Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Masharti ya Kusihi kwa Shirika la Mudharaba

May 23, 2018
4602

(Mfululizo wa majibu ya mwanachuoni mtukufu Ata Bin Khalil Abu al-Rashta, Amir wa Hizb ut Tahrir, kwa maswali ya wafuasi wa ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi")

Jibu la Swali

Masharti ya Kusihi kwa Shirika la Mudharaba

Kwa Khalil al-Abbasi

Swali:

Asalamu Alaykum ewe Sheikh wetu mtukufu. Mimi nina swali kuhusu shirika nililoingia na mtu mmoja ambaye ana viwanda na maduka makubwa (supermarkets). Niliweka kiasi cha pesa katika shirika hili ili aniendeshee, lakini ana washirika wengine ambao sijawaona wala sijakaa nao; mwenye shirika huyo aliwaambia tu kwamba nimeweka kiasi cha pesa kwake. Watu hao ni washirika wa mali tu kama mimi, na mwenye shirika ni mshirika wa mali na mwili (juhudi) na yeye ndiye anayesimamia shirika hili.

Swali ni je, shirika langu hili ni halali? Naomba unifafanulie suala hili na nini ninachopaswa kufanya kwa sababu baadhi ya vijana wameniambia kuwa shirika hili ni halali na wengine wameniambia kuwa halijuzu kisheria. Baraka za Allah ziwe nanyi.

Jibu:

Wa Alaykum Salam wa Rahmatullahi wa Barakatuh,

1- Kuhusu shirika la Mudharaba, inajuzu kuwa ni Mudharaba kati ya mali ya mmoja wa washirika na juhudi ya mshirika mwingine, na pia kati ya mali ya mmoja wa washirika na mali pamoja na juhudi ya mshirika mwingine. Kadhalika, inajuzu kati ya mali ya washirika zaidi ya mmoja na juhudi ya mwendeshaji (Mudharib)... Imeelezwa katika kitabu cha Mfumo wa Kiuchumi: "Na miongoni mwa Mudharaba ni kushirikiana mali mbili na mwili (juhudi) wa mmoja wao. Hivyo, ikiwa kuna elfu tatu kati ya watu wawili, mmoja akiwa na elfu moja na mwingine elfu mbili, kisha mwenye elfu mbili akamruhusu mwenye elfu moja azitumie kwa sharti kwamba faida iwe kati yao nusu kwa nusu, shirika hilo linasihi, na mfanyakazi atakuwa ni yule mwenye elfu moja akiwa ni Mudharib kwa upande wa mwenye elfu mbili na pia ni mshirika wake. Vilevile, miongoni mwa Mudharaba ni kushirikiana mali mbili na mwili wa mtu mwingine asiyekuwa wao, kwani yote hayo yanaingia katika mlango wa Mudharaba."

2- Na miongoni mwa masharti ya kusihi kwake ni kama ilivyoelezwa katika Mfumo wa Kiuchumi: "Mudharaba hausihi mpaka mali ikabidhiwe kwa mfanyakazi na aachiwe uhuru wa kuitumia; kwa sababu Mudharaba unahitaji kukabidhiwa mali kwa Mudharib. Na ni lazima katika Mudharaba kukadiria fungu la mfanyakazi, na iwe mali ambayo Mudharaba unafanyika kwayo ni kiasi kinachojulikana."

3- Kama unavyoona, miongoni mwa masharti ya kusihi kwa Mudharaba ni kwamba mali inayofanyiwa Mudharaba iwe kiasi kinachojulikana na fungu la mwenye juhudi katika faida likadiriwe kwa njia ya wazi kwa makubaliano ya washirika... Kwa msingi huo, haijuzu kwa Mudharib kuchukua mali kutoka kwa huyu na mali kutoka kwa yule na kukubaliana na kila mmoja wao kuhusu faida bila mmoja wao kujua mtaji ni kiasi gani na je, washirika waliobaki wamekubali uwiano wa faida au la... Hivyo basi, yale yaliyotajwa katika swali hayajuzu, bali ni lazima washirika wakutane na kukubaliana juu ya faida na kukubaliana juu ya mtaji kwa njia iliyo wazi na inayojulikana.

Hivi ndivyo ninavyoona kuwa na nguvu zaidi katika suala hili, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi zaidi na Mwenye Hekima zaidi.

Ndugu yenu, Ata Bin Khalil Abu al-Rashta

06 Ramadhan 1439 H Inayoambatana na 22/05/2018 M

Link ya jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir (Mungu amuhifadhi) kwenye Facebook

Link ya jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir (Mungu amuhifadhi) kwenye Google Plus

Link ya jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir (Mungu amuhifadhi) kwenye Web

Share Article

Share this article with your network