Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Ni nini kipo nyuma ya Makubaliano ya Kiunzi na Iran kuhusu Mpango wake wa Nyuklia?

April 07, 2015
3010

Jibu la Swali

Ni nini kipo nyuma ya Makubaliano ya Kiunzi na Iran kuhusu Mpango wake wa Nyuklia?

Swali:

Mnamo jioni ya tarehe 02/04/2015, makubaliano ya kiunzi yalitiwa saini mjini Lausanne, Uswisi kati ya mataifa ya 5+1 na Iran kuhusu mpango wake wa nyuklia, huku makubaliano ya mwisho yakitarajiwa kutiwa saini tarehe 30/06/2015. Jambo la kushangaza ni kwamba mara baada ya kukamilika kwa usomaji wa taarifa ya pamoja kati ya pande hizi, Rais wa Marekani Obama alitokea na kutoa hotuba mbele ya waandishi wa habari katika Ikulu ya Marekani akitangaza kuwa makubaliano haya ni ya kihistoria. Hivyo, ni nini kipo nyuma ya makubaliano haya? Na Mwenyezi Mungu akubariki.

Jibu:

Ili jibu liwe wazi, tunapitia mambo yafuatayo:

1- Mara tu baada ya makubaliano hayo, Rais wa Marekani alitoa hotuba katika Ikulu ya Marekani iliyohusu makubaliano haya, akisema: "Tumefikia maelewano ya kihistoria na Iran kuhusu mpango wake wa nyuklia, ambayo yakitekelezwa yataizuia Tehran kupata silaha ya nyuklia." Alisema pia, "Tumefikia dili ya kusitisha maendeleo ya Iran katika mpango wa nyuklia," na kuongeza kuwa "Tehran imetekeleza wajibu wake na kufungua mlango wa uhakiki wa jambo hili." Alielezea dili hiyo kuwa ni "nzuri inayofikia malengo yetu ya msingi" na kusema "Iran imekubali mfumo wa ufuatiliaji wa uhakiki ambao haujawahi kushuhudiwa, na mlango utafungwa kwa Iran kurutubisha urani, pia akiba nyingi ya urani iliyorutubishwa na mashinepewa (centrifuges) itapunguzwa kwa theluthi mbili." Aliongeza kuwa "Iran haitaruhusiwa kamwe kutengeneza silaha ya nyuklia, na kwa upande mwingine, tutalegeza hatua kwa hatua vikwazo tulivyoweka sisi na vile vya Baraza la Usalama." Alibainisha kuwa "mazungumzo yataendelea hadi Juni kwa ajili ya kukubaliana kuhusu maelezo ya kina" na akasisitiza kuwa "wakaguzi wa nyuklia watakuwa na mamlaka ambayo hayajawahi kushuhudiwa kwenye vituo vya nyuklia vya Iran." Alisema: "Kwa upande wa watu wa Iran, tuko tayari kufanya kazi kwa ajili ya maslahi ya pamoja" (Radio Sawa ya Marekani 02/04/2015)... Matamshi haya ya Rais wa Marekani yanaonyesha jinsi utawala wa Marekani ulivyokuwa na hamu ya kufikia makubaliano haya, na kwamba makubaliano haya yalikuwa kwa maslahi ya Marekani ambapo imepata kile ilichotaka. Aidha, hakuna hoja kwa wengine kuyapinga, kwani aligusia msimamo wa wapinzani wa makubaliano hayo kutoka chama cha Republican katika Congress na Waziri Mkuu wa dola ya Kiyahudi, Netanyahu. Obama aliongeza kuwa anataka kufanya kazi na Iran chini ya kile kinachoitwa maslahi ya pamoja, yaani kuitumia Iran kufikia miradi ya Marekani katika kanda hiyo. Hivyo, hataki Iran ibaki ikishughulishwa na vitisho vya dola ya Kiyahudi, na uchochezi wa mataifa matatu ya Ulaya (Uingereza, Ufaransa, na Ujerumani), na kuzushiwa matatizo mapya, na kuifanya iendelee kutaabika chini ya vikwazo.

