Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Hukumu ya Kisheria Kuhusu "Upasuaji wa Urembo"

April 12, 2018
5227

(Mfululizo wa majibu ya Mwanachuoni Mkubwa Ata bin Khalil Abu Al-Rashtah, Amir wa Hizb ut-Tahrir, kwa maswali ya wafuasi wa ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi")

Jibu la Swali

Kwa Mourad Maalej

Swali:

Swali kwa Mwanachuoni Mkubwa Ata bin Khalil Abu Al-Rashtah, Assalamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh, Sheikh wetu mpendwa, ni ipi hukumu ya kisheria inayohusu "upasuaji wa urembo"? Barakallahu feek.

Jibu:

Wa Alaykum Salam Warahmatullahi Wabarakatuh,

1- Ikiwa upasuaji wa urembo ni kwa ajili ya matibabu, kama vile upasuaji wa kurekebisha ulemavu mwilini unaotokana na ugonjwa, ajali za barabarani, kuungua kwa moto, au mengineyo; au kuondoa kasoro za kimaumbile alizozaliwa nazo mtu kama vile kukata kidole cha ziada au kutenganisha vidole vilivyoungana, na mfano wa hayo; aina hii ya upasuaji inaruhusiwa. Dalili yake ni hadith iliyopokelewa na al-Tirmidhi kutoka kwa 'Arfajah bin As'ad aliyesema:

أُصِيبَ أَنْفِي يَوْمَ الْكُلَابِ فِي الْجَاهِلِيَّةِ فَاتَّخَذْتُ أَنْفًا مِنْ وَرِقٍ فَأَنْتَنَ عَلَيَّ فَأَمَرَنِي رَسُولُ اللَّهِ ﷺ أَنْ أَتَّخِذَ أَنْفًا مِنْ ذَهَبٍ

"Pua yangu ilikatwa siku ya vita vya al-Kulab katika zama za Jahiliyyah, hivyo nikajifanyia pua ya fedha, lakini ikanuka vibaya, ndipo Mtume wa Allah ﷺ akaniamuru nijifanyie pua ya dhahabu."

Abu Isa amesema hii ni hadith hasan gharib. Pia imepokelewa na al-Nisai kutoka kwa 'Arfajah bin As'ad kwamba:

أصيب أنفه يوم الكلاب في الجاهلية فاتخذ أنفا من ورق فأنتن عليه فأمره النبي ﷺ أن يتخذ أنفا من ذهب

"Pua yake ilikatwa siku ya al-Kulab katika zama za Jahiliyyah, hivyo akajifanyia pua ya fedha, lakini ikanuka vibaya, ndipo Mtume ﷺ akaniamuru ajifanyie pua ya dhahabu." (Imesahihishwa na al-Albani).

Neno "pua ya wariq" lina maana ya fedha. Hii inaashiria kuwa upasuaji wa urembo kwa ajili ya tiba na matibabu unaruhusiwa.

2- Ama ikiwa ni kwa ajili ya kuboresha muonekano na urembo tu na si kwa ajili ya matibabu, basi hili hairuhusiwi. Dalili ya hili ni:

Hadith iliyopokelewa na al-Bukhari kutoka kwa Alqama, Abdullahi amesema:

لَعَنَ اللَّهُ الْوَاشِمَاتِ وَالْمُسْتَوْشِمَاتِ وَالْمُتَنَمِّصَاتِ وَالْمُتَفَلِّجَاتِ لِلْحُسْنِ الْمُغَيِّرَاتِ خَلْقَ اللَّهِ تَعَالَى

"Allah amewalaani wanawake wanaochanja chale na wanaochanjwa chale, na wanaopunguza nyusi na wanaochana meno kwa ajili ya urembo, wenye kubadilisha uumbaji wa Allah Ta'ala."

