Jibu la Swali
Ukweli wa Vuguvugu la Kusini na Utii Wake
Swali:
Je, Vuguvugu la Kusini (Al-Hirak al-Janubi) bado liko upande wa Marekani? Au utii wa Baraza hilo umehamia kwa Waingereza kutokana na Imarati kulidhibiti, na kwa kuwa Imarati inawakilisha Waingereza nchini humo? Kwa maneno mengine: Je, Marekani imeshindwa kulilinda Vuguvugu la Kusini na Uingereza imefanikiwa kupitia Imarati kulivuta upande wake? Au bado linafuata Marekani katika mienendo yake, na kwamba Imarati kutokana na nguvu ya jeshi lake mjini Aden imeweza tu kuliathiri bila Vuguvugu hilo kuwa mfuasi wa Waingereza?
Jibu:
1- Uingereza ilifadhaika ilipotambua kuwa Marekani iliweza kuwavuta Ali Salem al-Beidh na Ali Nasir Muhammad kupitia njia zake za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja kupitia Misri na Saudi Arabia wakati wa enzi ya Mfalme Fahd mapema miaka ya tisini. Hii ni licha ya kwamba Uingereza ndiyo iliyounda, kupitia vibaraka wake, kile kilichoitwa "Mstari wa mbele wa Ukombozi wa Kitaifa Kusini mwa Yemen" (National Liberation Front) na kuwaalika kwenye mazungumzo mjini Geneva kuanzia 1967/11/20, kisha Uingereza ikatoa uhuru kwa Yemen Kusini mnamo 1967/11/30 baada ya kuondoka kwa vikosi vya Uingereza. Al-Beidh akawa mtawala wa Kusini kwa uungaji mkono wa Uingereza, hivyo kitendo chake cha kwenda na Marekani kilionekana na Uingereza kama usaliti! Kwa hiyo, iliamua kuwaondoa madarakani, hasa kwa kuwa ilikuwa na uwezo huo kupitia mtu wake, Ali Saleh, ambaye alikuwa na nguvu kubwa Kaskazini... Hivyo, vita vilizuka kati ya vikosi vya pande hizo mbili mwaka 1994, ikiwa imepita miaka minne tu tangu kuunganishwa kwa Yemen! Vita vilipoisha kwa kushindwa kwa vikosi vya kijeshi vilivyoelezewa kama vya "Kusini", Ali Salem al-Beidh alitoroka, na pia Ali Nasir Muhammad... na wakajificha kwa muda.
Kisha serikali ya Saleh mjini Sana'a ikaanza kuwakandamiza na kuwawinda wanajeshi wa Kusini, na hali hiyo iliendelea kwa miaka mingi. Baadaye, chama cha wastaafu wa kijeshi waliofutwa kazi kiliundwa Kusini; kilikuwa chama chenye madai yanayohusiana na ukandamizaji, uwindaji, na kunyimwa haki. Kutokana na kuendelea kwa dhuluma hizo, mwelekeo wa kujitenga ulipenyeza miongoni mwa wanajeshi wa zamani waliojiunga na chama hicho. Hivyo kikageuka kuwa kitovu cha utengano na msingi wa mkusanyiko wa wanaotaka kujitenga, ambao mienendo yao ilikuja kujulikana leo kama Vuguvugu la Kusini (Al-Hirak al-Janubi), ambalo lilijitangaza rasmi Kusini mwa Yemen mwaka 2007. Hii ni pamoja na harakati nyingine ndogo na zenye ufanisi mdogo ambazo hatutaziangazia.
2- Marekani ilitumia hali hii Kusini ili kupata kiti nchini Yemen, kama ilivyopata kiti kingine Kaskazini mwa Yemen kupitia harakati ya Wahouthi na uungaji mkono wa Iran kwao. Kwa upande wa mapambano ya kimataifa, Vuguvugu la Kusini limegeuka kutoka madai ya kuondolewa dhuluma na kuwa chombo kipya cha Marekani cha kuingilia kati nchini Yemen, nchi ambayo serikali yake inatii Waingereza. Nchi kubwa zimezoea kutumia hali ya ndani na mivutano katika nchi ndogo ili kupata ushawishi. Marekani, kupitia shirika la ujasusi la Mfalme Fahd nchini Saudi Arabia, ilikuwa ikijaribu kuwasiliana na wanajeshi Kusini mwa Yemen wakati wa miaka ya tisini, yaani baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vya 1994. Ingawa Salem al-Beidh alikuwa mmoja wa wafuasi wake wakati huo, kujificha kwake na wito wake akiwa uhamishoni wa kufanya vitendo vya kijeshi dhidi ya utawala wa Saleh haukutosha kwa Marekani kuona mafanikio. Kwa hiyo, ilianza kutafuta mtu atakayeasisi hatua kali za kisiasa za kuwakusanya watu wa Kusini ili kuunda shinikizo kubwa linaloathiri utawala wa Saleh kwa ufanisi. Marekani ilimpata mwanaharakati wa upinzani Hassan Baoum; alikuwa akihamasisha kwa kiwango kikubwa akitaka kujitenga kwa Yemen Kusini, akihama mapema kutoka mji mmoja kwenda mwingine, na kutembelea makabila kwa bidii akiwataka wamuunge mkono katika madai yake ya kujitenga. Haya yote yalifanyika huku kukiwa na mateso na kutengwa kulikokuwa kukiwapata watu wa Kusini. Baoum alikuwa akiandaa shughuli baada ya shughuli ili kujenga maoni ya umma yanayotaka kutenganisha Kusini na Yemen, na mbinu yake ilikuwa ya amani na alikataa vitendo vya vurugu. Ilionekana