(Sfululizo wa majibu ya mwanachuoni mtukufu Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah, Ameer wa Hizb ut-Tahrir, kwa maswali ya wafuasi wa ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi")
Jibu la Swali
Kwa Mustafa al-Maqdisi
Swali:
Assalam Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh,
Imetajwa katika kitabu cha Ash-Shakhsiyyah al-Islamiyyah Juzuu ya 1, chini ya kichwa cha habari "Kuporomoka kwa Fiqhi ya Kiislamu" ukurasa wa 392 (nakala ya Kiarabu), nukuu isemayo: (Watu kama Al-Qaffal wanasema kufungwa kwa mlango wa Ijtihad). Lakini nimepekua kuhusu mwanachuoni huyu na sikuwapata isipokuwa wawili tu, na sijaona katika wasifu wao kwamba walilingania kufungwa kwa mlango wa Ijtihad; nao ni Al-Qaffal ash-Shashi na Al-Qaffal al-Marwazi, na wote wako kwenye fiqhi ya Shafi'i. Hivyo, ni mwanachuoni gani aliyekusudiwa katika kitabu hicho?
Jazakumullah Khayran.
Jibu:
Wa Alaykum Salam Warahmatullahi Wabarakatuh,
1- Swali lako linahusiana na yale yaliyokuja katika kitabu cha Ash-Shakhsiyyah al-Islamiyyah Juzuu ya Kwanza chini ya kichwa cha habari "Kuporomoka kwa Fiqhi ya Kiislamu", nayo ni kama ifuatavyo: (...bali walifikia hatua ya kuufunga mlango wa Ijtihad kwa Waislamu, na wakasema kutofaa kwa Ijtihad, mpaka wanachuoni wengi miongoni mwa wale wenye sifa za Ijtihad, na waliofikia uwezo wa Ijtihad, wakawa hawathubutu kufanya Ijtihad, wala kusema kuwa wao ni mujtahid. Na kudorora huku kulianza mwishoni mwa karne ya nne Hijiria. Isipokuwa kwamba mwanzoni, hadi mwisho wa karne ya sita Hijiria na mwanzoni mwa ya saba, kulikuwa na kiwango fulani cha kuinuka. Walipatikana mujtahid na walipatikana wanachuoni wakati ambao watu kama Al-Qaffal walikuwa wakisema kufungwa kwa mlango wa Ijtihad.)
2- Kuhusu Al-Qaffal, imetajwa katika baadhi ya vyanzo kwamba kuna watu watatu wenye lakabu ya Al-Qaffal na sio wawili kama ilivyokuja katika swali lako, nao ni:
a- Imekuja katika Siyar A’lam al-Nubala (16/ 283):
(Al-Qaffal ash-Shashi, Imam, Allamah, Faqihi, mtaalamu wa misingi (Usul), mtaalamu wa lugha, mwanachuoni wa Khorasan, Abu Bakr, Muhammad bin Ali bin Ismail bin ash-Shashi ash-Shafi’i, Al-Qaffal al-Kabir, Imam wa zama zake katika maeneo ya nyuma ya mto (Transoxiana), na mtunzi wa vitabu vingi. Al-Hakim amesema: Alikuwa mjuzi zaidi wa watu wa Transoxiana katika elimu ya Usul, na aliyesafiri zaidi katika kutafuta Hadith. Sheikh Abu Ishaq amesema katika "At-Tabaqat" kuwa alifariki mwaka wa 336. Lakini huu ni mkanganyiko wa wazi kwani Al-Hakim aliandika tarehe ya kufa kwake kuwa mwishoni mwa mwaka wa 365 huko Shash. Na hivyo ndivyo alivyoandika Abu Sa'd al-Sam'ani, na akaongeza kuwa alizaliwa mwaka wa 291. Amesema: Ana vitabu vingi ambavyo hakuna yeyote mwenye mfano wake, naye ndiye wa kwanza kuandika kuhusu mjadala mzuri (al-jadal al-hasan) miongoni mwa mafaqihi, na ana kitabu cha Usul al-Fiqh, na ana "Sharh al-Risalah", na kupitia kwake fiqhi ya Shafi'i ilienea Transoxiana. Al-Sam'ani amesema: Abu Bakr alitunga kitabu cha "Dala'il al-Nubuwwah", na kitabu cha "Mahasin al-Shari'ah"...)
