Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Swala Ambayo Muislamu Hakuitekeleza ni Deni Shingoni Mwake Ambalo ni Lazima Alilipe

May 05, 2021
4014

Silsila ya majibu ya mwanachuoni mtukufu Ata bin Khalil Abu al-Rashtah, Amir wa Hizb ut Tahrir, kwa maswali ya wafuasi wa ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi"

Jibu la Swali

Kwa Mohammad Alhajj

Swali:

Assalamu alaikum wa rahmatullahi wa barakatuh

Salamu za heshima baada ya hapo:

Nimeona ukurasa wenu hivi karibuni kupitia msaada wa rafiki yangu miongoni mwa vijana wa Hizb ut Tahrir. Nimevutiwa na uelewa wenu katika uwasilishaji na nguvu ya hoja, hasa majibu ya maswali ya kifikihi. Namuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu arefushe umri wenu kwa ajili ya kufanya kheri, azidishe elimu yenu, na aniongoze kwenye njia inayomridhisha Mwenyezi Mungu na Mtume Wake.

Naomba unijibu swali hili:

Nilianza kujitolea kuswali baada ya kupita miaka kadhaa tangu kufikia umri wa kuwajibika (ubaleghe), namshukuru Mwenyezi Mungu kwa hilo. Swali langu ni: Je, ni lazima nilipe swala zilizonipita, au Mwenyezi Mungu atanisamehe bila ya kuzilipa?

Shukrani kwako.

Jibu:

Wa alaikum assalam wa rahmatullahi wa barakatuh,

Mwanzoni, namhimidi Mwenyezi Mungu (swt) kwa kukuongoza kwenye kheri, ukawa unashika swala na kuwa na pupa ya kuitekeleza. Namuomba Mwenyezi Mungu (swt) akupe msaada na msimamo...

Ama kuhusu swala ambazo hukuitekeleza hapo awali tangu ulipobaleghe na kuwa mkalafishaji (mwenye kuwajibika kisheria), kwa kuwa wewe ni Muislamu, swala hizi ambazo hukuitekeleza ni deni shingoni mwako ambalo ni lazima ulilipe. Kwa hivyo, unapaswa kukokotoa muda tangu ulipobaleghe hadi wakati ulipoanza kushika swala. Tuseme kwa mfano muda huo ulikuwa ni miaka mitatu, basi ni lazima ulipe swala za miaka mitatu: swala tano kwa siku ambazo ni swala za faradhi, ama sunna zake si lazima kwako kuzilipa...

Inawezekana kupanga jambo hili na kulirahisisha kwa kuswali kila siku baada ya kila swala ya faradhi swala nyingine mfano wake kama kulipa (qadha) ya swala iliyokupita. Na ukitaka kuswali mara nyingine kwa ajili ya kulipa, yote ni kheri, hadi utakapomaliza miaka uliyopiga hesabu... Namuomba Mwenyezi Mungu (swt) akusaidie kulipa swala hizo zilizokupita na azidishe pupa yako ya kuswali kwa wakati...

Na ili kubainisha dalili za kishari'ah kuhusu jambo hili, nakunukulia baadhi ya yaliyokuja katika kitabu Ahkam as-Salah (Ali Raghib):

[Kuchelewesha swala baada ya wakati wake kwa makusudi bila udhuru wa kisheria ni haramu kabisa kwa nass (andiko) ya Qur'ani. Amesema Ta'ala:

فَوَيْلٌ لِلْمُصَلِّينَ * الَّذِينَ هُمْ عَنْ صَلاَتِهِمْ سَاهُونَ

"Basi ole wao wanaoswali. Ambao wanapuuza swala zao." (QS. Al-Ma'un [107]: 4-5)

Na amesema Ta'ala:

فَخَلَفَ مِنْ بَعْدِهِمْ خَلْفٌ أَضَاعُوا الصَّلاَةَ وَاتَّبَعُوا الشَّهَوَاتِ فَسَوْفَ يَلْقَوْنَ غَيّاً

"Lakini walifuata baada yao wafuasi wabaya, walioacha swala na wakafuata matamanio; basi watakutana na upotovu." (QS. Maryam [19]: 59).

Hili pia limethibiti kwa mafhum (maana inayoeleweka) ya hadith mutawatir ambayo imebainisha nyakati. Mwenyezi Mungu ameiwekea kila swala ya faradhi wakati wenye mipaka miwili, unaingia wakati maalum na kumalizika wakati maalum. Na amesema (saw):

مَنْ فَاتَتْهُ صَلَاةُ الْعَصْرِ فَكَأَنَّمَا وُتِرَ أَهْلَهُ وَمَالَهُ

"Mwenye kupitwa na swala ya Alasiri, ni kama amepoteza familia yake na mali yake."

