Mfululizo wa Majibu ya Mwanachuoni Mheshimiwa Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah, Amir wa Hizb ut-Tahrir, kwa Maswali ya Wageni wa Ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi"
Kwa: Fahed Zalloum
Swali:
Sheikh wetu mtukufu, Assalamu Alaikum Warahmatullahi Wabarakatuh,
Nini maana ya muujiza wa kisayansi katika Qur'ani Tukufu? Na je, ni kweli kwamba katika Qur'ani kuna muujiza wa kisayansi? Na je, jambo hili linatokana na mlango wa elimu (sayansi) au ni jambo jengine?
Allah akusaidie katika kila kheri.
Jibu:
Wa Alaikum Salaam Warahmatullahi Wabarakatuh,
Kuhusu muujiza wa kisayansi katika Qur'ani Tukufu, istilahi hii haikuwa inajulikana wakati wa Mtume (saw) wala wakati wa Maswahaba watukufu... Na ili kulifafanua jambo hili, hapa kuna maelezo yafuatayo:
1- Muujiza (Mu'jiza) ni "jambo linalotokea kinyume na mazoea (khaliful 'adah) mikononi mwa anayedai utume wakati wa kuwapa changamoto wanaopinga, kwa namna ambayo inawafanya wanaopinga washindwe kuleta mfano wake". Kwa hivyo, muujiza wa Mtume lazima uwe na mambo mawili: Kwanza uwe unakiuka mazoea, na pili uwe ni changamoto kwa wanaopinga kutoka kwa Mtume ambaye Allah (swt) amemuunga mkono kwa muujiza huo... Na muujiza wa Mtume Muhammad (saw) ambao aliutoa kama changamoto ili kuthibitisha utume wake ni Qur'ani Tukufu, na hakuwapa Waarabu changamoto ya kitu kingine ili kuthibitisha utume wake (saw):
قُلْ لَئِنِ اجْتَمَعَتِ الْإِنْسُ وَالْجِنُّ عَلَى أَنْ يَأْتُوا بِمِثْلِ هَذَا الْقُرْآنِ لَا يَأْتُونَ بِمِثْلِهِ وَلَوْ كَانَ بَعْضُهُمْ لِبَعْضٍ ظَهِيرًا
"Sema: Laiti wangeyakusanyika majini na watu ili walete mfano wa hii Qur'ani, wasingeweza kuleta mfano wake, hata kama baadhi yao wangesaidiana na baadhi nyingine." (QS Al-Isra [17]: 88)
أَمْ يَقُولُونَ افْتَرَاهُ قُلْ فَأْتُوا بِعَشْرِ سُوَرٍ مِثْلِهِ مُفْتَرَيَاتٍ وَادْعُوا مَنِ اسْتَطَعْتُمْ مِنْ دُونِ اللَّهِ إِنْ كُنْتُمْ صَادِقِينَ
"Au wanasema: Ameizua? Sema: Basi leteni Sura kumi zilizo zuliwa mfano wa hizi, na watakeni msaada mnao waweza asiyekuwa Mwenyezi Mungu, ikiwa mnasema kweli." (QS Hud [11]: 13)
وَإِنْ كُنْتُمْ فِي رَيْبٍ مِمَّا نَزَّلْنَا عَلَى عَبْدِنَا فَأْتُوا بِسُورَةٍ مِنْ مِثْلِهِ وَادْعُوا شُهَدَاءَكُمْ مِنْ دُونِ اللَّهِ إِنْ كُنْتُمْ صَادِقِينَ
"Na ikiwa mna shaka kwa hayo tuliyo mteremshia mja wetu, basi leteni sura moja mfano wake, na muwaite waidhinishaji wenu badala ya Mwenyezi Mungu, ikiwa mnasema kweli." (QS Al-Baqarah [2]: 23)
2- Muujiza (i'jaz) wa Qur'ani unadhihirika zaidi katika fashaa (fasaha) yake, ufasaha (balagha) wake, na kupanda kwake katika daraja ya kustaajabisha. Hilo linajitokeza katika mtindo (uslub) wa Qur'ani wa kutoa muujiza, kwani katika mtindo wake kuna uwazi, nguvu, na uzuri ambao wanadamu hawawezi kuufikia. Mtindo (uslub) ni maana zilizopangwa katika maneno yaliyoratibiwa, au ni namna ya kuelezea picha ya maana kwa kutumia misemo ya kilugha. Uwazi wa mtindo unakuwa kwa kudhihirika kwa maana zinazokusudiwa katika usemi uliotumika... Nguvu ya mtindo inakuwa kwa kuchagua maneno yanayobeba maana kulingana na uzito wake. Maana laini hutolewa kwa neno laini, na maana nzito hutolewa kwa neno zito, na maana inayochukiza hutolewa kwa neno linalochukiza na kadhalika... Ama uzuri wa mtindo huwa kwa kuchagua misemo iliyo safi kabisa na inayonasibiana zaidi na maana iliyokusudiwa, pamoja na maneno na maana zilizopo katika sentensi hiyo na sentensi nyinginezo...
