Mfululizo wa Majibu ya Mwanachuoni Mkubwa Ata bin Khalil Abu al-Rashtah, Ameer wa Hizb ut-Tahrir, kwa Maswali ya Wageni kwenye Ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi"
Jibu la Swali
Kuwapongeza Wakristo na Makafiri katika Sikukuu zao
Kwa Bahaa Alden Torman
Swali:
Assalamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh, ndugu yenu katika imani Bahaa kutoka Palestina, tunamuomba Mwenyezi Mungu awajaalie kuwa na afya njema.
Swali langu ni kuhusu kuwapongeza Wakristo katika sikukuu zao na kushiriki nao, na kilichonipelekea kuuliza swali hili ni jibu la swali la Sheikh Taqiuddin an-Nabhani (Mwenyezi Mungu amrehemu) ambapo aliruhusu jambo hilo, hivyo nakuombeni ufafanuzi wa jambo hili. Ambatanisho ni jibu la swali la Sheikh Taqi.
Jibu:
Wa Alaykum Assalam Warahmatullahi Wabarakatuh
Tumeshajibu swali hili huko nyuma, na hili hapa ndilo jibu:
(Ndugu mpendwa,
Wa Alaykum Assalam Warahmatullahi Wabarakatuh
Kuhusu swali lako la kuwapongeza Watu wa Kitabu (Ahl al-Kitab) katika sikukuu zao, kabla sijaibu nitakutajia baadhi ya matoleo yaliyopita yanayohusiana na jambo hili:
[1- Ilitolewa hapo awali tarehe 30/01/1970: (- Ni nini hukumu ya kuwatembelea Wakristo katika furaha zao na sikukuu zao, kuwaugua wagonjwa wao, na kufuata mazishi yao? Na Mwislamu afanye nini akiwatembelea? Na nini uhusiano wa jambo hili na hadith tukufu "Msianze kuwasalimia Mayahudi na Wakristo... Hadith"?
Jibu: Imethibiti kutoka kwa Mtume ﷺ kwamba alimtembelea Myahudi aliyekuwa mgonjwa, na imethibiti kwamba alisimama kwa ajili ya jeneza la Myahudi, na imethibiti kwamba yeye (rehema na amani ziwe juu yake) aliusia kuwatendea wema raia wasio Waislamu (Dhimmis). Haya yote na mfano wake ni dalili ya kuruhusiwa kuwatembelea Wakristo katika furaha zao na sikukuu zao, kuwaugua wagonjwa wao, kufuata mazishi yao, kuwafariji na mambo kama hayo. Ama hadith inayosema msiwaanze kuwasalimia, hiyo inahusu salamu pindi unapokutana nao njiani, na ni nukuu mahususi kuhusu salamu (As-Salam), hivyo haijumuishi mambo mengine. 23 Dhul-Qi'dah 1389 - 30/01/1970)
2- Kisha ikatoa tarehe 17/07/1976: (- Je, inaruhusiwa kuwapongeza Wakristo na Mayahudi katika furaha zao?
Jibu: Inaruhusiwa kuwapongeza Wakristo kwa sababu ni wema (birr), na jambo hilo linajuzu. 17/07/1976)
3- Vilevile ilitolewa tarehe 16/01/2010:
(Inaruhusiwa kuwapongeza Watu wa Kitabu katika sikukuu zao. Ama kusema "na kwenu pia" (wa lakum), ni kana kwamba umeilinganisha na ilivyopokelewa katika hadith kwa kusema "wa alaykum" wanaposema Assalamu Alaykum...
Lakini hili ni tofauti na lile, kwani kilichopokelewa katika hadith ni jibu la kauli yao "As-Samu Alaykum" na As-Sam maana yake ni kifo. Nukuu ya hadith katika Bukhari na Muslim kupitia kwa Mama wa Waumini Aisha (r.a) amesema: Kundi la Mayahudi liliingia kwa Mtume ﷺ wakasema: "As-Samu Alaykum" (Kifo kiwe juu yenu). Aisha akasema: Nikaelewa (walichosema) nikasema: "Na kifo kiwe juu yenu na laana pia". Akasema: Mtume ﷺ akasema: "Subiri ewe Aisha, hakika Mwenyezi Mungu anapenda upole katika mambo yote." Nikasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, kwani hukusikia walichosema? Mtume ﷺ akasema: "Nimeshasema: Na juu yenu pia (wa alaykum)." Na katika riwaya nyingine ya Muslim kupitia Ibn Umar (r.a) amesema: Mtume ﷺ amesema: "Hakika Mayahudi wanapowasalimia, mmoja wao husema: As-Samu Alaykum, basi sema: Alayka (na juu yako pia)." Na hivyo, unaona kwamba hili lilikuwa kwa sababu walikuwa wakisema "As-Samu Alaykum".
