Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

JAWABU LA SWALI: KINACHOCHUKULIWA KUWA HOJA KUTOKA KWENYE QUR'AN NI KILE KILICHONUKULIWA KWETU KWA NJIA YA MUTAWATIR

July 22, 2022
3153

Mfululizo wa majibu ya mwanachuoni mtukufu Ata bin Khalil Abu Al-Rashtah, Amiri wa Hizb ut Tahrir, kwa maswali ya wafuasi wa ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi".

Kwa: Tariq Mahmoud

Swali:

Assalamu Alaykum Wa Rahmatullahi Wa Barakatuh.

Sheikh wangu mpendwa, Mwenyezi Mungu akuzidishie afya na nguvu, na akuidhishe kwa Waislamu wenye nguvu na wacha Mungu, na ayafanye ushindi yatokee mikononi mwako, Amin ya Rabbil Alamin.

Sheikh wangu mpendwa, nilipokuwa nikisoma vitabu vya wanachuoni, nilikutana na nukuu zilizopokewa na baadhi ya Maswahaba kama Abdullah bin Mas'ud au Mama wa Waumini Aisha (ra) kwa msingi kwamba nukuu hizi ni aya za Qur'an, lakini hazikuchukuliwa na wala hazikuhesabiwa kuwa ni sehemu ya Qur'an kwa sababu zilikuja kupitia khabar Ahad (ripoti za mtu mmoja mmoja), na inajulikana kuwa Qur'an haithibiti kwa khabar Ahad kwani ni zanni (dhana) katika uthabiti wake.

Lakini tunashughulika vipi na nukuu hizi kwa kuwa ni sahihi na zimepokewa kutoka kwa watu waaminifu, waadilifu na madhubuti? Kwani ingawa hazikuthibiti kwa mutawatir, zime thibiti kwa wingi wa dhana (ghalabat ad-dhann). Je, nukuu hizi zinahesabiwa na mafaqihi na mujtahidina katika kuzitumia kama nukuu za kisheria ambazo hukumu za kisheria zinaweza kutolewa kutoka kwazo, au hazizingatiwi kana kwamba hazikuwepo?

Barakallahu fika na samahani kwa kurefusha.

Jibu:

Wa Alaykum Assalam Wa Rahmatullahi Wa Barakatuh,

Barakallahu fika kwa dua yako njema kwetu, na sisi tunakuombea kheri.

Ama kuhusu swali lako juu ya Qur'an Tukufu, kabla ya kujibu, ninakunukulia yafuatayo kutoka katika vitabu vyetu:

1- Imekuja katika kitabu cha Ash-Shakhsiyyah al-Islamiyyah Juzuu ya Tatu, mlango wa "Kile kinachochukuliwa kuwa hoja kutoka kwenye Qur'an" yafuatayo:

[Kile kilichonukuliwa kwetu kutoka kwenye Qur'an kwa mapokezi ya mutawatir, na tukajua kuwa ni kutoka kwenye Qur'an, hicho pekee ndicho kinachokuwa hoja. Ama kile kilichonukuliwa kwetu kwa njia ya Ahad, kama msahafu wa Ibn Mas'ud na wengineo, hicho hakitakuwa hoja; hii ni kwa sababu Mtume ﷺ alikuwa na jukumu la kufikisha kile alichoteremshiwa katika Qur'an kwa kundi ambalo kauli yao inasimamisha hoja ya kukatikiwa (qati'i). Na wale ambao kauli yao inasimamisha hoja ya kukatikiwa haiwezi kudhaniwa kuwa wataafikiana kutokunukuu kile walichokisikia. Hivyo, ikipatikana sehemu ya Qur'an ambayo haikunukuliwa na wale ambao kauli yao inasimamisha hoja, bali ikawa imenukuliwa na watu mmoja mmoja (Ahad), basi hiyo haizingatiwi; kwa sababu imekuja kinyume na kile alichopewa jukumu Mtume ﷺ katika upweke wa mtu mmoja kuinukuu, na kinyume na vile ilivyokuwa uwasilishaji wa Qur'an kutoka kwa Mtume kwenda kwa idadi ya Waislamu walioihifadhi, na wakawa ni miongoni mwa wale ambao kauli yao inasimamisha hoja, sambamba na amri yake ya kuiandika. Kwa hivyo, haiwezekani katika hali hii mtu mmoja au idadi ya watu ambao kauli yao haisimamishi hoja ya kukatikiwa wakawa peke yao katika kunukuu kitu chochote cha Qur'an; na kwa sababu hiyo, kile kilichonukuliwa kutoka kwenye Qur'an kwa njia ya Ahad hakitakuwa hoja kabisa.]

