Jibu la Swali
Uturuki, Kijidola cha Kiyahudi na Vituo vya Kijeshi nchini Syria
Swali: Tovuti ya Turk Press ilichapisha mnamo 2025/4/14 kuhusu sababu za kijidola cha Kiyahudi kupinga kuanzishwa kwa kituo cha jeshi la anga la Uturuki katika uwanja wa ndege wa "T4" ndani ya ardhi ya Syria. Ilitaja kuwa miongoni mwa sababu hizo ni (sababu ya kijeshi inayowakilishwa na ukweli kwamba uwepo wa Uturuki utazuia uhuru wa harakati wa jeshi la anga la Israel juu ya Syria, na kulazimisha uratibu wa usalama ambao Tel Aviv hauitaki kwa sasa...). Gazeti la Wall Street Journal lilikuwa limechapisha kwenye tovuti yake mnamo 2025/4/12 kwamba Trump aliashiria utayari wake wa kupatanisha wakati wa mkutano wake na Netanyahu wiki iliyopita (akisisitiza imani yake katika uwezo wake wa kutatua tofauti hizo kwa sharti kwamba pande zote mbili ziwe na busara). Je, hii inamaanisha kuwa kijidola cha Kiyahudi kinaweza kuizuia Uturuki kuwa na uwepo wa kijeshi nchini Syria licha ya makubaliano kati ya Uturuki na Syria? Na je, Marekani ina jukumu katika suala hili ambalo linaelezea utayari wa Trump wa kupatanisha?
Jibu: Ili jibu liwe wazi, tunarudi nyuma kidogo na kupitia mambo yafuatayo:
Kwanza: Wakati wa ziara ya Netanyahu nchini Hungary, Trump alimwalika kuja Marekani, na ulikuwa ni mwaliko wa kustaajabisha:
- Netanyahu alikuwa katika ziara nchini Hungary iliyoanza mnamo 2025/4/2 na kudumu kwa siku nne, ikiwa ni ziara yake ya kwanza katika nchi ya Ulaya tangu kutolewa kwa uamuzi wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai wa kumkamata mwaka jana.
- Katika hali isiyo ya kawaida, Rais wa Marekani Trump alimpigia simu Netanyahu na Orban (Waziri Mkuu wa Hungary) wakati wa mkutano wao mjini Budapest, akimwalika Netanyahu kutembelea Ikulu ya Marekani: (Trump alifunua, wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye ndege ya Rais, kwamba alifanya mazungumzo ya simu na Netanyahu jana Alhamisi, na kwamba walijadili masuala ya kisiasa ya kimataifa, akiashiria kuwa Waziri Mkuu wa Israel anaweza kuitembelea Marekani hivi karibuni. Afisa wa Israel alithibitishia tovuti ya Axios kwamba Trump alimtumia mwaliko rasmi Netanyahu kutembelea Ikulu ya Marekani, lakini tarehe ya mkutano huo bado haijapangwa, huku afisa wa Marekani akisema kuwa ziara hiyo inaweza kufanyika ndani ya wiki chache zijazo. Al-Qahera News, 2025/4/4).
- Kijidola cha Kiyahudi kilishangazwa na mwaliko huu wa haraka, hasa baada ya Ikulu ya Marekani kukataa kuufanya baada ya sikukuu za Kiyahudi: (Kuna wasiwasi katika ofisi ya Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, kuhusu msisitizo wa Ikulu ya Marekani kufanya mkutano kati ya Rais wa Marekani, Donald Trump, na Netanyahu kesho, Jumatatu, na si baada ya sikukuu ya Pasaka ya Kiyahudi, baada ya wiki mbili, kama ofisi ya Netanyahu ilivyotaka. Taarifa iliyotolewa na ofisi ya Netanyahu jana ilisema kuwa "ataelekea Washington kufuatia mwaliko aliopokea kutoka kwa Rais wa Marekani, Donald Trump. Watajadili mada za: Forodha... juhudi za kuwarejesha mateka wetu... uhusiano wa Israel-Uturuki... tishio la Iran, na mapambano dhidi ya Mahakama ya Kimataifa ya Jinai". Wasiwasi unaongezeka katika ofisi ya Netanyahu kutokana na haraka ya Ikulu ya Marekani kufanya mkutano huo kesho, na uwezekano wa Trump kumshangaza Netanyahu kwa mada au masuala ambayo Israel haiyatarajii, kama ilivyoripotiwa na Channel 12 leo, Jumapili... Arab 48, 2025/4/6).
- Netanyahu aliondoka Hungary na kuelekea moja kwa moja Washington bila kurejea katika kijidola chake, ikiwa ni ishara nyingine ya haraka!
