Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Hukumu ya Kisheria Kuhusu Bay’ as-Salam na Uhusiano Wake na Kuuza Nyumba Kabla ya Kujengwa

March 11, 2019
6854

(Silsila ya Majibu ya Mwanachuoni Mkubwa Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah, Amir wa Hizb ut-Tahrir, kwa Maswali ya Wageni kwenye Ukurasa Wake wa Facebook "Fiqhi")

Jibu la Swali

Hukumu ya Kisheria Kuhusu Bay’ as-Salam na Uhusiano Wake na Kuuza Nyumba Kabla ya Kujengwa

Kwa: Farah Farhat

Swali:

Bismillahir Rahmanir Rahim. Ndugu yangu, Mwenyezi Mungu akuhifadhi. Je, naweza kupata kwako jibu la kutosha kwa swali hili: Je, makampuni ya ukandarasi (phoprolos) – makampuni yanayouza nyumba kabla ya kujengwa – yanazingatiwa kuwa ni sehemu ya Bay’ as-Salam au la? Na je, jambo hili linajuzu kisharia, yaani kununua nyumba kabla haijajengwa?

Jibu:

Waalaykum Salam Warahmatullahi Wabarakatuh,

Unauliza kuhusu mambo mawili: La kwanza: Je, kuuza nyumba kabla ya kujengwa ni sehemu ya Bay’ as-Salam au la? Inafahamika kutokana na swali lako kwamba ikiwa ni sehemu ya Bay’ as-Salam, basi itakuwa inajuzu kwa sababu Bay’ as-Salam inajuzu kisharia... La pili: Je, kuuza nyumba kabla ya kujengwa kunajuzu kisharia?

Kuhusu jibu la swali la kwanza, kuuza nyumba kabla ya kujengwa hakuingii katika mlango wa Bay’ as-Salam, na ufafanuzi wa hilo ni kama ifuatavyo:

  • Bay’ as-Salam ni: "Kutoa malipo ya papo hapo kwa ajili ya bidhaa iliyoelezwa sifa zake itakayokabidhiwa baada ya muda maalumu. Yaani, kutoa pesa mapema kama thamani ya bidhaa ambayo ataikabidhi baada ya muda fulani uliowekwa." Huku ni kuuza kunakojuzu kisharia, na biashara hii hufanyika katika vitu vinavyopimwa kwa pishi/debe (makil), uzani (mawzun), na idadi (ma’dud) kama ilivyobainishwa katika kitabu cha Ash-Shakhshiyyah al-Islamiyyah, Juzuu ya Pili, ambapo imeelezwa:

"(Kujuzu kwa as-Salam kumethibiti kupitia Sunnah; imepokelewa kutoka kwa Ibn Abbas amesema:

مَنْ أَسْلَفَ فِي تَمْرٍ فَلْيُسْلِفْ فِي كَيْلٍ مَعْلُومٍ وَوَزْنٍ مَعْلُومٍ إِلَى أَجَلٍ مَعْلُومٍ

'Yeyote anayelipa mbele kwa ajili ya tende, basi alipe mbele kwa kipimo kinachojulikana na uzani unaojulikana hadi muda maalumu.' (Imepokelewa na Muslim).

Na kutoka kwa Abdurrahman bin Abza na Abdullah bin Abi Awfa walisema:

كُنَّا نُصِيبُ الْمَغَانِمَ مَعَ رَسُولِ اللَّهِ ﷺ فَكَانَ يَأْتِينَا أَنْبَاطٌ مِنْ أَنْبَاطِ الشَّامِ فَنُسْلِفُهُمْ فِي الْحِنْطَةِ وَالشَّعِيرِ وَالزَّبِيبِ إِلَى أَجَلٍ مُسَمًّى، قَالَ: قُلْتُ أَكَانَ لَهُمْ زَرْعٌ أَوْ لَمْ يَكُنْ لَهُمْ زَرْعٌ؟ قَالَا: مَا كُنَّا نَسْأَلُهُمْ عَنْ ذَلِكَ

'Tulikuwa tukipata ngawira pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw), na walikuwa wakitujia wakulima kutoka Sham, nasi tukiwalipa mbele kwa ajili ya ngano, shayiri, na zabibu hadi muda maalumu. Akasema (mpokezi): Nikasema, je, walikuwa na mimea au hawakuwa nayo? Wakasema: Hatukuwa tukiwauliza kuhusu hilo.' (Imepokelewa na Bukhari).

