Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Mazungumzo ya Marekani na Iran

May 12, 2025
3944

Jibu la Swali

Mazungumzo ya Marekani na Iran

Swali:

Sultanate ya Omani, ambayo inapatanisha katika mazungumzo ya Marekani na Iran, ilitangaza Alhamisi, (kuahirishwa kwa duru ya nne ya mazungumzo yaliyopangwa kufanyika Jumamosi katika mji mkuu wa Italia, Roma, "kwa sababu za kilojistiki", bila kutaja tarehe mpya. Asharq, 2025/5/1). Mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja kati ya Marekani na Iran yalianza mnamo Aprili 12, 2025, katika mji mkuu wa Omani, Muscat, kupitia upatanishi wa Waziri wa Mambo ya Nje wa Omani, Badr Al-Busaidi. Duru ya pili ilifanyika Aprili 19, 2025, katika ubalozi wa Sultanate ya Omani mjini Roma, pia kupitia upatanishi wa Waziri Al-Busaidi. Duru ya tatu ilifanyika Jumamosi, Aprili 26, 2025, nchini Omani, chini ya upatanishi huo huo wa Omani. Swali ni: Kwa nini Trump sasa anatafuta kusaini upya makubaliano ya kinyuklia na Iran, licha ya kwamba alijiondoa upande mmoja mnamo 2018 kutoka kwa makubaliano yaliyotiwa saini Julai 14, 2015? Kisha kwa nini duru ya nne iliahirishwa? Na nini maana ya sababu za kilojistiki? Je, kuahirishwa huku kunamaanisha kuvunjika kwa mazungumzo?

Jibu:

Ni lazima kwanza kupitia mazingira yaliyokuwepo mwaka 2015 wakati makubaliano ya kinyuklia yalipofikiwa kati ya Iran na nchi za Magharibi, kisha kurejea katika muktadha wa kujiondoa kwa Trump katika makubaliano hayo mwaka 2018 na mazingira ya wakati huo, na baada ya hapo kuangazia maendeleo ya hivi karibuni kuhusu mazungumzo kati ya Marekani na Iran:

1- Sababu zilizosukuma Marekani mwaka 2015 kufikia makubaliano ya kinyuklia na Iran:

Tulisema katika jibu la swali mnamo Julai 22, 2015, kuhusu kusainiwa kwa makubaliano hayo na Marekani: ("... Rais wa Marekani alikuwa akiongoza mazungumzo kwa mbali, kwa mawasiliano ya moja kwa moja na kwa maslahi makubwa ya kufikia makubaliano haya. Alimshughulisha waziri wake wa mambo ya nje kwa wiki tatu mfululizo, mbali na mawasiliano ya awali, jambo linaloashiria uzito wa makubaliano haya kwa Marekani, maslahi yake, na maslahi ya utawala wa Obama. Makubaliano haya yaliifunga Iran... na kuizuia kutengeneza silaha yoyote ya kinyuklia. Tukihusianisha hili na matamshi ya awali ya Rais wa Marekani na maafisa wengine wa Marekani kuhusu umuhimu wa jukumu la kimkakati la Iran katika eneo hilo na utayari wa kufanya kazi nayo, bali hata kufanya kazi nayo kivitendo kama inavyoonekana; kadhalika matamshi ya maafisa wa Iran ambao walitangaza ushirikiano wao na Marekani nchini Iraq na Afghanistan na utayari wao wa kufanya kazi nayo katika kupambana na ugaidi na itikadi kali; na kile kinachoonekana kivitendo cha idhini ya kimyakimya ya Marekani kwa kile ambacho Iran na chama chake wanakifanya nchini Syria... yote haya yanaashiria kuwa Marekani inalenga kupitia makubaliano haya kurahisisha mambo kwa Iran kwa kuiondolea vikwazo na kuanzisha uhusiano wa wazi nayo ili iendelee kutekeleza jukumu ambalo litairahisishia Marekani kazi yake, kuipunguzia mizigo, na kufunika matendo yake dhidi ya nchi na mataifa ya eneo hilo. Hivyo basi, Iran inatekeleza sera ya Marekani kivitendo kama inavyotokea Iraq, Syria, na Yemen, lakini badala ya utekelezaji huo kuwa nyuma ya pazia linalozuia kuonekana kama ilivyokuwa, sasa unakuwa nyuma ya pazia linalopenya mwanga au bila pazia kabisa...").

