** (Silsila ya Majibu ya Mwanachuoni Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah, Amiri wa Hizb ut-Tahrir, kwa Maswali ya Wafuasi wa Ukurasa Wake wa Facebook)**
Kwa Ayman Alfjjary
Swali:
Assalamu Alaikum. Swali kwa Amiri wetu wa sasa na Khalifa wetu mtarajiwa In Shaa Allah:
Imetajwa katika kitabu cha Ad-Dawla al-Islamiyya (Dola ya Kiislamu), katika mada ya Kiapo cha pili cha Aqaba na yaliyofuata baada yake, kwamba Mtume (saw) (alifikiria) katika sehemu zaidi ya moja, pamoja na kwamba jambo hilo linapaswa kuwa ni wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na si fikra kutoka kwa Mtume (saw). Mfano: alifikiria kuhusu Hijra, ilhali Hijra ni wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Naomba ufafanuzi wa nini kinachokusudiwa na neno "kufikiria" hapa, na Mwenyezi Mungu akubariki?
Jibu:
Wa Alaikum Salaam Wa Rahmatullahi Wa Barakatuh.
Kabla ya kujibu moja kwa moja kuhusu kufikiria kwa Mtume (saw) juu ya Hijra, nakurudisha nyuma kwenye mwanzo wa kutafuta Nusrah (msaada wa nguvu/kijeshi) mpaka kufikia Kiapo cha pili cha Aqaba kisha Hijra, ili jibu liwe wazi kwa idhini ya Mwenyezi Mungu:
1- Khadija (ra) alifariki miaka mitatu kabla ya Hijra, na katika mwaka huo huo alifariki Abu Talib, kama ilivyoelezwa katika kitabu cha Uyun al-Athar:
(...عَنْ قَتَادَةَ قَالَ: تُوُفِّيَتْ خَدِيجَةُ بِمَكَّةَ قَبْلَ الْهِجْرَةِ بِثَلاثِ سِنِينَ، وَهِيَ أول من آمن بالنبي صلى الله عليه وسلم، قَالَ... ثُمَّ أَنَّ خَدِيجَةَ بِنْتَ خُوَيْلِدٍ وَأَبَا طَالِبٍ مَاتَا فِي عَامٍ وَاحِدٍ، فَتَتَابَعَتْ عَلَى رَسُول اللَّهِ صلى الله عليه وسلم مُصِيبَتَانِ: وفاة خَدِيجَةَ وَأَبِي طَالِبٍ، وَكَانَتْ خَدِيجَةُ وَزِيرَةَ صِدْقٍ عَلَى الإِسْلامِ، وَكَانَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم يَسْكُنُ إِلَيْهَا، قَالَ: وَقَالَ زياد البكائي عن ابن إسحق: إِنَّ خَدِيجَةَ وَأَبَا طَالِبٍ توفيا فِي عَامٍ وَاحِدٍ، وَكَانَ ذلك بَعْدَ عَشْرِ سِنِينَ مَضَيْنَ مِنْ مَبْعَثِ رَسُولِ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم قَبْلَ مُهَاجِرِهِ صلى الله عليه وسلم إِلَى الْمَدِينَةِ بِثَلاثِ سِنِينَ. وَذَكَرَ ابْنُ قُتَيْبَةَ أَنَّ خَدِيجَةَ تُوُفِّيَتْ بَعْدَ أَبِي طَالِبٍ بِثَلاثَةِ أَيَّامٍ. وَذَكَرَ الْبَيْهَقِيُّ نَحْوَهُ.)
“...Kutoka kwa Qatada amesema: Khadija alifariki Makka miaka mitatu kabla ya Hijra, naye ndiye wa kwanza kumuamini Mtume (saw)... kisha Khadija bint Khuwaylid na Abu Talib walifariki katika mwaka mmoja, hivyo Mtume (saw) alipatwa na misiba miwili mfululizo: kifo cha Khadija na Abu Talib. Khadija alikuwa msaidizi mkweli kwa Uislamu, na Mtume (saw) alikuwa akipata utulivu kwake. Ibn Ishaq amesema: Khadija na Abu Talib walifariki mwaka mmoja, na hiyo ilikuwa baada ya miaka kumi tangu kuanza kwa utume wa Mtume (saw) na miaka mitatu kabla ya Hijra yake kwenda Madinah. Ibn Qutaybah ametaja kuwa Khadija alifariki siku tatu baada ya Abu Talib. Al-Bayhaqi naye ametaja mfano wa hayo.”