Na Muslim amepokea kwa tamshi:

لَعَنَ اللَّهُ الْوَاشِمَاتِ وَالْمُسْتَوْشِمَاتِ وَالنَّامِصَاتِ وَالْمُتَنَمِّصَاتِ وَالْمُتَفَلِّجَاتِ لِلْحُسْنِ الْمُغَيِّرَاتِ خَلْقَ اللَّه

"Allah amewalaani wanawake wanaochanja chale na wanaochanjwa chale, na wanaopunguza nyusi na wanaopunguzwa nyusi, na wanaochana meno kwa ajili ya urembo, wenye kubadilisha uumbaji wa Allah."

Ni wazi kutokana na hadith hii kwamba wanaochana meno kwa ajili ya urembo wanapata dhambi, kumaanisha kitendo hiki ni haramu. Kitendo hiki kimefungamanishwa na sababu ('illah) ya "kwa ajili ya urembo" (lil-husn), ambayo ni sifa inayofahamisha maana. Hii ina maana kuwa anayechana meno yake kwa ajili ya urembo pekee ndiye anayepata dhambi. Hii inamaanisha ikiwa si kwa ajili ya urembo, bali kama tiba au matibabu, basi inaruhusiwa. Imekuja katika Lisan al-Arab: (Al-Falaj katika meno ni nafasi kati ya meno ya mbele na yale yanayofuata kimaumbile, na ikiwa itafanywa kwa makusudi basi huitwa Taflij). Kwa hiyo, maana ya Al-Mutafallijah ni mwanamke anayekata meno yake ili kuyapunguza na kutengeneza nafasi ndogo kati yake ili yapendeze na aonekane kama msichana mdogo; yaani bila ya kuwa na upogo katika meno yake unaohitaji matibabu, bali ni kwa ajili ya urembo na uzuri tu. Hili hairuhusiwi kwa mujibu wa hadith iliyosema kuwa Mtume ﷺ amewalaani wanaochana meno kwa ajili ya urembo (lil-husn). Hivyo, urembo ndio sababu ('illah) ya kukatazwa, na ikiwa sababu hiyo haipo, yaani ikiwa si kwa urembo bali ni kwa ajili ya tiba na matibabu, basi inaruhusiwa.

Al-Nawawi amesema katika kuelezea neno Al-Mutafallijat lil-husn lililokuja katika hadith ya Muslim:

(Wanaokusudiwa ni wale wanaochana meno kwa kuyasugua ili kutengeneza nafasi kati ya meno ya mbele. Hili hufanywa na wanawake wazee au walio karibu na uzee ili kuonekana vijana na wenye meno mazuri, kwani nafasi hiyo ndogo kati ya meno huwa ni sifa ya wasichana wadogo... Ama kauli yake "wanaochana meno kwa ajili ya urembo" ina maana kuwa wanafanya hivyo kwa kutafuta uzuri. Katika hili kuna ishara kuwa haramu ni kile kinachofanywa kwa ajili ya kutafuta urembo, lakini ikiwa atahitaji kufanya hivyo kwa ajili ya matibabu au kasoro katika jino na mfano wake, basi hakuna neno, na Allah anajua zaidi).

Hivyo basi, sababu ('illah) ni "kwa ajili ya urembo". Ikiwa upasuaji ni katika mlango wa matibabu na tiba, basi unaruhusiwa; lakini ikiwa maumbile yake ni ya kawaida na upasuaji si wa kurekebisha hitilafu bali ni kwa ajili ya uzuri na urembo tu, basi hauruhusiwi.

Hili ndilo ninaloliona kuwa na nguvu katika suala hili, na Allah ni Mjuzi zaidi na Mwenye Hekima zaidi.

Ndugu yenu, Ata bin Khalil Abu Al-Rashtah

25 Rajab 1439 H Inayowafikiwa na 12/04/2018 M

Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir (Allah amuhifadhi) kwenye Facebook

Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir (Allah amuhifadhi) kwenye Google Plus

Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir (Allah amuhifadhi) kwenye Twitter

Kiungo cha jibu kutoka kwenye tovuti ya Amir (Allah amuhifadhi) Web

Share Article

Share this article with your network