2- Iran "imekubali kupunguza akiba ya urani iliyorutubishwa kwa kiwango cha chini kutoka kilo 10,000 hadi kilo 300 za urani iliyorutubishwa kwa asilimia 3.67 kwa muda wa miaka 15. Imeahidi kutojenga vituo vipya vya nyuklia vya kurutubisha urani kwa miaka 15. Pia imekubali kupunguza mashinepewa (centrifuges) zilizowekwa kwa theluthi mbili kutoka 19,000 za sasa hadi 6,104 chini ya makubaliano hayo, ambapo 5,060 pekee ndizo ziturutubisha urani kwa miaka 10. Kituo cha Natanz kitakuwa ndicho pekee kitakachorutubisha urani nchini Iran (kwa kiwango cha chini). Iran haitarutubisha urani katika kituo cha Fordo kwa miaka 15, bali itakitumia kwa ajili ya utafiti wa nyuklia na fizikia. Iran imejifunga kwa mpango wa urutubishaji na utafiti itakaowasilisha kwa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA) unaohakikisha kuzuiliwa kwake kutengeneza bomu la nyuklia kwa miaka 10. Makubaliano hayo yanawapa waangalizi wa kimataifa haki ya kufuatilia migodi ya urani na maeneo ya kutengeneza yellowcake kwa miaka 25. Waangalizi wa kimataifa wana haki ya ufuatiliaji endelevu wa mashinepewa na maghala kwa miaka 20 huku kukiwa na usitishaji wa utengenezaji wa mashinepewa." (Asharq Al-Awsat 03/04/2015). Rais wa Iran, Hassan Rouhani, alitangaza: "Iran itatekeleza ahadi zote ilizozitoa mradi tu upande mwingine utekeleze ahadi zake." (Ukurasa wa Al-Alam wa Iran 03/04/2015). Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Javad Zarif, alisema: "Kuondolewa kwa vikwazo kutakuwa hatua kubwa mbele. Tumesitisha mkondo ambao haukuwa unahitajika na kila mtu. Haukuwa unahitajika kwa mchakato wa kuzuia kuenea kwa silaha za nyuklia au upande mwingine wowote." (Radio Sawa ya Marekani 02/04/2015). Inaonekana kutokana na hili kuwa Iran imekubali kusitisha shughuli zake za kuongeza urutubishaji wa urani na kukubali urutubishaji uwe wa kiwango cha chini kabisa, kiasi kwamba haiwezekani kutengeneza silaha ya nyuklia. Imepunguza idadi ya mashinepewa hadi theluthi moja. Na itabaki chini ya ufuatiliaji wa kimataifa kwa miaka 25. Itajifunga na masharti hayo katika kipindi chote hicho kama alivyotangaza Rais wake. Kile kinachoihusu Iran ni kuondolewa kwa vikwazo, kama Javad Zarif alivyosema: "Vikwazo vilivyowekwa dhidi ya Iran vitakwisha wakati hatua zilizokubaliwa na mataifa makubwa zitakapotelekezwa." Vilevile, ili icheze nafasi iliyopangwa kwa ajili yake na Marekani katika kanda hiyo na kufikia maslahi yake ya kitaifa, kama baadhi ya viongozi wake walivyoanza kutamka kuhusu ndoto ya himaya (empire) ya Kiirani. Kwa ajili hiyo, imedhabihu mpango wake wa nyuklia!

