Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Kwa nini Mtume (saw) hakutaka Nusra kutoka kwa Maquraishi?

December 30, 2021
2747

Mfululizo wa majibu ya mwanachuoni mtukufu Ata' bin Khalil Abu Al-Rashtah, Ameer wa Hizb ut-Tahrir, kwa maswali ya wafuasi wa ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi"

Jibu la Swali

Kwa Raed Al-Harsh Abu Muadh

Swali:

Kwa ajili ya ufafanuzi, swali ni: Je, kutokuomba kwa Mtume ﷺ Nusra kutoka kwa Maquraishi kulitokana na wao kutofaa kwa jambo hilo asilia, au ni kwa sababu tu walikataa Uislamu, nikimaanisha viongozi wa Makka? Ikiwa ni hivyo, kwani Mtume ﷺ hakuomba Nusra kutoka kwa watu wa Yathrib (Madina) ilhali viongozi na wakuu wa Yathrib walikuwa bado hawajasilimu wala kutoa Nusra? Naomba ufafanuzi? Baraka za Allah ziwe nawe na akupe kila la kheri.

Jibu:

Kuhusu kutoomba Nusra kutoka kwa Maquraishi mjini Makka, suala liko kama ifuatavyo:

[Mtume ﷺ alikuwa akiwalingania wenye nguvu (Ahl al-Quwwah) wenye uwezo wa kubadilisha hali ya kijahili kuingia katika Uislamu; aliwalingania kwanza kwenye Uislamu... Iwapo wangesilimu na kuitikia, basi aliomba Nusra yao baada ya hapo... Na viongozi wa Maquraishi mjini Makka wenye uwezo wa mabadiliko hawakuukubali Uislamu, na ndiyo maana Mtume ﷺ hakuomba Nusra yao. Badala yake, Mtume ﷺ alitosheka na kutoa mwito wa Uislamu Makka, na kwa sababu ya kutokuitikia kwa wenye nguvu miongoni mwao kwenye Uislamu, hakuomba Nusra kutoka kwao... Nitakutajia hapa chini kutoka katika vitabu vya Sira jinsi jambo hilo lilivyokuwa likifanyika:

Kwanza: Kutoka katika Sira ya Ibn Hisham:

1- [(... na watu wake (Maquraishi) walikuwa katika hali mbaya zaidi ya kumfanyia upinzani na kuachana na dini yake, isipokuwa wachache waliofanywa madhaifu miongoni mwa walioamini. Mtume wa Allah ﷺ alikuwa akijitokeza katika misimu (ya Hijja) wakati makabila ya Kiarabu yalipokuwa yakikusanyika, akiwalingania kwa Allah na kuwaambia kuwa yeye ni Mtume aliyetumwa, na akawaomba wamsadiki na wamlinde mpaka Allah abainishe (kwao) kile alichomtuma nacho...

Ibn Ishaq amesema: Na amenihadithia Husayn bin Abdullah bin Ubaydullah bin Abbas, amesema: Nilimsikia Rabia bin Abbad akimhadithia baba yangu, akisema: Nilikuwa kijana mdogo nikiwa na baba yangu kule Mina, na Mtume wa Allah ﷺ alikuwa akisimama kwenye makazi ya makabila ya Kiarabu akisema: Enyi wana wa fulani, mimi ni Mtume wa Allah kwenu, anawaamuru mumuabudu Allah na msimshirikishe na chochote, na muvue mnavyoviabudu badala yake miongoni mwa masanamu haya, na mniame mimi, mnisadiki, na mnilinde, mpaka nibainishe kutoka kwa Allah kile alichonituma nacho...)

2- Ibn Ishaq amesema: Na amenihadithia Az-Zuhri kwamba (Mtume) aliwaendea Bani Amir bin Sa'sa'ah akawaalika kwa Allah (swt) na akajitokeza kwao. Mtu mmoja miongoni mwao – anayeitwa Bayhara bin Firas – akasema (Ibn Hisham amesema: Ni Firas bin Abdullah bin Salama (Al-Khair) bin Qushayr bin Ka'b bin Rabia bin Amir bin Sa'sa'ah): "Wallahi, kama ningemchukua kijana huyu kutoka kwa Maquraishi, ningewala Waarabu (ningewatawala) kupitia kweye." Kisha akasema: "Je, unaonaje tukikupa baia (kiapo cha utii) juu ya jambo lako hili, kisha Allah akakuwezesha kuwashinda wanaokupinga, je, uongozi utakuwa wetu baada yako?" (Mtume) akasema: "Uongozi ni wa Allah, anauweka pale anapotaka." Yule mtu akasema: "Je, tuiweke shingo yetu hatarini kwa Waarabu kwa ajili yako, kisha Allah akikupa ushindi uongozi uwe wa wengine? Hatuna haja na jambo lako..."]

