Jibu la Swali
Swali: Mkutano wa kilele wa Muungano wa Atlantiki ya Kaskazini (NATO) ulifanyika mjini Brussels, mji mkuu wa Ubelgiji na mji mkuu wa Umoja wa Ulaya, mnamo tarehe 11 na 12/07/2018, ulihudhuriwa na Rais wa Marekani pamoja na viongozi wa nchi wanachama 29 wa muungano huo. Mijadala mikali ilizuka kati yao na Trump na karibu ikajikita tu kwenye mada ya kuongeza matumizi ya kijeshi kufikia 2% ya pato la taifa (GDP). Kwa nini Marekani inafanya hivyo? Na nini hatima ya muungano huu?
Jibu: Ili jibu liwe wazi, tunapitia mambo yafuatayo:
1- Rais wa Marekani, Trump, anafuata mwenendo tofauti mbali na diplomasia na maneno ya kuzunguka. Yeye anatamka na kufunua wazi kila anachotaka, na anafanya shinikizo hadharani. Kile anachokisema na kukiomba nyuma ya pazia na katika mikutano ya faragha na wenzake wa nchi nyingine, anakisema na kukiomba hadharani kwa kiburi na utaka zaidi kuliko mfano wake George Bush Jr. Kadhalika, yeye ni kinyume na mtangulizi wake Obama; Obama alikuwa akifanya hivyo nyuma ya pazia, akifanya shinikizo kwa wenzake na kwa nchi mbalimbali, na akifanya ujanja wa kisiasa na maneno ya kuzunguka kwa siri kana kwamba ni mwanasiasa wa Kiingereza! Rais wa zamani wa Marekani, Obama, ndiye aliyeweka ongezeko la 2% ya pato la taifa kwa nchi wanachama mwaka 2014, na akaanza kufanya shinikizo kwao kwa mbinu mbalimbali ili wajifunge na makubaliano hayo. Habari zilikuwa zikizungumzia mawasiliano yake na nchi wanachama kuhusu ongezeko hili bila kuzua vurugu na ugomvi hadharani ili kuonyesha kwamba muungano huo ni imara na ni kitu kimoja, na kiongozi wake, Marekani, imeridhika na mwendo wake na mwendo wa wanachama wake, wakati kiuhalisia kulikuwa na hitilafu kali kati yao. Wanachama wa muungano waliahidi mbele ya Obama mwaka huo kutumia asilimia hii ya pato la taifa la nchi zao kwa masuala ya ulinzi ifikapo mwaka 2024, lakini takriban nchi 15 wanachama, zikiwemo Ujerumani, Kanada, Italia, Ubelgiji na Uhispania, bado matumizi yao yako chini ya 1.4% na hazitaweza kuheshimu ahadi zao, jambo ambalo linamkasirisha Trump. Katika mfumo wa mpango wa Marekani kuhusu mada hii, nchi za NATO zitajitolea kuwa na uwezo ifikapo 2030 wa kutuma ndani ya siku 30: batalioni 30 za kivita, vikosi 30 vya ndege, na meli 30 za kivita ili kuweza kukabiliana na operesheni ya kijeshi inayoweza kufanywa na Urusi, ambapo Marekani inamfanya Urusi kuwa adui wa kudhania ili kuweka utawala wake juu ya Ulaya na kuizuia isijitegemee katika maamuzi yake ya kijeshi na kisiasa, na hivyo kuilazimisha kubaki chini ya uongozi wake na mwavuli wake wa kijeshi angalau.
