Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Bajeti katika Dola ya Khilafah

September 04, 2015
3994

(Silsila ya Majibu ya Mwanachuoni Mtukufu Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah, Amir wa Hizb ut-Tahrir, kwa Maswali ya Wageni kwenye Ukurasa wake wa Facebook "Iqtisadi")

Jibu la Swali: Bajeti katika Dola ya Khilafah

Kwa Tahsin Hasan Hadyah

Swali:

Bismillahir Rahmanir Rahim... Assalamu Alaikum wa Rahmatullahi wa Barakatuh. Tafadhali fafanua kusudi la kile kilichoelezwa hapa chini; imeelezwa katika kitabu cha An-Nidham al-Iqtisadi (Mfumo wa Kiuchumi) kuhusu bajeti ya dola ibara ifuatayo: "Ama Dola ya Kiislamu, haiwekewi bajeti ya kila mwaka, kiasi kwamba jambo hilo lihitaji kutungwa kwa sheria kila mwaka. Wala haiwasilishwi mbele ya Majlis al-Ummah (Baraza la Ummah), na wala maoni hayachukuliwi kutoka kwao. Hii ni kwa sababu bajeti katika mfumo wa kidemokrasia ni sheria katika milango na mafungu yake, na kiasi cha fedha ilichonacho, na ni sheria ya mwaka mmoja. Na sheria kwao hutungwa na bunge. Kwa hiyo, jambo hilo linahitaji kuwasilishwa mbele ya bunge. Na haya yote Dola ya Kiislamu haiyahitaji; kwa sababu mapato ya Baitul Mal hukusanywa kulingana na hukmu za kisheria zilizoelezwa, na hutumiwa kulingana na hukmu za kisheria zilizoelezwa. Na hizo zote ni hukmu za kisheria za kudumu. Hivyo basi, hakuna nafasi ya maoni katika milango ya mapato, wala katika milango ya matumizi kabisa, bali hiyo ni milango ya kudumu iliyoamuliwa na hukmu za kisheria za kudumu. Hii ni kwa upande wa milango ya bajeti. Ama kwa upande wa mafungu ya bajeti, na kiasi cha fedha kilichomo katika kila fungu, na mambo ambayo kiasi hicho kimetengwa kwa ajili yake katika kila fungu; hayo yote yameachiwa maoni ya Khalifah na ijitihadi yake; kwa sababu ni katika usimamizi wa mambo ambayo Sheria imemwachia Khalifah aamue kila anachoona, na amri yake ni wajibu kutekelezwa."

Pia imeelezwa katika kitabu cha Al-Amwal (Fedha) cha Dola ya Khilafah kuhusu Idara ya Bajeti ya Jumla kama ifuatavyo: "Idara ya Bajeti ya Jumla, Idara ya Uhasibu ya Jumla, na Idara ya Udhibiti. Ama Idara ya Bajeti ya Jumla, ni idara inayotayarisha bajeti ya baadaye ya dola, kulingana na anavyoona Khalifah, kulingana na makadirio ya mapato ya dola, na matumizi ya fedha zake, na kwa kulinganisha mapato na matumizi halisi ya jumla na bajeti hiyo, na kufuatilia matokeo ya mapato ya dola na matumizi yake halisi. Idara hii itakuwa chini ya Ofisi ya Khilafah." Kutokana na hayo, naona kuna mgongano kati ya vitabu hivi viwili; cha kwanza kinakanusha kuwepo kwa bajeti ya dola na cha pili kinathibitisha kuwepo kwa bajeti ya dola. Tafadhali fafanua jambo hili na shukrani nyingi kwenu... Abu Hasan.

Jibu:

Wa Alaikum Assalam wa Rahmatullahi wa Barakatuh.

Kwanza: Ili jibu liwe wazi, tunataja yafuatayo:

1- Bajeti kwa ujumla inajumuisha mapato na matumizi. Na kila moja ina milango (Abwaab) na mafungu (Fusool)...