3- Kuhusu mataifa mengine ya kundi la "5+1", ilikuwa wazi kuwa nafasi yao ilikuwa ya kando tu. Mazungumzo halisi katika hali nyingi yalikuwa kati ya Marekani na Iran pekee, tena waziwazi na si kwa siri. Nafasi ya wengine ilikuwa karibu zaidi na ya mtazamaji kuliko mchezaji. Dalili zilionyesha kuwa Marekani ilikuwa imekamilisha makubaliano na Iran, na suala lililobaki lilikuwa ni mchakato wa utoaji (production) kwa hatua ambazo nchi nyingine za kundi hilo zilikuwa zikizitazama. Walipoona kitu wasichokipenda, walikasirika (sulk), wakatoka ili kutulizwa kisha wanarudi kutia saini au wanatuma wawakilishi badala yao! Hili lilidhihirika katika misimamo ya mawaziri wa nchi hizi... Lavrov alisema wakati wa ziara yake nchini Tajikistan kuwa "hali si ya kawaida, haina mfano wake..." Akabainisha kuwa "kiini cha hatua ya sasa kipo katika kuandaa makubaliano ya kiunzi cha kisiasa na imekuwa wazi katika vipengele vyake vyote." Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Urusi, Alexander Lukashevich, alisema: "Urusi haioni ulazima wa dharura wa Waziri wake wa Mambo ya Nje, Sergey Lavrov, kurudi Lausanne, na kile wanachokifanya washiriki wa mazungumzo kwa sasa ni kuhakiki makubaliano ya kimsingi..." (Russia Today, Novosti ya Urusi 02/04/2015). Inaonekana kutokana na maneno ya Warusi kuwa jambo hili lilikuwa limeandaliwa mapema na kukamilika, na kilichobaki ni kutia saini tu, ndiyo maana hawakuona haja ya waziri wao kwenda kutia saini. Yeye ndiye aliyesema kuwa jambo hili si la kawaida, akimaanisha Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani ambaye ndiye aliyekuwa akikutana zaidi na Wairani, wakiongozwa na Javad Zarif, tangu wiki kadhaa zilizopita akiwa peke yake... Na akazidisha mikutano hiyo bila kusimama katika wiki ya mwisho tangu tarehe 26/03/2015 hadi wakati wa kutia saini ulipofika mwishoni mwa mwezi uliopita, ndipo mawaziri wa mambo ya nje wa nchi nyingine za kundi hilo walipoitwa kushiriki kutia saini! Lakini kabla ya kutia saini kwa siku moja, waliacha mikutano walipokuta kila kitu kimeandaliwa, na kwamba Marekani inasisitiza kutia saini kama kilivyo. Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa alitoka kwa mlango wa nyuma kwa hasira, na yule wa Ujerumani alikuwa karibu kusafiri kwenda nchi za Baltic, na yule wa Urusi kama tulivyotaja hapo juu hakurudi bali alimwacha naibu wake. Ama Mchina, alionekana kama jambo halimuhusu, na yule wa Muingereza alitawaliwa na baridi yake ya kawaida, hakuondoka wala kuonyesha hasira wala kuridhika, bali alikuwa akisubiri kitakachotokea kwa mujibu wa tabia ya hila ya Waingereza... Lakini hatimaye wote walirudi kwenye kikao cha sherehe za kutia saini, lakini ili kuhifadhi heshima yao, walianza kujadili kile kilichoandaliwa na Marekani, na mjadala uliendelea kwa siku mbili, kisha wakatia saini makubaliano hayo bila kuweza, au kuruhusiwa, kubadilisha jambo lolote la maana ndani yake! Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi alizingatia kuwa makubaliano yalikuwa yamekamilika kati ya Marekani na Iran kabla ya siku hiyo, na kutia saini sasa si chochote isipokuwa suala la kisiasa tu, ndiyo maana hakuona haja ya kuhudhuria Lausanne na naibu wake akatia saini kwa niaba yake. Hivyo, nafasi kuu katika makubaliano hayo ilikuwa ya Marekani na Iran...

