Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Kuhusu Maana ya Hadithi Tukufu «إِنَّ اللَّهَ يَبْعَثُ لِهَذِهِ الْأُمَّةِ عَلَى رَأْسِ كُلِّ مِائَةِ سَنَةٍ مَنْ يُجَدِّدُ لَهَا دِينَهَا»

June 26, 2013
4830

(Sfululizo wa majibu ya mwanachuoni Ata bin Khalil Abu al-Rashtah, Amir wa Hizb ut-Tahrir, kwa maswali ya wafuasi wa ukurasa wake wa Facebook)

Jibu la Swali:

Kuhusu maana ya Hadithi Tukufu:

إِنَّ اللَّهَ يَبْعَثُ لِهَذِهِ الْأُمَّةِ عَلَى رَأْسِ كُلِّ مِائَةِ سَنَةٍ مَنْ يُجَدِّدُ لَهَا دِينَهَا

"Hakika Mwenyezi Mungu huiletea umma huu mwanzoni mwa kila miaka mia mmoja mtu atakayeuandalia upya dini yake." (Imepokewa na Abu Dawood [4291])

Kwa Abu Mu’min Hammad

Swali:

Assalamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh.

Mwenyezi Mungu akubariki sheikh wetu na aharakishe ushindi kupitia mikono yako... na Mwenyezi Mungu atunufaishe kwa elimu yako.

Miongoni mwa hadithi sahihi na maarufu, ni ile iliyopokelewa na sahaba mtukufu Abu Hurairah (ra) kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) kwamba alisema:

إِنَّ اللَّهَ يَبْعَثُ لِهَذِهِ الْأُمَّةِ عَلَى رَأْسِ كُلِّ مِائَةِ سَنَةٍ مَنْ يُجَدِّدُ لَهَا دِينَهَا

"Hakika Mwenyezi Mungu huiletea umma huu mwanzoni mwa kila miaka mia mmoja mtu atakayeuandalia upya dini yake."

Imepokewa na Abu Dawood (na. 4291) na kusahihishwa na Al-Sakhawi katika "Al-Maqasid al-Hasana" (149), na Al-Albani katika "Al-Silsila al-Sahiha" na. 599.

Swali ni: Nini maana ya hadithi hii? Je, neno "من" katika hadithi hiyo linamaanisha kuwa mujaddid (mrejesha upya dini) ni mtu mmoja au ni kikundi? Na je, inawezekana kuwabainisha katika karne zilizopita? Mwenyezi Mungu akulipe kheri.

Jibu:

Wa Alaykum Assalam Warahmatullahi Wabarakatuh.

Ndiyo, hadithi hiyo ni sahihi, na ndani yake mna masuala matano:

  1. Karne (miaka mia) inaanza kuhesabiwa kuanzia tarehe gani? Je, ni kuanzia kuzaliwa kwa Mtume (saw), au tangu kupewa utume, au tangu Hijra, au tangu kufariki kwake (saw)?
  2. Je, "mwanzoni mwa kila miaka mia" (رأس كل مئة) inamaanisha katika miaka ya kwanza, au katikati, au miaka ya mwishoni mwa kila karne?
  3. Je, neno "من" linamaanisha mtu mmoja miongoni mwa watu, au linamaanisha kikundi kinachowandalia watu upya dini yao?
  4. Je, kuna mapokezi yenye msingi sahihi kuhusu idadi ya wanaume waliohuisha dini (mujaddidun) katika karne zilizopita?
  5. Na je, tunaweza kumtambua mujaddid wa karne ya kumi na nne iliyoisha tarehe 30 Dhul-Hijjah 1399 Hijria?

Nitajaribu kadiri ya uwezo wangu kueleza maoni yenye nguvu zaidi (rajih) kwangu katika masuala haya bila kuingia ndani sana katika pointi za tofauti, nikisema na kutaraji taufiki kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ambaye ndiye Mwongozaji kuelekea njia iliyonyooka:

1- Karne inaanza kuhesabiwa kuanzia tarehe gani?