2- Na kutoka kwa Al-Waqidi:
(تُوُفِّيَتْ خَدِيجَةُ قَبْلَ أَبِي طَالِبٍ بِخَمْسٍ وَثَلاثِينَ لَيْلَةً، وَقِيلَ غَيْرُ ذَلِكَ، فَلَمَّا هَلَكَ أَبُو طَالِبٍ نَالَتْ قُرَيْشٌ مِنْ رَسُولِ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم مِنَ الأَذَى مَا لَمْ تَكُنْ تَطْمَعُ فِيهِ فِي حَيَاةِ أَبِي طَالِبٍ، حَتَّى اعْتَرَضَهُ سَفِيهٌ مِنْ سُفَهَاءِ قُرَيْشٍ فَنَثَرَ عَلَى رَأْسِهِ تُرَابًا، فَدَخَلَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم بَيْتَهُ وَالتُّرَابُ عَلَى رَأْسِهِ، فَقَامَتْ إِلَيْهِ إِحْدَى بَنَاتِهِ فَجَعَلَتْ تَغْسِلُ عَنْهُ التُّرَابَ وَهِيَ تَبْكِي ورَسُول اللَّهِ صلى الله عليه وسلم يقول: «لا تبك يَا بُنَيَّةُ فَإِنَّ اللَّهَ مَانِعٌ أَبَاكِ» وَيَقُولُ بَيْنَ ذَلِكَ: «مَا نَالَتْ مِنِّي قُرَيْشٌ شَيْئًا أَكْرَهُهُ حَتَّى مَاتَ أَبُو طَالِبٍ»)
“Khadija alifariki kabla ya Abu Talib kwa masiku thelathini na tano, na inasemekana tofauti na hivyo. Abu Talib alipofariki, Maquraishi walimfanyia Mtume (saw) maudhi ambayo hawakuthubutu kuyafanya wakati Abu Talib akiwa hai. Hata mmoja wa wapumbavu wa Kikuraishi alimkabili na kumvumulia mchanga kichwani mwake. Mtume (saw) aliingia nyumbani kwake akiwa na mchanga kichwani, mmoja wa binti zake akasimama na kuanza kumuoshia mchanga huo huku akilia, naye Mtume (saw) akimwambia: ‘Usilie ewe binti yangu, kwani Mwenyezi Mungu atamlinda baba yako.’ Na alikuwa akisema wakati huo: ‘Maquraishi hawakunifanyia jambo lolote ninalolichukia mpaka alipokufa Abu Talib.’”
3- Katika mazingira haya magumu, Mwenyezi Mungu alimkirimu Mtume Wake (saw) kwa matukio mawili makubwa: Isra na Mi'raj, na idhini kwa Mtume (saw) ya kutafuta Nusrah kutoka kwa wenye nguvu miongoni mwa makabila ili kulinda Da’wah na kuanzisha Dola. Kuhusu Isra na Mi'raj si mahali pake hapa, lakini kuhusu kutafuta Nusrah, mwandishi wa Uyun al-Athar na wengineo katika wanahistoria wa Sira wamesema:
“Mtume (saw) alitoka kwenda Taif mwishoni mwa mwezi wa Shawwal mwaka wa kumi wa Utume, alitoka kwenda Taif peke yake – na Ibn Saad amesema: alikuwa na Zaid bin Harithah – akitafuta Nusrah kutoka kwa kabila la Thaqif na ulinzi kupitia kwao dhidi ya watu wake, akitaraji kuwa watayakubali yale aliyoyaleta kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Alipofika Taif, aliwaelekea kundi la watu wa Thaqif ambao walikuwa viongozi na watukufu wao siku hizo, nao ni ndugu watatu: Abd Yalil, Mas’ud na Habib, wana wa Amr bin Umair... lakini hawakumuitikia... bali waliwachochea wapumbavu wao dhidi yake...”
