Jibu la Swali
Kushiriki katika Mifumo ya Kufuru
Swali:
Wakati wa utafiti kuhusu uharamu wa Mwislamu kushiriki katika mifumo ya sasa ya utawala ambayo haihukumu kwa Uislamu, kuna mtu alisema kuwa alimsikia mmoja wa mashekhe akijuzisha ushiriki huu akitolea dalili kuwa Yusuf (as) alihukumu kwa sheria ya mfalme nchini Misri... na kwamba Najashi alikaa miaka mingi akihukumu kwa kufuru akijulikana kuwa alikuwa Mwislamu na Mtume (saw) alimswalia swala ya jeneza akiwa mbali (swalatul ghaib)... kisha akasema kuwa maslahi (al-maslaha), ambayo ni dalili ya kisheria, yanahimiza hilo, kwani Mwislamu akiwa katika utawala anajali maslahi ya Waislamu zaidi kuliko mtu wa kidunia (sekularisti)...
Swali ni: Je, dalili hizi zina usahihi kiasi gani? Kisha, je, kuna mashekhe kweli wanaosema hivi? Tunaomba majibu yako, na Allah akulipe kheri.
Jibu:
Naam, baadhi ya mashekhe wa masultani wanasema kauli hizi, na hizi ni kauli ambazo hazina hoja yoyote, kwa sababu kuhukumu kwa yale aliyoyateremsha Allah kuna dalili zilizo wazi, za mkato katika ushahidi wake na maana yake (qat’iy ut-thubut qat’iy ud-dalalah), na si sehemu ya hitilafu miongoni mwa maimamu. Kuhukumu kwa aliyoyateremsha Allah ni fardhi (wajibu). Allah (swt) anasema:
فَاحْكُمْ بَيْنَهُمْ بِمَا أَنزَلَ اللَّهُ وَلَا تَتَّبِعْ أَهْوَاءَهُمْ عَمَّا جَاءَكَ مِنْ الْحَقِّ
"Basi hukumu baina yao kwa yale Aliyoyateremsha Allah, wala usifuate matamanio yao ukaacha haki iliyokujia." (QS. Al-Ma'idah [5]: 48)
Na Anasema (swt):
وَأَنْ احْكُمْ بَيْنَهُمْ بِمَا أَنزَلَ اللَّهُ وَلاَ تَتَّبِعْ أَهْوَاءَهُمْ وَاحْذَرْهُمْ أَنْ يَفْتِنُوكَ عَنْ بَعْضِ مَا أَنزَلَ اللَّهُ إِلَيْكَ
"Na uhukumu baina yao kwa Aliyoyateremsha Allah, wala usifuate matamanio yao, na uwe na tahadhari nao wasije wakakushawishi ukaacha baadhi ya yale Aliyokuteremshia Allah." (QS. Al-Ma'idah [5]: 49)
Maandiko (nusus) yenye maana hii ni mengi. Ama kutokuhukumu kwa aliyoyateremsha Allah na kukimbilia kuhukumu kwa sheria za kutungwa na wanadamu, hilo ni ukafiri ikiwa mtawala anaamini sheria hizo, na ni dhulma au ufuska ikiwa mtawala haziamini (lakini anazitumia). Hili limeelezwa katika kauli yake Allah (swt):
وَمَنْ لَمْ يَحْكُمْ بِمَا أَنزَلَ اللَّهُ فَأُوْلَئِكَ هُمْ الْكَافِرُونَ
"Na wasiohukumu kwa yale Aliyoyateremsha Allah, basi hao ndio makafiri." (QS. Al-Ma'idah [5]: 44)
Na kauli yake Allah (swt):
وَمَنْ لَمْ يَحْكُمْ بِمَا أَنزَلَ اللَّهُ فَأُوْلَئِكَ هُمْ الظَّالِمُونَ
"Na wasiohukumu kwa yale Aliyoyateremsha Allah, basi hao ndio madhalimu." (QS. Al-Ma'idah [5]: 45)