Al-Munawi alisema katika utangulizi wa Fath al-Qadir: "Kuna ikhitilafu kuhusu رأس المائة (kichwa cha miaka mia) ikiwa inazingatiwa kuanzia kuzaliwa kwa Mtume, au kupewa utume, au Hijra, au kufariki..." Maoni yenye nguvu zaidi kwangu ni kwamba inazingatiwa kuanzia Hijra, kwani hilo ndilo tukio ambalo kupitia kwalo Uislamu na Waislamu walipata utukufu kwa kusimamishwa kwa dola yake. Ndiyo maana Omar alipowakusanya maswahaba ili kukubaliana juu ya mwanzo wa tarehe (kalenda), walitegemea Hijra. Al-Tabari alipokea katika historia yake akisema:

"Alinihadithia Abdurrahman bin Abdullah bin Abdul Hakam, akasema: Alituhadithia Nu'aim bin Hammad, akasema: Alituhadithia Al-Darawardi, kutoka kwa Othman bin Ubaidullah bin Abi Rafi', akasema: Nilimvunua Said bin al-Musayyib akisema: Omar bin al-Khattab aliwakusanya watu na akawauliza: Ni kuanzia siku gani tuanze kuandika (tarehe)? Ali akasema: Kuanzia siku aliyohajiri Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) na kuiacha ardhi ya ushirikina. Basi Omar (ra) akafanya hivyo." Abu Ja'far akasema: "Na walizingatia mwaka wa kwanza wa Hijra kuanzia Muharram wa mwaka huo, yaani miezi miwili na siku kadhaa kabla ya Mtume (saw) kuwasili Madina, kwani kuwasili kwa Mtume (saw) kulikuwa tarehe 12 Rabi' al-Awwal."

Kwa hiyo, nimeona kuwa ni bora kuhesabu karne kupitia kalenda ya Hijra iliyopitishwa na maswahaba (ra).

2- Kuhusu "mwanzoni" (رأس المئة), basi lenye nguvu ni mwisho wake. Yaani mujaddid anakuwa katika miaka ya mwishoni mwa karne, akiwa ni mwanachuoni maarufu na mcha Mungu, na kifo chake kinatokea mwishoni mwa karne hiyo na si katikati yake. Sababu za kumpendekeza huyu ni hizi zifuatazo:

a) Imethibitika kupitia mapokezi sahihi kwamba walimhesabu Omar bin Abdulaziz kuwa mwishoni mwa karne ya kwanza, naye (ra) alifariki mwaka 101 Hijria akiwa na umri wa miaka 40. Na walimhesabu Al-Shafi’i kuwa mwishoni mwa karne ya pili, naye alifariki mwaka 204 Hijria akiwa na umri wa miaka 54. Ikiwa tafsiri ya "رأس كل مئة سنة" itachukuliwa tofauti na hivi, yaani ikatafsiriwa kuwa ni mwanzo wa karne, basi Omar bin Abdulaziz asingekuwa mujaddid wa karne ya kwanza kwa sababu alizaliwa mwaka 61 Hijria, na Al-Shafi’i asingekuwa mujaddid wa karne ya pili kwa sababu alizaliwa mwaka 150 Hijria. Hii inamaanisha kuwa "رأس كل مئة" iliyotajwa katika hadithi inamaanisha mwishoni mwa karne na si mwanzo wake; hivyo anakuwa amezaliwa ndani ya karne hiyo, kisha akawa mwanachuoni maarufu mujaddid mwishoni mwake, na kufariki mwishoni mwake.

b) Ama ushahidi kwamba Omar bin Abdulaziz ndiye mujaddid wa karne ya kwanza na Al-Shafi’i ni mujaddid wa pili ni jambo lililoenea miongoni mwa wanachuoni wa umma na maimamu wake. Al-Zuhri, Ahmad bin Hanbal na wengineo miongoni mwa maimamu wa zamani na wa sasa wamekubaliana kuwa miongoni mwa mujaddidun mwishoni mwa karne ya kwanza ni Omar bin Abdulaziz (rehema za Allah ziwe juu yake) na mwishoni mwa karne ya pili ni Imamu Al-Shafi’i (rehema za Allah ziwe juu yake). Al-Hafiz bin Hajar alisema katika Tawali al-Ta'sis: "Abu Bakr al-Bazzar alisema: Nilimvunua Abdul Malik bin Abdul Hamid al-Maimuni akisema: Nilikuwa kwa Ahmad bin Hanbal, likatajwa jina la Al-Shafi’i, nikamuona Ahmad akimtukuza na kusema: Imepokewa kutoka kwa Mtume akisema kuwa Mwenyezi Mungu huleta mwishoni mwa kila miaka mia mmoja mtu anayewafundisha watu dini yao. Akasema: Omar bin Abdulaziz alikuwa mwishoni mwa karne ya kwanza, na natumai Al-Shafi’i atakuwa mwishoni mwa karne nyingine (ya pili)."

