Swali: Mnamo Alhamisi, 18/2/2010, vyanzo vya kijeshi nchini Niger vilitangaza kuwa wanajeshi wakiongozwa na Meja Adamou Harouna wamefanya mapinduzi ya kijeshi dhidi ya Rais wa nchi hiyo, Mamadou Tandja. Walitangaza kumzuilia rais huyo na wanachama wa serikali katika eneo lililo karibu na jumba la rais mjini Niamey, na kutangaza kusitishwa kwa katiba na kuvunjwa kwa taasisi zote za dola. Je, mapinduzi haya ni kama yale yaliyotangulia ambayo yalikuwa yakitokea nchini Niger kama mgogoro wa ndani kati ya vibaraka wa Ufaransa yenye ushawishi katika koloni hili la zamani la Ufaransa, au ni mgogoro wa kimataifa? Allah akulipe heri.
Jibu:
Ndiyo, mapinduzi haya yametokea kama ulivyosema, na kuliidhinishwa kuundwa kwa "Baraza Kuu la Kurejesha Demokrasia", na kwamba mwenyekiti wake ni Salou Djibo, mkuu wa kikosi cha msaada mjini Niamey ambacho kinajumuisha silaha nzito kama vile magari ya kivita. Taarifa ya baraza hili ilisema: "Serikali imevunjwa, na Baraza Kuu la Kurejesha Demokrasia linaufahamisha umma kuwa usimamizi wa masuala ya kiserikali umekabidhiwa kwa wakurugenzi wakuu katika wizara na mikoa." (Reuters, AFP 19/2/2010)
Ili kuelewa ukweli wa kile kilichotokea, tunapitia viashiria vifuatavyo:
1- Shirika la habari la Ufaransa (AFP) liliripoti kuwa afisa mmoja wa Ufaransa ambaye hakutajwa jina lake aliliambia shirika hilo mapema: "Jaribio la mapinduzi linaendelea nchini Niger na Tandja hayuko katika hali nzuri." Shirika hilo liliongeza kuwa mwanadiplomasia huyo wa Ufaransa aliliambia: "Walinzi wa rais walishiriki katika mapinduzi," akifafanua: "Tunajua kuwa sehemu ya jeshi inampinga Tandja na ilijitokeza licha ya vifungu vya katiba, lakini tulifikiri kuwa walikuwa wachache." Alisema: "Kuna historia ya mapinduzi katika nchi hii, lakini hatukudhani kuwa yangetokea kwa kasi hii." Waziri Mkuu wa Niger, Ali Badjo Gamatié, alikuwa ameitisha mkutano muhimu wa baraza la mawaziri siku ya Jumatano, yaani siku moja kabla ya mapinduzi.
2- Haya yote yanaonyesha kuwa Ufaransa haikutarajia mapinduzi haya dhidi ya kibaraka wake, Mamadou Tandja, kutokea kwa kasi hiyo. Ilikuwa ikihisi kuwepo kwa vuguvugu miongoni mwa wanajeshi lakini ilidhani kuwa walikuwa wachache, yaani wasio na ushawishi au wasio na uwezo wa kufanya mapinduzi. Ilikuwa ikifanya mazungumzo nao na kujaribu kushughulikia hali hiyo na kuzuia mapinduzi, lakini yalitokea kinyume na matakwa yake. Serikali ilihisi kuwepo kwa tishio na ilitaka, yeye pamoja na Ufaransa iliyoko nyuma yake, kutatua tatizo hilo ili kuondoa tishio, lakini wanajeshi waliwashitukiza kama walivyoishitukiza Ufaransa.
3- Ufaransa ilionyesha kutoridhishwa kwake na mapinduzi haya na kuyalaani. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Ufaransa alisema: "Ufaransa inalaani unyakuzi wowote wa madaraka kwa njia zisizo za kikatiba, na inatoa wito wa mazungumzo kati ya waasi na rais wa nchi." (Chaneli ya Marekani ya Al-Hurra 19/2/2010). Taarifa ya msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Ufaransa inathibitisha kuwa Ufaransa iko dhidi ya wafanya mapinduzi na inataka mazungumzo kati yao na rais ili amrejeshe madarakani. Kutokana na hayo, inaeleweka kuwa mapinduzi hayo yalifanywa dhidi yake.