Na kauli yake Allah (swt):
وَمَنْ لَمْ يَحْكُمْ بِمَا أَنزَلَ اللَّهُ فَأُوْلَئِكَ هُمْ الْفَاسِقُونَ
"Na wasiohukumu kwa yale Aliyoyateremsha Allah, basi hao ndio mafasiki." (QS. Al-Ma'idah [5]: 47)
Ama kile walichokitolea dalili mashekhe wa masultani, kama tulivyosema, hakisimami kama hoja kwa sababu zifuatazo:
1- Kutolea dalili kwa kitendo cha Yusuf (as) kwa mujibu wa kauli ya wanaosema kuwa alikuwa akihukumu katika baadhi ya kadhia kwa sheria ya mfalme wa Misri, yaani kwa yale ambayo Allah hakuyateremsha, kutolea dalili huku hakuko mahali pake. Kwani sisi tumeamrishwa kufuata Uislamu uliokuja na Muhammad (saw) kwa wahyi kutoka kwa Allah (swt), na hatukuamrishwa kufuata sheria ya Yusuf (as) au manabii wengine (as). Hii ni kwa sababu sheria ya waliokuwa kabla yetu si sheria kwetu (shar'u man qablana laysa shar'an lana), kwani imefutwa na Uislamu. Allah (swt) anasema:
وَأَنْزَلْنَا إِلَيْكَ الْكِتَابَ بِالْحَقِّ مُصَدِّقًا لِمَا بَيْنَ يَدَيْهِ مِنَ الْكِتَابِ وَمُهَيْمِنًا عَلَيْهِ فَاحْكُمْ بَيْنَهُمْ بِمَا أَنْزَلَ اللَّهُ وَلَا تَتَّبِعْ أَهْوَاءَهُمْ عَمَّا جَاءَكَ مِنَ الْحَقِّ لِكُلٍّ جَعَلْنَا مِنْكُمْ شِرْعَةً وَمِنْهَاجًا
"Na Tumekuteremshia Kitabu kwa haki, kinachosadikisha yaliyokuwa kabla yake katika vitabu na kuwa na mamlaka (muhayminan) juu yake. Basi hukumu baina yao kwa yale Aliyoyateremsha Allah wala usifuate matamanio yao ukaacha haki iliyokujia. Kwa kila mmoja wenu Tumejaalia sheria na njia yake." (QS. Al-Ma'idah [5]: 48)
Maana ya "muhayminan" ni yenye kufuta (nasikhan). Hivyo, Uislamu ulifuta sheria za vitabu vilivyotangulia, na kwa sababu hiyo, sheria za waliotangulia si sheria kwetu.
Kuna baadhi ya maimamu wa usul al-fiqh wamechukua kanuni kwa namna nyingine: "sheria ya waliotangulia ni sheria kwetu maadamu haijafutwa". Hii inabainisha kuwa kutolea dalili sheria zilizopita kunakuwa tu katika hukumu ambazo hazikufutwa katika sheria hizo. Ama hukumu ambazo sheria yetu imekuja na kuzifuta, haijuzu kuzichukua kutoka katika sheria zilizopita; badala yake, tunatakiwa kufuata yale yaliyokuja katika sheria yetu. Kuhukumu kwa yale aliyoyateremsha Allah kuko wazi katika Uislamu, na ni chenye kufuta kila sheria iliyopita inayokhalifiana nalo. Hivyo, wanazuoni wote wa usul wanaozingatiwa, wawe wamesema kanuni ya kwanza au ya pili, wote wanawajibisha kuhukumu kwa aliyoyateremsha Allah kwa sababu imeelezwa katika Uislamu kwa namna ya wazi, ya mkato (qat'iy) na inafuta sheria zilizopita ikiwa zinatofautiana nayo.