Na kupitia njia ya Abu Said al-Firyabi, amesema: Ahmad bin Hanbal alisema: "Hakika Mwenyezi Mungu huwaandalia watu mwishoni mwa kila karne mtu anayewafundisha watu Sunnah na kuondoa uongo dhidi ya Mtume. Tukaangalia, tukakuta mwishoni mwa karne ya kwanza ni Omar bin Abdulaziz na mwishoni mwa karne ya pili ni Al-Shafi’i."

Ibn Adi alisema: Nilimvunua Muhammad bin Ali bin al-Hussein akisema: Niliwasikia wenzetu wakisema: "Katika karne ya kwanza alikuwa Omar bin Abdulaziz na katika ya pili alikuwa Muhammad bin Idris al-Shafi’i."

Al-Hakim alipokea katika Mustadrak yake kutoka kwa Abu al-Walid, akasema: "Nilikuwa katika kikao cha Abu al-Abbas bin Shuraih wakati mzee mmoja aliposimama kumsifu, nikamsikia akisema: ...Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) amesema: «إِنَّ اللَّهَ يَبْعَثُ عَلَى رَأْسِ كُلِّ مِائَةِ سَنَةٍ مَنْ يُجَدِّدُ لَهَا دِينَهَا» Basi bashiri ewe kadhi, kwani Mwenyezi Mungu alimtuma Omar bin Abdulaziz mwishoni mwa karne ya kwanza, na akamtuma Muhammad bin Idris al-Shafi’i mwishoni mwa karne ya pili..."

Al-Hafiz bin Hajar alisema: "Hii inaashiria kuwa hadithi hiyo ilikuwa maarufu katika zama hizo."

c) Inaweza kusemwa kuwa ra's ya kitu katika lugha inamaanisha mwanzo wake, sasa inakuwaje tunapendekeza kuwa "ra's" ya kila karne ni mwisho wake na si mwanzo wake? Jibu ni kwamba ra's ya kitu kama ilivyo katika lugha kuwa ni mwanzo wa kitu, vivyo hivyo ni mwisho wake. Imesemwa katika Taj al-Arus: "Ra's ya kitu ni ncha yake na imesemwa ni mwisho wake." Na imesemwa katika Lisan al-Arab kuhusu kinyonga kutoka katika shimo lake kwa kichwa chake au mkia wake. Hivyo, ra's ya kitu kama ilivyokuja kwa maana ya mwanzo katika lugha, imekuja pia kwa maana ya ncha yake iwe ni mwanzo au mwisho wake. Na tunahitaji ushahidi (qarinah) ili kupendekeza maana inayokusudiwa katika hadithi kwa "ra's" ya karne, ikiwa ni mwanzo au mwisho wake. Ushahidi huu unapatikana katika mapokezi yaliyotangulia kwa kumzingatia Omar bin Abdulaziz kuwa mujaddid wa karne ya kwanza naye alifariki mwaka 101 Hijria, na kumzingatia Al-Shafi’i kuwa mujaddid wa karne ya pili naye alifariki mwaka 204. Haya yote yanapendekeza kuwa maana katika hadithi ni mwishoni mwa karne na si mwanzo wake.

Kulingana na yaliyotangulia, napendekeza kuwa maana ya "رَأْسِ كُلِّ مِائَةِ سَنَةٍ" iliyotajwa katika hadithi ni mwishoni mwa kila karne.

3- Ama ikiwa "من" inamaanisha mmoja au kikundi, hadithi imepokewa «يبعث لهذه الأمة... من يجدد لها دينها». Lau kama "من" ingekuwa inaashiria wingi, basi kitendo kingekuwa katika hali ya wingi yaani "من يجددون", lakini kitendo kimekuja katika hali ya umoja "يجدد". Pamoja na kwamba dalili ya "من" ina maana ya wingi pia hata kama kitendo kilicho baada yake kiko katika hali ya umoja, lakini napendekeza hapa kuwa ni kwa ajili ya umoja kwa kutoa ushahidi wa يجدد. Nasema napendekeza kwa sababu dalili hapa ya umoja si ya mkato (qat'i) hata kama kitendo kilicho baada yake kiko katika hali ya umoja. Kwa sababu hiyo, wapo walioitafsiri "من" kwa maana ya kikundi, na wakahesabu katika mapokezi yao makundi ya wanachuoni katika kila karne, lakini hilo ni kauli dhaifu (marjuh) kama nilivyotaja hapo awali.

Kwa hiyo, lenye nguvu kwangu ni kwamba "من" inaashiria mmoja, yaani mujaddid katika hadithi ni mwanamume mmoja mwanachuoni mcha Mungu...

