(Sfululizo wa Majibu ya Mwanachuoni Mtukufu Ata Bin Khalil Abu Al-Rashta, Amir wa Hizb ut-Tahrir, kwa Maswali ya Wageni kwenye Ukurasa Wake wa Facebook "Fiqhi")
Jawabu la Swali
Kanuni ya Kisheria
Illah (Sababu) Huambatana na Ma’lul (Hukumu) Katika Kuwepo na Kutokuwepo Kwake
Kwa: Rafiq Ahmed Abu Jaafar
Swali:
Assalamu Alaikum Warahmatullahi Wabarakatuh, jitihada zenu zibarikiwe na Mwenyezi Mungu awalipe kheri...
Sheikh wetu mpendwa, nataka kuuliza swali kuhusu kanuni ya kisheria "Illah huambatana na Ma’lul katika kuwepo na kutokuwepo kwake..." Swali ni kama ifuatavyo: Kwamba Mtume ﷺ aliulizwa kuhusu kuuza tende mbichi (rutab) kwa tende kavu (tamr), akasema: Je, tende mbichi hupungua zinapokauka? Akambiwa ndiyo, akasema: Basi haijuzu... Sasa ikiwa tunajua kwa yakini kiasi cha upungufu huo na tukakifidia, je, biashara hiyo itaruhusiwa? Kwa maana nyingine, ikiwa tende mbichi ina uzito wa kilo moja na inapokuwa tende kavu inakuwa gramu 900, je, inaruhusiwa tuuze gramu 900 za tende kavu kwa kilo moja ya tende mbichi? Na ikiwa jibu ni kwamba haijuzu kuuza, kuna faida gani kusema kwamba Illah (sababu) ni ule upungufu?
Jibu:
Walaikum Assalam Warahmatullahi Wabarakatuh,
Unaashiria katika swali lako yale yaliyokuja katika kitabu cha Ash-Shakhsiyyah al-Islamiyyah, Juzuu ya Tatu, kuhusu Illah dalalah (sababu inayofahamika kupitia dalili ya ishara), na mimi nitakunukulia baadhi ya yaliyomo katika kitabu hicho ambayo yana uhusiano na swali lako:
(...Ama kuhusu Illah inayofahamika kupitia dalili ya matamshi (dalalah), ambayo huitwa At-Tanbih wa al-Ima’ (kuzindua na kuashiria), imegawanyika katika sehemu mbili:
Kwanza: Hukumu iambatane na sifa inayotoa maana fulani...
Pili: Maelezo ya sababu (ta'lil) yawe yanatokana na maana ya lafudhi kulingana na asili ya lugha, na si kwamba lafudhi yenyewe inaashiria moja kwa moja sababu (ta'lil). Nayo ni ya aina tano:
Moja: .............
Mbili: ..............
Tatu: Sharia itaje pamoja na hukumu sifa fulani ambayo kama tusingeichukulia kama sababu (ta'lil), basi kuitaja kwake kusingekuwa na faida yoyote, na Sharia imetakasika na jambo lisilo na faida. Maandiko ya kisheria kwa kawaida kila kinachotajwa ndani yake huwa na uzito wa kisheria; na kwa hiyo, sifa hii huchukuliwa kama Illah, na andiko linakuwa na sababu (mu'allalan). Mfano ni pale maneno yanapokuwa jawabu la swali, iwe sifa hiyo ipo kwenye kiini cha swali, au kama Sharia itatoa hukumu kwa kulinganisha na mfano mwingine badala ya kiini cha swali lenyewe. Na hilo ni kama ilivyopokewa kutoka kwake ﷺ:
أَنَّهُ سُئِلَ عَنْ جَوَازِ بَيْعِ الرُّطَبِ بِالتَّمْرِ، فَقَالَ النَّبِيُّ ﷺ: هَلْ يَنْقُصُ الرُّطَبُ إِذَا يَبِس؟ فَقَالُوا: نَعَمْ، فَقَالَ: فَلاَ إِذَنْ
"Kwamba yeye aliulizwa kuhusu kuruhusiwa kuuza tende mbichi (rutab) kwa tende kavu (tamr), Mtume ﷺ akasema: 'Je, tende mbichi hupungua zinapokauka?' Wakasema: 'Ndiyo', akasema: 'Basi haijuzu'." (Imepokewa na Ad-Daraqutni)
Kuambatanishwa kwa hukumu na sifa ya upungufu, katika jawabu lao kwamba tende mbichi hupungua inapokauka, hakuwezi kuwa kwa bure (bila faida), bali lazima kuwe na faida. Na kuunganishwa kwa jawabu la Mtume kuhusu kuuza tende mbichi na herufi "Fa" (ف) katika kauli yake: "Basi haijuzu" (Fa-la idhan), nayo ni miongoni mwa njia za kuelezea sababu (ta'lil), ni dalili kwamba upungufu huo ndio Illah (sababu) ya kukatazwa kuuza tende mbichi kwa tende kavu. Hii inatokana na kupangwa kwa hukumu juu ya sifa hiyo kwa kutumia "Fa", na kuambatanishwa na neno "Idhan" (basi/hivyo basi). Katika mfano huu, sifa iliyotajwa ilikuwa kwenye kiini cha swali.
