Swali:
Mazungumzo kuhusu uingiliaji wa kijeshi kaskazini mwa Mali yamepamba moto katika siku za hivi karibuni. Jana, Jumapili tarehe 11/11/2012, viongozi wa Jumuia ya Kiuchumi ya Mataifa ya Afrika Magharibi (ECOWAS) walikutana kujadili kurejesha kaskazini mwa Mali ndani ya mamlaka ya serikali ya Mali. Uamuzi wao ulikuwa wa kusuasua na usio thabiti; waliamua kutuma wanajeshi 3,300 nchini Mali, lakini wakati huo huo walitangaza kuwa mlango wa suluhu ya kisiasa haujafungwa, bali wameacha mlango wa mazungumzo wazi... Hii ilifuatia azimio la Baraza la Usalama namba 2071 la tarehe 15/10/2012 lililoipa jumuia hii muhula wa siku 45... Katikati ya hayo, misimamo ya madola makubwa yenye ushawishi wa kikoloni barani Afrika ilikuwa ikishika kasi; Ufaransa ilikuwa ikisisitiza zaidi uingiliaji wa kijeshi, ikifuatiwa na Marekani kwa kiasi kidogo, huku Uingereza ikionekana kutokuwa na shauku kubwa... Lakini la kustaajabisha ni kwamba Algeria ndiyo kitovu cha jambo hili, kwani ziara za maafisa wa nchi hizi kwenda huko zimekuwa za mara kwa mara, huku ujumbe mmoja ukiingia na mwingine kutoka... na bado inaendelea kupinga uingiliaji wa kijeshi.
Swali ni: Kwa nini Algeria imekuwa uwanja wa ushindani kati ya nchi hizi katika masuala ya mawasiliano, hususan kutoka Marekani na Ufaransa? Kisha kwa nini sauti ya Uingereza inaonekana kuwa ya chini? Na ni nini misimamo ya nchi hizi na malengo yao kupitia mawasiliano yao na Algeria?
Jibu:
Ili jibu liwe wazi, ni lazima kwanza tuangalie mambo mawili muhimu:
Kwanza: Ukweli wa kisiasa wa Algeria... Pili: Mapinduzi ya Mali...
Kuhusu ukweli wa kisiasa wa Algeria:
Inajulikana kuwa Rais Bouteflika, ambaye alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje wakati wa utawala wa Houari Boumédiène, amefuata nyayo za Boumédiène ambaye alikuwa na uhusiano na Waingereza. Boumédiène aliingia madarakani kupitia mapinduzi ya kijeshi aliyoyaongoza mwaka 1965 dhidi ya Ahmed Ben Bella aliyekuwa akiiunga mkono Marekani. Utawala uliendelea kuendeshwa na vibaraka wa Waingereza hadi vibaraka wa Ufaransa jeshini walipofanya mapinduzi mwaka 1992, ili kuzuia chama cha Islamic Salvation Front (FIS) kuingia madarakani baada ya kushinda uchaguzi... Kisha walimlazimisha Chadli Bendjedid kujiuzulu... Baada ya hapo, jeshi likawa linadhibiti nchi lakini likashindwa kuiendesha, na utawala ukawa wa machafuko. Baada ya kumlazimisha Chadli kujiuzulu mwaka 1992, walimleta Mohamed Boudiaf ambaye kisha aliuawa, kisha wakaja na Ali Kafi na baadae wakamwondoa. Kisha wakakabidhi utawala kwa Waziri wa Ulinzi Jenerali Liamine Zéroual, mmoja wa watu wao, lakini hawakuweza kutatua matokeo ya mapinduzi yao na kutuliza hali nchini baada ya kufanya mauaji ya kinyama dhidi ya watu wa Algeria ambao ni Waislamu... Mwaka 1999, walikubaliana na Abdelaziz Bouteflika kuwa Rais kwa sharti kwamba asiwahusishe na makosa yoyote ya jinai na uharibifu wa nchi, na afanye kazi ya kutibu majeraha kwa kuitisha amani na maridhiano... Hivyo akawa Rais tangu 1999 hadi leo, baada ya kutangazwa mshindi katika uchaguzi wa 2004 na kisha 2009. Bouteflika bado ana uhusiano wa karibu na Uingereza, na alidhihirisha hilo kwa kuitembelea Uingereza mwaka 2006, ikiwa ni ziara ya kwanza ya rais wa Algeria nchini humo. Ingawa kundi la Ufaransa jeshini nchini Algeria lina ushawishi kwa kiasi fulani, wanatambua uhusiano wa Bouteflika na Uingereza, na pia wanajua kuwa Bouteflika hakuwa na maelewano na sera ya Ufaransa. Alikataa mradi wa Umoja wa Mediterania uliopendekezwa na Ufaransa wakati wa Sarkozy, na miradi ya makubaliano yaliyozungumzwa mwaka 2008 wakati wa ziara ya Sarkozy nchini Algeria haikutekelezwa... Licha ya hayo yote wanayoyajua, wananyamaza kwa sababu mafaili ya uhalifu wa viongozi wa kundi hili dhidi ya watu wa Algeria hayajafungwa, na wakati wowote Bouteflika anaweza kuyatumia dhidi yao ikiwa watafikiria kufanya mapinduzi dhidi yake. Kwa hivyo, hawajapinga sera zake hususan anapokubaliana nao katika kulinda usekulari na jamhuri wanayoienzi.