4- Kuhusu kutaja majina ya mujaddidun katika karne zilizopita, kumekuja mapokezi kuhusu hilo na maarufu zaidi ni shairi (urjuza) ya Al-Suyuti ambapo alihesabu hadi karne ya tisa, na akamuomba Mwenyezi Mungu awe yeye ndiye mujaddid wa karne ya tisa. Nakunukulia baadhi ya yaliyomo katika shairi lake:

"Basi akawa mwishoni mwa karne ya kwanza Omar... Khalifa wa uadilifu kwa makubaliano na heshima..."

"Na Al-Shafi’i alikuwa mwishoni mwa ya pili... kwa sababu ya elimu yake ya juu..."

"Na wa tano ni mwanachuoni Al-Ghazali... na kuhesabiwa kwake hakuna bishara ndani yake..."

"Na wa saba aliyepanda daraja... Ibn Daqiq al-Eid kwa makubaliano..."

"Na hii ni karne ya tisa imeshafika... na ahadi ya Mwongozaji (Mtume) haivunjwi... na nimetumai kuwa mimi ndiye mujaddid ndani yake... kwani fadhila za Mwenyezi Mungu hazipingiki..."

Kuna kauli nyingine zinazoendelea baada ya hapo.

5- Na je, tunaweza kumjua mujaddid wa karne ya kumi na nne iliyoisha tarehe 30 Dhul-Hijjah 1399 Hijria?

Imevutia umakini wangu yale yaliyo maarufu kwa wanachuoni wanaoaminika kuwa "ra's" ya mwaka ni mwisho wake; kwani Omar bin Abdulaziz alizaliwa mwaka 61 Hijria na alifariki mwishoni mwa karne ya kwanza 101 Hijria, na Al-Shafi’i alizaliwa mwaka 150 Hijria na alifariki mwishoni mwa karne ya pili 204 Hijria...

Yaani, kila mmoja wao alizaliwa ndani ya karne na akawa maarufu mwishoni mwake na kufariki mwishoni mwake. Kama nilivyosema, napendekeza tafsiri hii kwa sababu ya yale yaliyo maarufu miongoni mwa wanachuoni wanaoaminika kuwa Omar bin Abdulaziz ndiye mujaddid mwishoni mwa karne ya kwanza, na Al-Shafi’i ndiye mujaddid mwishoni mwa karne ya pili. Kulingana na hili, napendekeza kuwa mwanachuoni Sheikh Taqiuddin al-Nabhani (rehema za Allah ziwe juu yake) ndiye mujaddid mwishoni mwa karne ya kumi na nne. Yeye alizaliwa 1332 Hijria na akawa maarufu mwishoni mwa karne hii ya kumi na nne, hususan alipoanzisha Hizb ut-Tahrir mnamo Jumada al-Thania mwaka 1372 Hijria, na alifariki mwishoni mwake 1398 Hijria. Da’wah yake kwa Waislamu kuelekea suala la kimsingi la kimaisha (al-qadhiya al-masiriyah), kurejesha tena maisha ya Kiislamu kwa kusimamisha dola ya Khilafah ya Rashidah, ilikuwa na athari kubwa katika maisha yao na katika juhudi zao, hadi Khilafah leo imekuwa hitaji la jumla la Waislamu. Mwenyezi Mungu amrehemu Abu Ibrahim, na amrehemu ndugu yake Abu Yusuf baada yake na awakusanye pamoja na Manabii, Wasidiki, Mashahidi na Waja wema, na hao ndio marafiki bora.

Hili ndilo ninalolipendekeza ewe ndugu yangu Abu Mu’min, na Mwenyezi Mungu ndiye anayejua zaidi ukweli, na Yeye utukufu ni Wake, kwake kuna marejeo mema.

Ndugu yenu, Ata bin Khalil Abu al-Rashtah

Link ya jibu kutoka ukurasa wa Facebook wa Amir: https://web.facebook.com/AmeerhtAtabinKhalil/photos/a.122855544578192.1073741828.122848424578904/143242869206126/?type=3&theater

Link ya jibu kutoka tovuti ya Amir: http://archive.hizb-ut-tahrir.info/arabic/index.php/HTAmeer/QAsingle/3365/

Link ya jibu kutoka ukurasa wa Google Plus wa Amir: https://plus.google.com/u/0/b/100431756357007517653/100431756357007517653/posts/ZmXkt65yd6N?sfc=false

Share Article

Share this article with your network