2- Milango ya mapato inahusiana na vyanzo vya mapato, na mafungu yanahusiana na kile kinachotengwa kutoka kwenye mapato kwa ajili ya matumizi kwenye sekta za dola na usimamizi wa mambo ya watu. Milango ya matumizi inahusiana na namna ya kutumia mapato, na mafungu yanahusiana na kuainisha aina ya sekta zinazogharimiwa na kudhibiti matumizi kulingana na kile kilichotengwa kwa ajili yake.

3- Katika nchi za kidemokrasia za kirasimali na mfano wake, bunge hukutana na kuamua milango ya bajeti na mafungu yake katika mapato na matumizi, yaani huamua vyanzo vya mapato ya kila mwaka kama vile kusema: kutoka kodi kiasi kadhaa, mikopo kiasi kadhaa, misaada kiasi kadhaa, sekta ya umma kiasi kadhaa... na kadhalika. Kisha hutenga kutoka vyanzo hivi kiasi fulani cha fedha, kwa mfano, kwa ajili ya ujenzi wa barabara kiasi kadhaa, na kwa baadhi ya viwanda kiasi kadhaa... na kadhalika. Na huamua namna ya matumizi na kuainisha matumizi na kudhibiti matumizi kulingana na kile kilichotengwa kwa ajili yake... Hivi ndivyo inavyofanyika katika nchi za sasa...

4- Ama katika Uislamu, milango ya bajeti katika mapato na matumizi yake ni thabiti na ni milango ya kudumu, haijuzu fedha kuchukuliwa kutoka vyanzo vinginevyo, wala isitumike kwa namna isiyo ya kisheria:

a- Ama milango ya mapato, ni vyanzo maalum kutoka kwenye milki ya umma na milki ya dola kama vile Kharaj na Fai’... vile vile Zakat... Na vyanzo hivi ni vya kudumu, haviamuliwi na Khalifah wala Majlis al-Ummah. Ama mafungu yake kama vile kukadiria kile kitakachoingia katika mwaka, kwa hiyo mapato ya mafuta yanayotarajiwa au Kharaj inayotarajiwa mwaka huu huhesabiwa, basi hili linaruhusiwa... au kukadiria kile kilichotengwa kutokana na mapato kwa ajili ya baadhi ya sekta, hili pia linaruhusiwa... Na kwa sababu hiyo, milango ya bajeti haiwekewi bajeti ya kila mwaka kwa sababu haibadiliki kwa kuongezeka wala kupungua. Ama mafungu yake, kama vile kukadiria kile kinachozalishwa au mgawanyo wake katika maslahi ya dola na usimamizi wa mambo ya watu, hili linaruhusiwa.

b- Ama milango ya matumizi, vivyo hivyo katika Uislamu imeainishwa na hukmu za kisheria, na inahusiana na namna ya kutumia vyanzo vya mapato kutoka kwenye milki ya umma na milki ya dola na kutoka kwenye Zakat, na hili haliwezi kukiukwa na Khalifah wala na Majlis al-Ummah. Ama mafungu yake kwa upande wa aina ya sekta zinazogharimiwa na kudhibiti matumizi ili yasivuke kile kilichotengwa kwa ajili yake, haya yanaweza kuamuliwa na Khalifah kwa maoni na ijitihadi yake na anaweza kushauriana na Majlis al-Ummah, hivyo basi gharama ya mradi huu inaamuliwa kuwa kiasi kadhaa, na mradi mwingine kiasi kadhaa... na kadhalika.

Yaani kuna sehemu katika bajeti ambayo haijuzu kuamuliwa na Majlis al-Ummah wala Khalifah nayo ni milango ya bajeti... Na kuna sehemu ambayo Khalifah anaweza kuamua na kushauriana na Majlis al-Ummah kuhusu hiyo nayo ni mafungu ya bajeti.

