Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

Jibu la Swali: Athari za Amerika katika Sera ya India ya Kukabiliana na China

April 12, 2014
3061

Swali:

Mnamo tarehe 7/4/2014, uchaguzi mkuu nchini India ulianza na unatarajiwa kuendelea hadi tarehe 12/5/2014, huku matokeo yakitangazwa tarehe 16/5/2014. Kambi mbili kuu za kisiasa zinachuana: Chama cha Bharatiya Janata (BJP) kinachofungamana na Marekani pamoja na muungano wake, na Chama cha Congress kinachounga mkono Uingereza, ambacho tangu kurejea kwake madarakani kwa ushindi wa uchaguzi wa mwaka 2004, kimeonyesha kusuasua katika uhusiano na Marekani kutokana na mafungamano yake na Uingereza, na kimeonyesha hofu katika kukabiliana na China... Swali ni: Je, Marekani ina athari gani katika sera ya India ya kukabiliana na China? Na nini uhusiano wa jambo hili na mkakati wa Marekani katika eneo la Asia-Pasifiki na kuchochea kwake Australia na Japan kuingia katika makabiliano haya? Je, sera hii itaathiriwa sana na aina ya chama tawala nchini India ikiwa Chama cha Janata au Chama cha Congress kitashinda? Na je, India ina uwezo wa kukabiliana na China? Na vipi mizani ya nguvu kati ya China na India?

Jibu:

Jibu la maswali haya linabainika kwa kupitia mambo yafuatayo:

1- Marekani inafanya kazi kuizingira China kupitia nchi zinazoizunguka na katika Bahari ya Pasifiki, hususan katika bahari za China Mashariki na Kusini. Inajenga aina mbalimbali za miungano na kambi na kuimarisha uhusiano na nchi za huko kwa madhumuni haya. Jambo hili lilianza zaidi ya mwongo mmoja uliopita, na kwa uzito zaidi wakati Marekani ilipoona kuwa sera ya kuidhibiti China imefika mwisho au ukingoni. Hiyo ina maana kuwa haiwezi kuidhibiti China zaidi ya ilivyofanya; ilijikurubisha kwayo kwa kuiingiza katika Shirika la Biashara Duniani (WTO), na uhusiano wa kibiashara uliongezeka, na mazungumzo ya kimkakati ya Marekani na China hayakuwa tena ya tahadhari kama hapo awali... Pamoja na hayo, China haijaingia katika mzunguko wa Marekani, wala kuwa mshirika wake kulingana na sera hiyo. Marekani haikuweza kuzuia matamanio ya China ya kuanzisha utawala wake katika eneo la Bahari ya China Mashariki na Kusini, ambalo China inaliona kuwa ni eneo muhimu, la lazima, na la hatima kwake. China imebaki kuwa nchi inayolinda chombo chake, mshikamano wake, na uhuru wake kama nchi kuu ya kikanda inayofanya kazi kuimarisha nguvu zake kijeshi na kiuchumi, kiasi kwamba imeanza kutumia nguvu yake ya kiuchumi kwa ushawishi wa kisiasa katika baadhi ya maeneo na sio tu kwa ajili ya kupata faida. Inafanya kazi kuimarisha ushawishi wake katika eneo lake, jambo ambalo linakinzana na sera ya Marekani au kuuweka ushawishi wa Marekani hatarini. China ina matamanio ya kikanda ya kudhibiti eneo lake ambalo inaliona kuwa ni la hatima, na haitaki kutosheka tu na ardhi yake kubwa kiasi cha kubaki imefungiwa katika ardhi hiyo kama nchi kubwa kiuchumi... Marekani pia inalichukulia eneo la bahari ya China kama eneo muhimu kwake. Marekani, kwa kiburi chake, haitosheki kuwa nchi ya kikanda ndani ya mipaka ya Amerika mbili, bali inauona ulimwengu mzima kama eneo lake! Kwa hiyo, inashindana na China katika eneo lake ili kupanua utawala wa kimataifa wa Marekani... Hivyo, sera ya udhibiti kwa kujikurubisha kwa China katika uhusiano wa kibiashara na mazungumzo ya kimkakati haikuifanya China kufuata sera za Marekani, wala kuwa mshirika wake kwa maana inayojulikana. Badala yake, sera yake ya kikanda ilianza kuitia wasiwasi Marekani, na hivyo sera ya udhibiti pekee haikuwa na tija tena. Marekani ilianza kuweka mpango wake mpya unaohusu Asia-Pasifiki, ambao unahitaji kukusanya takriban 60% ya nguvu zake za kijeshi za majini katika eneo hili. Hii ni pamoja na sera ya kuizingira China ambayo Marekani iliifuata kwa kuishughulisha China na masuala katika mazingira yake ya kikanda... Marekani imeelekeza juhudi zake katika kuzichochea nchi za eneo hilo katika sera hii ya uzingiraji, na nchi mashuhuri zaidi zinazoweza kuathiri kwa ufanisi uzingiraji huu ni tatu: India, Japan, na Australia...

