Jibu la Swali
Alhamdulillah, na swala na salamu zimwendee Mtume wa Allah, jamaa zake, maswahaba wake na waliomfuata, na baada ya hayo:
Kwa wale wote walionitumia maswali wakiuliza kuhusu kuacha nafasi ya mita mbili kati ya mswaliji na aliye pembeni yake katika swala ya Ijumaa na jamaa... Na wanasema kuwa watawala katika baadhi ya nchi za Kiislamu wanafunga misikiti, na wanapoifungua wanawalazimisha waswaliji kuachana nafasi ya mita mbili... Mamlaka zinahalalisha hilo kwa kusema kuwa mgonjwa ana udhuru, na kama anavyoswali akiwa amekaa, basi inapimwa (qiyas) kwake kuachana nafasi na aliye pembeni yake kwa mita mbili, bali hata kama si mgonjwa lakini anahofia ugonjwa basi anaachana nafasi... Na wanauliza, je inaruhusiwa kwa watawala kuwalazimisha waswaliji kutengana kwa namna hiyo iliyotajwa? Au kutengana huku ni bid'ah ambayo watawala wanabeba dhambi yake? Na waulizaji wanahimiza kupata jibu...
Na kwa kujibu maswali yao, nasema na kwa Allah ndio mafanikio:
Tumeshatoa majibu zaidi ya moja kuhusu bid'ah, na kama waulizaji wangeyatafakari, jibu lingewabainikia kuwa kutengana kwa namna iliyotajwa ni bid'ah ambayo watawala wanabeba dhambi yake ikiwa watawalazimisha watu kutengana huku, na ufafanuzi wa hilo ni kama ifuatavyo:
Kwanza: Tulitoa mnamo tarehe 28 Rajab 1434 H, sawa na 07/05/2013 M, ambapo ilisomeka: (... Hakika bid’ah ni kukiuka amri ya Mwenye kuweka Sheria (Ash-Shari') ambayo imekuja na namna ya utendaji (kaifiyyah). Bid’ah kilugha kama ilivyo katika Lisan al-Arab: "Mbunifu (al-mubtadi') ni yule anayekuja na jambo kwa mfano ambao haukuwepo..., na nimevumbua kitu: nimekitengeneza si kwa mfano uliotangulia". Na katika istilahi ni vivyo hivyo, yaani kuwepo kwa "mfano" uliofanywa na Mtume ﷺ kisha Muislamu akaja na kinyume chake. Hii inamaanisha kukiuka namna ya kisheria iliyobainishwa na Sheria kwa ajili ya kutekeleza amri ya kisheria. Na maana hii ndiyo inayolengwa na hadith:
وَمَنْ عَمِلَ عَمَلاً لَيْسَ عَلَيْهِ أَمْرُنَا فَهُوَ رَدٌّ
"Na yeyote atakayefanya kitendo ambacho hakiko katika amri yetu, basi kitendo hicho kitakataliwa." (Imepokelewa na Bukhari na Muslim na tamko ni la Bukhari).
Hivyo basi, yule anayesujudu mara tatu katika swala yake badala ya mbili amekuja na bid'ah, kwa sababu amekiuka kitendo cha Mtume ﷺ. Na yule anayerusha vijiwe vinane badala ya saba katika kurusha vijiwe (jamarat) kule Mina amekuja na bid'ah kwa sababu pia amekiuka kitendo cha Mtume ﷺ. Na yule anayezidisha maneno ya adhana au kuyapunguza amekuja na bid'ah kwa sababu amekiuka adhana aliyoithibitisha Mtume wa Allah ﷺ...
Ama kukiuka amri ya Mwenye kuweka Sheria ambayo haikuja na namna ya utendaji, basi hilo huangukia katika hukumu za kisheria, hapo husemwa kuwa ni haramu, au makruhu... ikiwa ni hotuba ya taklif (taklifu), au husemwa ni batili au fasidi... ikiwa ni hotuba ya kuwekwa (wad'i), na hiyo ni kulingana na ishara (qarina) inayoambatana na amri hiyo...
Kwa mfano: Muslim amepokea kutoka kwa Aisha, Mama wa Waumini (r.a), akielezea swala ya Mtume ﷺ, alisema: Mtume wa Allah ﷺ alikuwa...