Ama wakisema neno zuri katika kutupongeza, tunalikubali kutoka kwao. Ikiwa watasema sikukuu yenu iwe na baraka, tunawajibu kwa jibu zuri na sahihi, kama kusema asante kwa pongezi zenu, karibuni, au majibu kama hayo ambayo hayakiuki Sharia. 16/01/2010) Mwisho.
Kutokana na hayo inabainika yafuatayo:
1- Inaruhusiwa kuwapongeza raia wasio Waislamu (Ahl al-Dhimma) katika sikukuu zao kwa maneno mazuri yasiyokiuka Sharia. Hatusifii sikukuu yao, yaani hatusemi "sikukuu yenu ni yenye baraka" (Idkum Mubarak) au mfano wa hayo.
2- Lakini hili ni kwa wale tu ambao masharti yafuatayo yanapatikana kwao:
a- Wawe miongoni mwa Ahl al-Dhimma wanaoishi miongoni mwa Waislamu katika nchi za Kiislamu na mkataba wa Dhimmah unawahusu kwa kutowafanyia hiyana Waislamu...
b- Wasiwe wameturiga katika dini au kusaidiana katika kututoa... kama ilivyokuja katika aya tukufu...
- Ama dalili ya kuwa kwao ni Ahl al-Dhimma, jibu la kwanza la tarehe 30/01/1970 linabainisha hilo: (Imethibiti kutoka kwa Mtume ﷺ kwamba alimtembelea Myahudi aliyekuwa mgonjwa, na imethibiti kwamba alisimama kwa ajili ya jeneza la Myahudi, na imethibiti kwamba yeye (rehema na amani ziwe juu yake) aliusia kuwatendea wema raia wasio Waislamu (Dhimmis). Haya yote na mfano wake ni dalili ya kuruhusiwa kuwatembelea Wakristo katika furaha zao na sikukuu zao, kuwaugua wagonjwa wao, kufuata mazishi yao, kuwafariji na mambo kama hayo...) Na hii inapelekea kuwa makusudio ni Ahl al-Dhimma kwani walikuwa wakiishi miongoni mwa Waislamu chini ya ulinzi wao. Mtume ﷺ aliusia kuhusu raia wasio Waislamu (Dhimmis), na jeneza la Myahudi lilikuwa likipita katikati yao. Pia Myahudi ambaye Mtume ﷺ alimtembelea alipokuwa mgonjwa alikuwa akimtumikia Mtume ﷺ kama ilivyokuja katika hadith ya Bukhari 1356 kutoka kwa Anas (r.a):
أَنَّ غُلَاماً مِنَ اليَهُودِ كَانَ يَخدُمُ النَّبِيَّ ﷺ فَمَرِضَ، فَأَتَاهُ النَّبِيُّ ﷺ يَعُودُهُ، فَقَعَدَ عِندَ رَأسِهِ، فَقَالَ: أَسلِم. فَنَظَرَ إِلَى أَبِيهِ وَهُوَ عِندَ رَأسِهِ، فَقَالَ لَه: أَطِع أَبَا القَاسِمِ ﷺ. فَأَسلَمَ، فَخَرَجَ النَّبِيُّ ﷺ وَهُوَ يَقُولُ: الحَمدُ لِلَّهِ الذِي أَنقَذَهُ مِنَ النَّارِ
"Kwamba kijana mmoja katika Mayahudi alikuwa akimtumikia Mtume ﷺ kisha akaugua, Mtume ﷺ akamtembelea kumjulia hali, akaketi kichwani kwake na kumwambia: 'Silimu'. (Kijana) akamtazama baba yake naye yuko kichwani kwake, (baba) akamwambia: 'Mtii Abul Qasim ﷺ'. Basi akasilimu. Mtume ﷺ akatoka huku akisema: 'Shukrani zote ni za Mwenyezi Mungu ambaye amemwokoa na moto'."
Haya yote yanaonyesha kwamba yaliyotajwa katika jibu la kwanza yanawahusu mahususi Ahl al-Dhimma.
