Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Mkutano wa Kilele wa Uturuki na Urusi

August 18, 2016
5705

Jibu la Swali

Swali: Rais wa Uturuki, Erdogan, alitembelea Urusi mnamo tarehe 9/8/2016 huku "madhara" ya jaribio la mapinduzi lililofeli nchini Uturuki yakiwa bado hayajaisha. Kwa nini haraka hii? Kisha, nini lengo la ziara hiyo, hasa ikizingatiwa kuwa wawakilishi wa Wizara ya Mambo ya Nje, Jeshi, na Idara ya Usalama pia walitembelea Urusi? Je, ziara hii ina uhusiano na mgogoro wa Syria? Au ni kwa ajili ya "kukarabati" uhusiano wa Uturuki na Urusi baada ya mgogoro wa kutunguliwa kwa ndege ya Urusi? Mwenyezi Mungu akulipe kheri.

Jibu: Ili kujua sababu za haraka hiyo na lengo lake, tunapitia mambo yafuatayo:

1- Mazungumzo kuhusu ziara hiyo yalikuwepo kabla ya jaribio la mapinduzi la tarehe 15/7/2016, ambapo awali ilipangwa mkutano kati ya marais hao wawili ufanyike wakati wa mkutano wa kilele wa G20 utakaofanyika nchini China mnamo mwezi Septemba 2016. Lakini kulikuwa na haraka katika kufanya mkutano kati ya Rais wa Urusi Putin na Rais wa Uturuki Erdogan mnamo mwezi Agosti kwa sababu Marekani ilikuwa na shauku ya kuharakisha kuingizwa kwa Uturuki katika mkondo wa suluhu kama zana madhubuti baada ya zana zingine (Iran, Urusi... n.k.) kushindwa. Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki alitangaza kuharakishwa kwa mkutano huo na kwamba ungefanyika mwezi Agosti nchini Urusi. (Shirika la habari la Interfax lilimnukuu Waziri - Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki - akisema kuwa Rais wa Urusi Vladimir Putin na Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan wanaweza kukutana mwezi Agosti huko Sochi... Al-Arabiya Net, 2/7/2016). Mada ya ziara hiyo ilikuwa imejadiliwa ndani ya mazingira ya "maridhiano" ili Uturuki itekeleze jukumu la kutatua mgogoro wa Syria kulingana na sera ya Marekani. Tulibainisha hilo katika jibu la swali tulilotoa mnamo tarehe 14/7/2016 ambapo tulisema: (– Marekani inataka kupitia jukumu la sasa la Uturuki kuushinikiza kwa nguvu upinzani wa Syria ili uirudie mchakato wa Geneva na suluhu ya amani... na kutishia kuutelekeza upinzani wa Syria ikiwa utakataa kujiunga na mchakato wa mazungumzo, kupitia kuonyesha ushirikiano wa Uturuki na Urusi: "Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi alisema: Tunatumai kufanya mawasiliano kati ya majeshi ya Urusi na Uturuki kuhusu Syria. Al-Arabiya Net 2/7/2016"... Na kwamba Uturuki haipingi tena uingiliaji kati wa Urusi nchini Syria... Na si jambo lisilowezekana kwa Uturuki kuvuka mbinu za shinikizo za kisiasa na kufikia mbinu za kijeshi kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi wa shirika (ISIS), ambao hautenganishwi wala haupambanuliwi na upinzani mwingine wenye silaha, kisingizio kile kile kinachotumiwa na Urusi inaposhambulia upinzani! Kauli ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi kuhusu mawasiliano kati ya majeshi ya Urusi na Uturuki inaashiria uwezekano huu...), na tukaongeza (– Obama anataka kufanya kazi kama alivyofanya mtangulizi wake wa Chama cha Kidemokrasia, Clinton, ambaye alitumia juhudi zote katika mwaka wake wa mwisho wa utawala kuwakutanisha wawakilishi wa Palestina na Mayahudi katika suluhu ya mazungumzo ya mwisho ya kadhia ya Palestina, na ingawa alifeli katika hilo, aliweza kumkutanisha Abu Ammar na Ehud Barak... Na sasa Obama anatumia juhudi zote kuukutanisha upinzani na utawala katika suluhu ya mazungumzo ili isemwe kuwa amefanya kazi itakayokumbukwa mwishoni mwa utawala wake. Tofauti kati ya jaribio la Clinton na la Obama ni kwamba wa kwanza juhudi zake zilikuwa wazi mbele ya vibaraka wake, lakini Obama anafanya kazi kupitia vibaraka na zana zake... na juhudi zake zinajificha nyuma yao! Marekani katika zama zake inaonyesha utegemezi zaidi kwa wafuasi. Baada ya Iran na wafuasi wake, na baada ya Urusi, na kufuatia kukwama upya kwa Marekani nchini Syria, Marekani imemuashiria Erdogan kupatana na Urusi... Baada ya uingiliaji kati wa Iran na Urusi kufika mwisho wa barabara nchini Syria, Marekani inaharakisha kuitumbukiza Uturuki upande wa Iran na Urusi ili kulinda ushawishi wa Marekani nchini Syria na kuangamiza hali ya Kiislamu ya mapinduzi ya Syria... Na hivi ndivyo Urusi inayoshambulia Syria mchana na usiku, imekuwa yenyewe na Uturuki ni washirika wa vita dhidi ya "ugaidi" nchini Syria, na kwamba mazungumzo yanaendelea kati yao katika "mazingira ya kirafiki sana", bali hata Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi anaomba kufanyika kwa mawasiliano kati ya majeshi ya Urusi na Uturuki kuhusu Syria!!...) mwisho wa nukuu kutoka kwa jibu letu la awali la tarehe 14/7/2016.