Tunasema haya kwa kudhania tu kwamba Yusuf (as) alihukumu katika baadhi ya kadhia kwa sheria ya mfalme wa Misri, ingawa ukweli ni kwamba Yusuf (as) ni Nabii na ni ma'sum (aliyehifadhiwa na makosa), hivyo hahukumu ila kwa yale aliyoteremshiwa na Allah. Yeye, kama alivyosema Allah (swt) katika Surah Yusuf akizungumza na wenzake wawili gerezani kuwa hukumu ni ya Allah:
يَا صَاحِبَيِ السِّجْنِ أَأَرْبَابٌ مُتَفَرِّقُونَ خَيْرٌ أَمِ اللَّهُ الْوَاحِدُ الْقَهَّارُ (39) مَا تَعْبُدُونَ مِنْ دُونِهِ إِلَّا أَسْمَاءً سَمَّيْتُمُوهَا أَنْتُمْ وَآبَاؤُكُمْ مَا أَنْزَلَ اللَّهُ بِهَا مِنْ سُلْطَانٍ إِنِ الْحُكْمُ إِلَّا لِلَّهِ أَمَرَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ ذَلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ وَلَكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ
"Enyi marafiki zangu wawili wa gerezani! Je, waungu wengi wanaofarikiana ni bora au Allah Mmoja Mtendaji Nguvu? Hamuabudu badala Yake ila majina tu mliyoyaita nyinyi na baba zenu, ambayo Allah Hakuyateremshia ushahidi wowote. Hukumu haiko ila kwa Allah tu. Ameamrisha msiabudu yeyote ila Yeye tu. Hiyo ndiyo dini iliyonyooka, lakini watu wengi hawajui." (QS. Yusuf [12]: 39-40)
Yusuf (as) anasema: "Hukumu haiko ila kwa Allah". Hivyo, mamlaka ya kutoa hukumu ni ya Mola wa walimwengu ambaye Mwislamu anamuabudu na kuchukua sheria kutoka Kwake pekee, wala hachukui mola mwingine asiyekuwa Yeye.
Yusuf (as) asingekhalifisha vitendo vyake na kauli zake, ukamuona anaita kwenye mamlaka ya Allah (swt) na kisha anahukumu kwa kufuru. Kauli hii ina maana ya kutia doa katika kuhifadhiwa kwa Nabii miongoni mwa manabii wa Allah na kumzulia uongo, na jambo hilo ni zito... Hivyo basi, Yusuf (as) hakuwa akihukumu kwa kufuru, bali alikuwa akihukumu kwa yale aliyoteremshiwa na Allah, akiwa mkweli na mwenye ikhlasi kwa Allah (swt). Na kama tulivyosema, hata tukichukulia kuwa Allah alimruhusu Yusuf (as) katika sheria yake kuhukumu baadhi ya kadhia kwa sheria za mfalme wa Misri, basi Uislamu umefuta sheria zilizopita na imekuwa wajibu kwetu baada ya utume wa Rasulullah (saw) kuhukumu kwa Uislamu pekee.
