Mfululizo wa Majibu ya Mwanachuoni Mtukufu Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah, Amiri wa Hizb ut-Tahrir, kwa Maswali ya Wageni wa Ukurasa Wake wa Facebook "Fiqhi"
Kwa Anas M Hirbawi
Swali:
Assalamu Alaikum Warahmatullahi Wabarakatuh, salamu njema baada ya hayo...
Nina swali kuhusiana na safari ya mwanamke bila mahram...
Swali ni: Ni mipaka gani inayozingatiwa kuwa safari ya mwanamke ni safari na haijuzu kusafiri isipokuwa na mahram? Kwa mfano, tukitaka kuipima hapa Palestina: Ikiwa mwanamke anataka kusafiri kutoka Yerusalemu kwenda Umm al-Rashrash (Eilat), safari yake itakuwa ndani ya nchi moja, lakini akitaka kusafiri kutoka Yerusalemu kwenda Jordan, ni karibu zaidi kuliko Umm al-Rashrash. Hivyo mambo yanapimwaje? Je, yanapimwa kwa mipaka iliyowekwa (vituo vya ukaguzi), au yanapimwa kwa umbali fulani kama vile kilomita 80? Pia, kuna baadhi ya watu wa Al-Azhar wa sasa ambao si watu wa kuaminika wanasema: Katika zama hizi, mwanamke hahitaji mahram kwa safari kwa sababu mambo yamekuwa rahisi, na wamefungamanisha mambo na njia ya usafiri. Je, maneno yao yanachukuliwa au yanakataliwa...?
Mbakie katika amani na ulinzi wa Mwenyezi Mungu.
Jibu:
Wa Alaikum Salaam Warahmatullahi Wabarakatuh.
Tumeshawahi kutoa jibu la kina kuhusu safari ya mwanamke katika hali zake mbalimbali mnamo tarehe 05/11/2018, na nitakunukulia sehemu inayohusiana na swali lako:
[...
Kwanza: Safari ya mwanamke ikiwa inachukua muda wa siku moja na usiku wake, basi ni lazima awe na mahram. Dalili za kisheria ni nyingi katika maana hii, na tunataja miongoni mwazo:
- Bukhari amepokea kutoka kwa Abu Hurairah (ra), amesema: Mtume ﷺ amesema:
لَا يَحِلُّ لِامْرَأَةٍ تُؤْمِنُ بِاللَّهِ وَاليَوْمِ الآخِرِ أَنْ تُسَافِرَ مَسِيرَةَ يَوْمٍ وَلَيْلَةٍ لَيْسَ مَعَهَا حُرْمَةٌ
"Si halali kwa mwanamke anayemwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kusafiri mwendo wa siku moja na usiku wake bila ya kuwa na mahram (ndugu wa kiume)."
Katika riwaya ya Abu Said al-Khudri imetajwa "siku mbili", na katika riwaya ya Ibn Umar imetajwa "siku tatu".
- Muslim amepokea kutoka kwa Abu Hurairah kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ amesema:
لَا يَحِلُّ لِامْرَأَةٍ تُؤْمِنُ بِاللهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ، تُسَافِرُ مَسِيرَةَ يَوْمٍ وَلَيْلَةٍ إِلَّا مَعَ ذِي مَحْرَمٍ عَلَيْهَا
"Si halali kwa mwanamke anayemwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kusafiri mwendo wa siku moja na usiku wake isipokuwa awe na mahram yake."
Katika riwaya nyingine ya Abu Said al-Khudri imetajwa "mwendo wa siku mbili", na katika riwaya nyingine "siku tatu na zaidi".
- Tirmidhi amepokea, na akasema hadithi hii ni hasan sahih, kutoka kwa Said bin Abi Said, kutoka kwa baba yake, kutoka kwa Abu Hurairah, amesema: Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ amesema:
لَا تُسَافِرُ امْرَأَةٌ مَسِيرَةَ يَوْمٍ وَلَيْلَةٍ إِلَّا وَمَعَهَا ذُو مَحْرَمٍ
"Mwanamke asisafiri mwendo wa siku moja na usiku wake isipokuwa awe na mahram."
...
Kutokana na haya, inabainika yafuatayo:
1- Kufungamanishwa kwa safari ni kwa muda kama ilivyo katika maandiko sahihi. Ni haramu kwa mwanamke kusafiri peke yake bila mahram kwa muda uliotajwa, yaani siku nzima (masaa 24), usiku na mchana. Hii ina maana kwamba maandiko yanafafanua muda "siku na usiku" na si umbali. Hivyo, akisafiri kwa ndege bila mahram kwa umbali wa kilomita elfu moja, akaenda na kurudi bila kukaa muda huo, inajuzu kwake kufanya hivyo. Lakini akisafiri kwa miguu kilomita ishirini na safari hiyo ikamchukua zaidi ya mchana na usiku, ni haramu kwake bila mahram.