2- Ilitarajiwa kuwa jukumu la Uturuki lianze kwa haraka, isipokuwa jaribio la mapinduzi lililofanywa na maafisa wa Kikamali (Kemalists) wanaofungamana na Waingereza lilizuia jukumu hilo na kuushughulisha utawala na matatizo ya ndani. Kuzuiliwa kwa jukumu hili kungeweza kuendelea hadi Uturuki itakapomalizana na madhara ya tetemeko la mapinduzi yaliyofeli kama alivyosema Erdogan. Lakini kilichotokea mwanzoni mwa mwezi Agosti 2016 kutokana na operesheni ya wapiganaji ya kuvunja mzingiro wa Aleppo na mafanikio yao kwa kiasi fulani, kulifanya Marekani kuitumia operesheni hii kuharakisha jukumu la Uturuki na hivyo kuifanya itembelee Urusi na kurejesha mahusiano nayo na kuanza suluhu ya kisiasa ya Marekani kwa jukumu madhubuti la Uturuki... Marekani ilitaka operesheni hii yenye nguvu ipoteze matunda yake; badala ya kuwa mwanzo wa ushindi, ikaifanya kuwa mwanzo wa mazungumzo. Ikaifanya kuwa nyenzo inayobebwa na Uturuki ili kupigia debe mazungumzo yenye usawa yaliyotajwa na Erdogan, ikidhani kuwa Uturuki inaweza kupitia mbinu zake mbalimbali kufanya pande husika zikutane kwa ajili ya suluhu ya Kimarekani katika siku chache zilizosalia za Obama kwa kutumia mazungumzo hayo yenye usawa!! (Rais wa Uturuki "Recep Tayyip Erdogan" leo ameitisha mkutano wa kikanda kwa ajili ya Syria. Kauli yake ilikuja wakati wa mahojiano marefu yaliyofanywa naye na chaneli ya Al-Jazeera ya Qatar, yaliyorushwa leo Jumamosi jioni... Erdogan aliongeza kuwa hali ya Aleppo inasikitisha lakini upinzani umerejesha usawa katika kipindi cha hivi karibuni. Suriya Net, Al-Khaleej Al-Jadid 6/8/2016).