4- Wanachama wa Republican wanaodhibiti Congress walionyesha kutokuridhika kwao na makubaliano hayo kwa sababu za kichama na malengo ya uchaguzi ujao. Utawala wa Obama ulinitia saini licha ya upinzani wao ili utawala huu upate mafanikio katika sera za kigeni na kuweza kuitumia Iran kutekeleza miradi na mipango yake katika kanda hiyo. Spika wa Bunge la Marekani, John Boehner, alitoa tamko akisema: "Vigezo vya makubaliano ya mwisho vinawakilisha tofauti inayotia wasiwasi ikilinganishwa na malengo ya kimsingi yaliyowekwa na Ikulu ya Marekani." Alisema "Congress lazima iwe na haki ya kuangalia kwa kikamilifu maelezo ya makubaliano yoyote kabla ya vikwazo kuondolewa. Kiunzi cha makubaliano kilichotangazwa Alhamisi 02/04/2015 kinawakilisha mchepuko unaotia wasiwasi kutoka kwenye malengo ya awali ya Obama," (AFP 03/04/2015). Imepangwa kuwa Kamati ya Mambo ya Nje katika Congress itapiga kura tarehe 14 ya mwezi huu kuhusu pendekezo linaloulazimisha utawala wa Obama kuwasilisha makubaliano hayo bungeni na kisha yapigiwe kura. Lakini utawala wa Obama unakataa hilo na kusema kuwa kufikia makubaliano kama hayo ni mamlaka ya serikali kuu pekee na kuingilia kwa Congress katika suala hilo kutatengeneza mfano mbaya wa kisheria.

5- Kuhusu msimamo wa dola ya Kiyahudi, Netanyahu alitangaza akisema: "Makubaliano ya kiunzi kuhusu faili la nyuklia la Iran yanatishia kuendelea kuwepo kwa Israel" (AFP 03/04/2015). Ikumbukwe kwamba kabla ya kutangazwa kwa makubaliano hayo huko Lausanne, alidai kuwa makubaliano yoyote lazima yawe na kipengele cha "kupunguza kwa kiasi kikubwa uwezo wa nyuklia wa Iran" na kusema "Makubaliano bora yatapunguza miundombinu ya nyuklia. Makubaliano bora yataunganisha kuondolewa kwa vikwazo vilivyowekwa kutokana na mpango wa nyuklia wa Tehran na mabadiliko ya tabia ya Iran" (Reuters 01/04/2015), na hilo limetimia kwake katika makubaliano ya Lausanne. Hivyo, msimamo wa Netanyahu ni wa kuitisha (blackmail) ili kupata msaada zaidi na ahadi za Marekani za kuilinda dola ya Kiyahudi, na kusisitiza msimamo wake wa awali aliouonyesha kuhusu suala hili kwa madhumuni ya uchaguzi ambao alishinda, na kuimarisha uhusiano wake na Republicans wanaokuja madarakani kama anavyowaona katika uchaguzi ujao wa Rais wa Marekani mwaka 2016. Ndiyo maana Netanyahu alienda Marekani kutoa hotuba katika Congress kufuatia mwaliko wa Republicans na kuzungumzia hatari za makubaliano na Iran. Anajua kuwa makubaliano hayo yanadhoofisha uwezo wa Iran wa kutengeneza silaha za nyuklia, na anajua kuwa Iran inacheza nafasi katika kanda hiyo iliyopangwa na Marekani inayoinufaisha dola ya Kiyahudi kwa kiasi kikubwa, ambapo Iran inalinda utawala wa Syria unaoihakikishia usalama katika eneo la Golan na kuishughulisha kanda hiyo na vita vya ndani na kuzuia umoja wa Umma wa Kiislamu na utekelezaji wa mradi wake ambao ni kusimamisha Khilafah. Obama alisisitiza katika mazungumzo ya simu na Netanyahu ahadi ya Marekani ya kuilinda dola ya Kiyahudi... na Obama aliiagiza timu yake ya usalama "kuimarisha mazungumzo na serikali mpya ya Israel kuhusu njia za kuimarisha ushirikiano wa kiusalama kati ya nchi hizo mbili," (AFP 03/04/2015).