Hivyo, mwelekeo mkuu wa kisiasa wa Rais wa Algeria unafuata sera ya Uingereza katika suala la Mali kama itakavyobainishwa baadaye.
Kuhusu mapinduzi ya Mali, yalitokea tarehe 22/3/2012, na ilikuwa wazi kuwa Marekani ilikuwa nyuma yake. Marekani imekuwa ikifanya kazi ya kutafuta ushawishi nchini Mali, na mwanzo wa hilo ulikuwa ni kusaini mikataba na Mali kwa ajili ya kufundisha vikosi vya Mali kupambana na ugaidi na mbinu za kupambana na makundi ya waasi. Ilikuwa ikichagua maafisa na kuwapeleka Marekani kwa mafunzo. Tovuti ya Al-Asr tarehe 24/3/2012 ilinukuu vyanzo vya Kimarekani vyenye habari kuwa mwanadiplomasia wa Marekani aliyeomba jina lake lisitajwe aliiambia vyombo vya habari: "Kiongozi wa mapinduzi, Kapteni Amadou Sanogo, alichaguliwa miongoni mwa maafisa wasomi na ubalozi wa Marekani kupata mafunzo ya kijeshi ya kupambana na ugaidi nchini Marekani." Aliongeza kuwa "Sanogo alisafiri mara kadhaa kwenda Marekani kwa misheni maalum...".
Lengo la mapinduzi hayo lilikuwa kuondoa ushawishi wa Ufaransa nchini Mali uliokuwa tegemeo lake kuu, na kisha kuuweka ushawishi wa Marekani mahali pake.
Tayari tulishafafanua jambo hili kwa kina katika jibu la swali la tarehe 24/3/2012.
Sasa, baada ya kupitia mambo hayo mawili yaliyotangulia, jibu la swali linaweza kuwa kama ifuatavyo:
1- Kupungua kwa sauti ya Uingereza katika suala la uingiliaji wa kijeshi kunasababishwa na ukweli kwamba tatizo liko hasa kati ya Marekani na Ufaransa. Marekani iko nyuma ya mapinduzi hayo ili kung'oa ushawishi wa Ufaransa katika eneo hilo... Kwa hivyo, Uingereza kama ilivyo desturi yake, inataka pande zote mbili zishughulike na jambo hili ili mgogoro huo uwaidhoofishe, na yenyewe iwe mshindi au angalau isiwe mpotezaji!
Kuhusu msimamo wake wakati wa ziara za maafisa wake nchini Algeria kuhusiana na Mali, ulikuwa ni msimamo wa ujanja; wakionekana kuunga mkono uingiliaji wa kijeshi na wakati huo huo wakiiunga mkono Algeria katika kutounga mkono uingiliaji huo! Balozi wa Uingereza nchini Algeria, Martyn Roper, alitangaza: "Uingereza inasimama upande wa Algeria katika hatua hii ngumu sana," akisema "Uingereza inapendelea suluhu ya amani ikiwa inawezekana." (Gazeti la Al-Khabar la Algeria 22/6/2012). Alistair Burt, Waziri wa Uingereza anayeshughulikia Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini, alitembelea Algeria tarehe 23/6/2012 na kusoma hali ya kaskazini mwa Mali na kuimarisha uhusiano na maafisa wa Algeria kwa muda wa siku tatu. "Alithamini msimamo wa Algeria wa kukataa uingiliaji wa kijeshi kumaliza tatizo la uasi kaskazini mwa Mali, akisema kuwa Uingereza inaunga mkono utatuzi wa mgogoro katika eneo la Sahel kupitia mazungumzo." (Ukurasa wa Essalam Alyoum wa Algeria 24/6/2012). Uingereza haitaki Algeria ya Bouteflika iingie kwenye uingiliaji wa kijeshi kaskazini mwa Mali kwa sababu hiyo itatoa fursa kwa Marekani kuishawishi Algeria ili kueneza ushawishi wake katika nchi hiyo, jambo ambalo litakuwa kwa gharama ya ushawishi wa Uingereza nchini Algeria na Afrika Kaskazini.