Na hivi ndivyo ilivyokuwa, ziara ikafanyika. Haraka hii kutoka kwa Obama kwa Erdogan ilikuwa kwa ajili ya kuanza kazi ya kuzikutanisha pande husika katika duru mpya ya nne ya mazungumzo ambayo Obama angehitimisha nayo utawala wake. Duru hii ndiyo aliyoiashiria Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki: (Istanbul "Reuters" - Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki Mevlut Cavusoglu alisema siku ya Ijumaa kuwa mazungumzo kuhusu mustakabali wa Syria lazima yaanze tena na akatoa wito wa duru ya nne ya mazungumzo ya amani ya Geneva. Reuters Arabic 5/8/2016)... Na hivi ndivyo ziara na mkutano wa kilele ulivyokuwa...

3- Mkutano huu wa kilele unachukuliwa kuwa hatua ya mwisho ya mchakato wa kurejesha mahusiano kati ya Urusi na Uturuki baada ya mgogoro mkubwa ulioshuhudiwa kati yao baada ya kutunguliwa kwa ndege ya kivita ya Urusi. Mchakato huu wa kurejesha uhusiano ulitengenezwa kwa namna ya kuidhalilisha Uturuki. Kwa kunyenyekea masharti ya Putin, Erdogan aliomba radhi kwa kutunguliwa kwa ndege ya Urusi mnamo tarehe 27/6/2016, na Erdogan akachukua hatua mara moja mnamo tarehe 29/6/2016 kwa kumpigia simu Rais wa Urusi katika mazingira yaliyoelezwa kuwa ya kirafiki. Alifuatiwa na Waziri wake wa Mambo ya Nje ambaye alifanya mkutano na Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi, Lavrov, mnamo tarehe 1/7/2016 katika mji wa Sochi, Urusi. Mkutano huo ambao mawaziri hao pia walijadili tarehe ya mkutano wa kilele wa Putin na Erdogan huko Petersburg. Kisha kukawa na ishara kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki kuhusu uwezekano wa kuipa Urusi vituo vya kijeshi nchini Uturuki ili kutekeleza mashambulizi yake nchini Syria. Kuporomoka huku kwa msimamo wa Uturuki mbele ya Urusi hakukutokana na maumivu ya Uturuki kutokana na vikwazo vya kiuchumi vilivyowekwa na Urusi dhidi ya Ankara, bali kulikuwa hasa kwa sababu ya kukwama kwa Marekani nchini Syria. Marekani inataka kuisukuma Uturuki pia upande wa Urusi na Iran ili kutatua mgogoro wa Syria. Kwa ajili hiyo yote, taswira ya unyonge ya makubaliano ya Uturuki mbele ya Warusi ilikuwa kwa sababu ya mafungamano ya Uturuki na Marekani na utekelezaji wake wa sera ya Marekani. Hivyo ndivyo msukumo huu wa Uturuki ulivyokuwa...

4- Erdogan alisisitiza kukamilisha ziara nchini Urusi, iliyokuwa imepangwa kabla ya jaribio la mapinduzi lililofeli mnamo tarehe 15/7/2016, licha ya kuwa na shughuli nyingi na hali ya ndani nchini Uturuki, na kushughulikia kile alichokiita "tetemeko" na kuhofia kile alichokiita "mitetemo ya baadae ya tetemeko hilo". Pia aliuomba umati wa watu nchini Uturuki wakati wa mkutano mkubwa huko Istanbul mnamo Jumapili tarehe 7/8/2016 kubaki katika viwanja vya umma hadi Jumatano, yaani hadi baada ya kurejea kwake kutoka Urusi kwa kuhofia harakati mpya za wanajeshi wanaofungamana na Waingereza. Vilevile, licha ya kuongezeka kwa uhalifu wa kikatili wa Urusi huko Aleppo... lakini pamoja na haya yote, alisisitiza kufanya mkutano wake na Putin na kutoahirisha, kutokana na hamu yake kubwa ya kufunga ukurasa wa zamani na Urusi, na pia kutokana na msukumo mkubwa wa Marekani kwa Uturuki kuelekea upande wa Urusi. Putin aligusia msisitizo huu kwa kusema: ("Rais wa Uturuki amepata fursa ya kutembelea Urusi licha ya hali ngumu nchini Uturuki baada ya jaribio la mapinduzi lililofeli usiku wa Julai 15 na 16" Russia Today 9/8/2016).