2- Kuhusu India, ina mpaka na China wenye urefu wa kilomita 3488 na kuna matatizo yanayoendelea kati yao kuhusiana na mpaka huu. Kwa kipindi cha robo karne, duru za mazungumzo zimekuwa zikifanyika, na ya mwisho ilikuwa duru ya kumi na nne ya kuainisha mipaka kati ya nchi hizo mbili, kisha zikasimama na duru ya kumi na tano haikufanyika. Mnamo tarehe 15/4/2013, askari wa China walivuka mpaka na India na kuingia katika ardhi ya India katika eneo la Ladakh na kuweka mahema, lakini waliondoka baada ya wiki tatu katika operesheni ya kuonyesha nguvu iliyofanywa na China kuelekea India ili kuitumia ujumbe kuwa China iko tayari kuvuka mpaka na kuingia vitani nayo kama ilivyotokea mnamo Oktoba 1962, ambapo jeshi la China lilianzisha mashambulizi katika eneo la Arunachal Pradesh na kuyafukuza majeshi ya India. Baada ya mwezi mmoja wa operesheni hiyo, vikosi vya China vilifanya shambulio la pili kwenye ardhi ya India na kuua takriban Wahindi 2000. Jambo hili bado halijatatuliwa na linaitwa "Mstari wa Udhibiti wa Kweli", na ni eneo la msuguano kati ya nchi hizo mbili linalosababisha mvutano wa mara kwa mara. Hii ni pamoja na mvutano unaotokana na tatizo la eneo la Tibet ambalo China ililivamia mwaka 1950, ambalo liko mpakani mwa India. India inashirikiana na Marekani katika kuchochea tatizo hili kwa kuwahifadhi Wabudha wa eneo hili na kiongozi wao Dalai Lama, ambapo India ilimuanzishia Utawala wa Kati wa Tibet kama serikali ya uhamishoni. Sababu hizi zote zinafanya mvutano kati ya India na China kuwa wa kudumu na usiotulia...

3- Marekani ilijaribu kutumia mivutano hii kati ya China na India kwa kuisukuma India kupambana na China au kuchochea matatizo kati yao ili kuishughulisha China na suala hili. Hata hivyo, India ina hofu ya kukabiliana na China ardhini, na kile kilichotokea katika jumbe za mashambulizi ya China kwenye kingo za India kinathibitisha hilo. Kwa hiyo, Marekani ilihitaji vishawishi kwa India ili kuishajiisha kuendelea kuichokoza China na kuishughulisha na matatizo ya mpakani... Hivyo, Marekani iliingia ushirikiano wa kimkakati na India, na pia wakafanya makubaliano ya ushirikiano wa kinyuklia... Marekani pia imetia saini makubaliano kadhaa ya kiuchumi na kiusalama na India; makubaliano ya ulinzi yalifikiwa mwaka 2005 na makubaliano ya ushirikiano wa kinyuklia wa kiraia mwaka 2008, na yote haya yanapanua upeo wa ushirikiano wa usalama kati yao. Matokeo yake, nchi hizo mbili kwa sasa zinashiriki katika mazoezi mengi ya kijeshi ya pamoja ambayo hayajapata kushuhudiwa hapo awali, na mauzo makubwa ya silaha za Marekani kwenda India yanaongezeka kila mara... Wakati Mkuu wa Majeshi ya India, Jenerali Deepak Kapoor, aliposema mwishoni mwa Desemba 2009 akisema: "Ni lazima jeshi la India lijiandae kupigana vita katika pande mbili" (Al-Iqtisadiya 15/2/2010), Marekani ilifanya shinikizo kwa Pakistan kupunguza vikosi vyake kwenye upande wa Mashariki na India, na kuelekeza vikosi vyake upande wa Magharibi kupambana na mujahidina dhidi ya Marekani nchini Afghanistan na katika maeneo ya makabila, ili India iweze kuelekeza nguvu zake upande wa Kaskazini dhidi ya China... Vilevile, Marekani imefanya kazi kuongeza mabadilishano ya kibiashara na India; kiasi cha bidhaa za Marekani zinazouzwa nje kwenda India kiliongezeka kwa kasi katika miaka mitano ikilinganishwa na nchi nyingine yoyote. Kulingana na makadirio ya Shirikisho la Viwanda la India, biashara ya pande mbili katika huduma inawezekana kuongezeka kutoka dola bilioni sitini hadi zaidi ya dola bilioni 150 katika miaka sita ijayo... Pamoja na hayo, India ina hofu kubwa ya mzozo wa ardhini na China. Aidha, watawala wa India kutoka Chama cha Congress wanaunga mkono Uingereza zaidi kuliko Marekani, hivyo hawako tayari kuingia katika hatari ya makabiliano yatakayoshindwa na China kwa ajili ya maslahi ya Marekani...!