3- Mwenye kuifuatilia Qur'ani atakuta mwinuko mkubwa wa mtindo wake katika uwazi, nguvu, na uzuri... Hivyo, utaikuta Qur'ani kuwa ni aina ya kipekee (taraz khas), na utaikuta ikiweka kila maana katika neno linaloistahili, na maneno yanayoizunguka, na maana zilizopo pamoja nayo, na hutaona jambo hilo likikosekana katika aya yake yoyote. Kwa hivyo, muujiza wake ulikuwa wazi katika mtindo wake kwa kuwa ni aina ya kipekee ya usemi usiofanana na maneno ya wanadamu, wala maneno ya wanadamu hayawezi kuufanana. Na kwa upande wa kuweka maana katika maneno na sentensi zinazozistahili, na kwa upande wa athari ya maneno yake kwenye masikio ya yule anayediriki ufasaha wake na kuzama katika maana zake, hunyenyekea mpaka anakaribia kuisujudia. Pia kwa wale wasiodiriki hilo, hunaswa na mdundo wa maneno haya katika mpangilio wa kitojiza (mu'jiz) ambao msikilizaji hunyenyekea kwa lazima hata kama hakudiriki maana zake. Kwa sababu hiyo, Qur'ani imekuwa muujiza na itaendelea kuwa muujiza mpaka kusimama kwa Saa.
4- Miongoni mwa dalili zinazoonesha kuwa upande wa muujiza (i'jaz) katika Qur'ani Tukufu ni mtindo wa kilugha ni mambo yafuatayo:
a- Katika kawaida ya miujiza ya utume ni kwamba Allah humpa Mtume muujiza anaoutumia kuwapa changamoto watu wake katika jambo ambalo watu wake ndio wenye ujuzi na uwezo mkubwa nalo, ili changamoto hiyo iwe na mashiko. Musa (as) aliwapa changamoto watu wa Firauni kwa uchawi nao walikuwa ni watu wenye ujuzi zaidi wa uchawi, na Isa (as) aliwapa changamoto watu wake kwa kuponya wagonjwa na kufufua wafu nao walikuwa ni watu wenye ujuzi zaidi wa utibu... Na kadhalika. Ama Muhammad (saw), watu wake hawakuwa watu wenye ujuzi zaidi katika sayansi asilia, wala uchawi, wala utibu, bali walikuwa mabingwa wa lugha, ambayo ndiyo iliyokuwa shughuli yao kuu na kazi yao ya kila siku kiasi kwamba walikuwa hawajui vizuri kitu kingine isipokuwa hiyo. Walikuwa wabunifu katika kuifinyanga na kuitoa kwa njia ya nathari za kila aina, na mashairi yenye mizani na bahari mbalimbali... Hivyo, ilikuwa ni muwafaka zaidi kwa changamoto yao kuwa upande wa muujiza katika maneno wanayoyajua, yaani katika lugha ya Kiarabu kwa upande wa mtindo (uslub)...