5- Ilikuwa wazi kuwa mgogoro wa Syria ndiyo mada kuu katika mkutano wa kilele wa Erdogan na Putin. Marais hao wawili hawakujadili mada ya mgogoro wa Syria wakati wa mazungumzo yaliyohusisha wanachama wa wajumbe, bali waliahirisha mkutano kuhusu Syria hadi jioni kwa ushiriki wa mawaziri wa mambo ya nje na wawakilishi wa idara za usalama ili kujadili njia za suluhu ya Syria. Putin alisema akielezea mkutano huo unaotarajiwa: "Tubadilishana habari na tutatafuta suluhu." Kuahirisha mkutano kuhusu Syria hadi jioni, na kuwaweka mbali wanachama wa wajumbe isipokuwa mambo ya nje na usalama, kunaonyesha usiri na umuhimu mkubwa ambao pande zote mbili zinaupa mada ya Syria. Baada ya kuondolewa kwa vikwazo vya awali, hii ndiyo kadhia kuu kwa pande zote mbili, na kinachotakiwa na Marekani ni kuzikutanisha pande zote, utawala na upinzani, kwenye meza ya mazungumzo kama hitimisho la zama za Obama!

6- Wakati wa mkutano wa kilele na baada ya mkutano huo, jukumu la Uturuki lilianza kuonekana kwa ufanisi:

a- (Istanbul (Reuters) - Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki Mevlut Cavusoglu alisema siku ya Ijumaa kuwa mazungumzo kuhusu mustakabali wa Syria lazima yaanze tena na akatoa wito wa duru ya nne ya mazungumzo ya amani ya Geneva. Reuters Arabic 5/8/2016).

b- (Rais wa Uturuki "Recep Tayyip Erdogan" leo ameitisha mkutano wa kikanda kwa ajili ya Syria. Kauli yake ilikuja wakati wa mahojiano marefu yaliyofanywa naye na chaneli ya Al-Jazeera ya Qatar, yaliyorushwa leo Jumamosi jioni... Erdogan aliongeza kuwa hali ya Aleppo inasikitisha lakini upinzani umerejesha usawa katika kipindi cha hivi karibuni. Suriya Net, Al-Khaleej Al-Jadid 6/8/2016).

c- (Kwa upande wake, shirika la habari la Urusi liliripoti jana kutoka kwa Balozi wa Uturuki nchini Urusi, Umit Yardim, akisema kuwa serikali ya Uturuki inaamini kuwa uongozi wa sasa wa Syria unaweza kushiriki katika mazungumzo yanayolenga kutatua mgogoro nchini Syria. Na shirika la habari la TASS lilimnukuu Yardim akisema kuwa Ankara haipingi uongozi wa sasa wa Syria kutekeleza jukumu fulani katika mchakato wa mpito wa kisiasa. Al-Sabah 12/8/2016).

d- Ama Waziri Mkuu, yeye ndiye aliyekuwa wa kwanza katika mada ya suluhu ya kisiasa na utawala wa Syria tangu kuanza kwa maridhiano na Urusi kabla ya mapinduzi. Al-Arabiya Net iliripoti mnamo tarehe 13/7/2016 chini ya kichwa cha habari: "Mshangao... Uturuki yazungumzia 'kurejesha uhusiano' na utawala wa Syria": Waziri Mkuu wa Uturuki Binali Yildirim alitangaza: (Ankara (Uturuki) - Reuters: Waziri Mkuu wa Uturuki Binali Yildirim alisema leo Jumatano kuwa ana imani na kurejesha uhusiano wa kawaida wa nchi yake na Syria. Al-Arabiya Net, 13/7/2016). Vilevile iliripotiwa na BBC: (Waziri Mkuu wa Uturuki, Binali Yildirim, alisema kuwa Uturuki inatafuta kuendeleza uhusiano mzuri na Syria, katika hatua ya hivi karibuni ya jitihada zake za kuboresha mahusiano yake na majirani zake. BBC Arabic 13/7/2016).