3- Ibn Ishaq amesema: Mtume wa Allah ﷺ aliendelea na jambo lake hilo kila watu walipokusanyika katika msimu (wa Hijja), akiyaendea makabila na kuwalingania kwa Allah na kwenye Uislamu, akijitokeza kwao na kuwafikishia uongofu na rehema alizokuja nazo kutoka kwa Allah. Hakuwa akisikia kuhusu mgeni yeyote mwenye jina na heshima anayewasili Makka miongoni mwa Waarabu, ila alimwendea na kumlingania kwa Allah na kumpa kile alichonacho).

Kama unavyoona, Mtume ﷺ alikuwa akimlingania mwenye nguvu kwenye Uislamu kwanza, na akijitikia, basi aliomba Nusra yake.]

Pili: Kutoka katika Sira ya Ibn Kathir:

1- [... Akasema: Kisha tuliishia kwenye kikao kilichokuwa na utulivu na heshima, na kikiwa na wazee wenye hadhi na haiba. Abu Bakr akatangulia na kutoa salamu. Ali akasema: Na Abu Bakr alikuwa mstari wa mbele katika kila kheri. Abu Bakr akawauliza: "Watu hawa ni akina nani?" Wakasema: "Ni wa Bani Shayban bin Tha'labah." Abu Bakr akamgeukia Mtume wa Allah ﷺ na kusema: "Kwa baba yangu na mama yangu, hakuna baada ya hawa wenye heshima zaidi katika watu wao." Katika riwaya nyingine: "Hawa ni viongozi wa watu wao, na hawa ni watukufu wa watu." Na katika watu hao walikuwepo Mafruq bin Amr, Hani bin Qabisah, Al-Muthanna bin Harithah, na An-Nu'man bin Sharik... Na aliyekuwa karibu zaidi na Abu Bakr alikuwa Mafruq bin Amr, na Mafruq bin Amr alikuwa amewazidi kwa ufasaha na ulimi, na alikuwa na nywele mbili zilizosukwa zikiangukia kifuani mwake, naye ndiye aliyekuwa amekaa karibu zaidi na Abu Bakr. Abu Bakr akamuuliza: "Idadi yenu ikoje?" Akamjibu: "Sisi tunazidi elfu moja, na elfu moja haishindwi kwa uchache." Akamuuliza: "Ulinzi/Nguvu (al-man'ah) ikoje kwenu?" Akasema: "Juu yetu ni jitihada na kila watu wana bidii yao." Abu Bakr akauliza: "Vipi vita kati yenu na adui yenu?" Mafruq akasema: "Sisi ni wakali zaidi tunapokutana na adui tunapokuwa na hasira, na sisi hupendelea farasi bora kuliko watoto, na silaha kuliko maziwa, na ushindi unatoka kwa Allah; anatupa ushindi mara moja na wakati mwingine adui hushinda..."

"Labda wewe ni ndugu wa Maquraishi?" Abu Bakr akasema: "Ikiwa imewafikia habari kuwa yeye ni Mtume wa Allah, basi huyu hapa." Mafruq akasema: "Imetufikia habari kuwa anataja hilo." Kisha akamgeukia Mtume wa Allah ﷺ akasema: "Unahimiza nini, ewe ndugu wa Maquraishi?" Mtume wa Allah ﷺ akasogea mbele na kukaa, na Abu Bakr akawa anamkinga kivuli kwa vazi lake. (Mtume) ﷺ akasema: "Nawaita kwenye ushahidi kuwa hapana mungu anayestahiki kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah pekee, hana mshirika, na kwamba mimi ni Mtume wa Allah, na kwamba mnilipe hifadhi na mninusuru mpaka nifikishe kutoka kwa Allah kile alichoniamuru nacho, kwani Maquraishi wameungana kupinga amri ya Allah, wamemkadhibisha Mtume wake, na wamejiridhisha na batili badala ya haki, na Allah ndiye Mkwasi, Mhimidiwa." Mafruq akamuuliza: "Na unahimiza nini tena, ewe ndugu wa Maquraishi?" Mtume wa Allah ﷺ akasoma:

قُلْ تَعَالَوْا أَتْلُ مَا حَرَّمَ رَبُّكُمْ عَلَيْكُمْ أَلَّا تُشْرِكُوا بِهِ شَيْئًا وَبِالْوَالِدَيْنِ إِحْسَانًا

"Sema: Njooni nisome aliyo kuharamishieni Mola wenu Mlezi. Nayo ni kuwa: msimshirikishe Yeye na chochote. Na wazazi wenu wafanyieni wema..." mpaka mwisho wa aya:

ذَلِكُمْ وَصَّاكُمْ بِهِ لَعَلَّكُمْ تَتَّقُونَ

"...Hayo amekuonyeni ili mpate kuchunga." (Al-An'am [6]: 151-153)

Mafruq akasema: "Na unahimiza nini tena, ewe ndugu wa Maquraishi? Wallahi haya si maneno ya watu wa ardhini, lau yangekuwa maneno yao tungeyafahamu." Mtume wa Allah ﷺ akasoma:

إِنَّ اللَّهَ يَأْمُرُ بِالْعَدْلِ وَالْإِحْسَانِ وَإِيتَاءِ ذِي الْقُرْبَى وَيَنْهَى عَنِ الْفَحْشَاءِ وَالْمُنْكَرِ وَالْبَغْيِ يَعِظُكُمْ لَعَلَّكُمْ تَذَكَّرُونَ

"Hakika Mwenyezi Mungu anaamrisha uadilifu, na hisani, na kuwapa jamaa; na anakataza uchafu, na uovu, na dhulma. Anawaonyeni ili mpate kukumbuka." (An-Nahl [16]: 90)

Mafruq akamwambia: "Umehimiza, wallahi, ewe ndugu wa Maquraishi, tabia tukufu na matendo mema, na hakika wamepotea watu waliokukadhibisha na walioungana dhidi yako."

Na kama alivyopenda kumshirikisha katika mazungumzo Hani bin Qabisah, akasema: "Huyu ni Hani bin Qabisah, mzee wetu na kiongozi wa dini yetu." Hani akamwambia: "Nimesikia maneno yako ewe ndugu wa Maquraishi na nimesadiki kauli yako, lakini mimi naona kuwa kuacha dini yetu na kukufuata wewe katika dini yako kwa sababu ya kikao kimoja tu ulichoketi nasi, ambacho hakina mwanzo wala mwisho bila kufikiria jambo lako na kuangalia mwisho wa unacholingania, ni kuteleza katika maoni, wepesi wa akili, na uchache wa kuangalia mwisho wa mambo. Hakika kuteleza huja na haraka, na nyuma yetu kuna watu ambao tunachukia kuwafungia mkataba bila ridhaa yao. Lakini rudi na tutarudi, na ufikirie na tutafikiria." Na kama alivyopenda kumshirikisha katika mazungumzo Al-Muthanna bin Harithah, akasema: "Huyu ni Al-Muthanna mzee wetu na kiongozi wetu wa vita." Al-Muthanna akasema: "Nimesikia maneno yako na nimependezwa na kauli yako ewe ndugu wa Maquraishi, na yamenivutia uliyoyazungumza, lakini jibu ni lile lile jibu la Hani bin Qabisah; kuacha dini yetu na kukufuata kwa kikao kimoja ulichokaa nasi ni jambo gumu. Sisi tumepiga kambi kati ya Sarayayn (maeneo mawili ya maji), moja ni Yamama na lingine ni Samawa**." Mtume wa Allah ﷺ akamuuliza: "Ni nini haya Sarayayn?" Akamjibu: "Ama moja ni kingo za bara na ardhi ya Waarabu, na lingine ni ardhi ya Waajemi (Persia) na mito ya Kisra. Sisi tumepiga kambi kwa makubaliano aliyotupa Kisra kwamba tusizushe jambo jipya, wala tusimpe hifadhi mzushi, na labda jambo hili unayotulingania ni katika yale wanayoyachukia wafalme. Ama kile kinachopakana na nchi za Kiarabu, basi kosa la mwenye nalo husamehewa na udhuru wake hukubaliwa, lakini kile kinachopakana na nchi za Kiajemi, kosa la mwenye nalo halisamehewi na udhuru wake haukubaliwi. Ikiwa unataka tukunusuru na kukulinda dhidi ya yale yanayopakana na Waarabu, tutafanya hivyo."