4- Baada ya hapo, jitihada za kutafuta Nusrah ziliendelea. Mtume (saw) alikuwa akijitambulisha wakati wa msimu wa Hajj kwa makabila ya Kiarabu, akiwalingania kwa Mwenyezi Mungu na kuwajulisha kuwa yeye ni Mtume aliyetumwa, na akitaka wamsadiki na kumlinda mpaka abainishe yale ambayo Mwenyezi Mungu amemtuma kwayo. Aliwaendea kabila la Kinda katika makazi yao, ambapo alikuwepo kiongozi wao aitwaye Mulaih, akawalingania kwa Mwenyezi Mungu na kujitambulisha kwao lakini wakakataa. Aliwaendea kabila la Kalb, akaenda kwa tawi lao linaloitwa Banu Abdillah, akawalingania na kusema: “Enyi wana wa Abdillah, hakika Mwenyezi Mungu amelifanya vizuri jina la baba yenu,” lakini hawakukubali. Aliwaendea Banu Hanifa, akawalingania, lakini hapakuwa na Waarabu waliomrudisha kwa kauli mbaya zaidi kuliko wao. Aliwaendea Banu Amir bin Sa’sa’ah, wakatoa sharti kwamba uongozi uwe kwao baada yake, Mtume (saw) akasema: «الأمر لله يضعه حيث يشاء» “Jambo hili ni la Mwenyezi Mungu, hulipeleka anakotaka,” wakakataa na kusema hatuhitaji jambo lako. Kisha Mtume (saw) alitoka akiwa na Abu Bakr na Ali bin Abi Talib (ra). Ali amesema: Abu Bakr alikuwa mbele katika kila heri, akauliza: Nyinyi ni watu gani? Wakasema: Banu Shayban bin Tha'labah. Abu Bakr akamgeukia Mtume (saw) na kusema: Baba na mama yangu wawe fidia kwako, hawa ni watu mashuhuri katika watu wao, na miongoni mwao yupo Mafruq bin Amr. Mafruq akasema: Labda wewe ni ndugu wa Kikuraishi? Abu Bakr akasema: Je, imewafikia habari kuwa yeye ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, basi huyu hapa? Mafruq akasema: Imetufikia kuwa anataja hayo. Unalingania nini ewe ndugu wa Kikuraishi? Mtume (saw) akasogea mbele na kusema: «أدعو إلى شهادة أن لا إله إلا الله وحده لا شريك له وأني رسول الله وأن تؤووني وتنصروني فإن قريشا قد تظاهرت على أمر الله وكذبت رسله واستغنت بالباطل عن الحق والله هو الغنى الحميد» “Ninalingania kwenye ushuhuda kuwa hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu pekee, hana mshirika, na mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na kwamba mnilipe hifadhi na kuninusuru, kwani Maquraishi wameshirikiana dhidi ya amri ya Mwenyezi Mungu, wakawakadhibisha Mitume Wake na kutosheka na batili badala ya haki, na Mwenyezi Mungu ni Mkwasi, Mhimidiwa...” Watu wale wakasema... Sisi tumeweka ahadi na Kisra kwamba tusizushe jambo jipya wala kumpa hifadhi mleta mambo mapya, na naona jambo hili unalolilingania ni katika yale wanayoyachukia wafalme. Ukipenda tukuhifadhi na kukunusuru kwa yale yanayopakana na ardhi za Kiarabu tutafanya hivyo. Mtume (saw) akasema: «ما أسأتم في الرد إذ فصحتم في الصدق وإن دين الله لن ينصره إلا من حاطه من جميع جوانبه» “Hamjafanya vibaya katika majibu yenu kwa kuwa mmekuwa wakweli, na hakika dini ya Mwenyezi Mungu hatainusuru isipokuwa yule anayeilinda kutoka pande zake zote.”