7- Hivyo, Uturuki imeingia ndani ya mgogoro wa Syria kwa ufanisi, lakini si kwa ajili ya kuwanusuru watu wa Syria na kuwaokoa kutokana na ukatili wa Urusi na Iran, bali ili iwe pamoja na Urusi na Iran katika utatu wa kishetani unaorahisisha jinai zao na kuzisaidia kutekeleza suluhu ya unyonge ya Marekani kwa kufanya mazungumzo na utawala wa kidhalimu wa Sham... Mkutano ule uliowakutanisha Putin na Erdogan ni shari tupu; matokeo yake ni kuwa Uturuki imerudi nyuma kwa njia ya wazi kutoka kwa kila kitu ilichokuwa ikidai kuhusu kuunga mkono mapinduzi nchini Syria. Bali kurudi nyuma huko kulifikia hatua ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki kusema kuwa Urusi inaiomba Uturuki "vielelezo vya maeneo" (coordinates) nchini Syria, yaani maeneo ya wapiganaji yaliyokusanywa na idara ya usalama ya Uturuki ili kuelekeza mashambulizi ya Urusi dhidi yao. Kutokana na shinikizo hilo la Marekani la kuipa Urusi kile inachotaka, iliamuliwa baada ya mkutano wa kilele kuwa ujumbe wa ngazi ya juu wa idara ya usalama kutoka Uturuki usafiri kwenda Moscow siku iliyofuata ya mkutano huo, yaani mara moja.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki alikuwa amesema mnamo tarehe 10/8/2016 kupitia shirika la habari la Anadolu (kwamba mitazamo kati ya nchi yake na Urusi inafanana kuhusu ulazima wa kusitisha mapigano nchini Syria na kutoa misaada ya kibinadamu na kupata suluhu ya kisiasa, na kwamba kutajengwa mfumo imara wa ushirikiano na Moscow nchini Syria kwa ajili hiyo. Aliongeza kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Usalama, mwakilishi wa Wizara ya Mambo ya Nje, na mwingine kutoka Jeshi la Uturuki watajadili faili hizi huko Saint Petersburg jioni ya siku hiyo hiyo. Al-Jazeera Net, 11/8/2016).

Na kile kilichokuja katika kauli ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki (kusitisha mapigano nchini Syria, kutoa misaada ya kibinadamu na kupata suluhu ya kisiasa) ni msimamo wa Marekani wenyewe, ambao pia ndio Urusi inayolingania na kupigania. Kasi ya kuwatuma maafisa wa usalama, jeshi na mambo ya nje kwenda Moscow mara tu baada ya Erdogan kuondoka inaonyesha kuwa Uturuki imekamilisha pande za pembetatu ya Urusi-Iran-Uturuki! Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran alikuwa amesisitiza ("kwamba kanda inahitaji uhusiano mzuri kati ya nchi yake na Urusi na Uturuki. Ibrahim Rahimpur alitaka ushirikiano mpya chini ya muundo wa "Uturuki-Urusi-Iran" na akasisitiza kuwa nchi yake iko tayari kwenda katika mwelekeo huu." Al-Jazeera Net, 8/8/2016). Siku ya Ijumaa tarehe 12/8/2016, Javad Zarif, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, alikutana mjini Ankara na maafisa wa Uturuki ambao walisisitiza makubaliano ya kuongeza juhudi za pamoja na Iran kuhusu mgogoro wa Syria. Erdogan alimpokea Waziri wa Iran Javad Zarif katika ikulu ya rais katika mkutano wa siri wa saa tatu ambao hakuna chochote kilichotangazwa baada yake, jambo linaloashiria haraka na umuhimu wa mipango ya Marekani ya kuingiza Uturuki katika uwanja wa Syria na kuisaidia Urusi na Iran katika kutekeleza majukumu ya Marekani.