Pili: Mpangilio huu wote wa papo hapo unaonyesha jambo la dharura, na kwa kuchunguza mada za utafiti zilizotangazwa za mkutano wao, jambo moja angalau lilikuwa kichocheo kikuu cha mwaliko huu wa haraka, ambalo kuna uwezekano mkubwa ni hali nchini Syria kwa sababu zifuatazo:
- Kwa kuchunguza kauli za Rais wa Marekani Trump mbele ya idadi ndogo ya waandishi wa habari wakati wa mkutano wake na Netanyahu mnamo 2025/4/7, baada ya Ikulu ya Marekani kufuta mkutano na waandishi wa habari uliokuwa umepangwa kufanyika baada ya mkutano huo akiwa na Netanyahu, tunakuta kwamba matamshi yake kuhusu uwanja wa Syria na uhusiano na Uturuki yalikuwa na chanya kubwa kuhusu uhusiano wake na Rais wa Uturuki Erdogan na kuhusu mawasiliano kati yao, akisema: ("Nilimfahamisha Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan pongezi zetu... Umefanya kile ambacho wengine walishindwa kufanya kwa kipindi cha miaka elfu mbili... Umeichukua Syria bila kujali majina yake mengi kihistoria... kupitia mawakala wako (proxies)". Trump aliendelea: "Erdogan alisema la la la... Sikuwa mimi niliyeichukua Syria, hivyo nikamwambia... Ni wewe lakini sawa huna haja ya kukiri hilo, akasema sawa labda nilikuwa mimi niliyeichukua". Trump aliongeza: "Erdogan ni mtu mgumu na mwerevu sana na amekamilisha kitu ambacho hakuna mtu aliyeweza kufanya hapo awali... Lazima ukubali ushindi wake". Trump alimgeukia mgeni wake Benjamin Netanyahu, akisema: "Tatizo lolote ulilonalo na Uturuki nadhani naweza kulitatua mradi tu uwe na mantiki katika maombi yako... Lazima uwe na mantiki... Sote lazima tuwe na mantiki". Turk Press, 2025/4/8), na Trump alitaka kijidola cha Kiyahudi kiwe na busara katika masuala yanayohusu Uturuki nchini Syria.
- Na hakukuwa na chaguo kwa kijidola cha Kiyahudi isipokuwa kutii ombi hili la Marekani: (Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, alisisitiza kuwa Tel Aviv haitaruhusu Syria kutumika kama kituo cha kuanzishia mashambulizi dhidi yake, akibainisha kuwa uhusiano na Uturuki ulikuwa wa kirafiki lakini "umezorota" hivi karibuni. Alisema baada ya kukutana na Rais wa Marekani Donald Trump: "Tulizungumzia pia hali ya Syria. Tulikuwa na uhusiano wa kirafiki na Uturuki ambao umezorota". Aliongeza: "Hatutaki kuona hali ambapo wengine, ikiwemo Uturuki, wanaitumia Syria kama kituo cha kuishambulia Israel". Aliongeza: "Tulizungumza kuhusu jinsi tunavyoweza kuepuka mzozo huu na nadhani hakuna mhimili bora kwa lengo hili kuliko Rais wa Marekani". Al-Quds Al-Arabi, 2025/4/8).
- Kijidola cha Kiyahudi kilikuwa kimefanya mashambulizi makali ya anga dhidi ya viwanja vya ndege vya Syria, na RT iliripoti mnamo 2025/4/2 kutoka kwa taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Syria: (Vikosi vya Israel vilifanya mashambulizi ya anga katika maeneo matano tofauti nchini kote ndani ya dakika 30, jambo lililosababisha uharibifu karibu kamili wa uwanja wa ndege wa kijeshi wa Hama na kujeruhi makumi ya raia na wanajeshi". Wizara ya Mambo ya Nje ya Syria ilizingatia kuwa "uchochezi huu usio na msingi ni jaribio la makusudi la kuvuruga uthabiti wa Syria na kurefusha mateso ya watu wake".), na viwanja hivi vya ndege vilivyo katikati ya Syria ndivyo Uturuki inavyopanga kuanzisha vituo vyake huko ndani ya makubaliano na serikali mpya ya Syria: (Waziri wa Mambo ya Nje wa Israel aliishutumu Uturuki kwa kucheza "jukumu hasi" nchini Syria, na waziri huyo wa Israel alimuonya Rais wa kipindi cha mpito nchini Syria, Ahmed al-Sharaa, kwamba "atalipa gharama kubwa sana" ikiwa ataruhusu "nguvu za uadui" kuingia nchini mwake... Ankara kwa sasa inajadiliana kuhusu makubaliano ya ulinzi wa pamoja na serikali mpya ya Al-Sharaa, na kuna ripoti zinazosema kuwa Uturuki iko katika mchakato wa kupeleka ndege na mifumo ya ulinzi wa anga katika vituo vya anga vya T4 na Aleppo nchini Syria... Baadhi ya wachambuzi walilinganisha kati ya mashambulizi makali ya anga yaliyofanywa na Israel kwenye uwanja wa ndege wa Hama wiki hii, na mashambulizi ya kiwango cha chini yaliyolenga pembezoni mwa kituo cha T4, jambo linaloashiria kuwa Uturuki huenda tayari imehamisha baadhi ya vifaa vyake huko. BBC, 2025/4/5). Habari zilienea kuhusu kuuawa kwa wahandisi 3 wa Uturuki katika uwanja wa ndege wa Hama kutokana na mashambulizi ya kijidola cha Kiyahudi, (Vyanzo vya kijeshi vya Syria vilifichua kuuawa kwa wahandisi 3 wa Uturuki katika shambulio la Israel kwenye uwanja wa ndege wa kijeshi wa Hama Jumatano iliyopita, vikiashiria kuwa wahandisi hao walikuwa wakifanya kazi ya kufunga vifaa vya kiufundi katika uwanja wa ndege wa Hama ikiwemo ulinzi wa anga ambao Uturuki iliuleta uwanjani hapo. Erem News, 2025/4/4).
