(Mfululizo wa majibu ya mwanachuoni mtukufu Ata bin Khalil Abu Al-Rashta, Amir wa Hizb ut-Tahrir, kwa maswali ya wafuasi wa ukurasa wake wa Facebook "Fiqhi")
Jibu la Swali
Mikataba Miwili Katika Mkataba Mmoja
Kwa Abdülaziz Marouany
Swali:
Assalamu Alaikum,
Mimi ni kijana wa Kiislamu kutoka Tunisia, natamani kununua gari kwa njia ya halali. Kuna watu wamenielekeza kwenye makampuni yanayokodisha gari kwa muda mrefu kukiwa na uwezekano wa kulimiliki baada ya kumalizika kwa mkataba wa kodi, yaani kuna mikataba miwili tofauti... Je, jambo hili linaruhusiwa?
Wassalamu Alaikum Warahmatullahi Wabarakatuh.
Jibu:
Walaikum Salaam Warahmatullahi Wabarakatuh,
Hakika mikataba katika Uislamu iko wazi na ni sahali, mkataba mmoja hauchanganywi na mwingine, kiasi kwamba utekelezaji wake hautegemei utekelezaji wa mkataba mwingine. Badala yake, mkataba unakuwa imara kwa masharti yake ya kufungika na masharti ya usahihi wake. Kwa sababu hiyo, utekelezaji wake ni rahisi na mwepesi, hauingiliwi na utata wala hauzalishi matatizo kama ilivyo katika sheria za wanadamu, ziwe za kirasimali, kisoshalisti, au nyinginezo...
Mtume wa Allah (saw) amekataza kuwepo kwa mikataba miwili katika mkataba mmoja, kama vile mtu kusema: "Nimekuuzia nyumba yangu hii kwa sharti kwamba uniuzie nyumba yako nyingine kwa kiasi fulani," au "kwa sharti kwamba uniuzie nyumba yako," au "kwa sharti kwamba uniozeshe binti yako." Jambo hili halifai kwa sababu kauli yake "nimekuuzia nyumba yangu" ni mkataba mmoja, na kauli yake "kwa sharti kwamba uniuzie nyumba yako" ni mkataba wa pili, na yote miwili imekutana katika mkataba mmoja. Hili hairuhusiwi kutokana na yale aliyopokea Ahmad kutoka kwa Abdul-Rahman bin Abdillah bin Mas’ud, kutoka kwa baba yake, amesema:
نَهَى رَسُولُ اللهِ ﷺ عَنْ صَفْقَتَيْنِ فِي صَفْقَةٍ وَاحِدَةٍ
"Mtume wa Allah (saw) amekataza mikataba miwili katika mkataba mmoja." (HR Ahmad)
Maana yake ni kuwepo kwa mikataba miwili ndani ya mkataba mmoja.
Hivyo basi, kile ulichoulizia ni mikataba miwili ndani ya mkataba mmoja; kwani ni mkataba wa kukodisha kwa muda maalumu, kwa mfano miaka kumi, kisha unageuka kuwa mkataba wa kuuziana baada ya hapo. Mikataba hii miwili, yaani kukodisha na kuuza, inafanywa na mmiliki wa gari na mkodishaji katika mkataba mmoja. Kwa mujibu wa Hadith iliyotajwa hapo juu, jambo hili hairuhusiwi.
Ikiwa unataka suluhisho la suala hili, basi kubaliana naye kununua gari kwa malipo ya awamu (taqsit). Unamlipa kiasi fulani mwanzoni kisha unamalizia kwa awamu za kila mwezi mpaka ukamilishe thamani ya ununuzi mliyokubaliana tangu mwanzo. Katika hali hii, gari linakuwa mali yako kwa mujibu wa mkataba wa ununuzi mlioafikiana tangu mwanzo. Mkataba huu unakuwa mkataba wa kuuza kwa awamu, ambao unaruhusiwa na hauna shida yoyote, kwa sharti kwamba thamani ya mauzo iainishwe ikiwa ni ya pesa taslimu au ya awamu tangu mwanzo, na mkataba ufanyike kwa kile walichokubaliana.