  • Na imekuja katika chanzo hicho hicho yafuatayo:

[...Ama kutofautiana kwa masahafu, yale yaliyomo ambayo ni ya Ahad, hayo si katika Qur'an na wala si hoja. Na yale yaliyokuwa mutawatir, hayo ni sehemu yake na ni hoja. Kwa hivyo suala halihusiani na msahafu wenyewe, bali linahusiana na aya ambazo msahafu huo unazibeba. Ikiwa aya imenukuliwa kutoka kwa Mtume ﷺ kwa mapokezi ya mutawatir, yaani idadi iliyofikia kiwango cha tawatur iliipokea kutoka kwa Mtume ﷺ, yaani wale ambao kauli yao inasimamisha hoja ya kukatikiwa, basi hiyo inazingatiwa kuwa ni Qur'an na inakuwa hoja. Na kile ambacho si hivyo hakizingatiwi kuwa ni Qur'an; na kwa sababu hiyo, msahafu wa Othman wote ni Qur'an; kwa sababu aya zote zilizomo zilinukuliwa kwa mapokezi ya mutawatir, zilinukuliwa na wale ambao kauli yao inasimamisha hoja ya kukatikiwa. Lakini msahafu wa Ibn Mas'ud unatazamwa; aya zilizomo ambazo zilinukuliwa kwa mapokezi ya mutawatir zinazingatiwa kuwa ni Qur'an, na aya zilizomo ambazo zilinukuliwa kwa njia ya Ahad, kama vile aya "basi afunge siku tatu mfululizo", hiyo haizingatiwi kuwa ni Qur'an na wala si hoja.

Kutokana na hili, pingamizi lililojitokeza kuhusiana na wahifadhi wa Qur'an na kuhusiana na masahafu ya Maswahaba linakataliwa, na inathibiti kuwa Qur'an ni ile iliyonukuliwa kwa mapokezi ya mutawatir, na kile kilichonukuliwa kwa njia ya Ahad si katika Qur'an. Na miongoni mwa mambo yanayopaswa kuzingatiwa ni kwamba Qur'an ilinukuliwa kwa kushuhudiwa kutoka kwa Mtume ﷺ kupitia Wahyi wakati ilipokuwa ikishuka, na ikarekodiwa kwa maandishi sambamba na kuhifadhiwa kifuani. Maswahaba (ra) hawakuipokea Qur'an kama riwaya kutoka kwa Mtume, bali waliinukuu kama nakala, yaani walinukuu kile kile alichoshuka nacho Wahyi na kile ambacho Mtume ﷺ aliamrisha kiandikwe. Hii ni tofauti na Hadithi, kwani Hadithi ilipokewa kutoka kwa Mtume ﷺ kama riwaya na haikurekodiwa wakati wa kusemwa kwake wala wakati wa kupokewa kwake, bali uandishi na uwekaji kumbukumbu wake ulifanyika katika zama za wafuasi wa matabiina (tabi'u at-tabi'in). Ama Qur'an iliandikwa na kurekodiwa wakati wa kushuka kwa Wahyi, na Maswahaba walinukuu kile kile alichokuja nacho Wahyi; na kwa sababu hiyo inasemwa: Maswahaba wametinukulia Qur'an kwa njia ya nakala (naqlan).]

2- Imekuja katika kitabu cha Ash-Shakhsiyyah al-Islamiyyah Juzuu ya Tatu, mlango wa "An-Nasikh wal-Mansukh":

[Pili ni kwamba makusudio ni kufutwa hukumu ya aya na si kufutwa usomaji wake (tilawah), na kauli hii ndiyo iliyochaguliwa na wengi (jumhur) na ndiyo inayotegemewa. Inasuportiwa na ukweli kwamba aya zote za Qur'an zilithibiti kwa dalili ya kukatikiwa (qati'i), na aya isiyothibiti kwa dalili ya kukatikiwa haizingatiwi kuwa ni Qur'an. Na haikuthibiti kwa dalili ya kukatikiwa kufutwa kwa usomaji wa aya yoyote kati ya aya za Qur'an, na kile kilichokuja katika dalili ya dhana (zanni) kuhusu kuwepo kwa kufutwa usomaji haina thamani katika kuzingatia naskh; kwa sababu chenye kukatikiwa (qati'i) hakifutwi na chenye dhana (zanni), na hakifutwi isipokuwa na chenye kukatikiwa mfano wake au kilicho juu yake. Na haikuja dalili ya kukatikiwa juu ya kufutwa usomaji, na hii inasuporti kuwa makusudio ni kufutwa kwa hukumu na si kufutwa kwa usomaji.]