2- Trump anatambua ugumu wa jambo hilo na washirika wake na kuwashawishi, na ndiyo maana aliandika kwenye Twitter mnamo 10/07/2018 akielekea kwenye mkutano wa NATO mjini Brussels: "Mkutano wake (unaotarajiwa 16/07/2018) huko Helsinki na Rais wa Urusi Putin unaweza kuwa rahisi kuliko mkutano wa NATO." Maneno yake haya yana asilimia kubwa ya ukweli; Urusi inaonekana kama mtiifu na aliye tayari kutoa huduma kwa Marekani kwa ajili ya kufanikisha baadhi ya maslahi yake, na ili ionekane kama nchi kubwa yenye ushawishi ulimwenguni kando ya nchi namba moja, na pia kujiepusha na shari ya Marekani, hasa katika eneo lake la ushawishi na mazingira yake ambayo Marekani inafanyia kazi ili kuyadhibiti. Ama Ulaya, inaonekana kama mpinzani na mshindani, hivyo iliunda Umoja wa Ulaya ili kusimama dhidi ya Marekani na kuishindana, na ndiyo maana Marekani inachukua msimamo wa uadui dhidi ya umoja huu, na inafanya kazi ya kuusambaratisha hadharani. Iliunga mkono kujiondoa kwa Uingereza (Brexit), na Trump alishambulia sera ya serikali ya Theresa May wa Uingereza ambayo inalenga kuanzisha soko huru na Umoja wa Ulaya baada ya kujiondoa kwenye umoja huo akisema: "Mpango wa May huenda utaharibu makubaliano na Marekani, kwa sababu ikiwa wataingia makubaliano kama hayo, basi tutakuwa tunashughulika na Umoja wa Ulaya badala ya kushughulika na Uingereza." Na akasema: "Nilimwambia Theresa May kuwa ningeshughulikia Brexit kwa njia tofauti, na nikamwambia jinsi ya kufanya hivyo, lakini hakukubali, hakunisikiliza, na alitaka kufuata njia tofauti." Na alimmsifu Boris Johnson, Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza aliyejiuzulu kwa sababu ya kupinga mpango wa May, akisema kwamba "atakuwa mkuu wa serikali mkuu" (BBC ikinukuu The Sun 13/07/2018), na akatoa wito kwa nchi nyingine kujiondoa hadharani. Hata alimpendekezea Rais wa Ufaransa aliyemtembelea mwezi wa Aprili uliopita kujiondoa katika Umoja wa Ulaya. Gazeti la Washington Post mnamo 29/06/2018 liliripoti kwamba "Trump alimpendekezea mwenzake wa Ufaransa, Macron, kujiondoa katika Umoja wa Ulaya kwa sharti la kufikiwa makubaliano ya kibiashara ya nchi mbili na Marekani, wakati wa mkutano wao katika Ikulu ya White House mwezi wa Aprili uliopita." Na lilikunukuu maafisa wawili wa Ulaya kwamba "Trump alimwambia Macron: Kwa nini usijiondoe kwenye Umoja wa Ulaya?".
3- Kwa sababu hii, Trump aliukosoa Umoja wa Ulaya na hasa Ujerumani, kwani mgogoro wake na Marekani ndio mkali na mgumu zaidi! Tulitaja katika jibu la swali la tarehe 07/06/2017 sababu za kuongezeka kwa mgogoro na Ujerumani hasa, tukasema: "Ujerumani ndiyo kitovu kikubwa cha kifedha barani Ulaya, na uchumi wa nne duniani baada ya Marekani, Uchina na Japani, kwa hivyo macho ya Trump yameendelea kuelekezwa kwake katika jaribio la kupata pesa nyingi kutoka kwake kwa manufaa ya Marekani, hasa kwa vile Marekani inaitolea udhuru Ujerumani kwa hatari za Kirusi ili kuisukuma Ujerumani kutoa mchango zaidi na ushiriki ndani ya NATO, kwani Berlin inatumia 1.2% ya pato lake la taifa kwa masuala ya kijeshi (dola bilioni 42), na pia urari wa kibiashara kati ya Marekani na Ujerumani unaelekea upande wa mwisho kwa kiasi kikubwa, takriban euro bilioni sitini. Kiwango cha biashara kati ya Marekani na Ujerumani kilifikia euro bilioni 165 mwaka 2016, ambapo euro bilioni 107 ni kiwango cha uingizaji bidhaa wa Marekani kutoka Ujerumani..." Na tulitaja kuwa "... Mandhari ya Ulaya inaelekea kwenye kujitokeza zaidi kwa uongozi wa Ujerumani katika ngazi za kisiasa na kiuchumi, na kile kinachoashiria hili na kukithibitisha ni viongozi wa Ujerumani kuwa mstari wa mbele kujibu sera za Marekani, na kutangaza nia ya Ujerumani ya kuhamisha hitilafu na Marekani hadi hadharani... Na hili likipanuka sana litaitikisa Ulaya kwa kiasi kikubwa, na linaweza kusababisha mwishowe silaha za haraka za Ujerumani na za kiwango kizito."