وَكَانَ إِذَا رَفَعَ رَأْسَهُ مِنَ الرُّكُوعِ لَمْ يَسْجُدْ، حَتَّى يَسْتَوِيَ قَائِماً، وَكَانَ إِذَا رَفَعَ رَأْسَهُ مِنَ السَّجْدَةِ، لَمْ يَسْجُدْ حَتَّى يَسْتَوِيَ جَالِساً...
"...na alikuwa anapoinua kichwa chake kutoka kwenye rukuu hasujudu mpaka alingane akiwa amesimama wima, na alikuwa anapoinua kichwa chake kutoka kwenye sijda, hasujudu (sijda ya pili) mpaka alingane akiwa amekaa..."
Hapa Mtume ﷺ alibainisha kuwa Muislamu baada ya kuinuka kutoka kwenye rukuu hasujudu mpaka asimame wima, na anapoinuka kutoka kwenye sijda hasujudu sijda nyingine mpaka akae wima. Hii ni namna (kaifiyyah) aliyoibainisha Mtume ﷺ, hivyo anayeikiuka atakuwa amekuja na bid'ah. Ikiwa mswaliji atainuka kutoka kwenye rukuu kisha akasujudu kabla ya kusimama wima, atakuwa amekuja na bid'ah kwa sababu amekiuka namna aliyoibainisha Mtume ﷺ.
Lakini kwa mfano, Muslim amepokea kutoka kwa Ubada bin al-Samit, amesema: Nilimsikia Mtume wa Allah ﷺ:
يَنْهَى عَنْ بَيْعِ الذَّهَبِ بِالذَّهَبِ، وَالْفِضَّةِ بِالْفِضَّةِ، وَالْبُرِّ بِالْبُرِّ، وَالشَّعِيرِ بِالشَّعِيرِ، وَالتَّمْرِ بِالتَّمْرِ، وَالْمِلْحِ بِالْمِلْحِ، إِلَّا سَوَاءً بِسَوَاءٍ، عَيْناً بِعَيْنٍ، فَمَنْ زَادَ، أَوِ ازْدَادَ، فَقَدْ أَرْبَى
"Anakataza kuuza dhahabu kwa dhahabu, fedha kwa fedha, ngano kwa ngano, shairi kwa shairi, tende kwa tende, na chumvi kwa chumvi, isipokuwa ziwe sawa kwa sawa, mkono kwa mkono. Basi atakayezidisha au kuomba nyongeza, atakuwa amefanya riba."
Ikiwa Muislamu atakiuka hadith hii na kuuza dhahabu kwa dhahabu kwa nyongeza, na si uzito kwa uzito, haisemwi kuwa amekuja na bid'ah, bali inasemwa kuwa amefanya haramu, yaani riba.
Na hitimisho ni kwamba: kukiuka namna (kaifiyyah) aliyoibainisha Mtume wa Allah ﷺ ni bid'ah, na kukiuka amri ya jumla ya Mtume ﷺ bila ya kubainishwa namna ya utendaji huangukia katika hukumu za kisheria: haramu, makruhu... batili na fasidi... na hiyo ni kulingana na dalili) mwisho... Na tumeshatoa ufafanuzi zaidi kuhusu bid'ah mnamo tarehe 08 Dhul-Hijjah 1436 H sawa na 22/09/2015 M, na pia tulitoa majibu mengine kabla na baada ya hapo, ambayo yanatosheleza na kukidhi mahitaji kwa idhini ya Allah.
Pili: Na kwa hivyo, nchi katika ardhi za Waislamu zikiamua kuwalazimisha waswaliji kuachana nafasi mita moja au mbili, iwe katika swala ya Ijumaa au jamaa kwa kuhofia maambukizi, hasa bila ya kuwepo kwa dalili za ugonjwa, basi zinafanya dhambi kubwa kwani kutengana huku ni bid’ah. Hii ni kwa sababu ni ukiukaji wa wazi wa namna ya safu na kubanana kwake kulikobainishwa na Mtume wa Allah ﷺ kwa dalili za kisheria, miongoni mwazo ni:
- Al-Bukhari amepokea katika Sahih yake kutoka kwa Abi Sulayman Malik bin al-Huwayrith amesema: Tulimwendea Mtume ﷺ nasi tukiwa vijana wenye umri unaokaribiana, tukakaa kwake masiku ishirini... na alikuwa mpole na mwenye rehema...