- Inaonekana kuwa Uturuki ilikasirishwa sana na kijidola cha Kiyahudi kutokana na mashambulizi yake ya hivi karibuni hasa kwenye viwanja vya ndege vya Syria, na iliwasiliana na Marekani kwa haraka ili kuweka kikomo kwa kijidola cha Kiyahudi nchini Syria hasa kwa kuwa Uturuki inatekeleza jukumu lililokubaliwa na Marekani nchini Syria, kwa hivyo mwaliko wa haraka ulitolewa kwa Waziri Mkuu wa kijidola cha Kiyahudi kwenda Washington, na Trump akamtaka atatue matatizo kwa busara na Uturuki.
Tatu: Na kinachoashiria kuwa mada hii ndiyo ilikuwa ya dharura zaidi katika mkutano huo ni matamshi mengine mengi yanayoashiria hilo:
- Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki alisema (kwamba Marekani inapaswa "kumrekebisha" Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu na kumwekea mipaka. Anadolu, 2025/4/9).
- Mazungumzo ya moja kwa moja ya papo hapo yalitangazwa kati ya kijidola cha Kiyahudi na Uturuki, kwani RT iliripoti mnamo 2025/4/9 ikimnukuu Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki akisema: (Hakan Fidan aliripoti katika matamshi yake kwamba ili kuzuia "kutoelewana" nchini Syria, wanaanzisha "mawasiliano ya moja kwa moja" na Israel. Fidan alieleza kuwa Israel imeweka mkakati wa "kutobakiza chochote" kwa utawala mpya nchini Syria. Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki alisisitiza haja ya Israel kukomesha uvamizi wake wa ardhi za Syria, na kuacha kushambulia miundombinu yake. Alibainisha kuwa kutokuwa na uthabiti katika nchi jirani ya Uturuki kutaathiri nchi hiyo na kuisababishia madhara, akionya kuwa Ankara "haiwezi kukaa kimya mbele ya hilo"... Hatuna nia ya kuingia katika mapigano au makabiliano yoyote na nchi yoyote katika eneo hili, ikiwemo Israel... Sisi tunashirikiana na utawala mpya wa Syria katika nyanja ya usalama na katika kupambana na ugaidi).
- (Reuters ilikuwa imesema wiki iliyopita kuwa timu za kijeshi za Uturuki zilikagua vituo vitatu vya anga nchini Syria ili kupeleka vikosi vya Uturuki huko ndani ya mfumo wa makubaliano yanayokusudiwa ya ulinzi wa pamoja kabla ya Israel kulenga maeneo hayo kwa mashambulizi ya anga. Fidan aliliambia kituo cha CNN Turk siku ya Jumatano: "Wakati tunafanya operesheni fulani nchini Syria, lazima kuwe na utaratibu wa kuepuka mzozo na Israel ambayo ndege zake zinaruka katika eneo hilo, sawa na taratibu tulizonazo na Marekani na Urusi". Al-Arabiya, 2025/4/10).
- (Chanzo cha Syria kinachofahamu kinasema katika taarifa kwa Independent Arabia, kwamba "kwa kweli kuna mazungumzo kuhusu makubaliano, makubaliano haya ni makubaliano ya kutoingiliana na si kutenganisha vikosi, kwa sababu kimsingi hakuna mapigano kati ya Uturuki na Israel nchini Syria, kwa maneno mengine, makubaliano ni ya kuchora mipaka ili ikiwa kuna ndege za Israel katika anga ya Syria basi kutoa taarifa kuhusu muelekeo wake". Independent Arabia, 2025/4/9). Yaani sawa na makubaliano ya awali ya Uturuki na Urusi kuzuia mapigano kati yao nchini Syria!