Msimamo huu wa ujanja wa Uingereza uliakisiwa kwenye Algeria ya Bouteflika. Ndio maana matamshi ya Algeria upande mmoja yanakataa uingiliaji, na upande mwingine yanautaka kwa kusema suluhu ya kisiasa, na pia kusema kupambana na ugaidi kaskazini mwa Mali! Yaani inafanya msimamo wake kuwa wa giza. Inasema uingiliaji una athari mbaya hususan kwa watu wa Tuareg na lazima kuwe na suluhu ya kisiasa, lakini wakati huo huo inasema suluhu ya kijeshi ni muhimu dhidi ya ugaidi! Kama ilivyokuja katika taarifa ya msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Algeria, Amar Belani, akisema: "Tunaona kuwa matumizi ya nguvu lazima yafanyike kwa busara ili kuepuka mkanganyiko wowote kati ya wakazi wa Mali wa kabila la Tuareg ambao wana madai ya msingi, na makundi ya kigaidi na walanguzi wa dawa za kulevya ambao lazima wawe walengo wa kwanza kwa kuwa ndio chanzo cha hatari inayotishia eneo." (AFP 30/10/2012). Kwa hivyo, inashika fimbo katikati kwa namna ya Waingereza ili kuacha mgogoro kati ya Marekani na Ufaransa ukiwaka, na wakati huo huo ukae mbali nayo... Na kwa sababu Uingereza katika sera yake ya sasa haitaki kugongana hadharani na Marekani bali kuivuruga kwa njia nyingine, ndivyo ilivyo Algeria. Ingawa inasimama kidete dhidi ya Ufaransa katika mazungumzo yake kuhusu kaskazini mwa Mali, hadi ikafikia kuahirisha ziara ya Rais wa Ufaransa, lakini inaonyesha mwelekeo na ushirikiano na mashinikizo ya Marekani. Haiwezi kuahirisha ziara ya waziri wa Marekani wakati ziara ya rais wa Ufaransa inahairishwa! Inaonekana kuwa kuridhisha Marekani ndiko kulikuwa nyuma ya ombi lake kwa Ufaransa kuahirisha ziara ya Rais François Hollande. Inachukua msimamo mkali kwa Ufaransa, lakini inaonyesha ulaini katika matamshi yake kwa Marekani kama inavyoonekana kutokana na mwendo wa mambo.
2- Kuhusu Ufaransa, ilipata pigo kubwa kufuatia mapinduzi ya Mali, na suala hilo limekuwa la kufa na kupona kwao. Ikiwa haitaweza kurejesha ushawishi wake nchini Mali, basi ushawishi wake barani Afrika utaisha hatua kwa hatua. Ndio maana inafanya kazi kwa bidii kwa ajili ya uingiliaji wa kimataifa wa kijeshi na kuirejesha Mali chini ya himaya yake. Haitaki vibaraka wa Marekani wabaki madarakani kusini mwa Mali, na kuwe na "nusu-dola" kaskazini mwa Mali, jambo ambalo litafanya iwe vigumu kueneza ushawishi wake kama awali.
Ndio maana Ufaransa inahangaika sana kutaka uingiliaji wa kijeshi kaskazini mwa Mali, kwa sababu ushawishi wake umepata pigo kubwa baada ya mapinduzi ya kijeshi yaliyofanywa na maafisa wadogo walio na mfungamano na Marekani tarehe 22/3/2012. Ushawishi huu uko hatarini kuanguka katika eneo zima ikiwa Ufaransa haitaweza kutatua suala la Mali na kaskazini yake. Ndio maana tunaiona ikifanya kazi kwa bidii katika Baraza la Usalama kutoa maazimio yanayohusu uingiliaji wa kijeshi na kuwasiliana na nchi za eneo hilo, hususan Algeria...