4- Wakati huo, Marekani iliona ni vyema kuelekeza macho ya India upande wa Mashariki katika Bahari ya Pasifiki, hususan Bahari ya Kusini ya China, na kuishawishi kwa kuwepo kwa vyanzo vya nishati ya mafuta na gesi katika eneo hili ili kuishinda China, na kuikabili ndani ya mkakati wake wa Asia-Pasifiki. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa; India ilikubaliana na Vietnam kufanya utafiti wa mafuta na gesi baharini mkabala na visiwa vya Spratly vinavyozozaniwa na China. Kufuatia hayo, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya China, Lin Weimin, alisema: "Hatutarajii kuona vikosi vya nje katika Bahari ya Kusini ya China, wala hatutaki kuona kuhusika kwa makampuni ya kigeni katika kazi zinazokiuka mamlaka ya China, haki zake, na maslahi yake." (Asharq Al-Awsat 28/11/2011). Hapo awali, gazeti la People's Daily, ambalo ni sauti ya Chama cha Kikomunisti, lilizishutumu India na Vietnam kwa kufanya majaribio yasiyo ya kuwajibika ya kukabiliana na China. Majaribio ya Marekani ya kuishajiisha India kuelekea eneo hilo yaliendelea. Mnamo tarehe 22/7/2013, Makamu wa Rais wa Marekani Joseph Biden alifanya ziara nchini India, na alitoa matamshi huko Washington kabla ya ziara hiyo akitayarisha na kuishawishi India kuelekea Mashariki katika Bahari ya Pasifiki akisema: "India inatazama zaidi Mashariki kama nguvu ya usalama na ukuaji, na kwetu sisi habari kama hii inakaribishwa." Alisema pia: "Tunakaribisha ushiriki wa India katika eneo hili na tunakaribisha juhudi zake za kukuza mahusiano mapya katika biashara na usafirishaji wa nchi kavu na baharini katika eneo hili." (IIP Digital 23/7/2013). Mwezi mmoja kabla ya hapo, tarehe 24/6/2013, Kerry alikutana na mwenzake wa India Shri Salman Khurshid huko New Delhi na walishiriki katika kuongoza duru ya nne ya Mazungumzo ya Kimkakati kati ya Marekani na India, na walisisitiza tena maono yao ya pamoja kuhusu amani na utulivu katika Asia na Bahari ya Hindi na Pasifiki, wakisisitiza uungaji mkono wao wa kuendelea kuimarisha mawasiliano ya kikanda na kusisitiza tena umuhimu wa usalama wa baharini..." (IIP Digital 24/6/2013). Yote haya yanaonyesha wazi nia ya Marekani ya kuisukuma India kuelekea Mashariki katika Bahari ya Pasifiki, hususan katika Bahari ya Kusini ya China... Pamoja na hayo, India haikuitikia wito huo wa Marekani inavyotakiwa katika kipindi cha miaka miwili iliyopita baada ya Marekani kuweka mpango wake mpya kuhusu Asia-Pasifiki na kuisukuma kuelekea Mashariki. Hii ni kutokana na sababu zinazohusu sera ya Chama tawala cha Congress kinachounga mkono Uingereza, na pia hofu ya India ya kukabiliana na China...