Na katika riwaya nyingine:

إِنَّا كُنَّا نُسْلِفُ عَلَى عَهْدِ رَسُولِ اللَّهِ ﷺ وَأَبِي بَكْرٍ وَعُمَرَ فِي الْحِنْطَةِ وَالشَّعِيرِ وَالتَّمْرِ وَالزَّبِيبِ إِلَى قَوْمٍ مَا هُوَ عِنْدَهُمْ

'Hakika sisi tulikuwa tukilipa mbele (tukifanya salaf) katika zama za Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw), Abu Bakr, na Umar katika ngano, shayiri, tende, na zabibu kwa watu ambao hawakuwa nazo (bidhaa hizo).' (Imepokelewa na Abu Dawood).

Hadithi hizi zote ni ushahidi wa wazi wa kujuzu kwa as-Salam. Ama kuhusu vitu gani ambavyo as-Salam inajuzu ndani yake, na vitu gani haijuzu, hilo liko wazi katika hadithi na Ijma’ (makubaliano ya wanachuoni). Hiyo ni kwa sababu as-Salam ni kuuza kitu ambacho mtu hakumiliki, na kuuza kile ambacho umiliki wake haujakamilika, na mambo haya mawili yamekatazwa. Lakini as-Salam imevuliwa katika hayo kupitia andiko (nass), hivyo ukatazwaji ukabaki katika vitu vingine. Kwa sababu hiyo, ni lazima kitu ambacho as-Salam inasihi ndani yake kiwe kimetajwa katika andiko.

Tukirejea katika maandiko, tunakuta kuwa as-Salam inajuzu katika kila kitu kinachopimwa kwa pishi (makil) na uzani (mawzun), kama inavyojuzu katika kila kitu kinachohesabika (ma’dud). Kuhusu kujuzu kwake katika vinavyopimwa na kupimwa uzani ni kutokana na hadithi ya Ibn Abbas aliyesema: 'Mtume (saw) alifika Madina na wao walikuwa wakilipia mbele tende kwa miaka miwili na mitatu, Mtume (saw) akasema:

مَنْ أَسْلَفَ فَلْيُسْلِفْ فِي ثَمَنٍ مَعْلُومٍ، وَوَزْنٍ مَعْلُومٍ إِلَى أَجَلٍ مَعْلُومٍ

'Yeyote anayelipa mbele, basi alipe katika thamani inayojulikana na uzani unaojulikana hadi muda maalumu.' (Bidayat al-Mujtahid wa Nihayat al-Muqtasid cha Ibn Rushd al-Hafid). Na katika riwaya nyingine kutoka kwa Ibn Abbas amesema: Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) amesema:

مَنْ أَسْلَفَ فِي شَيْءٍ فَفِي كَيْلٍ مَعْلُومٍ وَوَزْنٍ مَعْلُومٍ إِلَى أَجَلٍ مَعْلُومٍ

'Yeyote anayelipa mbele katika kitu chochote, basi iwe katika kipimo kinachojulikana na uzani unaojulikana hadi muda maalumu.' (Imepokelewa na Bukhari). Hii inaashiria kuwa mali inayofanyiwa as-Salam ni lazima iwe miongoni mwa vitu vinavyopimwa kwa pishi au uzani.

