Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali

June 20, 2012
1284

Swali:

Mnamo tarehe 1/6/2012, Waziri wa Ulinzi wa Marekani Leon Panetta alitangaza katika mkutano wa usalama nchini Singapore: kwamba "Marekani itahifadhi meli sita za kubebea ndege katika eneo la Asia-Pasifiki na itahamisha 60% ya meli zake za kivita kwenda eneo hilo katika miaka ijayo hadi mwaka 2020. Alieleza kuwa uhamishaji wa vikosi vya majini vya Marekani unakuja katika muktadha wa kutekeleza mkakati mpya wa Marekani unaolenga kupandisha kiwango cha uwepo wa kijeshi wa Marekani katika eneo la Asia-Pasifiki". Je, ni nini sababu ya Marekani kuhamisha sehemu kubwa ya zana zake za kijeshi za baharini kwenda eneo la Asia-Pasifiki? Je, Marekani imeanza kuichukulia Uchina kama tishio kubwa kwa sasa au katika miaka ijayo? Na ni lini Uchina inaweza kuchukua hatua ya kuweka udhibiti wake katika eneo hilo?

Jibu:

Ili kujibu hilo, tunataja yafuatayo:

1- Eneo la Asia-Pasifiki linajumuisha nchi zenye umuhimu mkubwa:

  • Kama vile Japani, Uchina, Taiwan, Korea Kaskazini na Kusini, na kati ya nchi hizi kuna mzozo juu ya suala la mamlaka katika Bahari ya Mashariki ya China na mzozo juu ya baadhi ya visiwa vilivyomo, pamoja na uhuru wa upitishaji wa meli na uvuvi.

  • Na kama vile Ufilipino, Vietnam, Cambodia, Thailand, Brunei, Malaysia, Singapore na Indonesia, na kati ya nchi hizi kuna mzozo juu ya suala la mamlaka katika Bahari ya Kusini ya China na mzozo juu ya baadhi ya visiwa vilivyomo, pamoja na Mlango-bahari wa Malacca na uhuru wa upitishaji wa meli na uvuvi.

  • Kisha eneo hilo linachukuliwa kuwa ni mwendelezo wa Bahari ya Hindi ambayo katika pwani zake za kaskazini kuna Burma, Bangladesh, na India hadi kufika Pakistan ambayo iko karibu na Bahari ya Arabia ambayo ni mwendelezo wa Bahari ya Hindi, na kisha inakuja Ghuba ya Oman ili kufika eneo la Ghuba na kuelekea kusini hadi Ghuba ya Aden kisha Bab-el-Mandeb ili kufika Bahari Nyekundu ambayo inapitia kuelekea Bahari ya Mediterania.

  • Pia katika eneo la Asia-Pasifiki, mbali na pwani za kaskazini za Bahari ya Hindi, kuna msongamano mkubwa zaidi wa watu duniani na msongamano mkubwa zaidi wa Waislamu; katika eneo hili kuna takriban nusu ya watu wote duniani na nusu ya idadi ya Waislamu.

2- Njia za baharini zinachukuliwa kuwa muhimu zaidi kuliko njia za nchi kavu kwa sababu kiasi kikubwa cha mizigo kinaweza kubebwa na meli kwa gharama nafuu na urahisi wa meli kusafiri mbali na vikwazo vya mipakani vya nchi, isipokuwa wakati wa kupita kwenye milango-bahari au njia za baharini ambazo ziko chini ya uangalizi wa nchi zinazozisimamia. Hadi leo, 90% ya bidhaa bado zinasafirishwa kupitia njia za baharini kwa kutumia meli licha ya maendeleo ya njia za nchi kavu na utengenezaji wa malori makubwa, pamoja na maendeleo katika usafiri wa anga lakini ni ghali na hauwezi kubeba kiasi kikubwa kama kile kinachobebwa na meli. Aidha, 65% ya mafuta yanasafirishwa kupitia baharini kwa kutumia meli licha ya maendeleo katika ujenzi wa mabomba ya mafuta. Kwa hiyo, Bahari ya Pasifiki ina umuhimu mkubwa ambapo inaenea hadi Bahari ya Hindi ambapo 70% ya usambazaji wa mafuta na gesi kutoka eneo la Ghuba hupita kuelekea nchi hizo, na mahitaji ya eneo hili, hasa Uchina na India, kwa mafuta yataongezeka maradufu katika muongo ujao. Kuna Mlango-bahari wa Malacca ambao unachukuliwa kuwa njia muhimu kati ya bahari hizo mbili na una urefu wa kilomita 800 kati ya rasi ya Malaysia na kisiwa cha Sumatra cha Indonesia, na takriban 40% ya bidhaa za ulimwengu hupita hapo, pamoja na nusu ya biashara ya mafuta na gesi duniani. Mlango-bahari huu ni muhimu kwa Uchina na India kwa ajili ya kupitisha bidhaa mashariki na magharibi. Hivyo eneo hili lina umuhimu mkubwa kutokana na kuwepo kwa njia hizi za baharini...