5- Kisha imetajwa katika Uyun al-Athar na vitabu vingine vya Sira:
(قَالَ ابن إسحق: فَلَمَّا أَرَادَ اللَّهُ إِظْهَارَ دِينِهِ وَإِعْزَازَ نَبِيِّهِ وَإِنْجَازَ مَوْعِدِهِ لَهُ، خَرَجَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم فِي الْمَوْسِمِ الَّذِي لَقِيَ فِيهِ النَّفَرَ مِنَ الأَنْصَارِ، رَهْطًا مِنَ الْخَزْرَجِ فَقَالَ لَهُمْ الرسول صلى الله عليه وسلم: «أَفَلا تَجْلِسُونَ أُكَلِّمُكُمْ؟» قَالُوا: بَلَى، فَجَلَسُوا مَعَهُ، فَدَعَاهُمْ إِلَى اللَّهِ، وَعَرَضَ عَلَيْهِمُ الإِسْلامَ... فَلَمَّا كَلَّمَ رَسُول اللَّهِ صلى الله عليه وسلم أُولِئَك النَّفَرَ وَدَعَاهُمْ إِلَى اللَّهِ قَالَ بَعْضُهُمْ لِبَعْضٍ: تَعْلَمُوا وَاللَّهِ إِنَّهُ لَلنَّبِيُّ الَّذِي تَوَعَّدَكُمْ بِهِ يَهُودُ، فَلا يَسْبِقَنَّكُمْ إِلَيْهِ، فَأَجَابُوهُ فِيمَا دَعَاهُمْ إِلَيْهِ بِأَنْ صَدَّقُوهُ وَقَبِلُوا مِنْهُ مَا عَرَضَ عَلَيْهِمْ مِنَ الإِسْلامِ وَقَالُوا لَهُ: إِنَّا تَرَكْنَا قَوْمَنَا وَلا قَوْمَ بَيْنَهُمْ مِنَ الْعَدَاوَةِ وَالشَّرِّ مَا بَيْنَهُمْ، فَإِنْ يَجْمَعُهُمُ اللَّهُ عَلَيْكَ فَلا رَجُلَ أَعَزُّ مِنْكَ، ثُمَّ انْصَرَفُوا رَاجِعِينَ إِلَى بِلادِهِمْ قَدْ آمَنُوا وَصَدَّقُوا...)
“Ibn Ishaq amesema: Mwenyezi Mungu alipotaka kuidhihirisha dini Yake, kumtukuza Mtume Wake na kutimiza ahadi Yake kwake, Mtume (saw) alitoka katika msimu (wa Hajj) ambapo alikutana na kundi la Ansar kutoka kabila la Khazraj. Mtume (saw) akawaambia: ‘Je, hamtaketi nikazungumza nanyi?’ Wakasema: ‘Ndiyo.’ Wakaketi naye, akawalingania kwa Mwenyezi Mungu na kuwatolea Uislamu... Mtume (saw) alipozungumza na watu wale na kuwalingania kwa Mwenyezi Mungu, wakaanza kuambiana: ‘Jueni, Wallahi huyu ndiye Mtume ambaye Mayahudi walikuwa wanawatishia naye, basi wasiwatangulieni kumfikia.’ Wakamtikia katika yale aliyowalingania, wakamsadiki na kukubali Uislamu. Wakamwambia: ‘Sisi tumeacha watu wetu, na hapana watu wenye uadui na shari baina yao kama wao, Mwenyezi Mungu akiwaunganisha kupitia wewe, basi hakuna mtu atakuwa mtukufu kuliko wewe.’ Kisha wakarudi kwao wakiwa wameamini na kusadiki...”
Mwaka ulipozunguka na miezi mitukufu kurejea, wakati wa Hajj ulifika katika mwaka wa kumi na mbili wa Utume, wakaja wanaume kumi na wawili kutoka Yathrib (Madinah). Walikutana na Mtume Aqaba na wakampa kiapo cha utii (Bay'ah) cha kwanza cha Aqaba. Imetajwa katika Hada'iq al-Anwar: “Katika msimu wa mwaka wa kumi na mbili: walimjia wanaume kumi na wawili kutoka kwa Ansar, wakampa kiapo cha utii Aqaba, kiapo cha wanawake...”