Kuhusu kujuzu kwake katika kila idadi (ma’dud), kumekuwa na Ijma’ kwamba as-Salam katika chakula inajuzu, na Ijma’ hii imenakiliwa na Ibn al-Mundhir. Bukhari amepokea amesema: Shu'bah alituhadithia akisema: Muhammad au Abdullah bin Abi al-Mujalid aliniambia: 'Abdullah bin Shaddad bin al-Had na Abu Burdah walitofautiana kuhusu as-Salaf, wakanituma kwa Ibn Abi Awfa (ra) nikamuuliza, akasema: Sisi tulikuwa tukilipia mbele katika zama za Mtume wa Mwenyezi Mungu, Abu Bakr, na Umar katika ngano, shayiri, zabibu na tende.' Hii inaashiria kuwa as-Salam katika chakula inajuzu. Na chakula hakiachi kuwa ni chenye kupimwa kwa pishi, uzani, au idadi... Hadithi ina andiko kuhusu kujuzu kwa kinachopimwa pishi na uzani na haikutaja kinachohesabika. Lakini Ijma’ ya kujuzu kwa as-Salam katika chakula inafanya kile kinachohesabika kuingia katika as-Salam. Isipokuwa ni sharti vitu vinavyofanyiwa as-Salam viwe vimebainishwa sifa zake kwa usahihi... na kubainisha kipimo au uzani... yaani ni lazima kipimo na mzani viwe vinajulikana na kuelezwa sifa zake.)" Mwisho wa nukuu kutoka katika kitabu cha Ash-Shakhshiyyah al-Islamiyyah, Juzuu ya Pili.

Kwa hiyo, as-Salam inajuzu katika vitu vinavyopimwa kwa pishi (makil), uzani (mawzun), na idadi (ma’dud) pekee.

  • Kuhusu kujua vipi kitu kinakuwa ni makil, mawzun, na ma’dud, ni kwa kutambua uhalisia wa mali ikiwa ni mali zinazofanana (amwal mithliyah) au mali zenye thamani ya kipekee (amwal qimiyah):

Mali zinazofanana (amwal mithliyah) ni mali ambazo mfano wake unapatikana sokoni kwa sifa zake bila tofauti yoyote ya maana, kama vile ngano. Kilogramu moja ya ngano yenye sifa maalumu ni sawa kabisa na kilogramu nyingine ya ngano ya aina hiyo hiyo...

Mali zenye thamani ya kipekee (amwal qimiyah) ni mali ambazo hazina mfano wake kamili sokoni, yaani ni vitu ambavyo sifa zake hazijirudii kwa namna ile ile moja kama mali zinazofanana. Nyumba ni mali ya kipekee (qimiyah) na sio mali inayofanana (mithliyah), kwa sababu kila nyumba inatofautiana na nyumba nyingine katika mambo mengi kama vile mahali ilipo, kiwanja ilipojengwa, aina ya ujenzi, n.k.

  • Vitu vinavyopimwa kwa pishi, uzani, na idadi ni sehemu ya mali zinazofanana kama tende, ngano, shayiri, zabibu na mfano wake. Mali hizi zina mfano wa aina yake ikiwa sifa zinalingana bila tofauti inayotajika. Katika mali hizi, wakati as-Salam inapofanyika, muuzaji anaahidi kumkabidhi mnunuzi baada ya muda maalumu kiasi maalumu cha bidhaa hizi zinazofanana kwa kipimo, uzani, au idadi bila kuainisha bidhaa mahususi (yaani haahidi kukabidhi ile ile aliyonayo, bali anaahidi kukabidhi mali yoyote yenye sifa zile zile). Katika Bay’ as-Salam, cha msingi ni kukabidhi mali yenye sifa zilizotajwa kwa muda uliopangwa, bila kujali mali hiyo imetoka katika ardhi gani, au ameinunua, au amepewa zawadi...

  • Nyumba haziwezi kuingia katika Bay’ as-Salam kwa sababu si miongoni mwa vitu vinavyopimwa kwa pishi, uzani, wala idadi, kwani si mali zinazofanana (mithliyah). Nyumba yoyote inayokusudiwa kuuzwa kabla ya kujengwa, hata kama imeelezwa sifa zake kwa usahihi na inafanana na nyumba nyingine, bado kutakuwa na tofauti kati yake na nyumba nyingine kama vile mahali ujenzi ulipo, kiwanja ilipojengwa, n.k. Hivyo basi, nyumba si mali inayofanana inayoweza kuingia katika Bay’ as-Salam.