فَقَالَ ارْجِعُوا إِلَى أَهْلِيكُمْ فَعَلِّمُوهُمْ وَمُرُوهُمْ وَصَلُّوا كَمَا رَأَيْتُمُونِي أُصَلِّي وَإِذَا حَضَرَتِ الصَّلَاةُ فَلْيُؤَذِّنْ لَكُمْ أَحَدُكُمْ ثُمَّ لِيَؤُمَّكُمْ أَكْبَرُكُمْ
"Akasema: Rejeeni kwa familia zenu mkawafundishe na mkawaamrishe, na swalini kama mlivyoniona nikiswali, na wakati wa swala unapofika, basi mmoja wenu awakidhisheni adhana kisha awaongoze katika swala mkubwa wenu."
- Na al-Bukhari amepokea katika Sahih yake kutoka kwa Anas bin Malik amesema: Swala ilikimiwa, basi Mtume wa Allah ﷺ akatugeukia kwa uso wake na akasema:
أَقِيمُوا صُفُوفَكُمْ، وَتَرَاصُّوا، فَإِنِّي أَرَاكُمْ مِنْ وَرَاءِ ظَهْرِي
"Simamisheni safu zenu, na mshikane (mubananane), kwani mimi nawaona kutokea nyuma ya mgongo wangu."
- Na Muslim amepokea katika Sahih yake kutoka kwa al-Nu'man bin Bashir (r.a) amesema: Mtume wa Allah ﷺ alikuwa akizinyoosha safu zetu mpaka ikawa kama ananyoosha mishale kwayo, mpaka alipoona kuwa tumeshafahamu kutoka kwake. Kisha akatoka siku moja akasimama, mpaka akakaribia kupiga takbira, akaona mtu kifua chake kimejitokeza nje ya safu, akasema:
عِبَادَ اللهِ لَتُسَوُّنَّ صُفُوفَكُمْ، أَوْ لَيُخَالِفَنَّ اللهُ بَيْنَ وُجُوهِكُمْ
"Enyi waja wa Allah, lazima mnyooshe safu zenu, au Allah atatofautisha nyuso zenu (atatia mifarakano baina yenu)."
- Na Muslim pia amepokea katika Sahih yake kutoka kwa Jabir bin Samurah amesema: Mtume wa Allah ﷺ amesema:
أَلَا تَصُفُّونَ كَمَا تَصُفُّ الْمَلَائِكَةُ عِنْدَ رَبِّهَا؟ فَقُلْنَا يَا رَسُولَ اللهِ، وَكَيْفَ تَصُفُّ الْمَلَائِكَةُ عِنْدَ رَبِّهَا؟ قَالَ: يُتِمُّونَ الصُّفُوفَ الْأُوَلَ وَيَتَرَاصُّونَ فِي الصَّفِّ
"Kwani hamupangi safu kama Malaika wanavyopanga safu mbele ya Mola wao? Tukasema: Ewe Mtume wa Allah, na vipi Malaika wanapanga safu mbele ya Mola wao? Akasema: Wanatimiza safu za kwanza na wanashikana (wanabanana) katika safu."
- Na al-Hakim amepokea, na akasema ni hadith sahihi kwa sharti ya Muslim, kutoka kwa Abdullah bin Amr, kwamba Mtume wa Allah ﷺ amesema:
مَنْ وَصَلَ صَفّاً وَصَلَهُ اللَّهُ، وَمَنْ قَطَعَ صَفّاً قَطَعَهُ اللَّهُ
"Yeyote mwenye kuunga safu Allah humuunga, na yeyote mwenye kukata safu Allah humkata."
- Na Ahmad amepokea kutoka kwa Abdullah bin Umar kwamba Mtume wa Allah ﷺ amesema:
أَقِيمُوا الصُّفُوفَ فَإِنَّمَا تَصُفُّونَ بِصُفُوفِ الْمَلَائِكَةِ وَحَاذُوا بَيْنَ الْمَنَاكِبِ وَسُدُّوا الْخَلَلَ وَلِينُوا فِي أَيْدِي إِخْوَانِكُمْ وَلَا تَذَرُوا فُرُجَاتٍ لِلشَّيْطَانِ وَمَنْ وَصَلَ صَفّاً وَصَلَهُ اللَّهُ تَبَارَكَ وَتَعَالَى وَمَنْ قَطَعَ صَفّاً قَطَعَهُ اللَّهُ
"Simamisheni safu kwani nyinyi mnapanga safu kwa safu za Malaika, na sawazisheni baina ya mabega, na fungeni nafasi, na muwe laini mikononi mwa ndugu zenu, wala msiache nafasi kwa ajili ya shetani. Na yeyote mwenye kuunga safu Allah aliyebarikiwa na kutukuka humuunga, na yeyote mwenye kukata safu Allah humkata."