3- Kisha eneo hili ni muhimu kimkakati; Uchina inafanya kazi kuleta utawala au udhibiti wake katika eneo hili kwa sababu inalichukulia kama eneo lake kihistoria na kijiografia, mbali na umuhimu wake wa kimkakati na kiuchumi kwake. Uchina ni nchi kubwa kieneo na inafanya kazi ili kuwa na ushawishi katika eneo hili, lakini haijaweza kuweka udhibiti wake juu yake. Bado udhibiti na utawala wa Marekani ndio mkubwa zaidi na wenye ushawishi mkubwa zaidi. Marekani ilikuwa ikijali eneo hili wakati wa kipindi cha Vita Baridi kutokana na kuwepo kwa tishio kutoka kwa Umoja wa Kisovieti wakati huo, kwani Urusi ina mipaka ya baharini kaskazini mwa Bahari ya Pasifiki. Marekani katika kipindi hicho ilikuwa na zaidi ya meli za kivita 600, na wakati Vita Baridi vilipoisha kwa kuanguka kwa ukomunisti na kusambaratika kwa Umoja wa Kisovieti na kutoweka kwa hatari yake, Marekani ilipunguza idadi ya meli zake za kivita hadi kufikia chini ya nusu, ikifikia meli 279, na idadi hiyo ilitulia mwaka 2008 ikifikia meli za kivita 285. Ikaishia na idadi hii kwani hakuwa na mshindani tena wala tishio kwa uwepo wake katika eneo hili.

Hii ni mbali na ukweli kwamba Marekani ina uwepo wa kijeshi wa kudumu katika kambi za kijeshi nchini Japani na Korea Kusini zilizoko kwenye pwani ya Bahari ya Mashariki ya China, na pia ina uwepo kama huo nchini Ufilipino iliyoko kwenye pwani ya Bahari ya Kusini ya China. Marekani ina takriban robo milioni ya wanajeshi katika eneo hilo... na imekuwa na uwepo wa kijeshi wa kudumu katika eneo hilo tangu miaka ya hamsini ya karne iliyopita.

4- Katika hali ya kuyumba kwa nafasi ya Marekani ulimwenguni kufuatia vipigo ilivyopata nchini Iraq na Afghanistan mikononi mwa Waislamu na kufuatia mgogoro wa kifedha uliolipuka mwaka 2008, Uchina ilianza kutathmini hali hiyo na kufanya kazi ya kuitumia ili kuongeza nguvu zake hadi iweke ushawishi wake katika eneo lake ikiwa Marekani itaanguka kabisa au itakabiliwa na mtikisiko mkubwa zaidi kuliko ule uliotokea kiasi kwamba isiweze kudumisha ushawishi wake katika eneo hilo, au ikiwa Waislamu wataifukuza Marekani kutoka eneo hilo.