Kwa hiyo, kuuza nyumba ambayo haijajengwa hakuingii katika mlango wa as-Salam na dalili za as-Salam hazitumiki kwake. Kwa hivyo, haijuzu kisharia kwa kuifungamanisha na Bay’ as-Salam inayojuzu kisharia.

Ama kuhusu jibu la swali la pili ambalo ni nini hukumu ya kuuza nyumba kabla ya kujengwa, tulishajibu swali kama hili mnamo 31/03/2016 kama ifuatavyo:

"(Kuuza nyumba za ghorofa kulingana na ramani kabla ya kujengwa:

a- Kuuza kitu ambacho mtu hakimiliki haijuzu, na hadithi nyingi zimekuja kuhusu hilo, miongoni mwazo:

  • Amepokea At-Tirmidhi katika Sunan yake kutoka kwa Hakim bin Hizam amesema: Nilimwendea Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) nikasema: Anakuja mtu ananiomba nimuuzie kitu ambacho sina, nikiende nikamnunulia sokoni kisha nimuuzie? Akasema:

لَا تَبِعْ مَا لَيْسَ عِنْدَكَ

'Usiuze kile ambacho huna.'

  • Amepokea At-Tirmidhi kutoka kwa Abdullah bin Amr kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) amesema:

لَا يَحِلُّ سَلَفٌ وَبَيْعٌ، وَلَا شَرْطَانِ فِي بَيْعٍ، وَلَا رِبْحُ مَا لَمْ يُضْمَنْ، وَلَا بَيْعُ مَا لَيْسَ عِنْدَكَ

'Hairuhusiwi mkopo na uuzaji, wala masharti mawili katika uuzaji mmoja, wala faida ya kitu ambacho hakijadhaminiwa, wala kuuza kile ambacho huna.'

Kwa sababu hiyo, haijuzu kuuza nyumba au sehemu ya ghorofa ambayo haijajengwa kwa sababu haijamilikiwa, na zaidi ya hapo, haipo na haijasimama...

b- Muhtasari ni kwamba kuuza nyumba za ghorofa ambazo hazijajengwa bado haijuzu, kwa sababu bidhaa inayouzwa (mube'e) haipo. Na ili uuzaji uwe sahihi, ni lazima nyumba iwepo uwepo unaoashiria kuwepo kwake kama vile msingi wake, nguzo, kuta, na mapaa, na mfano wa hayo ambayo yanatosha kidesturi kuashiria nyumba hiyo na kwamba imesimama na inaweza kukabidhiwa. Huu ndio msimamo wenye nguvu zaidi kwangu ambao unaondoa migogoro, hasa kwa kuwa matatizo mengi yametokea katika uuzaji wa namna hii wakati wa kukabidhiwa.

c- Mwisho, mikataba katika Uislamu imekusudiwa kuzuia migogoro, na kwa hivyo inapaswa kuwa juu ya kitu kinachomilikiwa na muuzaji, kilichopo, na kinachoweza kukabidhiwa bila vikwazo... Hivyo wanunuzi wanapaswa kuhakikisha upatikanaji wa mambo haya. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mpaji wa mafanikio.)" Mwisho.

Natumai jibu hili limekutosheleza, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi zaidi na Mwenye Hekima zaidi.

Ndugu yenu, Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah

04 Rajab 1440 H Sawa na 11/03/2019 M

Link ya jibu kutoka kwa ukurasa wa Amir (Mwenyezi Mungu amhifadhi) kwenye Facebook: https://web.facebook.com/AmeerhtAtabinKhalil/photos/a.122855544578192/1016227921907612/

Link ya jibu kutoka kwa ukurasa wa Amir (Mwenyezi Mungu amhifadhi) kwenye Google Plus: https://plus.google.com/u/0/b/100431756357007517653/100431756357007517653/posts/DGcibQ51Zqf

Link ya jibu kutoka kwa ukurasa wa Amir (Mwenyezi Mungu amhifadhi) kwenye Tovuti: http://archive.hizb-ut-tahrir.info/arabic/index.php/HTAmeer/QAsingle/3940

Share Article

Share this article with your network