Kwa hivyo, Obama alifanya makubaliano ya kinyuklia na Iran mnamo 2015/7/14 ili kuimarisha jukumu lake nchini Syria.

2- Sababu zilizosukuma utawala wa Trump mwaka 2018 kufuta makubaliano ya kinyuklia yaliyotiwa saini na Iran mwaka 2015:

a- Washington iliingiza Saudi Arabia na Uturuki kwa nguvu katika matukio ya eneo hilo, ambapo Uturuki ilichukua hatua madhubuti; mnamo 2016, Uturuki ilitekeleza operesheni ya "Euphrates Shield", na mnamo Machi 2018 ilizindua operesheni ya "Olive Branch". Aidha, jukumu lililokuwa likitekelezwa na Saudi Arabia katika eneo hilo. Hivyo basi, hapakuwa na haja tena ya jukumu kuu la Iran nchini Syria, na ilikuwa lazima lipunguzwe. Na hili ndilo hasa Trump alilolifanya; alipunguza jukumu la Iran katika eneo hilo, na kuigeuza kutoka mchezaji mkuu na kuwa mchezaji wa ziada au msaidizi tu.

b- Nchi za Ulaya nazo zilikuwa upande katika makubaliano ya kinyuklia ya mwaka 2015, na ndizo zilikuwa wanufaika wakubwa zaidi. Lakini Trump hakutaka Ulaya inufaike na makubaliano yaliyotiwa saini wakati wa enzi ya Obama, hivyo akayafuta.

Hivyo ndivyo lilivyokuwa tangazo la Trump la kujiondoa katika makubaliano ya kinyuklia na Iran, ambapo maslahi ya Marekani yalichochea kujiondoa katika makubaliano hayo ili kuweka masharti mapya yanayopunguza jukumu la Iran katika eneo hilo.

3- Sababu zilizomfanya Trump kurejea mwaka 2025 kwenye makubaliano ya kinyuklia aliyoyafuta mwaka 2018:

Kwa kuangalia matukio yaliyofuata baada ya Trump kuchukua majukumu ya urais katika Ikulu ya Marekani kuanzia Januari 20, 2025, inatubainikia motisha zilizoisukuma Marekani kurejea tena kwenye makubaliano ya kinyuklia:

a- Ni wazi kwamba utawala wa Trump ndio ulioanzisha kurejesha mazungumzo ya kinyuklia na Iran. Trump alituma ujumbe kwa Tehran mnamo Machi 7 kupitia upatanishi wa Omani, akionyesha hamu yake ya wazi ya kurejea kwenye mazungumzo ili kufikia makubaliano mapya. (Rais wa Marekani, Donald Trump, katika mahojiano na mtandao wa Fox Business, alisema kuwa alituma ujumbe kwa Kiongozi Mkuu wa Iran, Ali Khamenei, siku ya Alhamisi Machi 6, ambapo alielezea upendeleo wake wa kufanya mazungumzo kuhusu makubaliano na Tehran. Trump aliongeza katika mahojiano yake, yaliyopangwa kurushwa hewani keshokutwa Jumapili: "Chaguo jingine ni kwamba hatua lazima zichukuliwe, kwa sababu Iran haipaswi kupata silaha ya kinyuklia." Na kuhusu maandishi ya ujumbe aliomtuma Khamenei, Trump alisema: "Nilimwambia kuwa natumai mtafanya mazungumzo, kwa sababu hiyo itakuwa bora zaidi kwa Iran"... Iran International, 2025/03/07).