Na amesema ﷺ kuhusu kuchelewesha swala baada ya wakati wake:

لَيْسَ التَّفْرِيطُ فِي النَّوْمِ إِنَّمَا التَّفْرِيطُ فِي الْيَقَظَةِ

"Hakuna uzembe katika kulala, bali uzembe uko katika kuwa macho..."

Na mwenye kupitwa na swala ya faradhi hulipa, iwe imempita kwa udhuru au bila udhuru. Kwa sababu kulipa swala pekee kumethibiti kwa hadith sahihi. Imepokewa katika Sahihayn kutoka kwa Imran bin Husayn amesema: Tulikuwa safarini pamoja na Mtume ﷺ, tukasafiri usiku kucha hadi mwisho wa usiku tukalala, na hakuna usingizi mtamu kwa msafiri kama huo, basi hakuna kilichotuamsha isipokuwa joto la jua... Mtume ﷺ alipoamka, walimshitakia yaliyowasibu, akasema:

لَا ضَيْرَ أَوْ لَا يَضِيرُ ارْتَحِلُوا، فَارْتَحِلُوا فَسَارَ غَيْرَ بَعِيدٍ، ثُمَّ نَزَلَ فَدَعَا بِمَاءٍ فَتَوضَّأَ، ثُمَّ نَادَى بِالصَّلَاةِ فَصَلَّى بِالنَّاسِ

"Haidhuruni, au hakuna neno, ondokeni. Basi wakaondoka na kutembea umbali mdogo, kisha akashuka akaitisha maji akatawadha, kisha akatoa wito wa swala na akaswalisha watu."

Na kwa yaliyopokewa kutoka kwa Jabir (ra) "Kwamba Umar bin Al-Khattab alikuja siku ya handaki (vita vya Al-Ahzab) baada ya jua kuzama akaanza kuwatukana makafiri wa Kikuraishi, akasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, sikuwa nakaribia kuswali Alasiri hadi jua likawa karibu kuzama. Mtume ﷺ akasema: Wallahi mimi sijaichukua (sijaiswali). Basi tukasimama kuelekea But'han akatawadha kwa ajili ya swala na tukatawadha, akaswali Alasiri baada ya jua kuzama kisha akaswali baada yake Magharibi."

Na kwa yaliyopokewa kutoka kwa Abi Said amesema: "Tulizuiwa siku ya handaki kuswali hadi ikawa baada ya Magharibi kwa sehemu ya usiku hadi tulipotoshelezwa (na maadui), na hio ndiyo kauli ya Mwenyezi Mungu:

وَكَفَى اللَّهُ الْمُؤْمِنِينَ الْقِتَالَ وَكَانَ اللَّهُ قَوِيّاً عَزِيزاً

"Na Mwenyezi Mungu aliwatosheleza Waumini katika vita. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye kushinda." (QS. Al-Ahzab [33]: 25).

Akasema: Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ akamwita Bilal, akasimama akaswali Adhuhuri na akaifanya vizuri kama alivyokuwa akiswali katika wakati wake, kisha akamuamuru akasimama Alasiri na akaifanya vizuri kama alivyokuwa akiswali katika wakati wake, kisha akamuamuru akasimama Magharibi akaswali vivyo hivyo."

Na kwa yaliyopokewa kutoka kwake ﷺ kwamba binti wa kwaya ya Khath'am alipomuuliza akisema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika baba yangu amefikiwa na faradhi ya Hajj akiwa ni mzee asiyeweza kupanda (mnyama), je nikimfanyia Hajj itamnufaisha? Akamwambia:

أَرَأَيْتِ لَوْ كَانَ عَلَى أَبِيكِ دَيْنٌ فَقَضَيْتِهِ أَكَانَ يَنْفَعُهُ ذَلِكَ؟ قَالَتْ: نَعَمْ. قَالَ: فَدَيْنُ اللهِ أَحَقُّ بِالْقَضَاءِ

"Je, unaonaje kama baba yako angekuwa na deni nawe ukalilipa, je, hilo lingemnufaisha? Akasema: Ndio. Akasema: Basi deni la Mwenyezi Mungu lina haki zaidi kulipwa."