4- Shirika la habari la AFP mnamo 19/2/2010 lilimnukuu afisa mmoja wa Marekani mjini Washington ambaye hakutajwa jina akisema: "Tandja hafai kulaumu yeyote isipokuwa yeye mwenyewe kwa kutokea kwa mapinduzi." Shirika hili pia liliripoti tarehe hiyo hiyo, kama yalivyoripoti mashirika mengine ya habari, kwamba msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, Philip Crowley, alisema: "Hii ni hali ngumu. Rais Tandja alikuwa akijaribu kurefusha muda wake wa kukaa madarakani. Ni wazi kuwa hili ndilo lililoharakisha matukio ya leo." Alisema: "Tunaamini kuwa hii inasisitiza haja ya Niger kusonga mbele katika kuandaa uchaguzi na kuunda serikali mpya."
5- Kauli za afisa wa Marekani ambaye jina lake halikutajwa na shirika la Ufaransa, na kauli za msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, zinaonyesha kuwa Marekani imeridhishwa na mapinduzi hayo na inamtwisha rais aliyepinduliwa, Tandja, dhima halisi ya mapinduzi hayo. Hii ni kwa kuashiria suala la Rais Tandja kujiongezea muda wa miaka mitatu kupitia kura ya maoni ya marekebisho ya katiba aliyoifanya Agosti mwaka jana. Wakati huo, nguvu za upinzani zilipinga hatua hiyo, jambo ambalo lilisababisha hali ya machafuko ya kisiasa nchini humo. Tandja alichaguliwa mara mbili baada ya mapinduzi yaliyofanywa na wanajeshi wakiongozwa na Meja Daouda Malam Wanké mwaka 1999. Katiba haimruhusu kugombea kipindi cha tatu, hivyo akafanya marekebisho hayo. Alikuwa amevunja Mahakama ya Katiba kwa sababu ya kutoidhinisha kufanyika kwa marekebisho ya katiba yatakayomruhusu kugombea kipindi cha tatu au kurefusha muda wake wa urais. Pia alivunja bunge mnamo Mei 26 mwaka jana, na kisha akafanya uchaguzi wa bunge mnamo Novemba mwaka jana uliosusiwa na upinzani.
Ishara ya matamshi ya Marekani kuhusu tukio la kuongeza muda ni kumtwisha rais dhima halisi na kuhalalisha mapinduzi. Aidha, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani hakutoa wito wa kurejeshwa kwa rais, wala kufanya mazungumzo kati ya wafanya mapinduzi na rais aliyepinduliwa, bali alitoa wito wa kuandaa uchaguzi mpya na kuunda serikali mpya. Haya yote yanathibitisha kuwa Marekani ilikuwa nyuma ya mapinduzi haya.
6- Inajulikana kuwa Niger, ambayo ni nchi ya Kiislamu ambapo wakaazi wake wengi ni Waislamu, ilikuwa koloni la moja kwa moja la Ufaransa ambapo ilipewa uhuru wa kijuujuu tu mnamo mwaka 1960. Lakini ushawishi wa Ufaransa wa kila aina ulibaki nchini humo, na bado kuna Wafaransa "1500" wanaoishi huko ili kulinda maslahi ya nyuklia ya Ufaransa, kwani Niger ni nchi ya tatu duniani kwa uzalishaji wa urani, na makampuni ya Kifaransa ndiyo yanayowekeza katika uzalishaji wa urani nchini humo. Kwa hiyo, ni mahali pa matamanio ya Marekani ili kuidhibiti na kuondoa ushawishi wa Ufaransa kama ilivyo katika nchi nyingine za Afrika, ambazo nyingi ni nchi za Kiislamu na tajiri kwa rasilimali nyingi za asili. Nchi hizo ni vyanzo vya malighafi za kila aina, pamoja na vyanzo vya nishati. Ndiyo maana zimekuwa uwanja wa mgogoro kati ya wakoloni wa Magharibi wenye tamaa, wakiwemo Waulaya na Wamarekani.
7- Kutokana na umuhimu wa Niger katika uzalishaji wa urani, na hasa kwa vile makampuni ya Ufaransa ndiyo yanayowekeza hapo, haitegemewi kuwa hali itakuwa shwari kwa Marekani kwa urahisi, na kwamba Ufaransa itaacha makoloni yake na kuyaachia hivi hivi bila upinzani kwa Marekani. Hivyo basi, siku zijazo zitashuhudia mgogoro mkali wa kimataifa katika nchi hii ya Kiislamu, tofauti na ilivyozoeleka nchini Niger hapo awali ambapo migogoro ilikuwa ya ndani kati ya vibaraka wa Ufaransa.
6 Rabi'ul Awwal 1431 H 20/02/2010 M