Ahmad amepokea katika Musnad yake kutoka kwa Ubadah bin al-Samit amesema: Nilikuwa miongoni mwa waliohudhuria Aqaba ya kwanza, tulikuwa wanaume kumi na wawili, tukampa Mtume (saw) kiapo cha utii cha wanawake, na hiyo ilikuwa kabla ya vita kufaradhiwa:
«أَنْ لَا نُشْرِكَ بِاللهِ شَيْئًا، وَلَا نَسْرِقَ، وَلَا نَزْنِيَ، وَلَا نَقْتُلَ أَوْلَادَنَا، وَلَا نَأْتِيَ بِبُهْتَانٍ نَفْتَرِيهِ بَيْنَ أَيْدِينَا وَأَرْجُلِنَا، وَلَا نَعْصِيَهُ فِي مَعْرُوفٍ، فَإِنْ وَفَّيْتُمْ فَلَكُمُ الْجَنَّةُ، وَإِنْ غَشِيتُمْ مِنْ ذَلِكَ شَيْئًا، فَأَمْرُكُمْ إِلَى اللهِ إِنْ شَاءَ عَذَّبَكُمْ، وَإِنْ شَاءَ غَفَرَ لَكُمْ»
“Kwamba tusimshirikishe Mwenyezi Mungu na chochote, wala tusiibe, wala tusizini, wala tusiue watoto wetu, wala tusilete kusingizia (tuhuma za uongo) tunazozizua baina ya mikono na miguu yetu, wala tusimuasi katika jambo la kheri (ma’ruf). Mkitekeleza hayo, basi mtapata Pepo, na mkifanya lolote katika hayo, basi jambo lenu liko kwa Mwenyezi Mungu; akitaka atawaadhibu na akitaka atawasamehe.” (Musnad Ahmad)
6- Walipoondoka, Mtume (saw) alimtuma Mus’ab bin Umayr pamoja nao, kama ilivyoelezwa katika Sira ya Ibn Hisham na vitabu vingine vya Sira:
“Ibn Ishaq amesema: Watu wale walipoondoka, Mtume (saw) alimtuma Mus’ab bin Umayr pamoja nao. Alifikia kwa As’ad bin Zurarah... As’ad bin Zurarah alitoka na Mus’ab bin Umayr kuelekea makazi ya Banu Abd al-Ashhal na Banu Zafar... wakaketi kwenye bustani miongoni mwa bustani za Banu Zafar... Wakakusanyika kwao watu walioslimu. Sa’d bin Mu’adh na Usayd bin Hudayr walikuwa viongozi wa watu wao siku hiyo kutoka Banu Abd al-Ashhal... Lakini Mwenyezi Mungu akaifungua mioyo yao kwa Uislamu, wakaslimu. Sa’d akaenda kwenye kikundi cha watu wake akiwa na Usayd bin Hudayr... Akasema: Enyi wana wa Abd al-Ashhal, mnanichukuliaje miongoni mwenu? Wakasema: Wewe ni kiongozi wetu, mwenye maoni bora na mbarikiwa. Akasema: Basi ni haramu kwangu kuzungumza na wanaume na wanawake wenu mpaka mumuamini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake. Wallahi hapakubaki nyumba katika Banu Abd al-Ashhal isipokuwa mwanamume na mwanamke walikuwa Waislamu. As’ad na Mus’ab wakarudi kwa As’ad bin Zurarah, akakaa kwake akiwalingania watu kwenye Uislamu...”