Ikiwa watakubaliana bei fulani, na muuzaji akamuuzia mnunuzi kwa bei ya papo hapo kisha mnunuzi akakubali, au akamuuzia kwa bei ya muda mrefu (awamu) na mnunuzi akakubali, basi hilo ni sahihi. Kwani huko ni kupatana bei (musawamah) kabla ya kufunga mkataba wa mauzo kwa bei yoyote itakayokuwa, na si mkataba wenyewe bado. Kupatana bei kunaruhusiwa, kwani Mtume (saw) alipatana bei. Kutoka kwa Anas bin Malik kwamba Mtume wa Allah (saw) aliuza zulia (hils) na kikombe, akasema:
مَنْ يَشْتَرِي هَذَا الحِلْسَ وَالقَدَحَ؟ فَقَالَ رَجُلٌ: أَخَذْتُهُمَا بِدِرْهَمٍ، فَقَالَ النَّبِيُّ ﷺ: مَنْ يَزِيدُ عَلَى دِرْهَمٍ، مَنْ يَزِيدُ عَلَى دِرْهَمٍ؟ فَأَعْطَاهُ رَجُلٌ دِرْهَمَيْنِ: فَبَاعَهُمَا مِنْهُ
"Ni nani atakayenunua zulia hili na kikombe hiki?" Mtu mmoja akasema: "Nimevichukua kwa dirham moja." Mtume (saw) akasema: "Ni nani atakayezidisha juu ya dirham moja? Ni nani atakayezidisha juu ya dirham moja?" Mtu mmoja akatoa dirham mbili, basi (Mtume) akamuuzia." (Imetolewa na Tirmidhi na akasema: Hii ni hadith hasan).
Mauzo ya mnada ni mapatano ya bei (musawamah) juu ya thamani yoyote mkataba utakapotulia. Pia Ibn Majah amepokea katika Sunan yake kutoka kwa Suwaid bin Qais, amesema: "Mimi na Makhrafah Al-Abdi tulileta bidhaa za nguo kutoka Hajar, Mtume (saw) akatujia na akatupatana bei ya suruali, na tulikuwa na mpimaji aliyekuwa akipima kwa ujira, Mtume (saw) akamwambia:
يَا وَزَّانُ زِنْ وَأَرْجِحْ
"Ewe mpimaji, pima na uongeze uzani." (Imeidhinishwa na Al-Albani).
Hivyo basi, uuzaji wa awamu unaruhusiwa kwa sababu ni mapatano ya bei juu ya ipi kati ya bei mbili mauzo yatafanyika. Hii ni ikiwa mapatano ni juu ya thamani ya bidhaa iwe ya papo hapo au ya muda, kisha mkataba unafanyika kwa moja ya bei hizo ikiwa imeteuliwa peke yake. Jumuiya kubwa ya mafaqihi wameeleza kuwa inaruhusiwa kuuza kitu kwa bei zaidi ya bei yake ya sasa kwa ajili ya kuchelewesha malipo (nasi'ah). Imepokewa kutoka kwa Tawous, Al-Hakam, na Hammad kuwa walisema: "Hakuna neno mtu kusema: Nakuuzia kwa pesa taslimu kwa kiasi hiki na kwa mkopo kwa kiasi kile, kisha anaondoka na moja kati ya hizo mbili." Imam Ali (ra) amesema: "Mwenye kupatana bei kwa thamani mbili, moja ya hapo hapo na nyingine ya muda, basi na ateue moja wapo kabla ya kufunga mkataba."
Kwa hiyo, suluhisho ni kukodisha gari (bila sharti la kuimiliki mwishoni katika mkataba huo huo) au kuinunua kwa awamu kama ilivyofafanuliwa hapo juu. Huenda mtu akasema kuna tofauti gani kati ya kuinunua kwa awamu na kuikodisha kisha kuiuza katika mkataba mmoja? Jibu ni kwamba tofauti ni kubwa; nayo ni sawa na tofauti kati ya halali na haramu. Allah (swt) anajua kinachowafaa watu na kinachowadhuru, na kinachowatengeneza na kinachowafisidi:
أَلَا يَعْلَمُ مَنْ خَلَقَ وَهُوَ اللَّطِيفُ الْخَبِيرُ
"Je! asijue aliye umba, naye ndiye Mjuzi wa yaliyofichikana, Mwenye khabari?" (QS. Al-Mulk [67]: 14)
Haki ina haki zaidi kufuatwa, na Allah (swt) ndiye Mwongozaji kwenye njia iliyonyooka.
Ndugu yenu, Ata bin Khalil Abu Al-Rashta
17 Rabi’ al-Awwal 1438 H Inayolingana na 16/12/2016 M
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir kwenye Facebook
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir kwenye Google Plus
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amir kwenye Twitter
Kiungo cha jibu kutoka kwenye tovuti ya Amir