b- Qur'ani Tukufu iliwapa changamoto Waarabu walete sura moja ya mfano wake, kama sura ya Al-Kawthar kwa mfano, na bila shaka sura ya Al-Kawthar na sura nyinginezo fupi-fupi hazina kitu cha kisayansi au mfano wake, bali kinachozidi kudhihiri ndani yake ni mtindo wa kilugha wa ajabu ambao Waarabu walishindwa kuleta mfano wake...
c- Kitu kilichowafanya Waarabu wapigwe na mshangao wanapoisikia Qur'ani na kuonesha kushindwa kwao ni mtindo wake wa kilugha na si upande wa kisayansi uliotajwa ndani yake, na hili linajulikana kutoka kwao na limepokewa kwa mutawatir (tawatur)... Mpaka mmoja wao akasema kuhusu Qur'ani kuwa ni "uchawi wa ufasaha" (sihru-l bayan)...
d- Haikupokewa kutoka kwa Mtume (saw) kwamba aliweka upande wa changamoto kwa Waarabu kuwa ni masuala ya kisayansi yaliyotajwa ndani ya Qur'ani Tukufu, bali alikuwa akiwataka walete mfano wa Qur'ani katika mpangilio wake (nazm)...
e- Qur'ani Tukufu ilikuja na maana ambazo Waarabu walikuwa wakizijua wakati wa Mtume (saw), bali wakati mwingine ilitaja nukuu ya maneno kutokana na maneno yao kama nukuu ya maneno yao kama kauli ya Allah (swt):
وَقَالُوا لَنْ نُؤْمِنَ لَكَ حَتَّى تَفْجُرَ لَنَا مِنَ الْأَرْضِ يَنْبُوعًا * أَوْ تَكُونَ لَكَ جَنَّةٌ مِنْ نَخِيلٍ وَعِنَبٍ فَتُفَجِّرَ الْأَنْهَارَ خِلَالَهَا تَفْجِيرًا * أَوْ تُسْقِطَ السَّمَاءَ كَمَا زَعَمْتَ عَلَيْنَا كِسَفًا أَوْ تَأْتِيَ بِاللَّهِ وَالْمَلَائِكَةِ قَبِيلًا * أَوْ يَكُونَ لَكَ بَيْتٌ مِنْ زُخْرُفٍ أَوْ تَرْقَى فِي السَّمَاءِ وَلَنْ نُؤْمِنَ لِرُقِيِّكَ حَتَّى تُنَزِّلَ عَلَيْنَا كِتَابًا نَقْرَؤُهُ قُلْ سُبْحَانَ رَبِّي هَلْ كُنْتُ إِلَّا بَشَرًا رَسُولًا
"Na wakasema: Hatutakuamini mpaka ututimbulie chemchem katika ardhi. Au uwe na bustani ya mitende na mizabibu, na utupitishie mito katikati yake ikatitika. Au utuangushie mbingu vipande vipande kama ulivyo dhihaki; au utuletee Mwenyezi Mungu na Malaika uso kwa uso. Au uwe na nyumba ya dhahabu, au upande mbinguni, na wala hatutaamini kupanda kwako mpaka ututeremshie kitabu tukisome. Sema: Ametakasika Mola wangu Mlezi! Kwani mimi ni nani isipokuwa ni mwanadamu na Mtume?" (QS Al-Isra [17]: 90-93)
Hizi aya tukufu ni nukuu ya maneno ya Maquraishi, yaani maana iliyotajwa ndani yake ni miongoni mwa maana walizozisema Maquraishi, lakini Qur'ani imeisimulia kwetu kwa mtindo mzuri wa ajabu ambao watu wa Quraish walishindwa kuleta mfano wake ijapokuwa ni nukuu ya yale waliyoyasema wao wenyewe. Hili linadhihirisha kuwa muujiza uko katika mtindo wa kilugha wa Qur'ani Tukufu...
Hizi ni baadhi ya dalili zinazoonesha kuwa upande wa muujiza katika Qur'ani Tukufu umejiegemeza katika mtindo wa kilugha...