Na mfano wa sifa inayotajwa nje ya kiini cha swali, ni pale inapoelezwa hukumu kwa kutoa mfano unaofanana na kile kilichoulizwa. Hilo ni kama ilivyopokewa kutoka kwake ﷺ kwamba binti mmoja wa Kikhath'amiyya alimuuliza akisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, baba yangu amefikiwa na mauti na ana wajibu wa Hija, je nikimuhijia itamfaa?" Mtume ﷺ akasema:
أرأيتِ لوْ كانَ على أبيكِ دَيْنٌ أَكُنْتِ قاضِيَتَه؟ قالت: نعم. قال: فَدَيْنُ اللَّهِ أَحَقُّ بالقَضاء
"Je, unaonaje kama baba yako angekuwa na deni, ungekuwa unamlipia? Akasema: Ndiyo. Akasema: Basi deni la Mwenyezi Mungu lina haki zaidi kulipwa."
Yule mwanamke wa Kikhath'amiyya aliuliza kuhusu Hija, lakini Mtume ﷺ akataja deni la mwanadamu. Alimtaja mfano unaofanana na kile alichoulizwa, na si jawabu la lile swali lenyewe moja kwa moja, lakini alilitaja huku akipanga hukumu ambayo aliulizwa juu yake. Hivyo, kuambatana kwa hukumu na sifa fulani, ambayo ni deni, hakuwezi kuwa ni jambo la bure, bali ni lazima kuwe na faida. Kutajwa kwa sifa hii na Mtume ﷺ pamoja na kupanga hukumu juu yake kunaonyesha kuelezea sababu (ta'lil), la sivyo kuitaja kwake kungekuwa ni jambo lisilo na faida.) Mwisho wa nukuu.
Kama unavyoona, nukuu hii imejumuisha jawabu la swali lako ambalo umesema ndani yake: "Na ikiwa jibu ni kwamba haijuzu kuuza, kuna faida gani kusema kwamba Illah ni ule upungufu?"... Utafiti huo umeweka wazi ni nini faida ya upungufu wa tende mbichi inapokauka, ukasema: (Kuambatanishwa kwa hukumu na sifa ya upungufu, katika jawabu lao kwamba tende mbichi hupungua inapokauka, hakuwezi kuwa kwa bure, bali lazima kuwe na faida. Na kuunganishwa kwa jawabu la Mtume kuhusu kuuza tende mbichi na herufi "Fa" katika kauli yake: "Basi haijuzu", nayo ni miongoni mwa njia za kuelezea sababu, ni dalili kwamba upungufu huo ndio Illah ya kukatazwa kuuza tende mbichi kwa tende kavu, kutokana na kupangwa kwa hukumu juu ya sifa hiyo kwa kutumia "Fa", na kuambatanishwa na neno "Idhan". Katika mfano huu, sifa iliyotajwa ilikuwa kwenye kiini cha swali).
Hivyo faida hapa ni kuwepo kwa Illah, yaani kutajwa kwa upungufu ndiko kulikobainisha sababu (Illah) ya kukatazwa kuuza tende mbichi kwa tende kavu. Kwa hivyo, si sahihi kuuliza: "Kuna faida gani kusema upungufu ni Illah"! Swali hili limekosewa, bali kama ilivyokuja katika utafiti, swali linapaswa kuwa ni nini faida ya kutajwa kwa upungufu. Kuambatanishwa kwa hukumu na sifa ya upungufu ndiko lazima kuwe na faida, nayo ni kwamba upungufu ndio Illah ya kukatazwa kuuza tende mbichi kwa tende kavu, na kama isingekuwa hivyo basi kuitaja sifa ya upungufu kusingekuwa na faida yoyote... Hivyo faida yake ni kubainisha sababu ya kukatazwa kwa mauzo hayo. Mtume ﷺ aliulizwa kuhusu kuuza tende mbichi kwa tende kavu, Mtume ﷺ akamuuliza muulizaji: "Je, tende mbichi hupungua zinapokauka?" Alipoambiwa ndiyo, akasema ﷺ: "Basi haijuzu".