Na imekuja kumhusu yeye katika Tabaqat al-Shafi’iyyah:
(Muhammad bin Ali bin Ismail Abu Bakr ash-Shashi Al-Qaffal al-Kabir, mmoja wa magwiji wa madhehebu na maimamu wa Waislamu. Alizaliwa mwaka wa 291... Sheikh Abu Ishaq amesema alikuwa Imam na alikuwa na vitabu vingi ambavyo hakuna mfano wake, na yeye ndiye wa kwanza kuandika mjadala mzuri miongoni mwa mafaqihi, na ana kitabu kizuri cha Usul al-Fiqh na ana Sharh al-Risalah. Kupitia kwake fiqhi ya Shafi'i ilienea Transoxiana na Al-Hakim amesema: Alikuwa mjuzi zaidi wa watu wa Transoxiana - yaani katika zama zake - kuhusu Usul na aliyesafiri zaidi katika kutafuta Hadith. Na Al-Halimi amesema: Sheikh wetu Al-Qaffal alikuwa mjuzi zaidi niliyewahi kukutana naye miongoni mwa wanachuoni wa zama zake. An-Nawawi amesema katika Tahdhib yake: Ikitajwa Al-Qaffal ash-Shashi basi anakusudiwa huyu, na ikija Al-Qaffal al-Marwazi basi huyo ni mdogo (Al-Saghir)... Na miongoni mwa vitabu vya Ash-Shashi: Dala’il al-Nubuwwah, Mahasin al-Shari’ah, Adab al-Qada' ambacho ni juzuu kubwa, na Tafsir kubwa. Alifariki Dhul-Hijjah mwaka 365...).
b- Imekuja katika Siyar A’lam al-Nubala (17/ 405):
(Al-Qaffal, Imam, Allamah mkubwa, Sheikh wa Mashafii, Abu Bakr, Abdullah bin Ahmad bin Abdullah, Al-Marwazi al-Khurasani. Alibobea katika ufundi wa makufuli mpaka akatengeneza kufuli pamoja na zana zake na ufunguo wake lenye uzito wa chembe nne, na alipofikisha umri wa miaka thelathini, alihisi ndani yake akili ya kipekee, akapenda fiqhi, akaielekea kwa kuisoma mpaka akabobea, na akawa anapigiwa mfano kwayo, naye ndiye mwenye njia ya Wakhurasani katika fiqhi. Faqihi Nasir al-Umari amesema: Hapakuwa na faqihi zaidi kuliko Abu Bakr Al-Qaffal katika zama zake, wala hakutakuwepo na mfano wake baada yake, na tulikuwa tukisema: Hakika yeye ni malaika katika umbo la mwanadamu... Na Abu Bakr al-Sam'ani amesema katika "Amali" zake: Alikuwa wa pekee katika zama zake katika fiqhi, kuhifadhi, uchamungu (wara') na zuhudi, na ana athari katika madhehebu ambazo hakuwa nazo mwingine miongoni mwa watu wa zama zake. Njia yake iliyonyooka katika madhehebu ya Shafi'i ambayo wanafunzi wake waliibeba kutoka kwake ndiyo njia imara zaidi na yenye uhakiki zaidi. Mafaqihi walimsafiria kutoka miji mbalimbali, na maimamu walihitimu kupitia kwake. Alifariki mwaka wa 417 mwezi wa Jumada al-Akhira akiwa na umri wa miaka tisini...)
Na imeelezwa kumhusu katika Tabaqat al-Shafi’iyyah yafuatayo:
(Abdullah bin Ahmad bin Abdullah al-Marwazi, Imam mtukufu Abu Bakr Al-Qaffal al-Saghir, Sheikh wa njia ya Khorasan. Alitwa Al-Qaffal kwa sababu alikuwa akitengeneza makufuli mwanzoni mwa maisha yake, na alibobea katika ufundi huo mpaka akatengeneza kufuli na vifaa vyake na ufunguo wake lenye uzito wa chembe nne. Alipofika umri wa miaka thelathini, alihisi akili ndani yake akaielekea fiqhi akajishughulisha nayo kwa Sheikh Abu Zaid na wengineo, akawa Imam anayefuatwa, na watu wengi wa Khorasan walijifunza fiqhi kwake, akasikiliza Hadith na akahadithia... Hafidh Abu Bakr al-Sam'ani amesema katika Amali zake: Abu Bakr Al-Qaffal alikuwa wa kipekee katika zama zake katika fiqhi, kuhifadhi, uchamungu na zuhudi... Alifariki Marwa mwezi wa Jumada al-Akhira mwaka 417 akiwa na umri wa miaka tisini. Miongoni mwa vitabu vyake ni Sharh al-Talkhis ambacho ni juzuu mbili, Sharh al-Furu’ katika juzuu moja, na Kitab al-Fatawa chenye juzuu kubwa na faida nyingi.)