Msimamo wake katika mawasiliano na Algeria ni kuhimiza kwa nguvu uingiliaji wa kijeshi, lakini Algeria haijaitikia. Gazeti la Al-Khabar la Algeria lilinukuu gazeti la Le Canard enchaîné la Ufaransa tarehe 31/10/2012 kwamba "kuchelewa kwa ziara ya Rais wa Ufaransa Hollande nchini Algeria ambayo ilipangwa mwezi Novemba hadi mwezi Desemba kulikuwa kufuatia ombi la Rais wa Algeria Bouteflika." Ilibainisha kuwa "Ufaransa inatuma ishara za urafiki (kwa Algeria) kama vile ziara za Waziri wa Mambo ya Nje Laurent Fabius na Waziri wa Mambo ya Ndani Manuel Valls na kukiri kwa ikulu ya Élysée kuhusu hali ya umwagaji damu ya matukio ya tarehe 17/Oktoba 1961." Ilinukuu kutoka kwa "washauri wa Hollande kuwa alikuwa na matumaini ya kumshawishi Bouteflika asikae kimya mbele ya makundi ya Kiislamu yenye silaha yanayodhibiti kaskazini mwa Mali." Licha ya yote haya, Algeria haikuitikia... Hivyo, lengo la Ufaransa ni kurejesha ushawishi wake nchini Mali haraka iwezekanavyo, na inaona njia ya kufanya hivyo ni uingiliaji wa kijeshi ili kukalia kaskazini mwa Mali na kisha kuelekea kusini ikitumia "ushindi" huo, na kuwafanya watu wake kusini mwa Mali kuanza harakati kama mstari wa mbele wa Ufaransa.
3- Ama Marekani, ingawa inataka uingiliaji ili kuwaunga mkono watu wake kusini mwa Mali, haina haraka na uingiliaji huo. Badala yake, inataka kutumia tatizo la Mali kuivuta Algeria katika ushawishi wake, ikitumaini kuifanya Algeria kuwa kituo chake barani Afrika dhidi ya kile inachokiita ugaidi kama ilivyo Pakistan kwa upande wa Kusini mwa Asia dhidi ya Taliban. Kwa hivyo, imeongeza harakati zake nchini Algeria kwa kisingizio cha Mali, lakini mazungumzo yanajikita kwenye mambo mengine!
Hii ina maana kwamba Marekani inajali zaidi sasa kuingiza ushawishi wake Algeria ili kuanzia hapo kuelekea Afrika zaidi kuliko inavyojali uingiliaji wa kijeshi kaskazini mwa Mali. Ingawa uingiliaji huu ni sehemu ya sera yake, inataka uwe njia ya kuingiza ushawishi wake Algeria. Wakati huo huo, haitaki Ufaransa iwe na nafasi yenye ushawishi katika uingiliaji huo wa kijeshi wakati Marekani itakapoamua kwa dhati kuukubali.
Mawasiliano ya maafisa wake na Algeria yanaonekana kwa nje kama kujadili kaskazini mwa Mali, lakini ukweli ni kutafuta kuanzisha mafungamano na Algeria. Hii inabainika wazi kwa kuangalia ziara zake za hivi karibuni nchini Algeria. Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Hillary Clinton alitembelea Algeria na kukutana na Rais Abdelaziz Bouteflika tarehe 29/10/2012. Clinton alitangaza mwishoni mwa mkutano wake na Rais wa Algeria akisema: "Tumejadili uhusiano wetu wa nchi mbili ambao ni imara sana, na tukaashiria kuwa tumetoka kufanya kongamano bora la mazungumzo ya kimkakati yaliyoandaliwa na Washington wiki iliyopita. Tulikuwa na mazungumzo ya kina sana kuhusu hali ya eneo hili na hususan nchini Mali." (AFP, Reuters 30/10/2012).
Alitaja uhusiano wa nchi mbili na mazungumzo ya kimkakati... kisha akataja mazungumzo ya kina kuhusu eneo na hasa Mali. Lengo lilikuwa Algeria kwanza kabla ya hali ya Mali. Kinachothibitisha umuhimu huu kwa Algeria ni kwamba Clinton alimwacha msaidizi wake, Elizabeth Jones, kuendelea na mazungumzo na maafisa, jambo linaloashiria kuwa kuna mambo ambayo Marekani iliweza kuyafanikisha katika ziara hii na kwamba msaidizi wa waziri anafanya kazi ya kuyakamilisha. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Algeria, Amar Belani, alisema kuhusiana na hilo: "Mazungumzo yaliyofanyika kati ya Waziri wa Mambo ya Nje Mourad Medelci na Msaidizi wa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Elizabeth Jones yaliruhusu kutathmini matokeo yaliyorekodiwa katika kikao cha kwanza cha mazungumzo ya kimkakati kati ya Algeria na Marekani na kuimarisha mashauriano kuhusu masuala kadhaa ya kikanda." (Shirika la Habari la Algeria 1/11/2012).