Pili: Hili linafafanuliwa na kile kilichoelezwa katika Muqaddimat ad-Dustur (Utangulizi wa Katiba) katika Ibara ya (36) kipengele (f), na hii ndiyo nukuu yake:

"(f- Yeye [Khalifah] ndiye anayepitisha hukmu za kisheria ambazo kwa mujibu wake bajeti ya dola huwekwa, na yeye ndiye anayeamua mafungu ya bajeti na kiasi cha fedha kinachohitajika kwa kila upande, iwe hilo linahusiana na mapato au matumizi)" mwisho.

Na jambo hili limefafanuliwa katika Ibara ya 148 na hii ndiyo nukuu yake:

"(Ibara ya 148: Bajeti ya dola ina milango ya kudumu iliyoamuliwa na hukmu za kisheria. Ama mafungu ya bajeti na kiasi cha fedha kilichomo katika kila fungu, na mambo ambayo kiasi hicho kimetengwa kwa ajili yake katika kila fungu, basi jambo hilo limeachiwa maoni na ijitihadi ya Khalifah.)" Na imeelezwa katika ufafanuzi wake yafuatayo:

"(Ama kuandaa bajeti hii katika milango yake, mafungu yake, na kiasi cha fedha kinachowekwa ndani yake, basi hukmu za kisheria zimekwishaamua... Hivyo basi milango ya bajeti ni ya kudumu kwa misingi hiyo, kwa sababu imeamuliwa na hukmu za kisheria, na hukmu ya kisheria ni ya kudumu haibadiliki. Ama mafungu yake ambayo ni matawi yanayotokana nayo kama vile Kharaj ya ardhi inayotegemea mvua, na Kharaj ya ardhi ya umwagiliaji au mfano wa hayo, basi Khalifah ndiye anayeyaweka, kwa sababu ni katika usimamizi wa mambo, na katika yale yaliyoachiwa maoni na ijitihadi yake. Hali kadhalika kiasi cha fedha kinachowekwa, kwani huwekwa kulingana na maoni na ijitihadi yake, kama vile kiasi cha Jizya, na kiasi cha Kharaj, na mfano wa hayo. Kwa sababu ni miongoni mwa mambo aliyoachiwa yeye. Hivyo basi, dalili za hukmu za kisheria zitakuwa juu ya mapato ya Baitul Mal na matumizi yake, na kufanya utumiaji wa kile kilichomo katika Baitul Mal miongoni mwa mambo ambayo Sheria haikuyaainisha kuachiwa maoni ya Khalifah na ijitihadi yake... Na maadamu Khalifah anaweza kuweka kwa maoni na ijitihadi yake mafungu ya mapato na kiasi cha fedha kinachowekwa katika kila fungu, na mafungu ya matumizi na kiasi cha fedha kinachowekwa katika kila fungu, basi hakuna kinachozuia kuwekwa kwa bajeti ya kila mwaka ya dola katika mafungu yake na kiasi cha fedha cha kila fungu, iwe ni katika mapato au katika matumizi. Kinachokatazwa ni kuweka bajeti ya kila mwaka kwa ajili ya milango ya bajeti, si kwa mapato yake wala kwa matumizi yake kwa sababu tayari yameamuliwa na hukmu za kisheria hivyo ni ya kudumu.)" mwisho.

Kwa hiyo, inaruhusiwa kwa dola kuwa na bajeti inayowekwa na Khalifah kwa ajili ya mafungu na matawi yake... kulingana na maoni na ijitihadi yake, na inaruhusiwa kuwa ya kila mwaka... Na hili ndilo linalofaa zaidi kwa sababu fedha nyingi katika Uislamu hukusanywa mara moja kwa mwaka, kama vile Zakat, na Jizya... Hivyo ni vyema bajeti iwe ya kila mwaka, kwa msisitizo kwamba mwaka unaokusudiwa hapa ni mwaka wa Hijri si wa Miladi, yaani ni vyema kwa Dola ya Khilafah kuweka bajeti kwa maana iliyotajwa hapo juu kila mwaka wa Hijri.