2- Ama kutolea dalili msimamo wa Najashi, nako pia hakuko mahali pake. Kwani anayechunguza suala hili atagundua kuwa Najashi alikuwa mfalme kabla ya kusilimu kwake. Alisilimu kwa siri na alifariki muda mfupi baada ya kusilimu, na hakuwa na uwezo wa kutekeleza Uislamu wala hakuthubutu kutangaza kusilimu kwake kwa sababu watu wake walikuwa makafiri... Hali hii haifanani na yule ambaye ni Mwislamu anayejulikana Uislamu wake miongoni mwa watu. Tunaongeza ufafanuzi kwa kusema:
a- Neno Najashi si jina la mtawala wa Uhabeshi, bali ni cheo cha kila aliyekuwa akitawala Uhabeshi, aliitwa "Najashi" kama mtawala wa Uajemi alivyokuwa akiitwa Kisra na wa Rumi Kaisari... Najashi aliyesilimu na Mtume (saw) akamswalia hakuishi miaka mingi katika Uislamu kama ilivyoelezwa kwenye swali, bali ni kipindi kifupi kisichozidi siku au mwezi mmoja au miwili... Hivyo, yeye si yule Najashi ambaye Waislamu walihamia kwake kutoka Makka, na wala si yule Najashi ambaye Rasulullah (saw) alimtumia Amru bin Umayya ad-Damri baada ya Sulhu ya Hudaybiyyah wakati alipotuma wajumbe kwa watawala. Bali ni Najashi mwingine aliyetawala baada ya Najashi ambaye Rasulullah (saw) alimtumia barua pamoja na watawala wengine. Mapokezi ya suala hili yapo katika Bukhari na Muslim. Amekosea yule anayedhani kuwa Najashi aliyesilimu ndiye Najashi wa Uhabeshi ambaye Waislamu walimkimbilia kutoka Makka, au ndiye yule Najashi ambaye Rasulullah (saw) alimtumia Amru bin Umayya ad-Damri baada ya Hudaybiyyah. Mapokezi yanayopingana na yaliyo katika Bukhari na Muslim yanatupiliwa mbali. Kuhusu dalili za tuliyoyataja, tunataja miongoni mwake:
Ametoa Muslim kutoka kwa Qatada, kutoka kwa Anas: ("Kwamba Nabii wa Allah (saw) alimwandikia Kisra, Kaisari, Najashi, na kila jabari akiwaita kwa Allah Ta'ala", na hakuwa yule Najashi aliyeswaliwa na Nabii (saw).) Mwisho.
Ametoa Tirmidhi kutoka kwa Qatada, kutoka kwa Anas: ("Kwamba Rasulullah (saw) aliandika kabla ya kifo chake kwenda kwa Kisra, Kaisari, Najashi, na kila jabari akiwaita kwa Allah", na hakuwa yule Najashi aliyeswaliwa na Nabii (saw). "Hii ni hadith hasan sahih".) Mwisho.
Ni wazi kutokana na hadith ya Muslim na Tirmidhi kuwa Najashi aliyesilimu na Mtume (saw) akamswalia si yule Najashi ambaye Mtume alimtumia barua zake pamoja na watawala wengine.
b- Kwa kuwa Rasulullah (saw) alituma barua kwa watawala baada ya kurudi kwake kutoka Hudaybiyyah, yaani baada ya mwezi wa Dhul-Qi'dah mwaka wa sita Hijria, na kwa kuwa Najashi huyu aliyesilimu si yule Najashi aliyetumiwa barua na Mtume (saw) pamoja na watawala wengine, bali ni Najashi aliyekuja baada yake, basi atakuwa ameshika utawala karibu mwaka wa saba Hijria.
c- Na kwa sababu Abu Hurairah alikuwa pamoja na Rasulullah (saw) katika swala ya Najashi aliyesilimu kama ilivyo katika hadith za swala ya Najashi, na inajulikana kuwa Abu Hurairah baada ya kusilimu alikuja Madina na ujumbe wa kabila la Daws karibu watu sabini au themanini, akiwemo Abu Hurairah, na Rasulullah (saw) alikuwa Khaybar. Wakaenda kwake na kukutana naye huko. Rasulullah (saw) akawagawia sehemu ya ngawira za Khaybar. Khaybar ilikuwa mwaka wa saba Hijria, na hii ina maana kwamba Najashi aliyesilimu alichukua utawala wa Uhabeshi karibu mwaka wa saba Hijria na kufariki mwaka wa saba Hijria, yaani hakuishi isipokuwa siku chache au miezi michache tu...
