili zimezaa matunda; kwani watu wengi sasa hawaelekei kuchukua hukumu kutoka kwa mashekhe wenye mavazi hayo rasmi kutokana na kutowaamini.

Na ama kuhusu kufanya mambo ya "kiroho" yawe ya wenye mavazi rasmi ya "kidini", jambo hili pia limekaribia kutoweka miongoni mwa Waislamu. Waislamu leo hii wanawakubali mashekhe wanaozungumzia utawala na siasa, wanawathamini na kuwaheshimu. Ama mashekhe wanaozingatia ibada pekee na wasioingilia katika kuwahisabu watawala, watu wanawaangalia bila uthamini wala heshima.

Pamoja na hayo, kuhusishwa kwa mashekhe na maimamu wa misikiti na mavazi haya kunaweza kuleta mkanganyiko kwa watu wa kawaida. Wanaweza kudhani kuwa kuna watu maalumu kwa ajili ya dini kwa maana ya ibada na mfano wake, na kwamba watu hawa hawana uhusiano na siasa na mambo yake, bali kuna viongozi wa dola kwa ajili ya kazi hizo.

Kwa sababu hiyo, Dola itafanya kazi ya kuondoa muonekano wa mavazi maalumu kwa mashekhe na maimamu wa misikiti. Hata hivyo, si kwa kuwakataza kuyavaa, bali kwa kuondoa ule upekee wa mavazi hayo. Kwa mfano, watu wamuone mtoza bili za maji na umeme akija amevaa joho na kilemba, au wamuone Khalifa na Gavana akiwa na kilemba kama ilivyokuwa katika zama za mwanzo za Uislamu, na wamuone imamu wa msikiti amevaa mavazi ya kawaida. Yaani, kuondoa ule upekee wa mavazi. Hili halihitaji amri rasmi bali baadhi ya mbinu mwafaka. Kwa mfano, ukienda kuchukua kibali cha ujenzi ukamkuta mhandisi anayetoka kwenda kukagua amevaa kilemba, na ukamkuta kadi (ma’dhun) anayefungisha ndoa amevaa kilemba cha kiarabu (iqal na hutta). Hali iwe hivi kiasi kwamba huoni vazi maalumu la mtawala au shekhe. Hili ni jambo linalokubalika na lenye mantiki katika Uislamu, bali ndivyo Waislamu walivyokuwa. Khalifa alikuwa akiwaongoza watu na kuswali nao, na hakuna Mwislamu yeyote aliyeweza kumtofautisha kiongozi, kadhi, au mtu wa kawaida kupitia mavazi yao. Na yule mtu aliyewajia Waislamu waliokuwa wameketi na Mtume (saw), alisimama na kuwauliza: "Ni yupi miongoni mwenu aliye Mtume wa Allah?"

Kwa hiyo, Dola haitotoa amri ya kupiga marufuku mavazi ya mashekhe, bali itaondoa dhana yake na kuyafanya mavazi haya yasiwe maalumu kwa taaluma fulani kwa dhana inayopingana na Uislamu. Vilevile, itafanya hivyo kwa vazi lolote linaloashiria kuwepo kwa watu maalumu kwa ajili ya "dini" na watu wengine maalumu kwa ajili ya Dola. Kila raia atavaa vazi lolote miongoni mwa mavazi yaliyoruhusiwa bila vazi fulani kuhodhiwa na mtu maalumu wa "dini", ambapo watu humwelekea yeye kumuuliza kuhusu masuala ya "kiroho", na kuwaelekea wengine kumuuliza masuala ya kisiasa. Badala yake, Waislamu wote watakuwa na jukumu la Uislamu katika nyanja zake mbalimbali, na kila anayejua suala fulani atakuwa ni mwanachuoni katika suala hilo, awe amevaa kilemba au ana kichwa wazi.

03 Jumada al-Ula 1425 H 21/06/2004 M

Share Article

Share this article with your network