Huu ni ufafanuzi kamili kutoka kwa Mtume wa Allah ﷺ kuhusu namna ya utekelezaji wa swala ya jamaa, na Maswahaba (r.a) walikuwa wakishikamana na hilo. Malik amepokea katika al-Muwatta na al-Bayhaqi katika al-Sunan al-Kubra kwamba Umar bin al-Khattab (r.a) alikuwa "akiamrisha kunyooshwa kwa safu, na wanapomjia na kumwambia kuwa zimeshalingana, hapo hupiga takbira".
Tatu: Na haisemwi kuwa ugonjwa wa kuambukiza ni udhuru unaoruhusu kutengana katika swala, haisemwi hivyo, kwa sababu ugonjwa wa kuambukiza ni udhuru wa kutokwenda msikitini na si udhuru wa kwenda na kuachana nafasi na mswaliji aliye pembeni yake kwa mita moja au mbili!! Kwani magonjwa ya kuambukiza yalikuwepo katika zama za Mtume wa Allah ﷺ (Tauni) na haikupokelewa kutoka kwa Mtume ﷺ kwamba aliyeambukizwa tauni huenda kuswali na kuachana nafasi na mwenzake mita mbili, bali yeye ana udhuru hivyo huswali nyumbani kwake... Kwani eneo ambalo ugonjwa umeenea, matibabu yake huimarishwa bure kwa juhudi na bidii chini ya usimamizi wa dola, na wagonjwa hawachanganyiki na wazima... Anasema swala na salamu za Allah zimwendee katika kile alichopokea Muslim katika Sahih yake kutoka kwa Usama bin Zaid amesema: Mtume wa Allah ﷺ amesema:
الطَّاعُونُ آيَةُ الرِّجْزِ ابْتَلَى اللَّهُ عَزَّ وَجَلَّ بِهِ نَاساً مِنْ عِبَادِهِ، فَإِذَا سَمِعْتُمْ بِهِ فَلَا تَدْخُلُوا عَلَيْهِ وَإِذَا وَقَعَ بِأَرْضٍ وَأَنْتُمْ بِهَا فَلَا تَفِرُّوا مِنْهُ
"Tauni ni alama ya adhabu ambayo Allah (a.z) amewatahini kwayo watu miongoni mwa waja wake. Basi mkisikia ipo mahali msiingie huko, na ikitokea katika ardhi mliyopo msiikimbie."
Yaani, mgonjwa wa ugonjwa wa kuambukiza hachanganyiki na wazima na anawekewa matibabu ya kutosha na kamili kwa idhini ya Allah. Ama mzima, huenda msikitini kuswali Ijumaa na jamaa kama kawaida bila ya kutengana.
Nne: Na vivyo hivyo, haisemwi kuwa kutengana katika swala wakati wa janga kunapimwa (qiyas) kwa ruhusa ya kuswali ukiwa umekaa wakati wa ugonjwa. Huu si qiyas ya kisheria, kwa sababu mgonjwa kuswali amekaa ni ruhusa kutoka kwa Allah (s.w.t), yaani kwa sababu ya udhuru ambao ni ugonjwa. Na udhuru ni sababu (asbab) na si sababu za kisheria zinazoweza kupimwa ('illat). Sheria haikuipa sababu (hakuifanyia ta'lil), bali imefanya kila udhuru miongoni mwao kuwa udhuru wa hukumu uliokuja kwa ajili yake na si kwa mwingine. Hivyo inachukuliwa kuwa ni udhuru maalum kwa ajili ya hukumu uliokuja kwa ajili yake, na si udhuru wa jumla kwa kila hukumu; hivyo haieleweki upande wa 'illat (sababu ya kisheria); na kwa sababu hiyo haipimwi (haifanyiwi qiyas) kwayo. Sababu ni maalum kwa kile kilichokuwa sababu ya kuwepo kwake, na haivuki kwenda kwa kingine, hivyo haipimwi kwayo. Hii ni tofauti na 'illah, kwani yenyewe si maalum kwa hukumu iliyowekwa kwa ajili yake, bali huivuka na kwenda kwa nyingine, na hupimwa kwayo... Na kutokea hapa inabainika kuwa yale yaliyokuja katika ibada, kuwa ni sababu na si 'illat, hufanya ibada ziwe ni tawqifiyyah (zinazofuata maandiko pekee), hazifanyiwi ta'lil (kutafuta sababu ya kiakili) wala hazipimwi (hazifanyiwi qiyas); kwa sababu hiyo sababu ni maalum kwa kile kilichokuwa sababu yake.