d- Watu wa Uhabeshi wakati huo walikuwa makafiri wa dini ya Kikristo, na mtawala wao Najashi alisilimu kwa siri bila wao kujua, bali hata bila yeyote kujua, mpaka Rasulullah (saw) – kama inavyoeleweka kutokana na hadith za swala ya Najashi huyu – alijua kuhusu kifo cha Najashi kupitia wahyi. Maana ya hadith katika kumswalia inaonyesha hilo:
Ametoa Bukhari kutoka kwa Abu Hurairah (ra): "Kwamba Rasulullah (saw) alitangaza kifo cha Najashi siku aliyofariki, akatoka kwenda mahali pa kuswalia, akawapanga safu na akapiga takbir nne." Na katika mapokezi mengine: "Rasulullah (saw) alitutangazia kifo cha Najashi, mtawala wa Uhabeshi, siku aliyofariki," akasema: "Muombeeni msamaha ndugu yenu."
Ametoa Bukhari kutoka kwa Jabir bin Abdullah (ra), akisema: Nabii (saw) alisema: "Leo amefariki mtu mwema kutoka Uhabeshi, basi njooni, mswalieni." Akasema: Tukajipanga safu, na Nabii (saw) akamswalia na sisi tulikuwa pamoja naye katika safu. Abu Zubair akasema kutoka kwa Jabir: "Nilikuwa katika safu ya pili." Na katika mapokezi mengine kutoka kwa Jabir, Nabii (saw) alisema wakati Najashi alipofariki: "Leo amefariki mtu mwema, basi simameni mkamswalie ndugu yenu As-hama."
Maana ya maneno yaliyokuja katika hadith: "alitangaza kifo cha Najashi siku aliyofariki," "Rasulullah (saw) alitutangazia kifo cha Najashi, mtawala wa Uhabeshi, siku aliyofariki," akasema: "Muombeeni msamaha ndugu yenu," "Leo amefariki mtu mwema...". Kutangaza kifo siku aliyokufa, wakati Najashi yuko Uhabeshi na Mtume (saw) yuko Madina, ina maana kuwa habari hiyo imetokana na wahyi. Kadhalika, kauli ya Mtume (saw): "Muombeeni msamaha ndugu yenu," "Leo amefariki mtu mwema...", inamaanisha kuwa hawakuwa wakijua kuhusu kifo chake...
e- Hivyo basi, hali ya Najashi haitumiki hapa, kwani yeye alisilimu kwa siri, na watu wake walikuwa makafiri, na alifariki baada ya muda mfupi, na hakuna aliyejua kusilimu kwake isipokuwa Rasulullah (saw) kupitia wahyi... Hali hii hailingani na ushiriki wa Mwislamu anayejulikana Uislamu wake katika utawala usiohukumu kwa aliyoyateremsha Allah. Wanaosema kuwa inalingana hawana dalili, wala shaka ya dalili (shubhatu dalil).
3- Ama kutolea dalili kwa maslahi (al-maslaha), na kwamba ni dalili, nako pia hakuko mahali pake, na tunalichambua kama ifuatavyo:
Miongoni mwa wanazuoni wa usul al-fiqh kuna waliosema kuwa maslahi ni dalili, lakini walishurutisha kuwa kusiwe kumekuja amri au katazo katika sheria kuhusu jambo hilo. Ama ikiwa imekuja amri au katazo, basi hukumu ya maslahi haichukuliwi, bali kinachochukuliwa ni kile kilichokuja katika sheria. Hakuna mwanazuoni yeyote wa usul anayezingatiwa aliyesema kuwa maandiko ya wahyi yaachwe kwa hoja kuwa maslahi yanahitaji hilo.
Riba ni haramu, sheria imeiharamisha kwa maandiko ya wahyi. Hivyo ikiwa maslahi yanaihitaji, basi sheria inaikataa na kuiharamisha. Na ikiwa baadhi ya wanaoitwa wanazuoni watatoa fatwa ya kuiruhusu, basi fatwa yao inakataliwa na inagongana na sheria iliyokuja na wahyi.