4- Trump aliona changamoto ya Ujerumani kwake na kuendelea kwake kutomjali sana, hasa baada ya kufunua uadui wake kwa Umoja wa Ulaya ambao Ujerumani inauona kama soko lake imara la kiuchumi, na inauona kama chombo ambacho Ujerumani inapanda kuelekea anga la ulingo wa kimataifa ili kuathiri sera za ulimwengu... Kwa hiyo, Trump aliongeza ukosoaji wake kwa Ujerumani hasa na kuitaka ilipe mamia ya mabilioni kwa Marekani kuilinda tangu Vita Kuu ya Pili ya Dunia. Alisema kabla ya kuanza mkutano huo akishambulia Ujerumani wakati wa mkutano wake na Katibu Mkuu wa NATO kwamba "Ujerumani inaitajirisha Urusi, ni mateka wa Urusi, iko chini ya udhibiti kamili wa Urusi. Inalipa mabilioni ya dola kwa Urusi ili kupata usambazaji wake wa nishati na lazima tuwalinde dhidi ya Urusi. Jambo hili linawezaje kufafanuliwa? Hii si haki." Trump alisema wakati wa mkutano: "Ujerumani iko chini ya udhibiti wa Urusi kabisa kwa sababu itapata 60% hadi 70% ya nishati yake kutoka Urusi pamoja na bomba jipya la bomba, na nadhani hii haifai, ni jambo baya sana kwa Muungano wa NATO." (BBC 12/07/2018). Chansela wa Ujerumani Merkel alimjibu akisema: "Ujerumani ina sera zake yenyewe na inachukua maamuzi yake kwa kujitegemea. Mimi binafsi niliishi katika sehemu ya Ujerumani iliyokuwa imekaliwa na Umoja wa Kisovieti. Nafurahi sana kwamba leo tuko kitu kimoja chini ya bendera ya uhuru, na kwa sababu hiyo tunaweza kusema kwamba tunaweza kuweka sera zetu huru na kuchukua maamuzi huru." Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Heiko Maas alisema "sisi si wafungwa wa Urusi wala Marekani" (BBC 12/07/2018). Trump na Merkel walipuuzana kila mmoja wakati wakitembea katika korido ya makao makuu mapya ya muungano kuelekea jukwaani kwa ajili ya kupiga picha ya jadi. Trump alikuwa amekashifu mara kadhaa mradi wa bomba la gesi wa Nord Stream utakaounganisha Urusi na Ujerumani na kuitaka iachane nao. Mradi huu unapingwa na baadhi ya Waulaya na kusababisha mgawanyiko katika sera ya Umoja wa Ulaya, kwani Poland inaona kuwa Ulaya haiuhitaji. Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland Jacek Czaputowicz alisema alipowasili makao makuu ya muungano: "Nord Stream ni mfano wa nchi za Ulaya zinazotoa fedha kwa Urusi na kuipa njia zinazoweza kutumika dhidi ya usalama wa Poland." (AFP 11/07/2018). Hivyo anazungumza kwa ulimi wa Trump, kwa sababu Poland inaifuata Marekani, na inafanya kazi kwa niaba ya Marekani ndani ya Umoja wa Ulaya. Hivyo Marekani imekuwa ikifanya kazi ndani ya Umoja wa Ulaya kuumaliza kutoka ndani kwa muda mrefu, lakini jipya katika zama za Trump ni kwamba aliongeza kazi ya moja kwa moja na ya wazi ya kuubomoa umoja huo, akifanya suala la kuilazimisha Ulaya kutekeleza asilimia 2 kuwa suala lake la kimaamuzi ili kuonyesha mafanikio yake katika kile ambacho mtangulizi wake Obama hakufanikiwa nacho katika kuwashinikiza Waulaya kuongeza matumizi ya ulinzi kufikia 2%... Na kisha kuboresha hali yake ndani ya nchi, jambo ambalo linaboresha nafasi za Chama cha Republican katika uchaguzi wa katikati ya muhula na pia nafasi zake katika muhula wa pili wa urais...