b- Trump mnamo 2018 alibatilisha makubaliano ya kinyuklia kwa sababu faida kubwa kutoka kwa makubaliano yaliyosainiwa mwaka 2015 kati ya nchi tano wanachama wa kudumu wa Baraza la Usalama na Ujerumani zilikuwa za Waulaya. Kwa hiyo, Trump alizitenga nchi za Ulaya katika mazungumzo ya kinyuklia na Iran, kinyume na ilivyotokea mwaka 2015, na hakuwashirikisha wala kuwataarifu kuhusu mazungumzo yaliyofanyika Omani, ili kuziba njia kwa Ulaya katika jitihada zake za mazungumzo ya kinyuklia iliyokuwa ikijaribu kuyafanya na Iran. (Wanadiplomasia wa Ulaya waliiambia Reuters kuwa walikuwa wakitafuta kufanya mkutano mpya na Iran, lakini jitihada hizo zinaonekana kukwama wakati Tehran ilipoanza mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja kuhusu mpango wake wa kinyuklia na utawala wa Rais wa Marekani Donald Trump mapema mwezi huu. Marekani haikuzijulisha nchi za Ulaya kuhusu mazungumzo ya kinyuklia nchini Sultanate ya Omani kabla ya Trump kuyatangaza... Asharq, 2025/04/24). Hata uchaguzi wa Italia, chini ya uongozi wa Waziri Mkuu wa mrengo wa kulia Meloni ambaye alipata uungaji mkono kutoka kwa utawala wa Trump, uchaguzi huu kama makao makuu ya duru ya pili ni ujumbe unaoelekezwa kwa nchi za Ulaya ambazo zimeingia katika mgogoro na upinzani naye, hasa Uingereza, Ufaransa, na Ujerumani, chini ya kisingizio cha NATO.

c- Aidha, Marekani inakusudia kuelekeza umakini na rasilimali zake zote kuelekea ushindani wa kimataifa na China; kwa hiyo inatafuta kuondokana na mambo yoyote yanayounda tatizo kwake na kutawanya nguvu zake. Mazungumzo yanayoendelea na Urusi yanaweza kufafanuliwa kwa mantiki hiyo hiyo: yanalenga kuivuta Urusi kwenye meza ya mazungumzo kupitia mzozo wa Ukraine, na hivyo kuitenga na China, kwa lengo la kudhoofisha mhimili wa China na Urusi. Hivyo basi, Trump anaweka kuidhibiti China kama kipaumbele cha kimkakati.

d- Hamu ya chombo cha Kiyahudi kuishambulia Iran kwa kisingizio cha kuizuia kupata silaha za kinyuklia. Kama tujuavyo, chombo cha Kiyahudi kilishambulia Iran mnamo Oktoba 2024, na Iran ikajibu kwa kurusha makombora ili kuonyesha nguvu zake, baada ya kuitaarifu Marekani na chombo hicho mapema. Sasa, Marekani haitaki kushughulisha akili yake na mashambulizi kama hayo katika kipindi cha kulenga China. Kwa sababu hiyo, inataka kufikia makubaliano ya kinyuklia na Iran, na kwa kufanya hivyo itahakikisha usalama wa chombo cha Kiyahudi, na itaondoa kisingizio cha mashambulizi mikononi mwao. Kwa hatua hii, yaani baada ya kufikia makubaliano ya kinyuklia na Iran, Trump—ambaye ndiye muungaji mkono mkubwa zaidi wa chombo cha Kiyahudi katika Ikulu ya Marekani—ataondoa kisingizio cha mgogoro mikononi mwa chombo cha Kiyahudi na kuondoa hoja yao. Wakati huo huo, anaweka maslahi ya kiuchumi ya Marekani na kukabiliana na China mbele ya vipaumbele vyake ili aweze kuelekeza nguvu zake kikamilifu kwa China, bila kitu chochote kuvuruga umakini wake au kizuizi chochote kumzuia.