Na suala la kuhukumu kwa yale ambayo Allah hakuyateremsha ni haramu kwa namna ya mkato (qat'iy) kama ilivyo haramu riba kwa sababu maandiko ya wahyi yamekuja na hilo. Hivyo hakuna nafasi yoyote ya kuhukumu kwa kutumia maslahi, kwani palipo na sheria ndipo penye maslahi na si kinyume chake.
Sisi katika utafiti huu tunakubaliana na wanazuoni wa usul waliokuwa wepesi na kusema kuhusu al-masalih al-mursalah, lakini hata kwa mujibu wa madhehebu ya hawa, hakuna nafasi ya kutolea dalili kwa maslahi. Pamoja na kwamba ukweli ni kuwa al-masalih al-mursalah haipo, bali ipo tu machoni pa wale waliosema kuwa sheria iliacha baadhi ya mambo bila kuyaamrisha au kuyakataza, na wakasema kuwa wanatumia maslahi katika uwanja huo. Ukweli ni kwamba sheria haikuacha jambo lolote bila kubainisha hukumu yake, bali imebainisha hukumu ya kila kitu:
تِبْيَانًا لِكُلِّ شَيْءٍ
"...ubainifu wa kila kitu..." (QS. An-Nahl [16]: 89)
مَا فَرَّطْنَا فِي الْكِتَابِ مِنْ شَيْءٍ
"...Hatukuacha katika Kitabu kitu chochote." (QS. Al-An'am [6]: 38)
الْيَوْمَ أَكْمَلْتُ لَكُمْ دِينَكُمْ وَأَتْمَمْتُ عَلَيْكُمْ نِعْمَتِي وَرَضِيتُ لَكُمُ الْإِسْلَامَ دِينًا
"Leo nimekukamilishieni Dini yenu, na nimekutimizieni neema Yangu, na nimekupendeleeni Uislamu uwe Dini yenu." (QS. Al-Ma'idah [5]: 3)
4- Muhtasari ni kwamba ushiriki katika mifumo ya kufuru na kuhukumu kwa yale ambayo Allah hakuyateremsha ni ukafiri ikiwa mtawala anayehukumu kwa yasiyoteremshwa na Allah anaamini hukumu hiyo, na ni dhulma na ufuska ikiwa mtawala anayehukumu kwa yasiyoteremshwa na Allah haamini hukumu hiyo, kama ilivyo katika aya tukufu:
وَمَنْ لَمْ يَحْكُمْ بِمَا أَنزَلَ اللَّهُ فَأُوْلَئِكَ هُمْ الْكَافِرُونَ
"Na wasiohukumu kwa yale Aliyoyateremsha Allah, basi hao ndio makafiri." (QS. Al-Ma'idah [5]: 44)
وَمَنْ لَمْ يَحْكُمْ بِمَا أَنْزَلَ اللَّهُ فَأُولَئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ
"Na wasiohukumu kwa yale Aliyoyateremsha Allah, basi hao ndio madhalimu." (QS. Al-Ma'idah [5]: 45)
وَمَنْ لَمْ يَحْكُمْ بِمَا أَنْزَلَ اللَّهُ فَأُولَئِكَ هُمُ الْفَاسِقُونَ
"Na wasiohukumu kwa yale Aliyoyateremsha Allah, basi hao ndio mafasiki." (QS. Al-Ma'idah [5]: 47)
Na wanaosema kuwa inajuzu kwa Mwislamu kushiriki katika utawala usiohukumu kwa aliyoyateremsha Allah hawana dalili wala shaka ya dalili, kwa sababu maandiko ya kuzuia hilo ni ya mkato katika ushahidi na maana yake (qat’iy ut-thubut wa ad-dalalah).
Natumai jibu hili liko wazi, linajitosheleza na kuponya (shaka) kwa idhini ya Allah (swt).