7- Imetajwa katika Sira ya Ibn Hisham na Hada'iq al-Anwar: “Kisha Mus’ab bin Umayr akarudi Makka, na Waislamu miongoni mwa Ansar wakatoka kwenda kwenye msimu wa Hajj mwaka wa kumi na tatu wa Utume pamoja na washirikina wa watu wao. Walipofika Makka, walifanya miadi na Mtume (saw) kukutana Aqaba katikati ya siku za Tashriq. Mwenyezi Mungu alipotaka kuwakirimu na kumnusuru Mtume Wake, na kuutukuza Uislamu na watu wake... Ka’b amesema: Tulipotoka kwenda Hajj, tulifanya miadi na Mtume (saw) Aqaba katikati ya siku za Tashriq... Usiku ule tulilala na watu wetu kwenye mizigo yetu, mpaka ulipopita thuluthi ya usiku, tulitoka kwa siri kama wanavyojificha ndege wa Qata, mpaka tukakusanyika kwenye bonde karibu na Aqaba, tukiwa wanaume sabini na watatu na wanawake wawili... tukamsubiri Mtume (saw)... Mtume (saw) akazungumza, akasoma Qur’ani, akalingania kwa Mwenyezi Mungu, na akawahimiza kwenye Uislamu. Kisha akasema: ‘Nawapa kiapo cha utii (Bay’ah) kwa sharti kwamba mnilinde kama mnavyolinda wanawake na watoto wenu.’ Al-Bara’ bin Ma’rur akamshika mkono na kusema: ‘Ndiyo, naapa kwa Yule aliyekutuma kwa haki kama Mtume, tutakulinda kama tunavyolinda familia zetu. Tupe kiapo ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, kwani sisi Wallahi ni watu wa vita...’ Abu al-Haytham bin al-Tayyihan akasema: ‘Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika baina yetu na watu (Mayahudi) kuna mafungamano na tutayakata – je, ukishinda na Mwenyezi Mungu akakupa ushindi utarudi kwa watu wako na kutuacha?’ Mtume (saw) akatabasamu na kusema: «بل الدَّمَ الدَّمَ، وَالْهَدْمَ الْهَدْمَ، أَنَا مِنْكُمْ وَأَنْتُمْ مِنِّي، أُحَارِبُ مَنْ حَارَبْتُمْ، وَأُسَالِمُ مَنْ سَالَمْتُمْ» ‘Bali damu ni damu, na uharibifu ni uharibifu, mimi ni miongoni mwenu na nyinyi ni miongoni mwangu, nitampiga vita mtakayempiga vita, na nitakuwa na amani na mtakayekuwa na amani naye.’ Ibn Ishaq amepokea kutoka kwa Ubadah bin al-Samit amesema: Tukampa Mtume (saw) Kiapo cha Vita... kiapo cha kusikia na kutii katika uzito na wepesi, katika furaha na chukizo, na kutowafanyia fujo wenye mamlaka, na kusema haki popote tulipo, tusiogope lawama za mwenye kulaumu kwa ajili ya Mwenyezi Mungu...”
8- Na hivi ndivyo Kiapo cha pili cha Aqaba kilivyotimia, kiapo cha Nusrah (msaada wa nguvu/kijeshi) baada ya Uislamu kuenea Madinah, kisha Hijra na kufuatiwa na kuanzishwa kwa Dola. Inabainika kutokana na yote haya kuwa Mtume (saw) alikuwa ameamriwa kutafuta Nusrah tangu mwaka wa kumi wa Utume, yaani takriban miaka mitatu kabla ya Kiapo cha Aqaba. Hii ina maana kuwa Mtume (saw) alikuwa akifunuliwa (wahyi) kufanya vitendo vya kutafuta Nusrah, hivyo akawa anatafuta wenye nguvu miongoni mwa makabila na kuomba msaada wao. Zilipomfikia habari za Madinah kutoka kwa Mus’ab bin Umayr, kisha wakaja wale wanaume sabini na watatu na wanawake wawili wakatoa Kiapo cha pili cha Aqaba, Mtume (saw) aliona kuwa Madinah imehitimu kumnusuru kwa ajili ya kuanzisha Dola na kuutukuza Uislamu na Waislamu. Akifikiria kuhama kwenda huko kwa sababu yeye (saw) alikuwa akitafuta wenye nguvu ili wamnusuru na aende kwao kuanzisha utawala wa Kiislamu. Hivyo, kufikiria Hijra kulihitajika na kile kile