  • Imekuja pia katika chanzo hicho hicho yafuatayo:

[Ama kufutwa kwa Qur'an katika usomaji wake (tilawah) ni jambo lililozuiwa, na halijaruhusiwa, na halikuthibiti kutokea kwake kwa dalili ya kukatikiwa. Na dalili ya kutojuzu ni kwamba aya ambayo kwayo kuruhusiwa kwa naskh kulithibiti inasema:

نَأْتِ بِخَيْرٍ مِنْهَا أَوْ مِثْلِهَا

"Tunaleta iliyo bora kuliko hiyo au mfano wake." (QS. al-Baqarah [2]: 106)

Na Qur'an yote ni kheri bila ya kuwepo tofauti ndani yake, hivyo kama makusudio ya kufutwa aya yangekuwa ni kuiondoa katika ubao uliohifadhiwa (Lawh al-Mahfuz) na kuandika nyingine badala yake, sifa ya kheri isingepatikana. Kwa hivyo maana yake siyo aya yenyewe bali ni hukumu yake. Pia, Qur'an imethibiti kuteremka kwake, kuhifadhiwa kwake na kuandikwa kwake kwa njia ya tawatur, na kuiamini kwa njia hii ni itikadi (aqidah), na hiyo haichukuliwi isipokuwa kutoka kwenye dalili ya kukatikiwa kwa uthabiti na kukatikiwa kwa maana (qati'i al-thubut qati'i al-dalalah). Na hili halikutokea kwani haikuja dalili ya kukatikiwa inayoonyesha kujuzu kwa kufutwa Qur'an katika usomaji; hivyo haijuzu kuifuta katika usomaji. Ama kutokutokea kwa naskh ya Qur'an katika usomaji, dalili yake ni kwamba haikuja dalili ya kukatikiwa inayothibitisha kuwa aya yoyote miongoni mwa aya zake zilizothibiti kwa dalili ya kukatikiwa imefutwa. Ama yale yaliyopokewa kutoka kwa Zaid bin Thabit amesema: Nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ akisema:

الشَّيْخُ وَالشَّيْخَةُ إِذَا زَنَيَا فَارْجُمُوهُمَا الْبَتَّةَ. فَقَالَ عُمَرُ: لَمَّا أُنْزِلَتْ هَذِهِ أَتَيْتُ رَسُولَ اللَّهِ ﷺ فَقُلْتُ: أَكْتِبْنِيهَا

"Mzee mwanamume na mzee mwanamke wakizini, basi wapigeni mawe kabisa. Omar akasema: Ilipoteremshwa hii, nilimwendea Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ nikamwambia: Niandikie." (Imetolewa na Ahmad).

Na kile alichopokea Aisha kwamba alisema: "Ilikuwa miongoni mwa yaliyoteremshwa katika Qur'an kunyonya mara kumi kulikojulikana kunaharamisha, kisha kukafutwa kwa mara tano zinazojulikana" (Imetolewa na Muslim). Na kile kilichopokewa kutoka kwa Ubayy bin Ka'b na Ibn Mas'ud kwamba walisoma: "basi afunge siku tatu mfululizo", na yaliyopokewa kwamba sura ya al-Ahzab ilikuwa inalingana na sura ya al-Baqarah, na mengineyo, yote hayo ni khabar Ahad ambazo hoja hazisimami kwayo juu ya kufuta kile kilichokatikiwa (qati'i); kwa sababu hizo ni habari za dhana (zanni), na chenye kukatikiwa hakifutwi na chenye dhana, na hakifutwi isipokuwa na chenye kukatikiwa. Kwa hivyo ni lazima ithibiti kwa dalili ya kukatikiwa kuwa aya hii ilishuka ili iaminiwe kuwa ni miongoni mwa Qur'an, kisha ithibiti pia kwa dalili ya kukatikiwa kuwa imefutwa, na hili halijawahi kutokea kabisa. Na kwa mujibu wa hayo, kufutwa Qur'an katika usomaji wake halijatokea.]