Hivyo basi, Trump alianza mazungumzo haya na Iran ili kufikia makubaliano yanayoweka mipaka ya uwezo wa kinyuklia wa Iran, akiwa mbali na nchi za Ulaya.

4- Ama kuhusu kwa nini duru ya nne iliahirishwa, ni kwa sababu za kilojistiki kama ilivyoelezwa kwenye vyombo vya habari. Maana ya neno logistics kama ilivyoelezwa kwenye Wikipedia ni: ("Sanaa ya usambazaji na ugavi". Logistics, au kile kinachojulikana kwa Kiarabu kama fann al-suqiyat: ni sanaa na sayansi ya kusimamia mtiririko wa bidhaa, nishati, na habari...). Inaonekana kinacholengwa ni kuandaa mazingira na kutuliza hali baada ya Marekani kuweka vikwazo sanjari na mazungumzo yanayoendelea kati ya Marekani na Iran. Afisa wa Iran aliliambia shirika la habari la Reuters kuwa: (mazungumzo ya Iran na Marekani yatafanyika kwa tarehe tofauti kulingana na mienendo ya Marekani, akibainisha kuwa vikwazo vya Washington dhidi ya Tehran havijengi mazingira mazuri kwa mchakato wa kidiplomasia unaotafuta kutatua mzozo wa kinyuklia). Hii ilikuja baada ya Washington kuweka vikwazo vipya dhidi ya vyombo ilivyovishutumu kwa kuhusika katika biashara haramu ya mafuta na petrokemikali za Iran. Marekani ilikuwa (imeweka vikwazo siku ya Jumatano dhidi ya vyombo ilivyovishutumu kwa kuhusika katika biashara haramu ya mafuta na petrokemikali za Iran, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Washington za kuongeza shinikizo kwa Iran. Asharq, 2025/5/1). Vikwazo hivi vilikuja wakati duru za mazungumzo zilikuwa zikiendelea kwa uzito kama ilivyoelezwa. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmaeil Baghaei, alisema: (Tehran itaendelea kushiriki kwa umakini na uthabiti katika mazungumzo yanayolenga kupata matokeo na Marekani. Asharq, 2025/5/1).

Kwa hiyo, ni vigumu kuahirishwa huku kuwa ni kuvunjika kwa mazungumzo kati ya pande hizo mbili, bali ni kuahirishwa kwa muda ili kutuliza hali kutokana na vikwazo vya Marekani wakati wa mazungumzo yanayoendelea.

5- Na ni jambo la kushangaza kwamba watawala katika nchi za Waislamu wanakubali kuingiliwa na Marekani katika kuainisha nguvu, silaha, na viwanda walivyonavyo Waislamu! Watawala hawa hawatambui kwamba kuandaa nguvu katika Uislamu ni kwa ajili ya kumshinda adui, kumtisha, na kumhofisha. Ikiwa adui anadhibiti kile tulicho nacho kwa undani, basi huo ni ushindi kwake dhidi yetu hata kabla ya wakati wake! Je, Iran inaruhusuje Marekani kuingilia kati nguvu zake, makombora yake, na silaha zake za kinyuklia wakati ambapo Marekani inajaza maghala yake kwa silaha za kinyuklia, na hata ilizitumia miongo kadhaa iliyopita huko Hiroshima na Nagasaki?! Marekani inatangaza waziwazi kwamba haitaruhusu Iran kumiliki silaha za kinyuklia, na ilikuwa ni wajibu kwa Iran na watawala wengine wa Kiislamu kuiambia Marekani kwa sauti kuu: Haribuni silaha za kinyuklia mlizonazo kabla hamjawataka wengine wasimiliki silaha hizo... na haribuni makombora mliyonayo kabla hamjawataka wengine waharibu makombora yao. Ama kuhusu maadui kumiliki silaha nzito na kuwataka Waislamu wasizimiliki, huo ni usemi uliokithiri katika udhalimu, kiburi, na kudharau wengine, laiti wangekuwa na akili.