5- Kuhusu Australia, Marekani ilianza kuimarisha jukumu la Australia, ambayo inafuata sera za Marekani, na kuimarisha ushirikiano nayo katika nyanja za kiuchumi na kiusalama ili kukabiliana na China ndani ya mpango wa Marekani kuhusu Asia-Pasifiki. Kwa ajili hiyo, viongozi wa Marekani wa ngazi za juu, hususan Waziri wa Mambo ya Nje wa zamani Hillary Clinton, Waziri wa Ulinzi wa zamani Leon Panetta, na Mkuu wa Majeshi Martin Dempsey, walielekea mjini Perth, Australia, kukutana na wenzao wa Australia. Siku hiyo, wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Marekani-Asia katika Chuo Kikuu cha Australia Magharibi mjini Perth, Clinton alisema: "Australia ni makutano ya kimkakati kati ya bahari mbili kubwa: Bahari ya Hindi na Bahari ya Pasifiki, ambazo zinafungua mlango wa biashara inayostawi na njia panda za nishati zinazotiririka duniani kote." Alisema pia: "Haishangazi kuona uwekezaji wa kigeni ukiongezeka kwa kiwango hiki nchini Australia, ikiwemo zaidi ya dola bilioni 100 kutoka Marekani, kwa sababu maji haya yamekuwa kiini cha uchumi wa dunia na ni sehemu kuu ya ushiriki wa Marekani unaopanuka katika eneo hili, ambao wakati mwingine tunauita mhimili wetu kuelekea Asia (pivot to Asia)." Aliongeza: "Marekani haijawahi kuondoka katika eneo la Asia-Pasifiki, na Marekani ingali ni nguvu katika Bahari ya Pasifiki, na iko hapa kubaki." Aliongeza kuwa: "Njia ya kufikiri ya Marekani kuhusu eneo la Asia-Pasifiki na maeneo yaliyopo kati ya Bahari ya Hindi na Pasifiki itakuwa muhimu kwa mustakabali wa Australia na Marekani." (IIP Digital 15/11/2012). Clinton pia alitaja katika kituo hiki mtazamo wa Marekani kwa India na kile inachokitaka kutoka kwayo, akisema: "Moja ya vipaumbele vya kimkakati vya Marekani ni kuunga mkono sera ya India ya kutazama Mashariki na kuishajiisha New Delhi kuchukua jukumu kubwa katika taasisi na masuala ya Asia." Alisema: "Marekani inakaribisha mazoezi ya kijeshi ya majini kati ya Australia na India hapo baadaye, na ina shauku ya kufanya kazi pamoja na Muungano wa Nchi Zinazopakana na Bahari ya Hindi kwa Ushirikiano wa Kikanda (IORA) ambao utaongozwa na Australia mwaka 2013, ambapo Marekani imejiunga kama mshirika wa mazungumzo." (Chanzo hicho hicho). Mawazo haya yanaonyesha njia ya kufikiri ya Marekani kuhusu eneo hili; inataka kuitumia Australia kama mdau muhimu katika kukabiliana na harakati za China katika eneo hilo. Hii inaonyesha kuwa Marekani haijafikia malengo yake kupitia India inayopakana na China ardhini, na inataka Australia ishirikiane na India katika maji ya Bahari ya Kusini ya China. Australia iko karibu zaidi kutekeleza sera ya Marekani kuliko India, kwani inachukuliwa kuwa nchi ya Magharibi inayofuata mfumo wa ubepari, na ina shauku ya ukoloni kama nchi yoyote ya kibeberu ya Magharibi. Kwa hiyo, inashiriki na Marekani katika uvamizi wa kikoloni kama ilivyokuwa ikishiriki na Uingereza, na inaendelea kushiriki nazo kwa sababu inafuata sera za nchi hizi mbili...