Ama kuhusu kwa nini haijuzu kufidia upungufu huo, yaani kama ilivyokuja katika swali lako: "Ikiwa tunajua kwa yakini kiasi cha upungufu na tukaufidia, je, mauzo yataruhusiwa?" Kwa maana nyingine, ununue ratili moja ya tende mbichi kwa ratili moja ya tende kavu, kisha uchukue ziada juu ya ile ratili ya tende mbichi kiasi cha tofauti ya uzito kati yake na ile ratili ya tende kavu. Kwa mfano, ikiwa ratili ya tende mbichi inapokauka hupungua kwa kiasi cha gramu 100, na ukataka kumpa ratili ya tende kavu naye akupe ratili ya tende mbichi pamoja na gramu 100 kwa mfano... Hili haijuzu katika bidhaa za riba (asnaf ribawiyyah). Ukizibadilisha kwa jinsia ile ile, haijuzu kuchukua kile kinachoitwa Al-Arsh, yaani tofauti ya ubora au tofauti ya sifa kati ya aina mbili za jinsia moja. Hili halijuzu katika bidhaa za riba, bali unauza tende kwa thamani (fedha) na kisha unanunua tende mbichi kwa thamani hiyo. Dalili ya hilo ni:
Al-Bukhari ametoa katika Sahih yake kutoka kwa Yahya, amesema: Nilimsikia Uqbah bin Abd al-Ghafir akimsikia Abu Said al-Khudri (ra) akisema:
جَاءَ بِلَالٌ إِلَى النَّبِيِّ ﷺ بِتَمْرٍ بَرْنِيٍّ فَقَالَ لَهُ النَّبِيُّ ﷺ مِنْ أَيْنَ هَذَا قَالَ بِلَالٌ كَانَ عِنْدَنَا تَمْرٌ رَدِيٌّ فَبِعْتُ مِنْهُ صَاعَيْنِ بِصَاعٍ لِنُطْعِمَ النَّبِيَّ ﷺ فَقَالَ النَّبِيُّ ﷺ عِنْدَ ذَلِكَ أَوَّهْ أَوَّهْ عَيْنُ الرِّبَا عَيْنُ الرِّبَا لَا تَفْعَلْ وَلَكِنْ إِذَا أَرَدْتَ أَنْ تَشْتَرِيَ فَبِعْ التَّمْرَ بِبَيْعٍ آخَرَ ثُمَّ اشْتَرِهِ
"Bilal alimjia Mtume ﷺ na tende za aina ya barni, Mtume ﷺ akamuuliza: 'Zimetoka wapi hizi?' Bilal akasema: 'Tulikuwa na tende mbaya, nikauza pishi (sa'a) mbili kwa pishi moja ili tumlishe Mtume ﷺ'. Wakati huo Mtume ﷺ akasema: 'Owe! Owe! (Lo! Lo!), hiyo ndiyo riba yenyewe, hiyo ndiyo riba yenyewe! Usifanye hivyo, lakini ukitaka kununua, uza zile tende kwa mauzo mengine kisha ununue (hizi)'." (Pia imepokewa na Muslim)
Muhtasari ni kwamba faida ya kutajwa kwa upungufu ni kubainisha sababu (Illah) ya kukatazwa mauzo ya tende kavu kwa tende mbichi kwa sababu tende mbichi hupungua inapokauka... Ama kutokuruhusiwa kutoa tofauti au kile kinachoitwa Arsh, ni kwa sababu bidhaa za riba haijuzu kuchukua tofauti (ziada) ndani yake.
Natumai jibu hili linatosheleza, na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi zaidi na Mwenye Hekima zaidi.
Ndugu yenu Ata Bin Khalil Abu Al-Rashta
06 Jumada al-Akhira 1439 H Inayoambatana na 22/02/2018 M
Kiungo cha jawabu kutoka kwenye ukurasa wa Facebook wa Amir (Mungu amhifadhi): Facebook
Kiungo cha jawabu kutoka kwenye ukurasa wa Google Plus wa Amir (Mungu amhifadhi): Google Plus
Kiungo cha jawabu kutoka kwenye ukurasa wa Twitter wa Amir (Mungu amhifadhi): Twitter
Kiungo cha jawabu kutoka kwenye tovuti ya Amir (Mungu amhifadhi): Web