3- Kutokana na hayo, haya ndiyo majibu ya maswali yako:

a- Qur'an Tukufu inafafanuliwa kama ifuatavyo: (Ni maneno ya Mwenyezi Mungu yaliyoteremshwa kwa Mtume wake Muhammad ﷺ kupitia Wahyi "Jibril" amani iwe juu yake, kwa tamshi na maana, yenye muujiza, yenye kuabudiwa kwa kuisoma na iliyonukuliwa kwetu kwa mapokezi ya mutawatir). Hivyo basi, ni Qur'an iliyoteremshwa kwa bwana wetu Muhammad ﷺ na ni ile iliyonukuliwa kwetu katikati ya majalada ya msahafu kwa mapokezi ya mutawatir. Na ufafanuzi huu unalingana kikamilifu na msahafu wa Othman (ra), yaani msahafu ulionakiliwa katika zama za Khalifa Mwongofu Othman bin Affan katika nakala kadhaa kutokana na kurasa alizozikusanya Abu Bakr (ra) kutokana na kile kilichoandikwa mbele ya Mtume ﷺ, na Othman (ra) akatuma nakala hizo katika miji mikuu ya Waislamu, na Maswahaba wa Mtume ﷺ wakaiitafakiana kama ilivyobainishwa kwa kina katika vitabu vyetu...

b- Hii ina maana kwamba kile kilichonukuliwa kwetu kutoka kwenye Qur'an kwa njia ya Ahad kama vile msahafu wa Ibn Mas'ud na wengineo si Qur'an na wala si hoja. Kadhalika, si sehemu ya Sunnah kwa sababu ilipokewa kwa msingi kuwa ni Qur'an na haikupokewa kuwa ni hadithi ya Mtume ﷺ. Na maadamu si Sunnah, haijuzu kuitolea dalili katika hukumu za kisheria na mambo mengine yanayopaswa kutolewa katika dalili za kisheria.

c- Kusoma Qur'an kwa riwaya kama hizo na kwa usomaji usio wa kawaida (shadh) haiswihi. Tumetaja kile kinachoashiria hilo katika jawabu la swali la tarehe 18 Dhul-Qi'dah 1434 AH - 24 Septemba 2013 AD, ambapo ilikuja:

[Ama kusoma Qur'an kwa qira'a zisizo za mutawatir, ziwe zimeafikiana na maandishi ya msahafu wa Kiothman au la, haijuzu kusoma kwazo, kwani hizo si Qur'an, bali Qur'an ni ile iliyonukuliwa kwa tawatur kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ].

d- Na maadamu nukuu hizi zilizopokewa kwa njia ya Ahad kuwa ni Qur'an hazikuthibiti kuwa ni Qur'an, na pia hazihesabiwi kuwa ni Sunnah kutoka kwa Mtume ﷺ kwa sababu hazikupokewa kama Sunnah, basi ukomo wa kile zinachoweza kuonyesha ni kwamba zihesabiwe kuwa ni sehemu ya tafsiri ya Swahaba kwa Qur'an na ubainifu wake. Yaani ihesabiwe kuwa ni kauli ya Swahaba aliyeipokea katika kubainisha maana ya aya inayohusiana na ziada hiyo au qira'a hiyo. Yaani, alisoma aya kisha akaifasiri bila kutofautisha kati ya aya na tafsiri yake, hivyo zikanukuliwa zikiwa zimefuatana na msikilizaji akadhani kuwa ni sehemu ya Qur'an, hali ya kuwa haikuwa Qur'an bali ilikuwa ni tafsiri ya Swahaba kulingana na maoni yake. Hivi ndivyo inavyoweza kufasiriwa, na haiwezi kuvuka hapo kwa namna yoyote ile. Hivyo, qira'a ya Ibn Mas'ud kwa mfano: "basi afunge siku tatu mfululizo", kwa ziada ya neno "mfululizo" ni kauli ya Ibn Mas'ud akibainisha kwayo ulazima wa mfuatano katika saumu ya kafara ya kiapo. Yaani ziada hiyo inakuwa ni ubainifu wa hukumu ya mfuatano kwa mujibu wa maoni ya Ibn Mas'ud (ra), na hii haivuki kuwa ni ijtihadi na uelewa wa Swahaba na haichukui hukumu ya dalili ya kisheria kutoka kwenye Sunnah.

e- Hivyo basi, kila nukuu ya Ahad kuhusu Qur'an Tukufu inayopingana na nukuu ya kukatikiwa inatazamwa:

  • Ikiwa mnyororo wake wa mapokezi (sanad) ni dhaifu, basi inakataliwa kwa udhaifu wake.
  • Ikiwa mnyororo wake ni sahihi, basi inakataliwa kwa upande wa maana (dirayah) kwa sababu ya kupingana na chenye kukatikiwa (qati'i).