Hadith hizi zote ziko wazi kuhusu kulipa swala (qadha), jambo linaloonyesha kuwa kulipa swala ni wajibu na hakuna kafara ya kuacha swala isipokuwa kuilipa, iwe kuiacha huko ni kwa udhuru au bila udhuru kwa sababu hadith ziko wazi. Na isisemwe kwamba hadith hizi zote zimefungika na matukio maalum ambayo ni kulala, kusahau, vita na kutojiweza, na haya yote ni udhuru wa kisheria ambao hakuna dhambi kwa kuacha swala ndani yake katika kuichelewesha baada ya wakati wake, hivyo basi kulipa swala kuwe ni mahususi kwayo na kusiyaingize mengine kinyume na kuacha kwa makusudi kwani hakukuja nass ya kuruhusu kuilipa. Isisemwe hivyo, kwa sababu matukio haya haikuja ndani yake sifa ya kulala, kusahau na vita kama sharti (qayd) ndani yake, bali imekuja kama sifa ya tukio lililotokea bila kufahamika sifa ya kisharti na tukio hili.

Je, huoni katika hadith ya Jabir jinsi Umar bin Al-Khattab alivyoanza kuwatukana makafiri wa Kikuraishi na akasema ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu sikuwa nakaribia kuswali Alasiri mpaka jua likakaribia kuzama, Mtume akamwambia: "Wallahi mimi sijaichukua (sijaiswali)" kisha akasimama akatawadha na kuswali. Iko wapi sifa ya kisharti katika tukio hili inayoonyesha kuwa ni mahususi kwake? Na sema vivyo hivyo katika matukio mengineyo, hakuna katika tamko lolote lile linaloonyesha kuwa limefungika nayo na kwamba haijuzu katika mengineyo, bali kila moja ya hadith hizi zilizotokea katika tukio maalum zimekuja kwa ajili ya kutolea mfano wa uhalisia wala si kwa ajili ya kutolea mfano wa sharti.

Na sifa ya sababu mahususi ya kulipa swala ndani yake pekee haionekani kama inavyobainika kutokana na kusoma hadith hizo. Ama hadith ambazo imekuja ndani yake kitendo kikileta maana ya sifa nacho ni kauli yake: "Mwenye kulala", "au akaisahau" anapolala: "au akaghafilika", "mwenye kusahau", basi zote hizi inazingatiwa sifa ndani yake kuwa ni sharti (qayd) na inazingatiwa ndani yake mafhum al-mukhalafah (maana kinyume) kwa sababu ni sifa, na mafhum al-mukhalafah katika sifa inazingatiwa. Na kwa sababu ikiwa kutajwa kwake hakutazingatiwa kuwa ni sharti, basi kutajwa kwake kwa sifa hii kungekuwa ni upuuzi, na hadith imetakata na hilo. Lakini mafhum al-mukhalafah ya nass hizi inatenguliwa na nass zingine. Na ikija nass inayoonyesha mantuq (tamko la wazi) wake kuwa ni kinyume na mafhum ya nass nyingine, basi mafhum hiyo inatenguliwa, na inachukuliwa mantuq kwa sababu dalili yake juu ya maana ni nguvu kuliko dalili ya mafhum... Na hadith hizi mafhum yake imetenguliwa na hadith zilizokuja kuhusu kulipa swala zilizopitwa katika hali nyinginezo ambazo ni vita.

Na katika hadith ya kulipa Hajj ambayo imekuja ndani yake kauli yake: "Basi deni la Mwenyezi Mungu lina haki zaidi kulipwa" kwa tamko la ujumla linalojumuisha kila deni la Mwenyezi Mungu, na swala ni deni la Mwenyezi Mungu, hivyo inaingia chini ya ujumla wa neno "Dainullah" (deni la Mwenyezi Mungu) kwa sababu ni ism jins mudhaf (jina la jinsia lililoegemezwa) nalo ni miongoni mwa sifa za ujumla kwa uhakika. Na mwenye kuacha swala kwa makusudi amekhatabiwa (ameelekezwa) kuswali kama alivyokhatabiwa kila Muislamu na ikawa wajibu kwake kuitekeleza, hivyo ikawa ni deni juu yake. Na deni haliondoki isipokuwa kwa kulitekeleza, na vivyo hivyo swala haiondoki kwa kupitwa na wakati wake isipokuwa kwa kuilipa, na juu yake kuna dhambi ya kuiacha katika wakati wake.] Mwisho wa nukuu kutoka katika kitabu Ahkam as-Salah.

Natumai katika hili kuna utoshelevu, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi zaidi na Mwenye hikima zaidi.

Ndugu yenu Ata bin Khalil Abu al-Rashtah

23 Ramadhan 1442 H Muwafaka 05/05/2021 M

Link ya jibu kutoka ukurasa wa Amir (Mungu amuhifadhi) kwenye Facebook

Link ya jibu kutoka ukurasa wa Amir (Mungu amuhifadhi) Web

Share Article

Share this article with your network