6- Kuhusu Japan, Marekani inafanya kazi kuimarisha nguvu zake nchini Japan na kuipa jukumu kubwa zaidi katika ulinzi wa eneo hilo dhidi ya China. Mnamo tarehe 6/4/2014, ilitangaza kutuma meli zaidi za ulinzi wa makombora kwenda Japan, kama ilivyokuja katika taarifa ya Waziri wa Ulinzi wa Marekani Chuck Hagel: "Marekani itatuma meli mbili zaidi za kuharibu makombora zenye mifumo ya ulinzi kwenda Japan ifikapo mwaka 2017, na hatua hii inakuja kama jibu kwa uchokozi wa Korea Kaskazini ambayo ilitishia kufanya majaribio mapya ya kinyuklia." Alionya China dhidi ya kutumia vibaya nguvu zake kubwa akisema: "Nchi kubwa hazipaswi kutumia shinikizo na vitisho, kwani hii inaweza kusababisha migogoro." Alisema: "Anataka kufanya mazungumzo na China kuhusu matumizi ya nguvu zake za kijeshi na kuhimiza uwazi." (Reuters 6/4/2014). Aliashiria kile Urusi ilichofanya huko Crimea ili kuionya China ambayo imefanya hivyo katika visiwa vinavyozozaniwa na Japan akisema: "Huwezi kuchora upya mipaka na kukiuka uadilifu wa ardhi na mamlaka ya nchi kwa nguvu, shinikizo au vitisho, iwe ni katika visiwa vidogo katika Bahari ya Pasifiki au katika nchi kubwa barani Ulaya." Alisema pia: "Jambo jingine nitakalozungumza na Wachina ni kuheshimu majirani zao. Shinikizo na vitisho ni jambo la hatari sana ambalo hupelekea migogoro pekee." Waziri huyo wa Marekani alikuwa amekutana wiki iliyopita na mawaziri wa ulinzi wa nchi za Kusini-Mashariki mwa Asia ambapo alionya juu ya kuongezeka kwa wasiwasi wa Marekani katika Bahari ya Kusini ya China. (Chanzo hicho hicho). Shirika la habari la Kyodo la Japan liliripoti mnamo tarehe 5/4/2014 kwamba "Inatarajiwa kwamba Waziri wa Ulinzi wa Marekani na Waziri wa Ulinzi wa Japan Itsunori Onodera watajadili suala la kuiruhusu Japan kutumia haki ya kujilinda kwa kurekebisha katiba ya Japan. Aidha, Onodera atajadili suala la kuhamisha silaha na vifaa vya ulinzi katika mkutano wake na Waziri wa Ulinzi wa Marekani, na pande hizo mbili zinaweza kufikia makubaliano ya kuimarisha ushirikiano katika nyanja ya vifaa vya ulinzi." Hiyo ina maana kuwa Marekani inataka kuipa Japan jukumu la kulinda eneo hilo dhidi ya China ili kupunguza mzigo kwake na kuchochea hisia za utaifa wa Wajapani ambao wanatamani kuwa na nguvu zao wenyewe kwa jina lao zinazofanya kazi kuwalinda na zinazojitegemea kutoka kwa Marekani.

