Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Zaka ya Mifugo

September 29, 2018
3954

(Mfululizo wa majibu ya mwanachuoni mtukufu Ata bin Khalil Abu al-Rashtah, Amir wa Hizb ut Tahrir, kwa maswali ya wafuasi wa ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi")

Jibu la Swali Zaka ya Mifugo Kwa Ali Al-Saidi

Swali: Amir wetu mtukufu, Assalamu Alaikum Warahmatullahi Wabarakatuh, Mwenyezi Mungu ayaongoze hatua zenu kuelekea kheri na atuletee ushindi na tamkini kupitia mikono yenu.

Imetajwa katika kitabu cha Al-Amwal katika Dola ya Khilafah ukurasa wa 153, katika mlango wa Zaka ya Mifugo aina ya ng'ombe, maandishi yasemayo: "Na Zaka ni lazima kwa ng'ombe wa as-sa’imah ambao hujilisha (malishoni) sehemu kubwa ya mwaka," na imetajwa pia katika Zaka ya mbuzi/kondoo katika ukurasa wa 155 maandishi yasemayo: "Na Zaka ni lazima kwa mbuzi/kondoo wa as-sa’imah ambao hujilisha zaidi ya mwaka (mzima) ikiwa umepita mwaka kamili tangu kufikia nisabu."

Swali ni: Je, hakuna Zaka kwa mbuzi/kondoo na ng'ombe ambao si sa’imah na ambao hulishwa (na mmiliki wao ghalani) sehemu kubwa ya mwaka? Na ikiwa wana Zaka, ni kiasi gani?

Na swali jingine ikiwa mtafanya ihsani kujibu: Kwa nini imetajwa Zaka ya mifugo kwa ng'ombe, mbuzi/kondoo, na ngamia pekee na haikutajwa Zaka ya ndege, hasa kuku ambao sasa hufugwa kwa maelfu ndani ya mabanda ya kisasa, au je, wao ni sehemu ya urudh at-tijarah (bidhaa za biashara)?

Mwenyezi Mungu awabariki kwa uvumilivu wenu, na Assalamu Alaikum Warahmatullahi Wabarakatuh.

Jibu: Walaikum Assalam Warahmatullahi Wabarakatuh,

1- Ndiyo, hakuna Zaka kwa mbuzi/kondoo na ng'ombe wanaolishwa (ghalani), na hiyo ni kwa sababu السَّوم ni sifa inayofahamisha illiyah (sababu ya hukumu), na mafhum as-sifah ni kuunganisha hukumu na sifa miongoni mwa sifa za dhati ya kitu, na hii inaashiria kukanusha hukumu kwa dhati hiyo wakati sifa hiyo inapokosekana. Sharti yake ni kwamba sifa hiyo iwe sifa inayofahamisha maana (وصفاً مفهماً), yaani miongoni mwa yanayofaidisha illiyah. Ikiwa si sifa inayofahamisha maana, basi haina mafhum... Na ninarudia kwamba sharti la mafhum as-sifah ni iwe sifa inayofahamisha maana, kama kauli yake ﷺ:

فِي صَدَقَةِ الغَنَمِ فِي سَائِمَتِهَا

"...katika sadaka (zaka) ya mbuzi/kondoo katika wale walio sa’imah (wanaojilisha)..." (Imepokelewa na Al-Bukhari).

Kwani mbuzi/kondoo ni jina la dhati, na ina sifa mbili: السَّوم (kujilisha malishoni) na العلف (kulishwa ghalani). Na ameweka ulazima wa Zaka kwenye sifa ya السَّوم, jambo ambalo linaashiria kutokuwepo kwa ulazima (wa Zaka) kwa wale wanaolishwa.

2- Kuhusu swali jingine, kwa nini Zaka iko kwenye Al-An'am (ngamia, ng'ombe, na mbuzi/kondoo) na si wanyama wengine kama ndege na kuku... n.k., hiyo ni kwa sababu nass (maandiko) yamekuja kuhusu hawa Al-An'am, hivyo yanafuatwa na kuishia hapo... Maandiko yamekuja kuhusu hawa watatu:

  • Abu Dharr amepokea kutoka kwa Mtume ﷺ akisema:

مَا مِنْ صَاحِبِ إِبِلٍ، وَلَا بَقَرٍ، وَلَا غَنَمٍ، لَا يُؤَدِّي زَكَاتَهَا، إِلَّا جَاءَتْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ، أَعْظَمَ مَا كَانَتْ، وَأَسْمَنَ، تَنْطَحُهُ بِقَرُونِهَا، وَتَطَؤُهُ بِأَخْفَافِهَا

"Hapana mmiliki wa ngamia, wala ng'ombe, wala mbuzi/kondoo, asiyetoa zaka yake, isipokuwa watakuja Siku ya Kiyama, wakiwa wakubwa zaidi na wanono zaidi kuliko walivyokuwa, wakimpiga kwa pembe zao na kumkanyaga kwa kwato zao." (Muttafaqun 'Alayh).