5- Lakini Ufaransa ilikuwa yenye kuitikia zaidi; rais wake Macron alisema "Ufaransa itatimiza lengo lililokubaliwa katika NATO la kuongeza matumizi ya ulinzi kuwa 2% ifikapo mwaka 2024, na kwamba mshikamano katika muungano hautawezekana isipokuwa ikiwa mzigo utashirikishwa kwa usawa." Alisema: "Trump alisisitiza kujitolea kwa Marekani kwa muungano licha ya kuelezea mashaka yake hapo awali na kwamba hakutishia moja kwa moja kujiondoa wakati wa mkutano wa kilele siku ya Alhamisi (12/07/2018)." (Reuters 12/07/2018). Ikumbukwe kwamba Ufaransa kwa sasa inatumia karibu 1.8% ya pato lake la taifa kwa ulinzi. Lakini inajitahidi kuilainishia Marekani ili iipe nafasi ya kimataifa kando yake ili kutosheleza hisia za kupenda ukubwa zinazowatawala Wafaransa, lakini bila kuacha Umoja wa Ulaya pamoja na hofu yake ya kuinuka kwa Ujerumani. Mara nyingine Ufaransa inajikaza kwa ajili ya Umoja wa Ulaya kama ilivyotokea katika mkutano wa G7 nchini Kanada hivi karibuni na vita vya kibiashara vilivyotangazwa na Trump, na katika suala la kudumisha makubaliano ya nyuklia na Iran licha ya Marekani kujiondoa, na wakati mwingine inalegeza msimamo kwa Marekani kama ilivyotokea katika mkutano wa Brussels wa hivi karibuni.
6- Trump ameonyesha kuwa Marekani iko tayari kuachana na NATO, na ingawa hajafanya hivyo sasa, tishio hili linabaki palepale, na ametangaza vita vya kibiashara dhidi ya washirika wake na maadui zake, na huu ni mwelekeo mpya katika sera ya Marekani inayoongozwa na rais wake mwenye kukurupuka kama vile alivyo tayari kuachana na miungano mingine. Tulasema katika jibu la swali la tarehe 16/06/2018: "Na haya yote yanaonyesha kuwa faili la vita vya kibiashara ni muhimu sana kwa Marekani, kwani bado inateseka na matokeo ya mgogoro wa kifedha uliolipuka mwaka 2008 na madeni yake yamefikia zaidi ya dola trilioni 20. Rais Trump, mwenye fikra za kibiashara, anafanya kazi ya kuokoa uchumi wa Marekani akinyanyua kaulimbiu yake ya 'Marekani Kwanza', jambo ambalo linaashiria kusambaratika kwa taasisi za kimataifa ambazo Marekani imekuwa ikizitumia kwa muda mrefu kuweka ushawishi wake ulimwenguni, na hivyo kusambaratika kwa mfumo wa ulimwengu na kujitokeza kwa msimamo mpya wa kimataifa ambapo Marekani haitoi tena mhanga ili kubaki kiongozi wa dunia kwa msaada wa nchi nyingine na kuvumilia kwa kufanya urari wa biashara uelekee kwao, bali imeanza kufikiria uongozi pamoja na faida ya kibiashara bila msaada kwa washirika ili iwaweke chini ya mwavuli wake na kuwaendesha nyuma yake."
7- Hivyo ndivyo vita vinavyowaka kati ya washirika, na hii inabashiri kusambaratika kwa miungano yao, na kuibuka kwa vita vya kiuchumi na kisiasa kati yao, na lau si hofu yao ya kutumia silaha za nyuklia, ingelipuka kati yao vita vya tatu vya dunia kwa mfano wa vita viwili vya dunia vilivyotangulia. Washirika hao ndio chanzo cha shari kwa ulimwengu, kwa kufuata kwao mfumo wa shari wa kirasimali ambao unafanya manufaa kuwa kipimo cha matendo na thamani ya kimali kuwa ndiyo thamani pekee inayotawala jamii. Hivyo ulimwengu umekuwa na hitaji kubwa la kujitokeza kwa Dola ya kheri, Dola ya Khilafah Rashidah kwa njia ya Utume, ambayo itaeneza thamani za kiroho, kimaadili na kiubinadamu na haitaishia tu katika kufanikisha thamani ya kimali. Na hakika Mwenyezi Mungu ana waja wanyofu kwa ajili Yake, wakweli kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu—na hatumtakasi yeyote mbele ya Mwenyezi Mungu—wanaounganisha usiku wao na mchana wao ili kufanikisha kheri hii kubwa. Ndimi zao ni mbichi kwa kumdhukuru Mwenyezi Mungu, na viungo vyao vimeshughulika na kulingania kwa Mwenyezi Mungu, na nyoyo zao zimetulia kwa nusura ya Mwenyezi Mungu:
إِنَّا لَنَنْصُرُ رُسُلَنَا وَالَّذِينَ آمَنُوا فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَيَوْمَ يَقُومُ الْأَشْهَادُ
"Hakika Sisi bila shaka tutawanusuru Mitume wetu na wale walioamini katika uhai wa dunia na siku watakaposimama mashahidi." (QS. Ghafir [40]: 51)
4 Dhul-Qa'dah 1439 H 17/07/2018 M