Kutokana na hayo yote, inabainika yafuatayo:

A- Marekani ndiyo iliyoandaa na "kupika" makubaliano haya na Iran, kama ilivyoandaa na kupika makubaliano ya Geneva mnamo 24/11/2013, na ilibaki kwa mataifa mengine matano kuyasoma makubaliano hayo ili yatiwe saini haraka. Lakini yalichelewa kwa siku mbili kwa sababu ya mijadala iliyoruhusiwa kwa nchi nyingine ili kuhifadhi heshima yao... kisha wakayakubali na kuyatia saini.

B- Lengo la Marekani ni kupunguza shinikizo na vikwazo dhidi ya Iran au kuviondoa kabisa ili iweze kuitumia Iran katika kanda hiyo na icheze nafasi iliyopangwa kwa ajili yake na Marekani. Kwa ajili hii, utawala wa Obama umeweka uzito wake wote na kuelekeza fikra zake zote kukamilisha makubaliano haya, na ili yahesabike kama mafanikio yake katika sera za kigeni, ndiyo maana Rais wa Marekani ameyataja kama maelewano ya kihistoria.

C- Kinasalia mbele ya utawala wa Obama kikwazo cha Republicans katika Congress ambao wanafanya kazi ili kutoonyesha kuwa utawala wa Obama wa chama cha Democrat umefanikiwa kwa sababu za uchaguzi. Wanataka kumfanya Rais awe chini ya udhibiti wao. Na inavyoonekana, mgogoro kati ya pande hizo mbili utaendelea. Inatarajiwa kuwa utawala wa Obama utaweza kuondoa baadhi ya vikwazo ulivyoweka dhidi ya Iran, lakini kuna baadhi ya vikwazo ambavyo utawala huu hautaweza kuviondoa isipokuwa kwa idhini ya Congress. Kwa hivyo, kuna uwezekano baadhi ya vikwazo dhidi ya Iran vikabaki vimesitishwa hadi wakati mwingine.

D- Msimamo wa Netanyahu, Waziri Mkuu wa dola ya Kiyahudi, ni wa kuitisha ili kupata msaada zaidi na ahadi za Marekani za kulinda chombo chake, na kusisitiza msimamo wake wa awali aliouonyesha kuhusu suala hili kwa ajili ya uchaguzi ambao alishinda, na kuimarisha uhusiano wake na Republicans kwa kudhani kuwa wao ndio watakaokuja madarakani katika uchaguzi ujao wa Rais wa Marekani, kwa sababu dola ya Kiyahudi haina uthubutu wa kukata kimbilio lake kwa Marekani.

E- Ama Iran, imesalimu amri na kuacha programu zake za kuongeza urutubishaji wa urani na kukubali uwe wa kiwango cha chini kabisa, kiasi kwamba haiwezekani kutengeneza silaha ya nyuklia. Imepunguza idadi ya mashinepewa hadi theluthi moja. Na itabaki chini ya ufuatiliaji wa kimataifa kwa miaka 25. Itajifunga na masharti hayo katika kipindi chote hicho kama alivyotangaza Rais wake. Kile kinachoihusu Iran ni kuondolewa kwa vikwazo na kujiingiza katika kanda hiyo ili kucheza nafasi iliyopangwa kwa ajili yake na Marekani kwa kisingizio cha maslahi ya pamoja na kujipatia nafasi katika kanda hiyo kwa kwenda sambamba na Marekani. Ikiwa mamlaka nchini Iran ingeyafahamu matukio vyema, ingejua kuwa hakuna matunda yanayotarajiwa kutoka kwenye miiba, wala kheri yoyote kutoka kwa Shetani Mkuu, na makubaliano ya nyuklia mjini Lausanne yanashuhudia hilo.

Share Article

Share this article with your network