kitendo cha kutafuta Nusrah. Kama vile Mtume (saw) alivyokuwa akienda kwa kabila na kuomba nusra yake, vivyo hivyo alifanya alipojua kuwa Madinah imekuwa tayari kutoa Nusrah na kuanzishwa Dola ndani yake. Kwa hivyo, kufikiria kwake (saw) kuhusu Hijra ya kwenda Madinah hakukuwa nje ya mahitaji ya kutafuta Nusrah ambayo Mwenyezi Mungu alimfunulia tangu miaka mitatu kabla ya Kiapo cha pili cha Aqaba. Pamoja na hayo, Mtume (saw) hakuhama kwenda Madinah mpaka Mwenyezi Mungu alipomuonyesha makazi ya Hijra (Dar al-Hijrah) na kumpa idhini (saw) ya kuhama, kama ilivyoelezwa katika Sahih al-Bukhari:
“Ibn Shihab amesema: Urwa bin al-Zubair aliniambia kuwa Aisha (ra), mke wa Mtume (saw), amesema: Sijawahi kuwatambua wazazi wangu isipokuwa wakiwa katika dini (ya Kiislamu), na hakuna siku iliyopita bila Mtume (saw) kututembelea mara mbili, asubuhi na jioni... Mtume (saw) akawaambia Waislamu: «إِنِّي أُرِيتُ دَارَ هِجْرَتِكُمْ، ذَاتَ نَخْلٍ بَيْنَ لاَبَتَيْنِ» ‘Hakika nimeonyeshwa makazi yenu ya Hijra, yenye mitende baina ya milima miwili ya mawe ya moto.’ Basi waliohama wakahamia Madinah, na wengi wa wale waliohama ardhi ya Uhabeshi wakarudi Madinah. Abu Bakr akajitayarisha kuelekea Madinah, Mtume (saw) akamwambia: «عَلَى رِسْلِكَ، فَإِنِّي أَرْجُو أَنْ يُؤْذَنَ لِي» ‘Subiri kidogo, kwani nataraji kupewa idhini.’ Abu Bakr akasema: ‘Je, unataraji hayo kwa baba yangu?’ Akasema: ‘Ndiyo.’ ... Aisha amesema: Siku moja tukiwa tumeketi nyumbani kwa Abu Bakr wakati wa adhuhuri, mtu mmoja akamwambia Abu Bakr: ‘Huyu hapa Mtume (saw) amekuja akiwa amejifunika kichwa, katika saa ambayo hakuwa akitujia.’ Abu Bakr akasema: ‘Baba na mama yangu wawe fidia kwake, Wallahi hakuja saa hii isipokuwa kwa jambo muhimu.’ Mtume (saw) akaja, akaomba ruhusa, akaingia, akamwambia Abu Bakr: «أَخْرِجْ مَنْ عِنْدَكَ» ‘Watoe walioko hapa kwako.’ Abu Bakr akasema: ‘Hawa ni watu wako (familia yako), fidia kwako ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu.’ Akasema: «فَإِنِّي قَدْ أُذِنَ لِي فِي الخُرُوجِ» ‘Hakika nimepewa idhini ya kutoka.’ Abu Bakr akasema: ‘Niambatane nawe ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?’ Mtume (saw) akasema: ‘Ndiyo’...”
9- Kwa hivyo, kufikiria Hijra ya kwenda Madinah baada ya kumfikia habari zake ni katika mahitaji ya kutafuta Nusrah ambayo Mwenyezi Mungu alimpa idhini tangu mwaka wa kumi wa Utume. Ni sawa na kwenda kwa Mtume (saw) Taif, Banu Shayban na Banu Amir... Lakini Mtume (saw) hakugeuza fikra hii kuwa kitendo isipokuwa baada ya Mwenyezi Mungu kumuonyesha makazi ya Hijra na kumpa idhini ya kutoka: «إِنِّي أُرِيتُ دَارَ هِجْرَتِكُمْ، ذَاتَ نَخْلٍ بَيْنَ لاَبَتَيْنِ» “Hakika nimeonyeshwa makazi yenu ya Hijra, yenye mitende baina ya milima miwili...” na «فَإِنِّي قَدْ أُذِنَ لِي فِي الخُرُوجِ» “Hakika nimepewa idhini ya kutoka,” kama ilivyopokelewa katika Bukhari kutoka kwa Aisha, Mama wa Waumini (ra).
Natumai jambo hili limekuwa wazi kwako, na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kutoa taufiki.
Ndugu yenu, Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amiri kwenye Facebook
Kiungo cha jibu kutoka kwenye tovuti ya Amiri
Kiungo cha jibu kutoka kwenye ukurasa wa Amiri kwenye Google Plus