Tano: Kisha ruhusa (rukhsah) ni hukumu miongoni mwa hukumu za kuwekwa (wad'i), nayo ni hotuba ya Mwenye kuweka Sheria inayofungamana na vitendo vya waja kwa kuwekwa. Na maadamu yenyewe ni hotuba ya Mwenye kuweka Sheria, basi lazima kuwe na dalili ya kisheria inayoashiria hilo. Kwa mfano, kuhusiana na swala ya mgonjwa akiwa amekaa, al-Bukhari amepokea katika Sahih yake kutoka kwa Imran bin Husain (r.a) amesema: Nilikuwa na ugonjwa wa bawasiri, nikamuuliza Mtume ﷺ kuhusu swala, akasema:
صَلِّ قَائِماً فَإِنْ لَمْ تَسْتَطِعْ فَقَاعِداً، فَإِنْ لَمْ تَسْتَطِعْ فَعَلَى جَنْبٍ
"Swali ukiwa umesimama, ikiwa huwezi basi ukiwa umekaa, na ikiwa huwezi basi kwa ubavu."
Basi hii ni ruhusa, yaani udhuru uliokuja na dalili ya kisheria. Na kila jambo lililokuja na dalili ya kisheria kuwa ni udhuru wa hukumu fulani huchukuliwa kuwa ni udhuru, na ambalo halikuja na dalili halina thamani, na halichukuliwi kuwa ni udhuru wa kisheria kabisa... Na kwa kuwa hakuna dalili inayoonyesha kuwa mgonjwa anaweza kutengana katika swala yake na aliye pembeni yake kwa mita moja au mbili, basi kauli hii haina thamani kisheria, na si sahihi... Itakuwaje ikiwa si mgonjwa bali ni kwa sababu tu anatarajia kupata ugonjwa?!
Sita: Na hitimisho kutokana na yaliyotangulia ni kama ifuatavyo:
1- Hakika kubadilisha namna (kaifiyyah) aliyoibainisha Mtume ﷺ kwa ajili ya swala huhesabiwa kuwa ni bid'ah. Bali hukumu ya kisheria katika hali hii ni kwamba mwenye mwili mzima huenda kuswali kama kawaida katika safu zilizoshikana, na bila ya nafasi, na mgonjwa wa ugonjwa wa kuambukiza haendi ili asiwaambukize wengine.
2- Ikiwa dola itafunga misikiti, na kisha kuwazuia watu wazima wasiende misikitini kwa ajili ya Ijumaa na jamaa, basi itakuwa inafanya dhambi kubwa kwa kuzuia swala ya Ijumaa na jamaa. Misikiti lazima iendelee kuwa wazi kwa ajili ya swala kama alivyobainisha Mtume ﷺ.
3- Vivyo hivyo, ikiwa dola itawazuia waswaliji kutekeleza swala kulingana na namna aliyoibainisha Mtume wa Allah ﷺ, bali ikawalazimisha kutengana mita moja au mbili kati ya mswaliji na aliye pembeni yake kwa kuhofia maambukizi, hasa bila ya kuwepo kwa dalili za ugonjwa, basi itakuwa inapata dhambi kubwa kwa hilo.
Hii ndiyo hukumu ya kisheria ninayoiona kuwa na nguvu katika suala hili, na Allah ndiye Mjuzi zaidi na Mwenye hekima zaidi... Na nina muomba Yeye aliyetakasika awaongoze Waislamu kwenye jambo lao lililo bora, na wamuabudu Yeye aliyetakasika kama alivyoamrisha, na washikamane na nyayo za Mtume wake ﷺ, na wasimamishe Sheria tukufu bila ya kugeuka upande kwa kusimamisha Ukhalifa wa Uongofu (Khilafah Rashidah)... Kwani katika hilo kuna kheri na ushindi kwa idhini ya Allah ambaye hakuna kinachomshinda mbinguni wala ardhini naye ni Mwenye Nguvu, Mwenye Hekima.
Wassalamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh
17 Shawwal 1441 H
08/06/2020 M
Ndugu yenu