8- Kutokana na haya yote, inabainika kuwa Uturuki imeingia kwa nguvu katika kutengeneza suluhu ya kisiasa nchini Syria kwa njia ya Marekani katika haraka ya kustaajabisha, ingawa Uturuki bado haijatulia katika masuala yake ya ndani baada ya jaribio la mapinduzi. Haya yote yanaonyesha ukubwa wa shinikizo kutoka Washington, na inaonekana kuwa Uturuki itatembea kulingana na mpango huu wa Marekani pamoja na Iran na Urusi kwa namna ifuatayo:

  • Kisiasa: Itaonekana kwa wapiganaji bila shaka yoyote kuwa Uturuki imebadilisha sera yake, na kuanza kuelekea kwa utawala wa Syria, Iran na Urusi. Kwamba inawalingania wapiganaji na kuwashinikiza ili kukubali muundo wa Marekani wa suluhu huko Geneva, ambayo ni kufanya mazungumzo na utawala na kukubaliana nao kuhusu mustakabali wa Syria, na kuingia katika serikali ya pamoja kati ya wapiganaji na utawala. Vilevile kuwashinikiza wapiganaji kwa kisingizio cha masuala ya kibinadamu ili kuzuia wapiganaji wasizingire maeneo ya utawala huko Aleppo, na kupigia debe usawa wa mazungumzo kwa madai kuwa wapiganaji wamepata ushindi huko Aleppo jambo linalofanya mazungumzo yao yawe katika nafasi ya nguvu. Kuchanganya hili na mbinu za shinikizo na kisha kusitisha mapigano kabla ya kuanza mchakato wa kisiasa unaopata kitu cha "ushindi" kwa Obama kabla ya mwisho wa utawala wake mwishoni mwa mwezi Januari mwakani. Labda hili ndilo aliloliashiria Waziri Mkuu wa Uturuki kuhusu miezi sita ijayo katika kauli yake (Waziri Mkuu wa Uturuki Binali Yildirim alisema Ijumaa kuwa inatarajiwa kutokea maendeleo muhimu sana nchini Syria katika kipindi cha miezi sita ijayo. Kauli za Yildirim zilikuja kufuatia mkutano wa pamoja na waandishi wa habari uliowakutanisha jana Ijumaa Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki Mevlut Cavusoglu na mwenzake wa Iran Mohammad Javad Zarif. Kwa upande mwingine, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Mohammad Javad Zarif alisema kuwa nchi yake inafurahishwa na ukaribu wa Urusi na Uturuki, akisisitiza kuwa kutatua tofauti na Uturuki kuhusu Syria kunawezekana kupitia kuongeza mazungumzo. Alibainisha kuwa ushirikiano wa Iran na Uturuki kuhusu Syria utasaidia kwa nguvu fursa za suluhu ya amani. Al-Arabiya Net, 13/8/2016).

  • Kijeshi: Chini ya kichwa cha kupambana na shirika la Daesh (ISIS), Uturuki itaingia katika vita nchini Syria kwa muungano na Urusi, ambao haraka utageuka kuwa nguvu ya pamoja ya kulazimisha kusitisha mapigano. Hii ni pamoja na kutoa kila namna ya urahisishaji kwa Urusi ili kushambulia wapiganaji kupitia "vielelezo vya maeneo" (coordinates) ambavyo Urusi haivijui na vinamilikiwa na idara ya usalama ya Uturuki. Uturuki inaweza kutoa vituo vya kijeshi kwa Urusi ili kurahisisha kazi yake ya kihalifu ya kuwachinja Waislamu nchini Syria.