7- Kuhusu kuathiriwa kwa sera ya Marekani na ushindi wa Chama cha Congress au Chama cha Janata kuhusiana na mpango wake wa Asia-Pasifiki, hapana shaka kuwa itaathirika. Chama cha Congress ni chama chenye historia ndefu ya utii kwa Waingereza, na kina ujanja wa kisiasa kwa kiasi fulani uliochukuliwa kutoka kwa bwana wake mzee Uingereza. Kwa hiyo, chama hicho kinatia wasiwasi Marekani, na wakati huo huo kinacheza na Marekani kama ifanyavyo Uingereza; kinaingia nayo baadhi ya makubaliano ya kijeshi na uhusiano wa kibiashara, lakini kinaiingilia katika mahusiano ya kisiasa na masuala ya kimkakati. Kwa mfano, Chama cha Congress kilikuwa kimeandaa taarifa katika kampeni yake ya uchaguzi ambayo ilishinda madaraka mwaka 2004 ikieleza mtazamo wake kwa Marekani na kukosoa sera ya Chama cha Janata kilichokuwepo kabla yake. Taarifa hiyo ilisema: "Inasikitisha kwamba nchi kubwa kama India imeshuka hadi kufikia kiwango cha kuwa na uhusiano wa kufuata Marekani, ambapo serikali ya Marekani inauchukulia utii wa India kama jambo la uhakika. Hii ilisababisha serikali za BJP kuwa tayari kufuata vipaumbele na sera za Marekani bila kuzingatia ipasavyo sera ya nje muhimu ya India na maslahi ya usalama wake wa kitaifa." Ni wazi jinsi chama hiki kinavyotia wasiwasi kwa Marekani. Pamoja na hayo, hakikusitisha mazungumzo ya kimkakati bali kilirejea mnamo Juni 2010, ambayo yalianza wakati wa utawala wa Rais Bush mwaka 2004. Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Clinton, mkuu wa ujumbe wa Marekani katika jukwaa la mazungumzo na India, aliielezea India kama "mshirika asiyeweza kuachwa na rafiki anayeaminika." Kwa hiyo, tangu kuingia kwa Chama cha Congress madarakani baada ya kuanguka kwa Chama cha Janata kinachounga mkono Marekani, imekuwa vigumu kwa India kufuata utekelezaji wa mpango wa Marekani wa kukabiliana na China isipokuwa baada ya Marekani kuipa vishawishi vingi kama tulivyotaja hapo awali. Pamoja na hayo, India bado inakataa ikitoa udhuru wa mazingira ambayo si mapya, bali yalikuwepo wakati wa Chama cha Janata, lakini chama hicho hakikuwa kikiyainua wakati wa kutekeleza sera ya Marekani. Ikumbukwe kuwa Uingereza imekifanya Chama cha Congress kiitii kwa utii wa jadi uliokamilika, na ikakikabidhi madaraka tangu kuondoka kwake, na hakikuondoka hapo isipokuwa kwa kipindi kifupi tangu mwaka 1998 hadi 2004 ambapo Chama cha Janata kinachounga mkono Marekani kilishinda, kisha Chama cha Congress kilishinda katika uchaguzi wa 2004-2009.

Kuhusu uchaguzi wa sasa ulioanza tarehe 7/4/2014, matokeo yake yatatangazwa tarehe 16/5/2014. Baadhi ya taasisi za kura za maoni zimesema kuwa matokeo yake yanaashiria kuwa Chama cha Bharatiya Janata na washirika wake wanatarajiwa kushinda katika uchaguzi huu. Ikiwa makadirio ya maoni ya umma na taasisi za ufuatiliaji wa maoni ya uchaguzi nchini India yatakuwa sahihi, na Janata kikashinda, iwe ni kwa wingi wa kuunda serikali peke yake—jambo ambalo halitarajiwi sana—au matokeo yake yakawa na umuhimu kiasi cha kuweza kuweka masharti yake kwa serikali yoyote itakayoundwa, ikiwa itakuwa hivyo, basi sera ya Marekani ya kuibana China kupitia India itakuwa rahisi zaidi kwa Marekani kuliko ilivyokuwa wakati wa Chama cha Congress. Badala yake, itakuwa rahisi kwake kutekeleza sera yake kama ilivyokuwa katika kipindi cha utawala wa Chama cha Janata kinachoifungamana nayo, ambapo Marekani ilipata nafuu wakati huo baada ya utawala wa Chama cha Congress kwa miongo kadhaa kabla ya hapo. Na wakati Chama cha Congress kilipokuja mwaka 2004, kilianza sera ya kuvuruga sera ya Marekani nchini India; badala yake, Chama cha Congress kilikuwa kikiichezea Marekani ili kupata makubaliano kwa faida yake kabla ya kupiga hatua ya kuisaidia Marekani katika sera yake.

8- Kuhusu ulinganisho kati ya China na India, mizani inaegemea China kwa dhahiri kutokana na nyanja kadhaa:

China, ingawa haibebi itikadi (mabda) yake na imeiacha katika sera ya nje na sera ya kiuchumi na kifedha, na pia imeiacha katika nyanja nyingi za maisha, lakini bado inaishikilia katika utawala kwa jina la Chama cha Kikomunisti ili kulinda maslahi ya chama hiki na wafuasi wake na kulinda mshikamano wa nchi na uhuru wake. Yote haya yanaifanya iongozwe na utashi wake yenyewe na kuipa ulinzi dhidi ya kuwa nchi inayofuata mkumbo au nchi inayofuata sera za nchi nyingine kubwa, na kuifanya nchi inayoota kuwa nchi kubwa duniani. Liu Mingfu, ambaye ni kanali wa China na profesa katika Chuo Kikuu cha Ulinzi wa Taifa anayewafunza maofisa vijana, alielezea hayo katika kitabu chake alichokiita "The China Dream" (Ndoto ya China), ambapo alitoa wito kwa nchi yake ya China kumiliki jeshi lenye nguvu zaidi duniani, na kuchukua hatua haraka ili kumuangusha bingwa wa dunia, Marekani. Aliitaka China kuacha unyenyekevu kuhusiana na malengo ya kimataifa na kupiga hatua ili kuwa namba moja duniani. Aliongeza kuwa: "Ikiwa China katika karne ya ishirini na moja haitaweza kuwa namba moja duniani na kuwa nguvu kuu duniani, basi itajikuta kando ya mfumo..." Kwa hiyo, China ina hisia ya nguvu na ushindani, na kama isingekuwa inatosheka na kulinda eneo lake tu, na kukubali kuwa mapambano yake na Marekani yawe tu ni jibu la harakati za Marekani kuelekea eneo lake, na China isitoke kwenda kuitikisa Marekani katika maeneo yake na maeneo ya ushawishi wake... Na kama isingekuwa imeanza kufuata mfumo wa ubepari katika nyanja nyingi, hususan za kiuchumi... kama si hivyo, sauti yake kimataifa ingekuwa ya juu zaidi, na athari yake katika maslahi ya Marekani ingekuwa na nguvu zaidi... Kwa vyovyote vile, China ina hisia ya nguvu, na inafanya kazi ili chombo chake kiendelee kujiendesha chenyewe hata kama ni katika eneo lake la kikanda...

Kuhusu India, haina itikadi wala haina mawazo yanayotokana na itikadi fulani, bali inatendewa kwa mfumo wa kibeberu ili kuhakikisha utii wake kwa Magharibi, hususan kwa Uingereza, na sio kwa ajili ya kuikomboa na kuifanya nchi inayojitegemea. Ni kama nchi nyingine zinazofuata mkumbo katika eneo hilo, imewekewa mfumo wa kibeberu kwa nguvu ya kikoloni, na bado umewekwa kwake kwa nguvu. Kwa sababu hiyo, haina msukumo wa ndani wala haina motisha ya kuanza kwa nguvu, kwa kasi, kwa ufahamu na kwa mipango yake yenyewe. Inabaki kuwa nchi inayofuata mkumbo na sio inayojitegemea kwa sera zake. Inajulikana kuwa inasogea polepole katika nyanja ya kisiasa na daima iko chini ya ushawishi na sio yenye kushawishi wala yenye kuanzisha mambo. Hivyo inaangukia chini ya ushawishi iwe kutoka kwa Uingereza, bwana wake wa kwanza, au kutoka kwa Marekani ambayo inanyoosha mikono yake kuelekea kwake ambapo imeanzisha ndani yake nguvu za kisiasa zinazoitii. Kwa hiyo, India ni tofauti na China katika upande huu; iko nyuma kifikra, na haijafungwa na misingi fulani ya kifikra. Wanaofanya kazi katika nyanja ya kisiasa hawajafungwa na misingi yoyote, na kwa hiyo ufisadi wa kifedha na kisiasa umeenea kiasi cha kuwajumuisha karibu wanasiasa wote. Ni vigumu kwa India kuwa nchi kubwa hata kama ni kikanda, na zaidi inaweza kuwa nchi ya mzunguko (satellite state) katika siku zijazo, yaani kuzunguka katika mzunguko wa nchi nyingine kubwa, iwe ni Marekani, Uingereza, au zote mbili kwa pamoja.

Hii ni upande wa kisiasa. Ama upande wa kiuchumi, uchumi wa China ni mara nne ya uchumi wa India. Wakati China imeweza kupunguza kiwango cha umaskini nchini mwake, asilimia 66 ya maskini duniani wanatoka India. India haiwezi kushindana na China kiuchumi; China imeendeleza sekta kubwa ya viwanda, jambo lililoifanya kuwa na akiba kubwa ya fedha iliyoiruhusu kuathiri uchumi wa dunia. Ama viwanda nchini India, bado viko mbali na kiwango cha China katika uzalishaji, hususan mashine nzito na teknolojia ya kisasa. Hii haimaanishi kuwa India haina mambo haya, bali iko nyuma ikilinganishwa na kiwango cha China...