5- Wale wanaotumia istilahi ya "Muujiza wa Kisayansi" wanakusudia yale yaliyokuja ndani ya Qur'ani Tukufu ambayo yanaweza kuendana na nadharia au ukweli wa kisayansi, kama kauli ya Allah (swt):
وَلَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنْسَانَ مِنْ سُلَالَةٍ مِنْ طِينٍ * ثُمَّ جَعَلْنَاهُ نُطْفَةً فِي قَرَارٍ مَكِينٍ * ثُمَّ خَلَقْنَا النُّطْفَةَ عَلَقَةً فَخَلَقْنَا الْعَلَقَةَ مُضْغَةً فَخَلَقْنَا الْعَلَقَةَ مُضْغَةً فَخَلَقْنَا الْمُضْغَةَ عِظَامًا فَكَسَوْنَا الْعِظَامَ لَحْمًا ثُمَّ أَنْشَأْنَاهُ خَلْقًا آخَرَ فَتَبَارَكَ اللَّهُ أَحْسَنُ الْخَالِقِينَ
"Na kwa hakika tulimuumba mtu kutokana na asli ya udongo. Kisha tukamjaalia awe tone la mbegu ya uzazi katika makao yaliyo dhibitiwa. Kisha tukaiumba mbegu kuwa pande la damu, na tukaliumba pande la damu kuwa pande la nyama, kisha tukaliumba pande la nyama kuwa mifupa, na mifupa tukaivisha nyama. Kisha tukamfanya kiumbe mwengine. Basi ametukuka Mwenyezi Mungu Mbora wa waumbaji." (QS Al-Mu'minun [23]: 12-14)
Lakini aya hizi na mfano wake zilikuja kwa ajili ya kuonesha uwezo wa Allah (swt) na si kwa ajili ya kuthibitisha upande wowote wa kisayansi, kwa dalili kwamba walioambiwa aya hizi wakati wa Mtume (saw) hawakudiriki vipengele vya kisayansi vilivyomo ndani yake... Kadhalika, changamoto haikutolewa kwa aya hizo. Hivyo, si katika mlango wa muujiza ambao Mtume anawapa changamoto watu wake kwa ajili ya kuonesha ukweli wa utume wake.
6- Muhtasari ni kwamba muujiza katika Qur'ani Tukufu uko katika mtindo wake wa kilugha na ndio uliotumika kutoa changamoto. Qur'ani haikuwapa Waarabu changamoto ya kuthibitisha utume wa Mtume (saw) kwa muujiza wa kisayansi... Bali muujiza wa Mtume Muhammad (saw) ni Qur'ani Tukufu yenyewe, kwani Allah amewapa changamoto wanadamu na majini walete mfano wake na hawakuweza, wala hawataweza kufanya hivyo hata kama baadhi yao wangesaidiana na wengine:
قُلْ لَئِنِ اجْتَمَعَتِ الْإِنْسُ وَالْجِنُّ عَلَى أَنْ يَأْتُوا بِمِثْلِ هَذَا الْقُرْآنِ لَا يَأْتُونَ بِمِثْلِهِ وَلَوْ كَانَ بَعْضُهُمْ لِبَعْضٍ ظَهِيرًا
"Sema: Laiti wangeyakusanyika majini na watu ili walete mfano wa hii Qur'ani, wasingeweza kuleta mfano wake, hata kama baadhi yao wangesaidiana na baadhi nyingine." (QS Al-Isra [17]: 88)
- Hivyo basi, muujiza wa Mtume (saw) ambao aliutoa kama changamoto ya kuthibitisha utume wake ni Qur'ani Tukufu.
Ndugu yenu, Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah
08 Ramadhan 1438 H Mtawalia 03/06/2017 M
Kiungo cha jibu kutoka ukurasa wa Facebook wa Amir: Facebook
Kiungo cha jibu kutoka ukurasa wa Google Plus wa Amir: Google Plus
Kiungo cha jibu kutoka ukurasa wa Twitter wa Amir: Twitter
Kiungo cha jibu kutoka tovuti ya Amir: Web