Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Ukweli wa Mgogoro nchini Sri Lanka

June 02, 2009
3277

Swali:

Mnamo 19/5/2009, Rais wa Sri Lanka Mahinda Rajapaksa alitangaza kupitia televisheni ushindi wa serikali yake dhidi ya wapiganaji wa Tamil Tigers akisema "Nchi yetu imekombolewa kikamilifu kutoka kwa magaidi wanaotaka kujitenga." Televisheni ya serikali ilikuwa imeonyesha mwili wa kiongozi wa wapiganaji wa Tamil Tigers baada ya mapigano kati ya serikali na kundi hilo kusitisha. Mkuu wa majeshi, Jenerali Sarath Fonseka, alitoa maoni yake juu ya tukio hili akisema, "Masaa machache yaliyopita, mwili wa kiongozi wa kigaidi Velupillai, aliyeiharibu nchi, ulipatikana." Rais alijaribu kutuliza hofu ya wakazi wa Kitamil walio na wasiwasi, akisema "Lengo letu lilikuwa kuwaokoa wakazi wa Kitamil kutoka mikononi mwa waasi, na sote sasa lazima tuishi kwa usawa katika nchi hii huru."

Basi, nini ukweli wa mgogoro nchini Sri Lanka? Je, ni mgogoro wa ndani, wa kikanda, au wa kimataifa? Matokeo ya mgogoro huu yalikuwa kwa maslahi ya nani? Na je, inaweza kusemwa kuwa mgogoro katika kisiwa hicho umekwisha au una athari zitakazofuata?

Jibu:

Ili kujibu maswali haya tunasema:

1- Mgogoro unaoendelea kati ya serikali ya Sri Lanka na harakati ya wapiganaji wa Tamil Tigers umefafanuliwa kuwa mgogoro mrefu zaidi, na ukweli wake ni kwamba ni mapambano kati ya Marekani na Uingereza juu ya udhibiti wa maji ya kimkakati ya Sri Lanka. Mgogoro huo ulikuwa ukichochewa kupitia nguvu za kikanda katika eneo hilo, ambazo ni Pakistan na India.

2- Umuhimu wa Sri Lanka upo katika nafasi yake ya kijiografia. Sri Lanka iko umbali wa maili 19 kutoka pwani ya kusini mwa India, ikimaanisha kuwa iko kwenye moja ya njia muhimu zaidi za maji zinazounganisha Asia ya Magharibi na Mashariki. Iko umbali wa maili 22 kutoka sehemu nyembamba zaidi ya bara Hindi inayoitwa Mlango wa Bahari wa Palk (Palk Strait). Marekani imejaribu mara kwa mara kudhibiti Mlango wa Palk ili kuugeuza kuwa kambi ya kijeshi ya Marekani kwa ajili ya kuisaidia kudhibiti Bahari ya Hindi na kudhibiti njia ya mafuta ya Mashariki ya Kati na Afrika inayofika China, na hivyo kupunguza tamaa za China za upanuzi wa baharini kuelekea magharibi. Mara tu baada ya mashambulizi ya Septemba 11, Waziri wa Ulinzi wa Marekani Rumsfeld alipanda meli ya kuimarisha uhusiano kati ya Marekani na Sri Lanka. Udhibiti wa Mlango wa Palk unatishia njia ya maji inayounganisha India na majimbo yake ya mashariki, jambo ambalo litaifanya India kulazimika kusafiri kuzunguka Sri Lanka, kumaanisha kurefusha umbali wa safari kufika kwenye majimbo hayo, na kuongeza gharama za safari kwa kiasi kikubwa. Kadhalika, kudhibiti Mlango wa Palk kunapunguza matamanio ya India kama nchi ya kikanda na kuzuia upanuzi wake kuelekea mashariki. Hili ndilo liliipelekea China kuimarisha uhusiano wake wa kijeshi na serikali ya Sri Lanka na kuipatia silaha na zana za kijeshi. Ni vyema kutambua kuwa kushindwa kwa India kudhibiti Mlango wa Palk kunamaanisha kuathirika kwa maslahi ya Uingereza katika eneo hilo. Kwa mamia ya miaka, Uingereza imekuwa ikitafuta kudhibiti Bahari ya Hindi ili kudhibiti njia za maji katika eneo hilo kwa ajili ya kusambaza bidhaa kwenye masoko ya Mashariki. Kwa upande mwingine, udhibiti wa Marekani juu ya Bahari ya Hindi na Mlango wa Palk unaumiza Ulaya pamoja na Uingereza. Hii inamaanisha kuwa kudhibiti Sri Lanka ni lengo muhimu sana kwa Marekani na kuiwezesha kudhibiti vitisho vya China, na kupunguza ushawishi wa Uingereza na Ulaya katika Asia ya Kusini na Mashariki ya Karibu.