- Na haya yote yanabainika kupitia matamshi ya maafisa nchini Uturuki kama ilivyoripotiwa na Asharq Al-Awsat mnamo 2025/4/13: [Uturuki ilithibitisha kuwa itaendelea na mazungumzo yake ya kiufundi na Israel ili kufikia utaratibu wa kupunguza mvutano na kuweka sheria za mapigano na kuzuia kutokea kwa ajali au mgongano katika ardhi ya Syria. Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki alisema kuwa nchi yake inataka kufikia uthabiti nchini Syria na kukaa mbali na uchochezi wowote, na inafanya kazi ili kutoingia katika mzozo wowote na nchi yoyote ndani ya Syria. Wajumbe wawili (Uturuki na Israel) walifanya mkutano mjini Baku, mji mkuu wa Azerbaijan, Jumatano iliyopita, mazungumzo yanayolenga kuepuka kutokea kwa ajali au mgongano nchini Syria, baada ya mvutano kuongezeka katika wiki mbili zilizopita... Asharq Al-Awsat 2025/4/13].
- Al-Jazeera iliripoti kwenye tovuti yake mnamo 2025/4/14 kuhusu ripoti ya mwandishi Andrea Muratore iliyochapishwa na tovuti ya Kiitaliano ya Inside Over [kwamba Uturuki inacheza jukumu muhimu kwa utawala mpya wa Marekani kama daraja la kutatua masuala mengi moto katika Mashariki ya Kati na katika sehemu mbalimbali duniani, baada ya miaka ya mvutano na utawala uliopita... Mwandishi alisema katika ripoti yake, kwamba Rais wa Marekani Donald Trump amesisitiza mara kwa mara kuvutiwa kwake na utu wa Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan na ujanja wake wa kisiasa, na ametuma tangu mwanzo wa muhula wake wa pili ishara za wazi zinazoonyesha hamu yake ya kumtumia katika kutatua idadi fulani ya mafaili... Al-Jazeera 2025/4/14].
Haya yote yanaonyesha kuwa Marekani inashughulika na kijidola cha Kiyahudi ambacho ni adui na utawala wa Uturuki kama washirika wake, ikisimamia mambo kati yao kwa njia inayotumikia maslahi yake!
Nne: Ni jambo la kuumiza kwamba Marekani imekuwa ikisimamia mambo katika nchi zetu inavyotaka, ikitoa kipaumbele katika eneo hili kwa kijidola cha Kiyahudi kilichopora ardhi iliyobarikiwa, ardhi ya Isra na Mi'raj, Palestina, na watawala katika nchi za Waislamu wanatii amri za Marekani, kiasi kwamba ardhi ya Khilafah katika dola yake ya mwisho, Dola ya Osmani ambayo Mayahudi walitaka kuwa na sehemu katika ardhi iliyobarikiwa mkabala na kulipa mamilioni ya sarafu za dhahabu, Khalifah aliwajibu jibu kali kwa kusema:
(Palestina si mali ya mkono wangu wa kulia bali ni mali ya Ummah wa Kiislamu na watu wangu wamepigana jihadi kwa ajili ya ardhi hii na kuimwagilia kwa damu yao, hivyo Mayahudi wabaki na mamilioni yao na ikiwa siku moja dola ya Khilafah itasambaratika basi wakati huo wataweza kuichukua Palestina bila malipo yoyote...) Na hivi ndivyo ilivyokuwa!
Uturuki hii baada ya kuondoka kwa Khilafah ya Osmani, inazuiliwa na kijidola cha Kiyahudi kuwa na kituo cha kijeshi nchini Syria, hata baada ya idhini ya utawala wa Syria kwa hilo..! Hii ndiyo hali ya Waislamu baada ya kutoweka kwa Khilafah... na ni jambo zito!
Hakika nguvu ya Waislamu na utukufu wao ni kwa Khilafah yao, na hakika Hizb ut Tahrir, kiongozi asiyewaambia uongo watu wake, anatoa wito kwa watu wenye nguvu katika nchi za Waislamu kuinusuru katika kuanzisha tena maisha ya Kiislamu duniani kwa kusimamisha Khilafah upya, na kisha utukufu wa Waislamu utarejea:
وَيَوْمَئِذٍ يَفْرَحُ الْمُؤْمِنُونَ * بِنَصْرِ اللَّهِ يَنْصُرُ مَنْ يَشَاءُ وَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ
"Na siku hiyo waumini watafurahi. Kwa nusura ya Mwenyezi Mungu. Yeye humnusuru amtakaye, Naye ni Mwenye nguvu na Mwenye kurehemu." (QS. Ar-Rum [30]: 4-5)
18 Shawwal 1446 H Inayoafikiana na 16/04/2025 M