- Hivyo, kigezo katika safari ya mwanamke bila mahram ni muda, mchana na usiku, bila kujali umbali. Ikiwa mwanamke hatakaa muda huu, bali akasafiri na kurudi kabla yake, basi inajuzu kwenda kwake bila mahram.
2- Ama yale yaliyokuja katika riwaya za Bukhari, Muslim, Tirmidhi, na Ahmad... (siku tatu au mikesha mitatu, siku mbili...), kwa kukusanya dalili hizo, hukumu ya kisheria ni kutokusafiri mwendo ule mdogo kabisa (siku moja na usiku wake) isipokuwa akiwa na mahram...
Hivyo basi, ni haramu kwa mwanamke kusafiri mwendo wa siku moja na usiku wake isipokuwa akiwa na mume au mahram, na hili ndilo tulilolichukua na kuliasisi katika Mfumo wa Kijamii.
Pili: ...
3- Haya ndiyo tunayoyasema, kwa kuzingatia mambo yafuatayo:
Tunasema maoni haya ndiyo yenye nguvu zaidi (rajih) na hatusemi kuwa ni maoni ya kukata moja kwa moja (قطعي), hilo ni moja...
Pili, tunasema inajuzu kwake kusafiri muda usiofika siku moja na usiku wake bila mahram na hatusemi kuwa ni wajibu kufanya hivyo. Hivyo basi, ikiwa mwanamke hataki kusafiri mwendo wa nusu mchana isipokuwa na mahram, ana haki hiyo. Jambo la msingi ni kwamba asisafiri mwendo wa siku moja na usiku wake isipokuwa awe na mahram...
Tatu, sharti la hadithi ya kuandamana na mahram wakati wa safari yake linaashiria ulazima wa kulinda na kuhifadhi heshima ya mwanamke na kwamba awe salama. Kwa hiyo, haijuzu kwa mwanamke kusafiri ikiwa hajisikii kuwa salama isipokuwa na mahram. Hivyo hasafiri bila mahram hata kama muda ni saa moja mchana, kwani usalama wa nafsi yake ni sharti jingine...
Nne, haijuzu kwake kusafiri isipokuwa akiruhusiwa na mume au mlinzi wake (wali) bila kujali muda, hata kama ataandamana na mahram, kutokana na dalili za kisheria kuhusu hilo.
...
Nne: Kufika sehemu inayokusudiwa:
...
- Ikiwa sehemu inayokusudiwa ipo katika nchi za Kiislamu ambazo si Dar al-Islam, hizi zimegawanyika katika sehemu mbili:
Kwanza: Ikiwa safari ni ndani ya maeneo ya nchi yake lakini ni nchi pana ambayo hadithi za safari ya mwanamke za siku moja na usiku wake au zaidi zinaingiliana nayo. Akifika sehemu anayokusudia, mahram amwandalie makazi salama kwa ndugu zake (maharim) ikiwa wapo. Ikiwa hawapo, na akawa na marafiki wanawake wema na waaminifu ambao mahram anaridhika na wema wao, basi mahram amwandalie makazi salama akiwa na mwanamke mmoja au wawili miongoni mwa wanawake hao, yaani asiwe katika nyumba peke yake. Akae hapo hadi amalize haja yake, huku akimjulia hali kwa simu au njia za mawasiliano (social media) angalau mara moja kwa wiki... Ikiwa mwanamke huyo anamhitaji mahram huyo, basi mahram ni lazima asafiri kwenda kwake... Na anapotaka kurejea, ni lazima mahram amfuate na kusafiri naye kurejea nyumbani kwake maadamu safari yake itachukua siku moja na usiku wake au zaidi...
Ikiwa hana mahram au marafiki wanawake wema na waaminifu, basi ima mahram abaki naye hadi amalize haja yake, au warejee wote wawili.
Pili: Ikiwa safari ni kutoka nchi moja ya Kiislamu kwenda nchi nyingine ya Kiislamu na kila moja iko katika serikali tofauti, na safari yake kati ya nchi hizo mbili inachukua siku moja na usiku wake au zaidi... Katika hali hii, inajuzu kwa mwanamke akifika eneo analosafiri kwenda, mahram kurejea eneo lake na asibaki naye kwa sharti kwamba:
- Mahram amwandalie makazi atakayoishi kwa amani na usalama, kama vile kuwa kwa ndugu zake (maharim) au kwa marafiki zake wanawake wema na waaminifu, yaani asiwe katika nyumba peke yake... Na mahram abaki kwa wiki moja baada ya kumwandalia makazi ili kujiridhisha na usalama wa harakati zake kutoka nyumbani kwenda kwenye shughuli yake katika siku za kazi na siku za mapumziko. Na kwa kuwa mapumziko haya yanajirudia kila wiki, sioni kama muda wake wa kubaki naye uwe chini ya wiki moja ili kujiridhisha... Na awasiliane naye kwa simu au njia za mawasiliano kila siku. Ikiwa itambainikia kuwa anamhitaji, basi ni lazima amsafirie mara moja kumjulia hali... Na anapotaka kurejea, ni lazima mahram amfuate na kusafiri naye kurejea nyumbani kwake maadamu safari yake itachukua siku moja na usiku wake au zaidi...