3- Mgogoro ulianza wakati Uingereza ilipowaleta raia wa Kitamil kutoka jimbo la Tamil Nadu nchini India kufanya kazi katika mashamba ya kahawa na chai, ambapo iligeuza kisiwa hicho kuwa shamba kuu la uzalishaji wa chai na kahawa. Lakini walio wengi wa Kisinhala (mabudha) walichukia ubaguzi wa Uingereza na hasa kuwapendelea Watamil wa Kihindu kuliko wao. Uhuru wa Sri Lanka kutoka kwa Uingereza mwaka 1948 ulikuwa ni uthibitisho wa uchungu wa uhusiano kati ya makundi hayo mawili. Serikali za Kisinhala zilizofuatana zilikuwa zikichelewesha makusudi kutoa haki za kisiasa zinazostahiki kwa Watamil wanaoishi kaskazini mwa Sri Lanka. Kwa sababu hii, Watamil walipoteza imani na viongozi wao wa kisiasa na mfumo wa kisiasa wa Sri Lanka ambao haukuwahi kuwatendea haki. Hilo lilikuwa sababu ya kuibuka kwa harakati nyingi za silaha, maarufu zaidi ikiwa ni harakati ya Tamil Tigers iliyoundwa mwaka 1976 ikiongozwa na mwanzilishi wake "Velupillai Prabhakaran". Lengo la harakati hiyo lilikuwa kuunda dola huru ya Kitamil iitwayo "Tamil Eelam" kaskazini na mashariki mwa kisiwa hicho. Harakati hiyo haikupata uungwaji mkono wa watu wengi hadi miaka ya nane ya karne iliyopita, hasa baada ya kufeli kwa jaribio la marekebisho ya katiba mwaka 1983.

Harakati hiyo ilikuwa imeingiliwa na mawakala wa Waingereza, Wahindi, na Wamarekani, jambo lililopelekea kuelekezwa kupigana na harakati nyingine za silaha. Lakini Uingereza ilikuwa na mkono mrefu, hasa katika zama za Chama cha Congress nchini India. Mnamo mwaka 1980, Uingereza iliisukuma India kuingilia kati suala la Tamil Tigers na serikali ya Sri Lanka ili kukabiliana na kukua kwa ushawishi wa Marekani katika kisiwa hicho. Hilo lilikuwa chini ya kifuniko kilichokubalika na serikali ya Sri Lanka, ambacho ni kuzuia Watamil wa India kujiunga na Watamil wa kaskazini mwa Sri Lanka ili kutenganisha kaskazini na kisiwa kingine, ingawa ukweli ni kwamba serikali ya Chama cha Congress nchini India wakati huo iliona kuwa jeshi la Sri Lanka lilikuwa karibu kuangamiza harakati ya Tamil Tigers. Uingiliaji wa India uliendelea kwa sura ya kisiasa kwa nje, na kwa namna ya uungaji mkono kwa Tamil Tigers nyuma ya pazia, hadi serikali ya India ilipoweza mnamo 29/7/1987 kufunga mkataba wa amani kati ya Waziri Mkuu wa India Rajiv Gandhi na Rais wa Sri Lanka Jayewardene. Kutokana na mkataba huu, serikali ya Sri Lanka ilitoa seti ya mapendeleo kwa Watamil, ikiwa ni pamoja na kushirikisha jimbo la Kitamil katika mamlaka, na kuruhusu kuwepo kwa vikosi vya amani vya India mkabala na India kutoziunga mkono harakati za silaha za Kitamil.