- Ama dalili ya kuwa wasitupige vita katika dini wala kusaidiana katika kututoa... n.k., ni aya tukufu:
لَا يَنْهَاكُمُ اللَّهُ عَنِ الَّذِينَ لَمْ يُقَاتِلُوكُمْ فِي الدِّينِ وَلَمْ يُخْرِجُوكُمْ مِنْ دِيَارِكُمْ أَنْ تَبَرُّوهُمْ وَتُقْسِطُوا إِلَيْهِمْ إِنَّ اللَّهَ يُحِبُّ الْمُقْسِطِينَ * إِنَّمَا يَنْهَاكُمُ اللَّهُ عَنِ الَّذِينَ قَاتَلُوكُمْ فِي الدِّينِ وَأَخْرَجُوكُمْ مِنْ دِيَارِكُمْ وَظَاهَرُوا عَلَى إِخْرَاجِكُمْ أَنْ تَوَلَّوْهُمْ وَمَنْ يَتَوَلَّهُمْ فَأُولَئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ
"Mwenyezi Mungu hakatazi kuwafanyia wema na uadilifu wale ambao hawajakupigeni vita katika dini, wala hawajakutoeni katika nchi zenu. Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao uadilifu. Mwenyezi Mungu anakatazeni tu kufanya urafiki na wale waliokupigeni vita katika dini, na wakakutoeni katika nchi zenu, na wakasaidia katika kutolewa kwenu. Na wanaowafanya hao kuwa marafiki, basi hao ndio madhalimu." (QS. Al-Mumtahanah [60]: 8-9)
Ibn Kathir anasema kuhusu sababu ya kushuka kwa aya hii tukufu: (Na kauli yake Taala: {Mwenyezi Mungu hakatazi kuwafanyia wema...} yaani hawakatazi kuwafanyia wema makafiri ambao hawajakupigeni vita katika dini, kama wanawake na walio dhaifu miongoni mwao, {kuwafanyia wema} yaani: kuwatendea ihsani {na uadilifu} yaani: kuwa na usawa {Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao uadilifu}... Na Imam Ahmad amesema: Aarem ametuhadithia, Abdullah bin Mubarak ametuhadithia, Mus'ab bin Thabit ametuhadithia, Amir bin Abdullah bin Zubair ametuhadithia, kutoka kwa baba yake amesema: Qutaylah alikuja kwa binti yake Asmaa bint Abi Bakr akiwa na zawadi: mchuzi, jibini na samli, naye alikuwa mshirikina. Asmaa akakataa kupokea zawadi yake na kumwingiza nyumbani kwake. Aisha akamuuliza Mtume ﷺ, ndipo Mwenyezi Mungu Aliyetukuka akateremsha: {Mwenyezi Mungu hakatazi kuwafanyia wema...} mpaka mwisho wa aya, akamuamuru apokee zawadi yake na amwingize nyumbani kwake.
Na kauli yake {Mwenyezi Mungu anakatazeni tu kufanya urafiki na wale waliokupigeni vita...} yaani: Hakika anakatazeni tu kufanya urafiki na hawa walioonyesha uadui kwenu, wakakupigeni vita na kukutoeni, na wakasaidiana katika kutolewa kwenu. Mwenyezi Mungu anakatazeni kufanya nao urafiki na anakuamuruni kuwa na uadui nao. Kisha akasisitiza onyo la kufanya nao urafiki akasema: {Na wanaowafanya hao kuwa marafiki, basi hao ndio madhalimu} kama kauli yake:
يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لا تَتَّخِذُوا الْيَهُودَ وَالنَّصَارَى أَوْلِيَاءَ بَعْضُهُمْ أَوْلِيَاءُ بَعْضٍ وَمَنْ يَتَوَلَّهُمْ مِنْكُمْ فَإِنَّهُ مِنْهُمْ إِنَّ اللَّهَ لا يَهْدِي الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ
"Enyi mlioamini! Msiwafanye Mayahudi na Wakristo kuwa ni marafiki; wao ni marafiki wao kwa wao. Na miongoni mwenu atakayewafanya marafiki, basi huyo ni mmoja wao. Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu madhalimu." (QS. Al-Ma'idah [5]: 51))
Hivyo basi, inaruhusiwa kuwapongeza Ahl al-Dhimma katika sikukuu zao kwa maneno yasiyokiuka Sharia, na inaruhusiwa vilevile kuwapongeza makafiri wasio Ahl al-Dhimma kwa maneno yasiyokiuka Sharia. Pongezi ni katika wema (birr), lakini hili lina sharti la kuwa aya tukufu iwe inawahusu, yaani wasiwe wameturiga katika dini na kututoa katika nchi zetu na kusaidiana katika kututoa: {Mwenyezi Mungu hakatazi kuwafanyia wema na uadilifu wale ambao hawajakupigeni vita katika dini, wala hawajakutoeni katika nchi zenu...} na hao ni wachache sana kwa sasa...
Natumai hili linatosheleza, na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi zaidi na Mwenye hekima zaidi.
Ndugu yenu Ata bin Khalil Abu al-Rashtah
10 Jumada al-Akhirah 1443 H Inayoambatana na 13/01/2022 M
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Ameer (Mwenyezi Mungu amlinde) kwenye Facebook
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Ameer (Mwenyezi Mungu amlinde) kwenye Tovuti