c- Imekuja katika Al-A’lam cha Az-Zirikli:
(Muhammad bin Ahmad bin al-Hussein bin Umar, Abu Bakr ash-Shashi Al-Qaffal al-Fariqi, mwenye lakabu ya Fakhr al-Islam, Al-Mustazhiri: Kiongozi wa Mashafii huko Iraq katika zama zake... Alizaliwa Mayyafariqin, akasafiri kwenda Baghdad akashika nafasi ya ualimu katika shule ya Al-Nidhamiyyah (mwaka 504) na aliendelea hadi alipofariki... Miongoni mwa vitabu vyake ni "Hilyat al-Ulama fi Ma'rifat Madhahib al-Fuqaha" - na akajulikana kupitia hicho kama Al-Mustazhiri - kwa sababu alikitunga kwa ajili ya Imam Al-Mustadhir Billah, na "Al-Mu'tamad" ambacho ni kama maelezo yake (sharh), na "Al-Shafi" sharh ya Mukhtasar al-Muzani, na "Al-Fatawa" - na inajulikana kama Fatawa za Ash-Shashi - na "Al-Umdah fi Furu’ al-Shafi’iyyah"... nk.)
Na imeelezwa kumhusu katika Tabaqat al-Shafi’iyyah yafuatayo:
(Muhammad bin Ahmad bin al-Hussein bin Umar, Fakhr al-Islam Abu Bakr ash-Shashi. Alizaliwa Mayyafariqin mwezi wa Muharram mwaka 429... Uongozi wa madhehebu uliishia kwake baada ya sheikh wake, na alifundisha katika shule ya Nidhamiyyah ya Baghdad kwa mwaka mmoja na nusu. Adh-Dhahabi amesema: Alikuwa Mwash'ari, Msufi... Alifariki mwezi wa Shawwal mwaka 507 na akazikwa pamoja na sheikh wake Abu Ishaq katika kaburi moja... Ana kitabu cha Al-Hilyah katika juzuu mbili, akataja humo tofauti nyingi za wanachuoni...)
Hivyo, hawa ni watu watatu miongoni mwa mafaqihi wa Shafi'i waliopewa lakabu ya Al-Qaffal:
Wa kwanza na ndiye mkongwe zaidi: Al-Qaffal ash-Shashi al-Kabir (291 - 365 H), naye ni Muhammad bin Ali ash-Shashi Al-Qaffal, Abu Bakr. Jina lake linanasibishwa na (Shash) ambayo ni mji katika nchi za Transoxiana...
Wa pili ni Al-Qaffal al-Marwazi (327 - 417 H), naye ni Abdullah bin Ahmad bin Abdullah, Abu Bakr, maarufu kama Al-Qaffal al-Marwazi. Jina lake linanasibishwa na "Marw al-Shahijan". Alipewa lakabu ya Al-Qaffal kwa sababu kazi yake ilikuwa ni kutengeneza makufuli, na pengine huitwa "Al-Qaffal al-Saghir" ili kumtofautisha na Al-Qaffal ash-Shashi al-Kabir aliyefariki mwaka 365 H... Naye ni faqihi wa Shafi'i. Sheikh wa Wakhurasani miongoni mwa Mashafii. Mwanzoni mwa maisha yake alikuwa akitengeneza makufuli, na alipofika umri wa miaka thelathini akajishughulisha na elimu mpaka wanafunzi kutoka miji mbalimbali wakamsafiria, wakihitimu kwake na kuwa maimamu. Alifariki Sijistan. Miongoni mwa vitabu vyake ni (Sharh Furu’ Ibn al-Haddad) katika fiqhi.
Na wa tatu ni Al-Qaffal al-Mustazhiri (429 - 507 H), naye ni Muhammad bin Ahmad bin al-Hussein bin Umar, Abu Bakr, Fakhr al-Islam ash-Shashi, Al-Qaffal, al-Fariqi, maarufu kama Al-Mustazhiri. Alizaliwa Mayyafariqin - mji maarufu zaidi katika Diyar Bakr - faqihi wa Shafi'i... Alikuwa mfuasi wa karibu wa Abu Ishaq al-Shirazi. Miongoni mwa vitabu vyake: "Hilyat al-Ulama fi Madhahib al-Fuqaha"... na huyu Al-Qaffal wa tatu sio vyanzo vyote vinavyomtaja kuwa alikuwa na lakabu ya Al-Qaffal, bali Az-Zirikli ndiye aliyetaja hilo katika Al-A’lam.