Tatu: Kulingana na hayo, kukanushwa kwa bajeti kulikoelezwa katika kitabu cha An-Nidham al-Iqtisadi kunaeleweka; ni kukanusha bajeti kama ilivyo katika nchi za kidemokrasia, ambapo hutolewa kwayo sheria ya kila mwaka na bunge kwa kuainisha milango ya bajeti, mafungu yake, maelezo yake ya kina na kiasi cha fedha kinachohitajiwa na maelezo hayo au mafungu hayo... Na hili halipo katika Uislamu kwa sababu Sheria imebainisha milango ya bajeti hivyo ni ya kudumu, haitungiwi sheria ya kila mwaka. Ama kuhusu mafungu, maelezo ya kina na kiasi cha fedha kinachohitajiwa na maelezo hayo au mafungu hayo, kama ilivyoelezwa katika kitabu "hayo yote yameachiwa maoni na ijitihadi ya Khalifah; kwa sababu ni katika usimamizi wa mambo ambayo Sheria imemwachia Khalifah aamue kila anachoona, na amri yake ni wajibu kutekelezwa"... Hivyo basi kukanusha hapa kulilenga kuifanya bajeti kuwa sheria katika milango yake, mafungu yake na matawi yake, na bunge kuwa ndio upande unaotoa sheria hiyo... kama ilivyo hali katika uwekaji na uandaaji wa bajeti katika nchi za kidemokrasia.

Nne: Hali kadhalika, inafahamika kuthibitishwa kwa bajeti katika kitabu cha Al-Amwal katika Dola ya Khilafah, kwani ni kuthibitisha "bajeti ya baadaye ya dola, kulingana na anavyoona Khalifah, kulingana na makadirio ya mapato ya dola, na matumizi ya fedha zake, na kwa kulinganisha mapato na matumizi halisi ya jumla na bajeti hiyo, na kufuatilia matokeo ya mapato ya dola na matumizi yake halisi." Kinachokusudiwa na bajeti hapa ni mafungu yake, matawi yake na kiasi cha fedha kinachohitajiwa na maelezo hayo au mafungu hayo kulingana na maoni na ijitihadi ya Khalifah. Na kuwepo kwa bajeti kwa maana hii hakukanushwi katika kitabu cha An-Nidham al-Iqtisadi ambapo kinasema mwishoni mwa mada ya "Bajeti ya Dola" yafuatayo: "... Na ikamwachia Khalifah amri ya kuamua mafungu na maelezo yake ya kina, na kiasi cha fedha kinachohitajika kwayo, wakati wowote maslahi yanapohitaji..."

Na hii ndiyo kazi ya Idara iliyotajwa katika Al-Amwal kwa upande wa kuwepo "bajeti" anayoiweka Khalifah kulingana na maoni na ijitihadi yake wakati wowote maslahi yanapohitaji... lakini si katika milango ya bajeti bali katika mafungu yake.

Muhtasari: Haijuzu kuweka bajeti ya kila mwaka kwa ajili ya milango ya bajeti kwa sababu katika Uislamu ni ya kudumu, imebainishwa na hukmu za kisheria ambazo haijuzu kuzizidisha wala kuzipunguza, bali inaruhusiwa kuweka bajeti ya kila mwaka katika mafungu yake na kiasi cha fedha kinachotarajiwa kutoka kwenye mafungu ya mapato wakati wa mwaka, hali kadhalika kiasi kilichotengwa kwa ajili ya mafungu ya matumizi wakati wa mwaka.

Natumai jibu limekuwa wazi... Vyovyote iwavyo, tukiona jambo linalohitaji ufafanuzi zaidi wa kuwekwa katika vitabu vyetu, tutaliangalia jambo hilo InshaAllah.

Ndugu yenu, Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah

Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir kwenye Facebook

Kiungo cha jibu kutoka kwenye tovuti ya Amir

Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir kwenye Google Plus

Share Article

Share this article with your network