Licha ya kwamba Marekani inatambua kuwa Uchina si nchi kubwa ya kimataifa, hivyo haifanyi kazi ya kuiondoa Marekani kwenye nafasi ya nchi ya kwanza duniani, lakini ni nchi kubwa kieneo, yaani katika eneo la Asia-Pasifiki ambalo Uchina inaliona kama eneo lake na ni muhimu kwake kiuchumi na kimkakati. Kwa hiyo Uchina inafanya kazi ili iwe na mamlaka katika Bahari ya Mashariki ya China na ikifanikiwa katika hilo, basi itaifanya Japani na Korea Kusini kuwa chini ya rehema au utawala wake, mbali na Korea Kaskazini ambayo tayari ina ushawishi juu yake. Uchina pia inafanya kazi ili iwe na mamlaka juu ya Bahari ya Kusini ya China ili kuifanya Ufilipino, Vietnam, Cambodia, Laos, Brunei, Malaysia, Singapore na Indonesia kuwa chini ya ushawishi au utawala wake na kisha kudhibiti Mlango-bahari wa Malacca ambao unachukuliwa kuwa mshipa wa maisha kwake. Na ikiwa Uchina itadhibiti eneo hili au kuweka ushawishi wake au kulifanya liwe chini ya utawala wake, basi inaweza kuathiri eneo la Bahari ya Hindi, na kutishia ushawishi wa Marekani katika eneo hilo kwa namna ya hatari. Na hili ni suala la kifo na kupona kwa Marekani ambalo halitaruhusu litokee kamwe haijalishi litagharimu gharama kiasi gani.

5- Marekani inatoa umuhimu katika kulinda ardhi yake kutoka pande mbili za Bahari ya Atlantiki na Bahari ya Pasifiki zinazoizunguka. Na kwa kuwa kwa sasa hakuna tishio lolote la kutajwa dhidi ya Marekani katika Atlantiki kwa sababu nchi za Ulaya hazifanyi kazi yoyote nzito inayoshindana na Marekani katika Bahari ya Atlantiki au upande wa pili wa Atlantiki magharibi, yaani Amerika Kusini, na Marekani haitarajii katika muda unaoonekana ushindani wa kweli na mzito kutoka Ulaya katika Atlantiki au kwingineko, ndiyo maana Marekani kwa sasa inatoa umuhimu katika maeneo mengine ambayo ni Bahari ya Pasifiki na Bahari ya Hindi na maeneo yanayofuata ya Bahari ya Arabia, Ghuba na Bab-el-Mandeb... na kwa ajili hiyo imepunguza nguvu zake katika Atlantiki kwa ajili ya nguvu zake katika Bahari ya Pasifiki kama alivyotaja Panetta katika maelezo kwamba 60% ya nguvu ya majini itakuwa katika eneo la Asia-Pasifiki ifikapo mwaka 2020 na hiyo inajumuisha meli 6 za kubebea ndege na sehemu kubwa ya meli za kivita (cruisers), waharibu (destroyers), meli za mapigano na nyambizi za Marekani. Ameashiria mizozo kati ya nchi za eneo hilo na Uchina akisema: "msimamo wa Marekani uko wazi, tunatoa wito wa kujizuia na utatuzi wa kidiplomasia, tunapinga uchochezi, kulazimisha na matumizi ya nguvu". Na alidai kuwa "nchi yake haiegemei upande mmoja dhidi ya mwingine" (Shirika la habari la Marekani UPI 2/6/2012) na shirika hili liliashiria kuwa: "Rais wa Marekani Barack Obama alisema mnamo mwezi Novemba; kwamba eneo la Asia-Pasifiki ni kipaumbele kikubwa kwa Marekani". Shirika hili lilitaja kuwa "lengo la Marekani katika eneo hili linakuja kufuatia kukua kwa Uchina na India kama nguvu za kiuchumi duniani na baada ya Marekani kujiondoa Iraq na kukaribia kujiondoa kwa vikosi vya Marekani kutoka Afghanistan".

Kisha kuongeza kwa Marekani uwepo wa kijeshi wa baharini katika eneo la Asia-Pasifiki kunaiwezesha kuongeza kiwango cha mazoezi na manuva ya kivita inayoyafanya huko katika miaka ijayo. Pia Marekani inapanga kuongeza ziara za meli za Marekani katika maeneo mapana zaidi ya Bahari ya Pasifiki hadi kujumuisha Bahari ya Hindi. Imetajwa kuwa "vikosi vya jeshi la Marekani vilishiriki katika mwaka uliopita katika operesheni 172 za mazoezi na manuva ya kivita (katika eneo hili) zilizojumuisha nchi 24". (BBC 2/6/2012)