Isitoshe, Marekani haitaki kuipa Ufaransa nafasi yoyote kuu katika uingiliaji wowote ikiwa itaamua kuingilia eneo hili, na haitaki kuisaidia katika kufanya misheni ya kijeshi huko, kwa sababu kimsingi inalenga kuondoa ushawishi wa Ufaransa nchini Mali na eneo hilo. Marekani sasa inajali zaidi Algeria na kueneza ushawishi wake huko, ikitumia suala la kaskazini mwa Mali kama kisingizio. Inafanya kazi kutafuta njia za kufikia lengo hili, na kubwa zaidi ni kufanya kazi ya kuanzisha ushirikiano wa kimkakati na Algeria kama ilivyofanya na Pakistan, Afghanistan, Iraq, na Uturuki. Ndio maana inafanya mazungumzo yanayolenga kuanzisha ushirikiano huu ambao ni mbinu ya kuleta ushawishi nchini kupitia ushirikiano wa kiusalama, kijeshi, na kiuchumi.
4- Watu wengi wa Algeria wanatambua kuwa nchi yao inalengwa na Marekani. Gazeti la Al-Khabar la Algeria mnamo 29/10/2012 lilimnukuu mkuu wa koo za Tuareg huko Tamanrasset (kilomita 2,000 kusini mwa mji mkuu) akikataa uingiliaji wa kijeshi kaskazini mwa Mali, akiona kuwa huo ni "utangulizi wa kuanzisha vituo vya kijeshi jangwani." Gazeti hilo hilo lilimnukuu mbunge mmoja katika eneo la Hoggar akisema: "Kile kinachoombwa na Marekani na Ufaransa kuhusu uingiliaji wa kigeni kitasababisha matatizo mengi, na sisi kama wakuu wa eneo la Hoggar tunaitaka Algeria kusimama kidete katika msimamo wake dhidi ya uingiliaji wa kigeni." Vilevile, Shirika la Habari la Kituruki la Anadolu mnamo 31/10/2012 lilimnukuu Abdelaziz Rahabi, aliyewahi kuwa Waziri wa Mawasiliano na msemaji wa serikali, akisema: "Wamarekani wanaweza kuitaka Algeria kucheza nafasi inayofanana na ile ya Pakistan katika vita vya kimataifa dhidi ya harakati ya Taliban na Al-Qaeda ndani ya ardhi ya Afghanistan." Akifafanua kuwa "Algeria itatakiwa kutoa usaidizi wa kiihabari au kuruhusu ndege kupita..."
Pamoja na haya yote, Algeria inaonyesha unyumbufu na ulaini kwa mawasiliano ya Marekani kwa namna iliyo wazi, kama njia ya kwenda nayo sawa kama ifanyavyo Uingereza. Bila shaka Marekani inatambua hilo, lakini kama inavyoonekana, inaona kuwa kwenda sawa ni hatua ya kwanza ya ushiriki. Ushawishi unavyouona, ni kwa kutumia vivutio vya kiuchumi, au kusingizia ugaidi, au njia nyingine za shinikizo...! Kwa vyovyote vile, unyumbufu huu uko wazi kupitia ziara kadhaa za maafisa wa Marekani nchini Algeria miezi ya hivi karibuni. Waziri wa Mambo ya Nje wa Algeria Mourad Medelci, wakati wa ziara yake mjini Washington mwezi Septemba uliopita, alisifu maendeleo katika uhusiano kati ya Marekani na Algeria na mashauriano kati yao kuhusu maeneo ya mvutano katika kanda hiyo, akisema: "Kuna uratibu na ushirikiano kati ya nchi za Sahel na nchi washirika, ikiwemo Marekani, ili kutoa mazingira mwafaka ya kupambana na ugaidi kupitia mifumo ya habari, teknolojia, na vifaa." Aliashiria maendeleo ya uhusiano kati ya Algeria na Washington katika upande wa ushirikiano wa kijeshi na kiuchumi, akizingatia kuwa Marekani ndiye mteja mkuu wa kibiashara wa Algeria kwa thamani ya dola bilioni 17 mwaka 2011. (Shirika la Habari la Algeria 1/11/2012). Shirika hilo lilibainisha kuwa mkutano wa pili wa mazungumzo ya kimkakati kati ya nchi hizo mbili utafanyika mwaka ujao nchini Algeria.