Ikiwa hana mahram wala marafiki wanawake wema, basi ima mahram abaki naye hadi apate marafiki wanawake wema na waaminifu na kisha amwandalie makazi salama na marafiki hao kisha akae wiki moja baada ya hapo... au warejee wote wawili...
- Ikiwa sehemu inayokusudiwa ipo katika nchi zisizo za Kiislamu, basi huangaliwa:
- Ikiwa ana ndugu wa kiume (maharim) huko anaoishi kwao au karibu nao (jirani yao) kiasi kwamba mahram aliyesafiri naye anajiridhisha kuwa atakuwa salama huko katika maisha yake binafsi na ya kijamii, au ana ndugu wa kike huko kama mama yake, dada yake, au shangazi yake na anaishi naye (haishi jirani naye tu)... Katika hali hizi mbili, inajuzu kwa mahram aliyesafiri naye kurejea baada ya kujiridhisha na usalama wake, kwa sharti la idhini ya mlinzi (wali) au mume na kwa sharti kuwa mawasiliano ya ana kwa ana au kwa barua yapo kila inapohitajika... Kisha anapotaka kurejea, mahram amfuate ili amsindikize katika safari ya kurudi maadamu inachukua siku moja na usiku wake au zaidi.
Ama ikiwa yaliyotajwa hapo juu hayatapatikana, basi ni wajibu kwa mahram kuendelea kubaki naye hadi arejee katika nchi yake ya asili, kwa sababu mahitaji ya amani na usalama yanayotakiwa katika maisha ya mwanamke kwa kuwa yeye ni heshima (ardh) inayopaswa kulindwa, mahitaji haya hayatimizwi katika nchi zisizo za Kiislamu isipokuwa akiwa kwa ndugu zake (maharim) kama tulivyotaja.
** b- Ikiwa sehemu inayokusudiwa iko baada ya safari fupi isiyohitaji mahram katika safari** na akataka kubaki sehemu hiyo kwa siku moja, mbili, tatu... nk, ni upi wajibu kwake katika hali hii? Je, anahitaji mahram?
Jibu ni kama ifuatavyo:
*- Ikiwa sehemu inayokusudiwa ni Dar al-Islam, iwe ni katika mkoa wake au mkoa mwingine, inajuzu kwake kusafiri bila mahram kwa sababu muda wa safari ni chini ya siku moja na usiku wake. Ikiwa hatarudi siku hiyo na akataka kubaki siku moja, mbili, tatu... nk, inajuzu kwake kubaki kwa ndugu zake (maharim) au kwa marafiki zake wanawake waaminifu na wema pekee, yaani asiwe katika nyumba peke yake, kwa sharti la kupata idhini mapema ya kuishi na marafiki hao kutoka kwa mlinzi au mume kwa utulivu.
Ama ikiwa hana mahram wala marafiki wanawake wema na waaminifu ambao mlinzi wake au mume wake amekubali aishi nao, basi ni lazima arejee siku hiyo hiyo au mahram asafiri naye ili amhakikishie makazi yake kama tulivyotaja katika hali ya safari na mahram.
- Ikiwa sehemu inayokusudiwa ipo katika nchi ya Kiislamu anayoishi lakini si Dar al-Islam na muda wa safari ni chini ya siku moja na usiku wake, inajuzu kwake kusafiri bila mahram. Ikiwa hatarudi siku hiyo na akataka kubaki siku moja, mbili, au tatu... nk, inajuzu kwake kubaki kwa ndugu zake (maharim) au kwa marafiki zake wanawake waaminifu na wema pekee, yaani asiwe katika nyumba peke yake, kwa sharti la kupata idhini mapema ya kuishi na marafiki hao kutoka kwa mlinzi au mume kwa utulivu.
Ama ikiwa hana mahram wala marafiki wanawake wema na waaminifu ambao mlinzi wake au mume wake amekubali aishi nao, basi ni lazima arejee siku hiyo hiyo au mahram asafiri naye ili amhakikishie makazi yake kama tulivyotaja katika hali ya safari na mahram.