Upande wa kijeshi, bajeti rasmi ya kijeshi ya China ni dola bilioni 119, ikiwakilisha zaidi ya mara tatu ya bajeti ya ulinzi ya India ambayo ni dola bilioni 38. China imepiga hatua muhimu katika kisasa cha vikosi vyake vya kijeshi; sasa inatengeneza vifaa vyake vya kijeshi (vifaa vikubwa vya kijeshi kama meli, vifaru, na ndege za kivita) na kupanua kundi lake la meli, na inachukua hatua madhubuti kudhibiti eneo lake. Lakini India imeanza hivi karibuni kuendeleza uwezo wake wa kufadhili mpango wa kisasa wa kijeshi ambao bado unakabiliwa na matatizo mengi. India pia bado ni mmoja wa waagizaji wakubwa wa vifaa vya kijeshi duniani. Licha ya juhudi za miongo miwili ya kukuza uwezo wake wa kijeshi wa ndani, imeshindwa kutoa matokeo yenye thamani. Peter D. Wezeman, mtafiti mkuu katika Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Amani huko Stockholm, alisema: "Sidhani kama kuna nchi nyingine duniani ambayo imejaribu kwa dhati kutengeneza silaha na kushindwa kabisa kama India." (Muagizaji mkubwa wa silaha duniani, India inatamani ununuzi wa ndani, The New York Times, Machi 2014).

Hivyo, ulinganisho kati ya China na India unaonyesha wazi kuwa China ina nguvu zaidi mara nyingi kuliko India...

9- Muhtasari ni kwamba Marekani imefanya kazi kuielekeza India upande wa mpaka wa Kaskazini kwa ajili ya mzozo na China, baada ya kuilindia mpaka wa Magharibi na Pakistan, ambapo watawala wake wanaofungamana na Marekani walitoa upendeleo mkubwa kwa India wakati wa utawala wa Chama cha Bharatiya Janata kinachoifungamana na Marekani. Na wakati Chama cha Congress kiliporejea madarakani, kilionyesha kurudi nyuma katika kazi kwenye mpaka huu ambao unaitwa "Mstari wa Udhibiti wa Kweli" kutokana na hofu nchini India ya kukabiliana na China na vitisho vya China kuelekea India, na kwa kuwa chama hiki kinaunga mkono Waingereza ambao hawahimizi India kufuata mipango ya Marekani. Wakati huo, Marekani ilielekeza India katika kile ilichokiita "Mwelekeo kuelekea Mashariki", yaani kuelekea eneo la Bahari ya Pasifiki na hususan kuelekea Bahari ya Kusini ya China, na kuishawishi kwa kuwepo kwa vyanzo vya nishati ya mafuta na gesi huko na kwamba ina haki ya kupata sehemu yake, na kuifanya ishirikiane na Vietnam ambayo inadai kuwa ina haki huko na inazozana na China katika visiwa vya Spratly huko... Vilevile, Marekani imeisukuma Australia kuelekea kwayo ili kuivutia katika jaribio la kuunda umoja wa nchi kadhaa kukabiliana na China... Marekani pia inafanya kazi kuipa Japan jukumu lenye ufanisi zaidi ili kupunguza mizigo ya ulinzi kwake. Ikiwa Chama cha Bharatiya Janata kitashinda uchaguzi unaoendelea hivi sasa na kuingia madarakani tena, kuna uwezekano wa kuongezeka kwa harakati za India pamoja na Marekani katika eneo la Mashariki, yaani katika Bahari ya Kusini ya China. Ama kuhusu ulinganisho kati ya nguvu ya China na India, kuna tofauti kubwa kwa faida ya China mara nyingi zaidi kuliko nguvu ya India... Na kama isingekuwa kwamba China inatosheka tu na kulinda eneo lake, na kukubali kuwa mapambano yake na Marekani yawe tu ni jibu la harakati za Marekani kuelekea eneo lake, na China isitoke kwenda kuitikisa Marekani katika maeneo yake na maeneo ya ushawishi wake... Na kama isingekuwa kwamba imeanza kufuata mfumo wa ubepari katika nyanja nyingi, hususan za kiuchumi... kama si hivyo, sauti yake kimataifa ingekuwa ya juu zaidi, na athari yake katika maslahi ya Marekani ingekuwa na nguvu zaidi.

Share Article

Share this article with your network