4- Ninataja miongoni mwa yaliyokuja katika baadhi ya vitabu vya mafaqihi wa Kiislamu kuhusu mambo kama haya, kwa ajili ya elimu:

a- Imekuja katika Al-Mawsu'ah al-Fiqhiyyah al-Kuwaitiyyah (uk: 11908) yafuatayo:

[- Qur'an ni ile iliyonukuliwa kwetu katikati ya majalada ya msahafu kwa mapokezi ya mutawatir, na imefungamanishwa na masahafu; kwa sababu Maswahaba (ra) walifanya juhudi kubwa katika kuinukuu na kuitakasa na kila kitu kingine, mpaka wakachukia kuweka alama za kila aya kumi (ta'shir) na vitone ili isichanganyike na vinginevyo. Hivyo tunajua kuwa kilichoandikwa katika msahafu uliokubaliwa ndiyo Qur'an, na kwamba kilicho nje yake si sehemu yake, kwani ni muhali kulingana na desturi na kawaida, pamoja na kuwepo kwa sababu nyingi za kuihifadhi Qur'an, kwamba sehemu yake ipuuzwe, kisha isinukuliwe, au ichanganywe na kile kisicho sehemu yake.]

Na elezo hilo la kifiqhi linaendelea: [Hakuna khitilafu kwamba kila kilicho miongoni mwa Qur'an lazima kiwe mutawatir katika asili yake na sehemu zake. Ama kuhusu mahali pake, uwekaji wake na mpangilio wake, kwa mujibu wa wanachuoni wachunguzi wa Ahlus Sunnah ni vivyo hivyo, yaani lazima iwe mutawatir. Imekuja katika Musallam al-Thubut na sharhi yake Fawatih al-Rahamut: Kile kilichonukuliwa kwa njia ya Ahad hakika si Qur'an kwa yakini, na hakuna khitilafu iliyojulikana kuhusu hili kwa yeyote miongoni mwa watu wa madhehebu. Alitoa dalili kwamba Qur'an ni miongoni mwa mambo ambayo kuna sababu nyingi za kunukuliwa kwake kwa sababu inajumuisha changamoto (tahaddi); na kwa sababu ni asili ya hukumu kwa kuzingatia maana na mpangilio wote mpaka hukumu nyingi zimefungamana na mpangilio wake; na kwa sababu inatumiwa kwa baraka katika kila zama kwa kusoma na kuandika. Kwa hivyo juhudi za Maswahaba zilijulikana katika kuihifadhi kwa tawatur inayokatikiwa, na kila kitu chenye sababu nyingi za kunukuliwa hupokelewa kwa tawatur kikawaida. Hivyo, uwepo wake unalazimu tawatur kwa kila mtu kikawaida, na ikiwa lazima (tawatur) haipo, basi kilicholazimiwa hakipo kwa yakini. Na kilichonukuliwa kwa njia ya Ahad si mutawatir, hivyo si Qur'an...] Mwisho.

b- Imekuja katika kitabu cha (Al-Itqan fi Ulum al-Qur'an "1/ 279") cha As-Suyuuti yafuatayo: [Abu Ubaid amesema katika Fadhail al-Qur'an: Makusudio ya qira'a isiyo ya kawaida (shadh) ni kutafsiri qira'a maarufu na kubainisha maana zake kama vile qira'a ya Aisha na Hafsa "na swala ya kati na kati, swala ya Alasiri", na qira'a ya Ibn Mas'ud: "basi kateni mikono yao ya kulia" na qira'a ya Jabir: "basi hakika Mwenyezi Mungu baada ya kulazimishwa kwao kwao ni Mwingi wa kusamehe, Mwenye Murehemu". Amesema: Herufi hizi na mfano wake zimekuwa ni zenye kufasiri Qur'an, na mfano wa haya ulikuwa ukipokewa kutoka kwa matabiina katika tafsiri na ikawa inapendeza, basi vipi ikiwa imepokewa kutoka kwa Maswahaba wakubwa...]

Natumai kuwa jawabu hili litakuwa limetosha, na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi zaidi na Mwenye hekima zaidi.

Ndugu yenu Ata bin Khalil Abu Al-Rashtah

22 Dhul-Hijjah 1443 AH Inayoafikiana na 21/07/2022 AD

Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amiri (Mungu amhifadhi) kwenye Facebook

Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amiri (Mungu amhifadhi) kwenye Tovuti

Share Article

Share this article with your network