  • Abu Dawood amepokea kutoka kwa Abu Bakr kutoka kwa Mtume ﷺ katika hadithi ndefu akisema:

وَفِي سَائِمَةِ الْغَنَمِ إِذَا كَانَتْ أَرْبَعِينَ، فَفِيهَا شَاةٌ

"...na katika mbuzi/kondoo wa sa'imah wakiwa arobaini, basi ndani yake mna mbuzi/kondoo mmoja..."

  • Na kutoka kwa Ali (ra) amesema:

لَيْسَ فِي الْبَقَرِ الْعَواملِ صَدَقَةٌ

"Hakuna sadaka (zaka) kwa ng'ombe wanaofanyishwa kazi." (Imepokelewa na Abu Ubaid na Al-Bayhaqi).

  • Na kutoka kwa Amr bin Dinar kwamba imemfikia kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ amesema:

لَيْسَ فِي الثَّوْرِ الْمُثِيرَةِ صَدَقَةٌ

"Hakuna sadaka (zaka) kwa fahali anayelima." (Imepokelewa na Abu Ubaid), na imepokelewa pia kutoka kwa Jabir bin Abdullah amesema: "Hakuna sadaka kwa muthirah", na al-muthirah ni yule anayegeuza ardhi, yaani anayelima.

  • Al-Hakim ametoa katika Al-Mustadrak 'ala al-Sahihayn kutoka kwa Bahz bin Hakim, kutoka kwa baba yake, kutoka kwa babu yake, amesema: Nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ akisema:

فِي كُلِّ إِبِلٍ سَائِمَةٍ فِي كُلِّ أَرْبَعِينَ ابْنُ لَبُونٍ

"Katika kila ngamia walio sa'imah, kwa kila arobaini kuna binti labun (ngamia wa miaka miwili)..." Al-Hakim amesema hadithi hii ina isnadi sahihi. "As-Sa’imah: Ni wanyama wanaojilisha nyikani na malishoni na hawalishwi (ghalani)."

3- Hivyo basi, hawa Al-An'am watatu ni lazima watolewe Zaka, na kama ilivyobainishwa hapo juu, Zaka iko kwa sa’imah, yaani wanaojilisha zaidi ya mwaka mzima. Na haikuja nass yoyote kuhusu Zaka ya aina yoyote ya wanyama wengine au ndege au wanyama wa majini, hivyo inaishia kwenye nass iliyokuja kuhusu Zaka ya Al-An'am kulingana na dhati zao. Ama ikiwa wanyama hao ni kwa ajili ya biashara, basi Zaka ni lazima kwao kulingana na Zaka ya urudh at-tijarah (bidhaa za biashara) kama ilivyofafanuliwa katika mlango wake kwenye kitabu cha Al-Amwal.

4- Muhtasari ni kwamba hakuna Zaka katika dhati ya wanyama isipokuwa Al-An'am: mbuzi/kondoo, ng'ombe, na ngamia. Ama katika urudh at-tijarah, basi kila mnyama hutolewa Zaka ikiwa ni wa biashara, yaani kwa ajili ya kuuza na kununua, kwa sababu ya kuwepo kwa maandiko kuhusu Zaka ya kila kinachowekwa kwa ajili ya biashara bila kujali aina yake, iwe ni nafaka, kitambaa, au mnyama... n.k. Miongoni mwa maandiko yaliyokuja kuhusu urudh at-tijarah:

  • Kutoka kwa Samurah bin Jundub amesema: "Baada ya hayo, hakika Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ alikuwa akituamrisha tutoe sadaka (zaka) kutoka kwa kile tulichokiandaa kwa ajili ya kuuza." (Imepokelewa na Abu Dawood).

  • Na kutoka kwa Abu Dharr kutoka kwa Mtume ﷺ amesema:

وَفِي الْبَزِّ صَدَقَتُهُ

"Na katika al-bazz mna sadaka (zaka) yake." (Imepokelewa na Al-Daraqutni na Al-Bayhaqi). Na al-bazz ni nguo na vitambaa vinavyofanyiwa biashara.

  • Na Abu Ubaid amepokea kutoka kwa Abu Amrah bin Hammas kutoka kwa baba yake amesema: "Umar bin al-Khattab alinipita, akasema: Ewe Hammas, toa zaka ya mali yako. Nikasema: Sina mali isipokuwa podo za mishale na ngozi. Akasema: Zikadirie thamani yake, kisha utoe zaka yake"...

Natumai hili lina utoshelevu, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi zaidi na Mwenye Hekima zaidi.

Ndugu yenu, Ata bin Khalil Abu al-Rashtah

19 Muharram Al-Haram 1439 H Sawiya na 29/09/2018 M

Link ya jibu kutoka kwa ukurasa wa Amir (Mwenyezi Mungu amhifadhi) kwenye Facebook Link ya jibu kutoka kwa ukurasa wa Amir (Mwenyezi Mungu amhifadhi) kwenye Google Plus

Share Article

Share this article with your network