- Ikiwa sehemu inayokusudiwa ipo katika nchi ya Kiislamu tofauti na anayoishi na si Dar al-Islam na muda wa safari ni chini ya siku moja na usiku wake, inajuzu kwake kusafiri bila mahram. Lakini kwa kuwa safari ni kutoka nchi yake kwenda nchi nyingine na kuna taratibu za mipakani, ni lazima asindikizwe na kundi la wanawake waaminifu wasiopungua mmoja, ambapo dhumuni la safari yake liwe dhumuni lile lile ambalo mwanamke huyo anasafiri kwa ajili yake, kwa maneno mengine dhumuni la wenzake na dhumuni la mwanamke msafiri liwe ni moja... Ikiwa akitaka kubaki huko siku moja au mbili inajuzu kwake kwa masharti yafuatayo:
Wawe na ndugu (maharim) huko, kila mmoja akae kwa mahram wake. Ikiwa hawana mahram, basi wawe na marafiki wanawake waaminifu na waaminifu, na walinzi au waume wakubali makazi ya wanawake hao wawili kwa marafiki hao kulingana na yaliyoelezwa katika masharti hapo juu.
Ikiwa masharti hayo hapo juu hayatatimia, yaani ikiwa kila mmoja wao hana mahram, wala marafiki kwa kila mmoja wao ambao walinzi au waume wameridhia makazi ya wanawake hao wawili na marafiki hao, basi ni lazima arejee siku hiyo hiyo.
*- Ikiwa sehemu inayokusudiwa ipo katika nchi isiyo ya Kiislamu, yaani katika nchi za makafiri, basi katika hali hii ni lazima mwanamke asafiri na mume wake, mlinzi wake, au mahram wake, na jambo hilo litakuwa kama lilivyokuja katika hali ya safari ndefu inayohitaji mahram...
Tano: Ama kuhusu dalili tulizozitegemea ili kutimiza amani na usalama wa mwanamke baada ya kufika sehemu inayokusudiwa, iwe ni baada ya safari ndefu inayohitaji mahram au baada ya safari fupi isiyohitaji mahram, hizo ni dalili tulizozitaja mwanzo wa kuwasili sehemu inayokusudiwa, na nazirejelea:
[Na kwa msingi huo, hukumu wakati wa kuwasili sehemu inayokusudiwa zinatofautiana na hukumu wakati wa safari njiani. Suala hili, yaani kuwasili sehemu inayokusudiwa bila kuifanya kuwa makazi ya kudumu, linategemea kupatikana kwa usalama katika sehemu hiyo kwa ajili ya makazi ya mwanamke, yaani usalama wake katika makazi yake na usalama wake katika harakati zake nje ya nyumba, na hili ni jambo linalohitajika na uhalisia wa mwanamke na usalama wa maisha yake. Imekuja katika Utangulizi wa Katiba katika Ibara ya 112: (Asili kwa mwanamke ni kwamba yeye ni mama na mlezi wa nyumba, na yeye ni heshima (ardh) inayopaswa kulindwa.), na kama ilivyo wazi kutokana na maelezo ya ibara hiyo, mwanamke anahitaji idhini ya mlinzi wake au mume wake katika kutoka... Na ana maisha binafsi yenye hukumu maalumu zinazomzuia kuishi na wanaume wageni, bali huishi na mume wake au na mahram zake... Na katika maisha ya umma anazuiwa kukaa faragha (khalwa) na kuchanganyika (ikhtilat) isipokuwa kwa haja inayokubaliwa na Sheria... Na ana mavazi ya kisheria maalumu "Jilbab, kusitiri uchi, na kuzuia urembo (tabarruj)".]
Na yote haya yanahitaji amani na usalama kwa mwanamke ili kutimiza uhalisia wake wa kuwa heshima inayopaswa kulindwa kwa kupatikana kwa amani na usalama, na hili linahitaji uhakiki wa mazingira husika (tahaqquq al-manat)... Na ninachokiona kuwa kina nguvu zaidi katika suala hili ni kile nilichokitaja hapo juu kwa kupatikana kwa masharti yote... Na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi zaidi na Mwenye Hekima.
... 27 Safar 1440H - sawia na 05/11/2018M] Mwisho.
Ama kuhusu uliyoyataja ya maneno ya baadhi ya masheikh (Pia, kuna baadhi ya watu wa Al-Azhar wa sasa ambao si watu wa kuaminika wanasema: Katika zama hizi, mwanamke hahitaji mahram kwa safari kwa sababu mambo yamekuwa rahisi, na wamefungamanisha mambo na njia ya usafiri. Je, maneno yao yanachukuliwa au yanakataliwa...?)
Hayo ni maneno yasiyokuwa na thamani wala uzito. Maandiko yapo wazi kuhusu wajibu wa mahram, na hiyo ni hukumu ya kisheria ambayo haibatilishwi na maneno yasiyokuwa na hoja...
Na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi zaidi na Mwenye Hekima.
Ndugu yenu, Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah
14 Rajab 1444H Sawia na 05/02/2023M
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amiri (Mungu amuhifadhi) kwenye Facebook