Hili lilibainika zaidi kupitia taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Algeria tarehe 28/10/2012, siku moja kabla ya ziara ya Clinton, ikisema: "Ziara ya Clinton inakuja katika muktadha wa kikao cha kwanza cha mazungumzo ya kimkakati kati ya Algeria na Marekani yaliyofanyika tarehe 19 Oktoba mwezi huu mjini Washington, ambayo yalitoa msukumo mkubwa wa mashauriano ya kisiasa kati ya nchi hizo mbili." Taarifa iliongeza: "Mazungumzo yatajikita katika kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kiusalama kati ya nchi hizo mbili na masuala ya sasa ya kikanda na kimataifa." (Shirika la habari la UPI la Marekani 28/10/2012).
5- Inatuma uchungu kuona nchi za Waislamu, ikiwemo Algeria, Mali na nyinginezo, zikiwa uwanja wa mapambano kati ya madola makubwa kutokana na kutokuwepo kwa Dola ya Khilafah. Madola haya makubwa, ambayo ni madola ya kikoloni ya kikafiri, yanashindania nchi za Waislamu ili kueneza ushawishi wao, kupora rasilimali zao, na kuzuia kurejea kwao katika kuhukumu dini yao katika maisha yao na kusimamisha mfumo unaotokana nayo uliodhihirishwa katika Dola ya Khilafah...
Ingawa mataifa ya Kiislamu yanapinga uingiliaji wowote wa kigeni, serikali zilizopo katika nchi zao zinaridhia uingiliaji huu. Serikali hizi ziko tayari kukubali uingiliaji wa kigeni, bali ni vibaraka wa madola ya kikoloni ya kikafiri, kwa sababu zilianzishwa kwa msingi wa utiifu kwa Magharibi kupitia katiba na mifumo yao, na watawala wao huwekwa ili wafuate misingi hiyo. Wameandaliwa kuwa marafiki na wafuasi wa nchi hizi. Isipopatikana njia ya kuziondoa serikali hizi, katiba zao, watawala wao, na akili za utawala zilizopo, nchi za Waislamu zitabaki kuwa uwanja wa mapambano kati ya nchi hizi. Ikumbukwe kwamba wakati Algeria ilipokuwa jimbo kati ya majimbo ya Dola ya Khilafah ya Kiislamu wakati wa utawala wa Waothmani, Marekani ilikuwa ikiilipia kodi kila wakati meli zake zilipopita katika maji ya jimbo hili la Kiislamu. Kama ilivyoandikwa katika nyaraka za Marekani: "Marekani ilisaini, kwa jina la rais wake na mwanzilishi wake George Washington mwenyewe, makubaliano na gavana wa Algeria, Hassan Pasha, tarehe 5/9/1795 ambapo Marekani ilijitolea kulipa lira za dhahabu 12,000 kila mwaka mkabala wa kupita kwa meli za Marekani katika maji ya jimbo la Algeria, na kulipa mara moja lira za dhahabu 642,000 mkabala wa kuachiwa kwa wafungwa wa Marekani waliokamatwa na vikosi vya majini vya Dola ya Khilafah wakati meli 11 za Marekani zilipopita kwa mara ya kwanza mnamo mwezi wa kumi na kumi na moja mwaka 1793"... Hivi ndivyo Marekani ilivyokuwa ikiitazama Algeria ikiwa jimbo lililo chini ya Dola ya Khilafah. Marekani wakati huo ilikuwa ikiogopa hasira ya Algeria dhidi yake, sembuse kufikiria kuwa na ushawishi nchini Algeria...!
Wajibu wa kila Mwislamu anayemwamini Mwenyezi Mungu (swt) na Mtume Wake (saw) ni kufanya kazi ya kusimamisha Khilafah itakayorejeshea Umma utukufu wake na ushindi wake, na kwanza kabisa kumridhisha Mola wake. Kwani huu ndio Umma bora uliotolewa kwa watu... Huu ndio msingi wa utukufu wa Umma huu na njia ya ushindi wake.
وَلَيَنْصُرَنَّ اللَّهُ مَنْ يَنْصُرُهُ إِنَّ اللَّهَ لَقَوِيٌّ عَزِيزٌ
"Na hakika Mwenyezi Mungu atamnusuru yule anayenusuru (dini) Yake. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye kushinda." (QS Al-Hajj [22]: 40)