3- Ama yule anayenasibishiwa kuwa alifunga mlango wa Ijtihad ni Al-Qaffal al-Marwazi Sheikh wa Wakhurasani, na miongoni mwa ushahidi wa hilo ni:
a- Hashiyat al-Attar (2/ 423) juu ya maelezo ya Al-Jalal al-Mahalli kuhusu (Jam' al-Jawami’ cha Abdul Wahab bin Ali Tajuddin al-Subki aliyefariki mwaka 771 H): (Na mtunzi amedai kuwa baba yake alifikia daraja ya Ijtihad huru (Al-Ijtihad al-Mutlaq), akasema katika Tarshih al-Tawshih: Ikiwa utasema: Madai yenu ya kufikia kwa Sheikh Imam daraja ya Ijtihad huru yanapingwa na kauli ya Al-Ghazali katika Al-Wasit kwamba: Zama zimekuwa tupu bila ya kuwa na mujtahid mustaqil (huru), na hili si yeye pekee aliyelisema bali alitanguliwa nalo na Al-Qaffal Sheikh wa Wakhurasani, na Ar-Rafi’i na An-Nawawi walilinukuu kutoka kwa Al-Wasit na wakanyamaza... Nimesema: Nimeyatazama maneno haya na nikayafikiria, ikanidhihirikia kuwa yeye na wale waliomtangulia walikusudia tu kuwa zama ziko tupu bila ya kuwa na mujtahid anayesimamia majukumu ya ukadhi...)
b- Amesema Imam Az-Zarkashi aliyefariki mwaka 794 H katika kitabu cha Al-Bahr: (Ama kauli ya Al-Ghazali: "Zama zimekuwa tupu bila ya kuwa na mujtahid mustaqil", basi alitanguliwa kwayo na Al-Qaffal Sheikh wa Wakhurasani, ikasemwa: Makusudio ni mujtahid anayeshika nafasi ya ukadhi, kwani wahakiki miongoni mwa wanachuoni walikuwa wakiikwepa, na kwa kawaida hawashiki nafasi hiyo katika zama zao isipokuwa wale walio chini ya daraja hiyo. Na inawezekanaje kuhukumu zama kuwa ziko tupu bila ya kuwa na mujtahid, wakati Al-Qaffal mwenyewe alikuwa akimwambia muulizaji katika suala la Al-Subrah: Unaniuliza kuhusu madhehebu ya Ash-Shafi’i au yale niliyo nayo mimi? Na akasema, yeye na Sheikh Abu Ali na Kadhi Hussein: Sisi si wafuasi (muqallidun) wa Shafi’i, bali maoni yetu yameoana na maoni yake...)
4- Kutokana na yaliyotangulia, inabainika kuwa kuna wanaomnasibishia Al-Qaffal Sheikh wa Wakhurasani, naye ni Al-Qaffal al-Marwazi (327 - 417 H), kufunga mlango wa Ijtihad, au angalau kwamba zama hizo zilikosa mujtahid huru, yaani asiyemfuata mujtahid aliyemtangulia... ingawa maneno hayo si ya wazi kabisa katika kukataza Ijtihad!
Lakini la kushangaza ni kwamba Al-Qaffal al-Khurasani ambaye ananasibishiwa kufungwa kwa mlango wa Ijtihad, kazi yake ilikuwa ni kutengeneza makufuli (aqfal) na alikuwa stadi kwayo... Na pengine ni miongoni mwa sadfa za ajabu kwamba kazi yake hii ya kutengeneza makufuli inaingiliana na yale anayonasibishiwa ya kufunga mlango wa Ijtihad! Sijui ikiwa kunasibishwa kwa kufungwa kwa mlango wa Ijtihad kwake kulitokana na athari ya kazi yake ya makufuli au ni sadfa tu! Nasema hivi kwa sababu kama ilivyokuja katika Al-Bahr cha Az-Zarkashi hapo juu, yeye alikuwa akifanya Ijtihad pamoja na kuwa alikuwa katika madhehebu ya Shafi’i. Imekuja katika chanzo hicho hicho: (Na Al-Qaffal mwenyewe alikuwa akimwambia muulizaji katika suala la Al-Subrah: Unaniuliza kuhusu madhehebu ya Ash-Shafi’i au yale niliyo nayo mimi? Na akasema, yeye na Sheikh Abu Ali na Kadhi Hussein: Sisi si wafuasi wa Shafi’i, bali maoni yetu yameoana na maoni yake...)
Hata hivyo, natumai kuwa katika haya pana kutosheka kama jibu la swali lako.
Ndugu yenu Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah
26 Sha'ban 1439 H Inayolingana na 12/05/2018 M
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Facebook wa Ameer (Mwenyezi Mungu amuhifadhi): https://web.facebook.com/AmeerhtAtabinKhalil/photos/pb.122848424578904.-2207520000.1526160079./811843495679390/?type=3&theater
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Google Plus wa Ameer (Mwenyezi Mungu amuhifadhi): https://plus.google.com/u/0/b/100431756357007517653/100431756357007517653/posts/V72mJDoSR4Y
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Twitter wa Ameer (Mwenyezi Mungu amuhifadhi): https://twitter.com/ataabualrashtah/status/995412736925421569
Kiungo cha jibu kutoka kwenye tovuti ya Ameer (Mwenyezi Mungu amuhifadhi)