Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Aina za Vyakula vya Ribaa

October 11, 2012
4973

Swali:

Imekuja katika kitabu cha Nizham al-Iqtishadi (Mfumo wa Kiuchumi) chini ya kichwa cha habari Ribaa na Sarf, uk. 261: "Na ama kauli yake Swallallahu 'alayhi wasallam: (Chakula kwa chakula mfano kwa mfano).... basi hayo yote hayaonyeshi kuwa sababu ya uharamu ('illah) ni chakula, bali inaonyesha kuwa ribaa hutokea katika chakula, hivyo inajumuisha jinsi ya chakula chote, kwani ni neno la jumla ('aam). Kisha ikaja hadithi ya Mtume aliyoipokea Ubada bin al-Samit na kuhusisha aina za vyakula vya ribaa katika: ngano, shayiri, tende, na chumvi. Kwa hivyo, tamko la chakula ambalo ni la jumla lililokuja katika maandiko yaliyotangulia ni katika mlango wa al-'aam al-murad bihi al-khusus (neno la jumla linalokusudiwa umahususi), yaani aina nne za vyakula." Mwisho.

Nina maswali mawili, naomba ufafanuzi wake na Mwenyezi Mungu akulipe kheri:

1- Kwa nini tumesema kuwa hadithi ya Ubada bin al-Samit - ambayo imetaja aina zote sita - inahusisha (takhsis) hadithi ya (chakula kwa chakula mfano kwa mfano), ilhali hakuna mgongano kati ya neno la jumla ('aam) na lile mahususi (khaas) hapa, kiasi kwamba tuseme neno la jumla lichukuliwe kwa maana ya lile mahususi? Kwani kuchukulia neno la jumla kwa maana ya lile mahususi (al-haml) huwa ni kwa ajili ya kuondoa mgongano (ta'arudh)?

2- Kwa nini chakula (الطُعم) kilichopo katika aina nne (ngano, shayiri, tende, na chumvi) hakikuchukuliwa kama sababu ya kisheria ('illah), ikizingatiwa kuwa ni tamko lililonyambulika (mushtaq), na pia ni sifa inayofahamisha maana (wasf mufhim) na inayonasibiana?

Jibu:

1- Kuhusu hadithi ya Muslim kutoka kwa Ma’mar bin Abdullah amesema: Nilikuwa nikimsikia Mjumbe wa Allah Swallallahu 'alayhi wasallam akisema:

الطَّعَامُ بِالطَّعَامِ مِثْلًا بِمِثْلٍ

"Chakula kwa chakula mfano kwa mfano." (Muslim)

Alisema: "Na chakula chetu siku hizo kilikuwa ni shayiri." Na ingawa Ma’mar bin Abdullah alitaja aina ya chakula cha siku hizo kuwa ni shayiri, lakini inaweza kusemwa kuwa hicho ndicho alichokitaja Ma’mar bin Abdullah, lakini andiko la hadithi linajumuisha hicho na kinginecho kwa kuzingatia kuwa tamko la chakula ni la jumla na inafahamika kutoka humo kuwa kila chakula hutokea ribaa ndani yake...

Ama hadithi ya Muslim kutoka kwa Ubada bin al-Samit, amesema: Nilimsikia Mjumbe wa Allah Swallallahu 'alayhi wasallam:

يَنْهَى عَنْ بَيْعِ الذَّهَبِ بِالذَّهَبِ، وَالْفِضَّةِ بِالْفِضَّةِ، وَالْبُرِّ بِالْبُرِّ، وَالشَّعِيرِ بِالشَّعِيرِ، وَالتَّمْرِ بِالتَّمْرِ، وَالْمِلْحِ بِالْمِلْحِ، إِلَّا سَوَاءً بِسَوَاءٍ، عَيْنًا بِعَيْنٍ، فَمَنْ زَادَ، أَوِ ازْدَادَ، فَقَدْ أَرْبَى

"Akikataza kuuzwa kwa dhahabu kwa dhahabu, fedha kwa fedha, ngano kwa ngano, shayiri kwa shayiri, tende kwa tende, na chumvi kwa chumvi, isipokuwa ziwe sawa kwa sawa, na mkono kwa mkono (papo hapo). Hivyo basi, yeyote atakayezidisha au kuomba nyongeza, kwa hakika amefanya ribaa." (Muslim)

Inafahamika kutoka hadithi hii kuwa ribaa imehusishwa kutokea katika aina nne tu za vyakula na haitokei katika vinginevyo. Hii ni kwa sababu muundo (sigha) uliokuja katika hadithi unafanya kazi ya kuhusisha (al-hasr) kwani umetaja majina ya jinsia yasiyonyambulika (asmaa jins jamida), na ukaunganisha hukumu ya sharti "ziwe sawa kwa sawa, mkono kwa mkono..." kwa kila jina miongoni mwayo. Hivyo muundo huu umefanya kazi ya kuhusisha hukumu katika aina hizi na kuizuia katika nyinginezo...

Kwa hivyo, kauli yako kuwa hakuna mgongano kati ya hadithi ya "chakula kwa chakula..." na hadithi ya "dhahabu kwa dhahabu..." imetokana na kudhani kwako kuwa hadithi ya dhahabu haifanyi kazi ya kuhusisha (al-hasr). Kama ungejua kuwa inafanya kazi ya kuhusisha kama tulivyobainisha hapo juu, ungesema kuwa kuna mgongano ambao haufanyi uwezekano wa kufanyia kazi hadithi zote mbili isipokuwa kwa kuhusisha (takhsis). Kwani hadithi ya kwanza inaonyesha kutokea kwa ribaa katika kila chakula, na ya pili inaonyesha kutokea kwa ribaa kwa kuhusisha tu katika sehemu ya chakula na si katika kila chakula, bali ni katika aina nne pekee. Kwa hiyo, hadithi hizo mbili zinajumuishwa kwa njia ya kuhusisha (takhsis).

2- Ama kuhusu kwa nini (الطُعم) inayotokana na chakula haikuchukuliwa kama 'illah, hasa ikiwa ni sifa inayofahamisha maana (wasf mufhim)... Jibu la hilo ni kwamba kuhusishwa kwa tamko la hadithi ya chakula na hadithi ya (ngano kwa ngano...) kumehamisha tamko la chakula ambalo ni mushtaq kwenda kwenye matamko ya ngano, shayiri, tende, na chumvi ambayo ni matamko ya jamid (yasiyonyambulika)... Na sifa inayofahamisha maana (wasf mufhim) haipatikani katika matamko ya jinsia yasiyonyambulika (alfadh al-jins al-jamida), bali hupatikana katika matamko yaliyonyambulika (al-mushtaq). Lau hadithi ingekuja (Chakula kwa chakula mfano kwa mfano) pekee, na isihusishwe na hadithi ya «...وَالْبُرِّ بِالْبُرِّ، وَالشَّعِيرِ بِالشَّعِيرِ، وَالتَّمْرِ بِالتَّمْرِ، وَالْمِلْحِ بِالْمِلْحِ...».. ingekuwa hivyo, ingewezekana kusemwa kuwa hapo kuna 'illah. Lakini takhsis imehamisha chakula kwenda kwenye majina ya jinsia yasiyonyambulika "ngano, shayiri...". Na andiko mahususi (khaas) likija, huwa ni hakimu juu ya neno la jumla ('aam), na ndilo linalofanyiwa kazi.

Kwa sababu hiyo, tumesema kuwa chakula (الطُعم) si 'illah kwa bidhaa za ribaa zilizotajwa.

Share Article

Share this article with your network