Na Mwenyezi Mungu Mwenye Nguvu na Mwenye Kushinda amebainisha hilo katika Kitabu chake kwa kusema:

وَأَعِدُّوا لَهُمْ مَا اسْتَطَعْتُمْ مِنْ قُوَّةٍ وَمِنْ رِبَاطِ الْخَيْلِ تُرْهِبُونَ بِهِ عَدُوَّ اللهِ وَعَدُوَّكُمْ وَآخَرِينَ مِنْ دُونِهِمْ لَا تَعْلَمُونَهُمُ اللهُ يَعْلَمُهُمْ وَمَا تُنْفِقُوا مِنْ شَيْءٍ فِي سَبِيلِ اللهِ يُوَفَّ إِلَيْكُمْ وَأَنْتُمْ لَا تُظْلَمُونَ

"Na waandalieni nguvu yoyote muipatayo, na kwa mafasili ya farasi, ili kuwatishia maadui wa Mwenyezi Mungu na maadui zenu, na wengineo wasio hao, ambao ninyi hamwajui, lakini Mwenyezi Mungu anawajua. Na kitu chochote mtakachotoa katika njia ya Mwenyezi Mungu mtarudishiwa kikamilifu, nanyi hamtadhulumiwa." (QS. Al-Anfal [8]: 60)

Na imekuja katika Utangulizi wa Katiba ukurasa wa 256: [Mada 69: (Ni lazima kwa jeshi kuwa na silaha, zana, vifaa, mahitaji na majukumu yatakayoliwezesha kutekeleza jukumu lake kama jeshi la Kiislamu...). Neno Lake Aliyetukuka: (تُرْهِبُونَ - muwatishie/muwahofishe) ni sababu ('illah) ya uandaaji, na uandaaji hautimii isipokuwa ikiwa sababu iliyowekewa sheria itafikiwa, nayo ni kuwahofisha maadui na wanafiki; kutokana na hapa imekuja faradhi ya kuandaa silaha, zana, mahitaji na vifaa vingine vyote vya jeshi ili kuwepo kwa hofu hiyo, na ni bora zaidi ili jeshi liwe na uwezo wa kutekeleza jukumu lake ambalo ni Jihad kwa ajili ya kueneza mwito wa Uislamu...].

Na yote haya yanaashiria kuwa ni lazima kwa Waislamu kufanya kila juhudi ili nguvu zao ziwe juu ya nguvu za adui, na ziingize hofu katika nyoyo zao. Na ili hilo lifanyike, ni lazima nguvu zetu ziwe ni hangaikio la adui ambalo linamshughulisha na kumtisha, na yote haya yanapingana na kuingia katika mazungumzo na adui ambapo anatuainishia silaha zetu na kutuzuia kudhibiti nguvu zetu za kumtisha na kumhofisha.

Nasi tunamuomba Mwenyezi Mungu (swt) akisaidie Hizbut Tahrir, kiongozi asiyewaambia uongo watu wake, kusimamisha Dola ya Kiislamu, Khilafah Rashidah, hivi karibuni, na kisha iwahofishe maadui kama ilivyokuwa hapo awali, na kueneza kheri katika pembe za dunia, na kurudisha vitimbi vya makafiri vishingoni mwao:

وَيَوْمَئِذٍ يَفْرَحُ الْمُؤْمِنُونَ * بِنَصْرِ اللهِ يَنْصُرُ مَنْ يَشَاءُ وَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ

"Na siku hiyo waumini watafurahi. Kwa nusura ya Mwenyezi Mungu. Humnusuru amtakaye, naye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu." (QS. Ar-Rum [30]: 4-5)

4 Dhul-Qa'dah 1446 H 2025/5/2 M

Share Article

Share this article with your network