Mtume wa Allah ﷺ akasema:

مَا أَسَأْتُمُ الرَّدَّ إِذْ أَفْصَحْتُمْ بِالصِّدْقِ، إِنَّهُ لَا يَقُومُ بِدِينِ اللَّهِ إِلَّا مَنْ حَاطَهُ مِنْ جَمِيعِ جَوَانِبِهِ

"Hamtukushindwa kutoa jibu mlipobainisha ukweli, hakika haisimami dini ya Allah isipokuwa kwa yule anayeilinda kutoka pande zake zote."...]

** Al-Lisan 19/192: "Na hakika tulipiga kambi kwenye Sarayayn Yamama na Samawa, nazo ni aina mbili za Sira. Nalo ni kila maji yaliyokusanyika."

2- Amesema: [Kisha tukaelekea kwenye kikao cha Aus na Khazraj, na hatukuondoka mpaka walipompa baia Mtume ﷺ.

Ali akasema: Walikuwa ni watu wa kweli na wenye subira, na Mtume wa Allah ﷺ alifurahishwa na ujuzi wa Abu Bakr (ra) kuhusu nasaba zao.

Akasema: Mtume wa Allah ﷺ hakukaa muda mrefu mpaka alipowatokea maswahaba wake na kuwaambia:

احْمَدُوا اللَّهَ كَثِيراً، فَقَدْ ظَفَرَتِ الْيَوْمَ أَبْنَاءُ رَبِيعَةَ بِأَهْلِ فَارِسَ، قَتَلُوا مُلُوكَهُمْ وَاسْتَبَاحُوا عَسْكَرَهُمْ وَبِي نُصِرُوا

"Mhimidini Allah kwa wingi, kwani leo wana wa Rabi'ah wamewashinda watu wa Uajemi, wamewaua wafalme wao na kutwaa kambi yao, na kupitia mimi wamenusuriwa."

Akasema: Na tukio hilo lilikuwa Qaraqir kando ya Dhi Qar... Hii ni hadithi ngeni sana (gharib jiddan), tumeiandika kwa sababu ndani yake mna alama za unabii, tabia njema, sifa tukufu na ufasaha wa Waarabu. Na imepokelewa kupitia njia nyingine, na ndani yake kuna maelezo kuwa walipopigana wao na Waajemi na kukutana nao Qaraqir, mahali karibu na Frati, walifanya nembo yao kuwa jina la Muhammad ﷺ na wakashinda Waajemi kwa hilo, na baada ya hapo wakaingia katika Uislamu.

Imamu Muhammad bin Omar Al-Waqidi ametafiti kwa kina na kuelezea makabila moja baada ya jingine, akitaja kujitokeza kwa Mtume (saw) kwa Bani Amir, Ghassan, Bani Fazara, Bani Murra, Bani Hanifa, Bani Sulaym, Bani Abs, Bani Nadhr bin Hawazin, Bani Tha'labah bin Ukaba, Kinda, Kalb, Bani Al-Harith bin Ka'b, Bani Udhra, Qays bin Al-Hatim na wengineo. Na habari zao zimeandikwa kwa kirefu, na tumetaja sehemu nzuri ya hayo na sifa zote njema ni za Allah. Na Imamu Ahmad amesema: Aswad bin Amir ametuhadithia, Israel ametuhadithia, kutoka kwa Othman, yaani Ibn Al-Mughirah, kutoka kwa Salim bin Abi Al-Ja'd, kutoka kwa Jabir bin Abdullah amesema: Mtume ﷺ alikuwa akijitokeza kwa watu katika kituo (cha Arafa) akisema: "Je, yuko mtu atakayenibeba (atakayenipeleka) kwa watu wake, kwani Maquraishi wamenizuia kufikisha maneno ya Mola wangu Aliyeshinda na Mtukufu?"].

Ni wazi kutokana na yote haya kwamba Mtume ﷺ alikuwa haombi Nusra ya yeyote isipokuwa baada ya kumlingania katika Uislamu; ikiwa hangeitikia Uislamu, hakuomba Nusra yake, na viongozi wa Maquraishi hawakuitikia Uislamu ndiyo maana Mtume ﷺ hakuomba Nusra yao.

Ndugu yenu Ata' bin Khalil Abu Al-Rashtah

26 Jumada al-Ula 1443 H Inalingana na 30/12/2021 M

Link ya jibu kutoka kwa ukurasa wa Ameer (Allah amhifadhi) kwenye Facebook

Link ya jibu kutoka kwa ukurasa wa Ameer (Allah amhifadhi) kwenye Web

Share Article

Share this article with your network