Vilevile Iran inafanya hivyo kwa kutoa vituo kwa Urusi ili kurahisisha lengo hili, na uratibu kati ya nchi hizi umeanza kweli:

(Cavusoglu pia alisema kuwa ndege za Uturuki zitajiunga na operesheni dhidi ya shirika la Daesh, akiongeza "Tutachunguza maelezo yote. Siku zote tumeialika Urusi katika operesheni za pamoja dhidi ya shirika hilo". Al-Jazeera Net, 1/8/2016). Bila shaka, kama ilivyo kisingizio cha Urusi, operesheni hizi zitajumuisha wapinzani wote kwa sababu maeneo yao hayatenganishwi!

Leo imekuja katika taarifa iliyotolewa na Wizara ya Ulinzi ya Urusi "kwamba ndege za kivita za masafa marefu za aina ya Tu-22M3 na ndege za aina ya Su-34 ziliruka Jumapili tarehe 16/8 kutoka uwanja wa ndege wa Hamadan nchini Iran na kufanya mashambulizi makubwa dhidi ya maeneo ya mashirika ya 'Daesh' na 'Jabhat al-Nusra' katika mikoa ya Aleppo, Deir ez-Zor na Idlib nchini Syria"... Mapema vyombo vya habari vilifichua kuwa ndege za kivita za aina ya Tu-22M3 za jeshi la anga la Urusi ziliwasili katika uwanja wa ndege wa Hamadan nchini Iran ili kushiriki katika kuelekeza mashambulizi dhidi ya maeneo ya shirika la "Daesh" nchini Syria. Russia Today 16/8/2016).

9- Hili ndilo ambalo Marekani inapanga litekelezwe na zana zake nchini Syria... Huu ndio udanganyifu wao,

وَمَكْرُ أُولَئِكَ هُوَ يَبُورُ

"Na vitimbi vyao hivyo vitatoweka." (QS Fatir [35]: 10)

Kwani nchini Syria kuna wanaume ambao biashara wala kuuza hakuwashughulishi na kumdhukuru Mwenyezi Mungu, wapo juu ya uoni wa jambo lao, na kwa idhini ya Mwenyezi Mungu hawatawaruhusu waovu hao kuyafanya mafanikio ya wapiganaji kuwa njia ya mazungumzo. Na kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, utatu huo uliozama katika jinai zake hautafanikiwa, wala usimamizi wa utatu huo kutoka Washington, kupata kile wanachokitamani katika ardhi ya Sham. Na kama zana za awali za Marekani zilivyofeli, basi zitafeli pia kwa idhini ya Mwenyezi Mungu zana zake za baadaye... Madhalimu wamejionea katika kipindi cha miaka mitano iliyopita kuwa nchini Sham kuna umati wa watu waaminifu na wakweli ambao azma yao haikudhoofishwa na makundi ya Marekani, Iran, Urusi, wafuasi na vibaraka, wala hata wale waliouacha mkono umati huo wa kweli katika ardhi ya Sham. Itabaki kwa idhini ya Mwenyezi Mungu ikiwa imara na iliyosimama bila kuinama, ikisimamisha sheria ya Mwenyezi Mungu, Khilafah ya Rashidah, mwaminifu kwa Mwenyezi Mungu (swt), mkweli kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw), na kisha kuitwaharisha nchi ya Uislamu kutokana na kila adui wa Uislamu. Na Mwenyezi Mungu atawajia kutokea ambapo hawakutarajia.

وَلَيَنْصُرَنَّ اللَّهُ مَنْ يَنْصُرُهُ إِنَّ اللَّهَ لَقَوِيٌّ عَزِيزٌ

"Na bila shaka Mwenyezi Mungu atamnusuru yule anayeinusuru dini yake. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye ushindi." (QS Al-Hajj [22]: 40)

13 Dhul-Qi'dah 1437 H 16/8/2016 M

Share Article

Share this article with your network