6- Mkakati wa kijeshi wa Marekani katika eneo la Asia-Pasifiki ambao ulitangazwa na Waziri wa Ulinzi wa Marekani ulikuja ndani ya mkakati mpya wa kijeshi wa Marekani uliotangazwa na Rais wa Marekani Obama mnamo tarehe 6/1/2012 ambao ulijikita katika misingi mikuu mitatu; wa kwanza: kupunguza idadi ya wanajeshi wa Marekani barani Ulaya, wa pili: kupunguza matumizi ya ulinzi huku ikidumisha ubora wa kiufundi, na wa tatu: kujikita katika eneo la Bahari ya Pasifiki ili kuepuka kukua kwa nguvu za Uchina huku ikitoa umuhimu kwa eneo la Mashariki ya Kati na Asia. Na kwa kuwa hakuna hatari wala tishio dhidi ya Marekani barani Ulaya, basi hakuna haja ya kuwepo kwa idadi kubwa ya wanajeshi wa Marekani huko ndani ya mpango wa kupunguza matumizi ya kijeshi, kwa sababu Marekani bado inateseka chini ya mzigo wa mgogoro wa kifedha na haijaweza kutoka humo, hivyo ilitegemea mpango wa kupunguza matumizi ya kijeshi katika miaka kumi ijayo kwa kiasi cha dola trilioni 1.2, na kuongeza vikosi vyake katika eneo la Asia-Pasifiki.

Hivyo basi, kuongezeka kwa vikosi vya majini vya Marekani katika eneo la Asia-Pasifiki kumelekezwa kimsingi dhidi ya Uchina na hatari yake inayotarajiwa dhidi ya ushawishi wa Marekani katika eneo hilo.

7- Lakini kuna jambo jingine linaloashiriwa na mienendo ya vikosi vya majini vya Marekani, na kusambaa kwa kambi zake katika Bahari ya Pasifiki kupitia Mlango-bahari wa Malacca kuelekea Bahari ya Hindi kisha Bahari ya Arabia, Ghuba na Bahari Nyekundu... yaani si tu kwenye pwani za Uchina na bahari zake... Jambo hili ni kile ambacho Marekani inakiweka katika mahesabu yake kutokana na kutarajia kuanza kwa nguvu ya Kiislamu katika eneo hilo "Dola ya Khilafah" jambo ambalo linaifanya Marekani kupiga mahesabu kwa nguvu ya Uchina iliyopo, na nguvu ya Dola ya Kiislamu inayotarajiwa... Kwa ajili hiyo, inatanua kambi zake na mienendo yake kando ya pwani za eneo la Kiislamu... Inaweka uwezekano wa mabadiliko yajayo katika miaka ijayo na katika muongo ujao wa kutokea kwa nguvu kubwa ya Kiislamu katika ulimwengu wa Kiislamu, hasa kwa kuwa nusu ya idadi ya Waislamu iko katika eneo la Asia-Pasifiki na kaskazini mwa Bahari ya Hindi, na ni mwendelezo wa maeneo ya Waislamu katika Ghuba, Mashariki ya Kati na Afrika, bali ni kina kikubwa cha kimkakati kwa Dola ya Kiislamu itakaposimama kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Na ni vyema kutaja kuwa Dola ya Kiislamu ilianza tangu karne zake za kwanza kufanya kazi ya kufika eneo hilo ili kueneza kheri katika pande zake hadi ikawa takriban eneo la Kiislamu, mpaka walipokuja wakoloni wa Magharibi na kuanza kupanda mbegu za shari humo ili waweze kulikoloni na kulidhibiti tangu karne tatu zilizopita ili kuvunja nguvu ya Waislamu kutoka Mashariki, wakati uleule walipokuwa wakianzisha vita vya kikoloni na njama dhidi ya Waislamu Magharibi, ili kuimaliza dola yao, Dola ya Khilafah, na nidhamu yake ya Kiislamu na yote hayo yaliwatimizia... Nao wanahofia kurejea kwake upya... Nayo inarejea kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, na kesho ni karibu kwa anayeisubiri.

Share Article

Share this article with your network