4- Kushindwa kwa India kukalia sehemu ya Sri Lanka kulipelekea kuondolewa kwa udhalilishaji kwa majeshi ya India. Kisha Marekani ilitumia hisia za chuki dhidi ya India kuingilia kati kati ya harakati ya Tamil Tigers na serikali ya Sri Lanka. Hata hivyo, Marekani ilipendelea kuimarisha uhusiano wake na serikali zaidi kuliko na harakati hiyo, kwa hivyo uhusiano kati ya Marekani na serikali ya Sri Lanka ulikua zaidi, hasa baada ya matukio ya Septemba 11. Kisha Marekani hivi karibuni iliipa serikali mwanga wa kijani ili kuangamiza Tamil Tigers ndani ya mfumo wa vita vya kimataifa dhidi ya ugaidi, kwani Marekani iliona haja ya kujenga mafungamano imara ya kijeshi na kiuchumi na Sri Lanka. Mnamo mwaka 2002, Washington iliweza kufikia makubaliano yanayowezesha meli za kivita na ndege za kivita za Marekani kutumia ardhi ya Sri Lanka. Mnamo mwaka 2002 pia, Rais wa Marekani Bush alikutana na Waziri Mkuu wa Sri Lanka "Wickremesinghe" katika Ikulu ya White House na kupata mkataba wa amani na maendeleo ya kiuchumi nchini Sri Lanka. Hivyo Marekani na Sri Lanka zilitia saini mkataba wa biashara ya pamoja (TIFA) mwaka 2002. Mwenye hasara kubwa kutokana na ushirikiano huu kati ya nchi hizo mbili alikuwa Uingereza ambayo ilijipata imetengwa kwa sababu mbili: Kwanza, kupoteza kwa Chama cha Congress cha India katika uchaguzi wa India na ushindi wa Chama cha Janata ambacho kilikuwa kikipinga kuchukua msimamo wa uadui dhidi ya mkataba wa kijeshi na kiuchumi wa Marekani na Sri Lanka. Sababu ya pili ni kwamba serikali ya Sri Lanka ilikuwa chini ya ushawishi wa Marekani, kumaanisha kuwa chaguo pekee la Uingereza lilikuwa kuunga mkono harakati ya Tamil Tigers hadi ilipoangamizwa hivi karibuni.

5- Marekani ilingoja kuchaguliwa kwa Rais Mahinda Rajapaksa kuwa rais wa Sri Lanka mwaka 2005 ili kuhakikisha uungaji mkono wa serikali ya Sri Lanka kwa ajili ya kuangamiza harakati ya Tamil Tigers. Katika ukweli, kampeni ya uchaguzi ya Mahinda Rajapaksa ilikuwa kwa msingi wa ahadi zake za kuangamiza harakati ya Tamil Tigers, hasa kwa vile Mahinda Rajapaksa alikuwa ameunda muungano na chama cha msimamo mkali cha Jathika Hela Urumaya na watawa wa Kibudha wenye msimamo mkali. Marekani ilikaribisha kuchaguliwa tena kwa Mahinda Rajapaksa, ambapo Naibu Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, Adam Ereli, alisema katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika Washington, "Tutaendelea kudumisha uhusiano wa kihistoria wa nchi zetu mbili. Tunatarajia ushirikiano na Rais Mahinda Rajapaksa kwa sababu amekabiliana na changamoto nyingi za kipekee." Marekani iliweza, kupitia Mahinda Rajapaksa na ndugu yake (Katibu wa Ulinzi) na mkuu wa majeshi, kuangamiza wapiganaji wa Tamil Tigers. Kwa kutambua hatua ya makubaliano ya Marekani na Sri Lanka, Uingereza, India na Ulaya walifanya kila wawezalo kuzuia serikali ya Mahinda Rajapaksa isiwaangamize wapiganaji wa Tamil Tigers.

6- Marekani iliunga mkono serikali ya Mahinda Rajapaksa kwa silaha madhubuti kupitia Pakistan. Mnamo Machi 2006, Sri Lanka iliiomba Pakistan kuipatia mfumo wa kurusha makombora wakati Rais wa Sri Lanka Mahinda Rajapaksa alipoizuru Pakistan. Mnamo Mei 2008, Mkuu wa Majeshi ya Sri Lanka Fonseka alifunga mkataba na Pakistan wa kununua vifaru 22 vya Pakistan vya aina ya Al-Khalid vyenye thamani ya dola milioni 100. Pamoja na hayo, mamlaka za Pakistan ziliipatia Sri Lanka silaha nyingi zenye thamani ya dola milioni 65. Mnamo 19/1/2009, katika mkutano uliowakutanisha Waziri wa Ulinzi wa Pakistan Syed Athar Ali na mwenzake wa Sri Lanka Gotabaya Rajapaksa huko Rawalpindi, pande hizo mbili zilikubaliana kuimarisha ushirikiano wa kijeshi ndani ya mfumo wa mazoezi ya kijeshi ya pamoja na kubadilishana taarifa za kintelijensia kwa ajili ya kupambana na ugaidi.

7- Wakati ushindi wa mara kwa mara dhidi ya Tamil Tigers ulipopatikana, Uingereza na kibaraka wake India, pamoja na Ulaya, walitafuta kufanikisha maridhiano kati ya serikali ya Mahinda Rajapaksa na Tamil Tigers. Lengo lao la kufanya suluhu lilikuwa ni kuzuia kuangamizwa kwa Tamil Tigers. Uingereza na India walikuwa wakipaza sauti zao kwa kisingizio cha kuuawa kwa raia wa Kitamil katika mgogoro unaoendelea. Uingereza, India na Ulaya walifanya juhudi katika siku za hivi karibuni kuhimiza usitishaji vita na kuwahimiza waandamanaji wa Kitamil kote ulimwenguni kuandamana dhidi ya mauaji ya raia yaliyofanywa na serikali ya Mahinda Rajapaksa. Ama Marekani, ilikuwa ikicheza na maneno kuhusu amani na kusitisha mapigano, lakini huku ikiishajiisha serikali ya Sri Lanka kukataa hilo, kisha kuiunga mkono kupitia Pakistan. Hayo yote yalimfanya Mahinda Rajapaksa kukataa ofa za amani na usitishaji vita. Hivyo, serikali ya Sri Lanka ilipuuza miito hiyo, na matokeo yake imeweza kusambaratisha vikosi vya Kitamil, shirika hilo la kijeshi ambalo lilikuwa likitawala maeneo makubwa kaskazini mwa kisiwa hicho, na kudhibiti jeshi la polisi na walikuwa wakijivunia jeshi lao la majini na anga.

Kushindwa kwa Tamil Tigers kunamaanisha kuwa ushawishi wa India na Uingereza kaskazini mwa kisiwa hicho umepungua kwa kiasi kikubwa, na hilo liliipa Marekani fursa ya kuimarisha udhibiti wake nchini Sri Lanka na kuanzisha kambi za kijeshi za kudumu nchini humo. Pia inatoa fursa kwa Marekani kudhibiti Mlango wa Palk na kuongeza uwepo wake wa kijeshi wa baharini katika Bahari ya Hindi ili kukabiliana na vitisho vya China. Zaidi ya hayo, Marekani inaweza kuitumia Sri Lanka kuishinikiza India – hasa baada ya kuwasili kwa Chama cha Congress nchini India kwa miaka mingine mitano ya utawala – kufuata sera za Marekani katika eneo hilo kwa mara nyingine. Kwa vyovyote vile, mengi yanamsubiri Mahinda Rajapaksa kurekebisha uhusiano na Watamil na kuendana na matakwa yao ya kisiasa, na kwa sababu Marekani inatambua hilo, ilitangulia kwa kuipatia serikali ya Mahinda Rajapaksa misaada kupitia Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) ili kufikia matakwa hayo. Kwani utulivu wa Sri Lanka ni maslahi muhimu kwa Marekani, na kuangalia historia ya eneo hilo kunaonyesha kuwa Uingereza na kibaraka wake India watafanya kazi ya kujenga upya ushawishi wao nchini Sri Lanka. Na pengine mgogoro kati ya Waingereza na Wamarekani umetulia kwa sasa, lakini bado haujaisha.

Share Article

Share this article with your network