kuwa mienendo ya Hassan Baoum ya kujitenga ilipata mwangwi na wakati mwingine msukumo katika maeneo ya Kusini ambako wazo la kuwa kutengwa ni sera ya kimfumo lilikuwa limezama... Wakati huo, alianza kukabiliwa na ukamatwaji na uwindaji kutoka kwa serikali ya Sana'a; alikamatwa mara kadhaa kwa kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja kati ya 2007 na 2008, kisha akakamatwa tena 2010, na kuachiliwa baada ya miezi miwili mnamo 2011, na kukamatwa tena mwaka huo huo. Hivyo, Baoum akawa alama kubwa ya Vuguvugu la Kusini kutokana na juhudi zake za dhati na kuchochea wanajeshi wa zamani, makabila, na wanaharakati dhidi ya serikali kuu mjini Sana'a, na kuimarisha madai ya kujitenga. Kutokana na mahusiano yake na Marekani na kupokea uungaji mkono wa Iran, hatua zake zilikuwa na kasi kubwa. Baoum akaunda Baraza Kuu la Vuguvugu la Kusini na akawa mwenyekiti wake (Baraza Kuu la Vuguvugu la Amani la Ukombozi wa Kusini linawakilisha mrengo mkuu wa Vuguvugu la Kusini ambalo pia linajumuisha makundi kama vile Tume Kuu ya Kitaifa ya Uhuru wa Kusini, Baraza Kuu la Kitaifa la Ukombozi na Urejesho wa Dola ya Kusini, Muungano wa Kidemokrasia wa Kusini, na Umoja wa Vijana na Wanafunzi wa Kusini... Mkoa wa Ad-Dali' unachukuliwa kuwa moja ya maeneo yenye vuguvugu kali na shughuli nyingi... Al-Jazeera Net. 2011/3/3). Kuna tovuti ambazo zilikuwa zikimuelezea Baoum waziwazi kama kibaraka wa Iran kama ilivyoelezwa kwenye tovuti ya "Huna Aden 2016/9/13". Hivyo, Vuguvugu la Kusini likiongozwa na Hassan Baoum ambacho kililishwa na hali ya kutengwa, ni harakati ya kisiasa iliyofungamana na uungaji mkono wa mapema wa Marekani, na kikawa msingi ambao Marekani inaweza kufanyia kazi ili kupenya Yemen kutokea upande wa Kusini pia. Harakati, shughuli, na migomo iliyokuwa ikifanywa na Vuguvugu hilo makao yake yakiwa mji wa Ad-Dali' – ingawa Hassan Baoum ni mtu wa Hadramaut kutoka Mukalla na si wa Ad-Dali' – mienendo hiyo yote ilikuwa kama mafunzo kwa kundi hili katika kazi za kisiasa. Serikali ya Sana'a mwanzoni haikuona hatari katika harakati hii kwa sababu shughuli zake zilikuwa za kisiasa, kwa hiyo ilitosheka na kuwakamata viongozi wake kama Hassan Baoum, Ahmad bin Farid, Ali al-Gharib, na Ali Manassar kwa vipindi fulani, kisha kuwaachilia.
3- Watu wa Marekani katika Vuguvugu la Kusini wamebobea katika wazo la kujitenga ambalo limekuwa itikadi kwao, na wamekuwa wagumu nalo. Ama wengine walioingizwa katika shughuli za Vuguvugu la Kusini linalolishwa na hali ya kutengwa, baadhi yao ni wanaharakati wa ndani, na wengine wako chini ya ushawishi wa Waingereza na watu wao nchini Yemen. Watu kama hawa walikuwa mara nyingine na umoja, na mara nyingine na utengano; utengano haukuwa itikadi yao. Serikali ya Sana'a ilikuwa ikifaidika na watu hawa kwa kupunguza makali ya wazo la kujitenga ambalo vibaraka wa Marekani wanalishikilia, na ilikuwa ikiwaingiza baadhi ya watu wake miongoni mwao kwa lengo hilo hilo... Kama tulivyosema, serikali ya Sana'a haikuwa ikiona hatari kwao. Lakini ilipobainika kwa serikali ya Rais Saleh mjini Sana'a na nyuma yake Waingereza, kwamba harakati hii inaanza kupata kasi inayoonekana, na kwamba hatari zake zinaongezeka hasa kwa kuwa vibaraka wa Marekani wako mstari wa mbele, serikali ya Sana'a pamoja na Waingereza na wafuasi wao wa kikanda walianza kulishughulikia vuguvugu hili kwa umakini ili kulidhibiti. Hasa ilipoonekana kuwa limekuwa gumu kung'olewa kutokana na hisia zinazokua Kusini za kutengwa. Mpango wa "Kiingereza" wa kudhibiti ulikuwa ukiendelea kulingana na maendeleo ya Vuguvugu la Kusini; kutoka kwa majaribio ya dhati ya kupenya hadi uwindaji ambao hautosheki na ukamataji tu bali unatumia vurugu... Hali hiyo iliendelea hadi Imarati ilipoingia kwa jeshi lake la nchi kavu ikitumia fursa ya kuwa katika Muungano wa Kiarabu (Arab Coalition), kisha ikafika kilele baada ya kuuawa kwa Saleh ambapo ushawishi wa Uingereza Kaskazini ulidhoofika na ikahofia pengo ikiwa Wahouthi watafanikiwa kueneza ushawishi wao Kaskazini. Kwa hiyo ilianza kufikiria kwa uzito kuwa na nguvu Kusini itakayokuwa karata ya shinikizo ili iwe na nafasi katika utawala wa Yemen, na ikiwa haiwezi, basi angalau Kusini. Hivyo ikaanza kufikiria kwa uzito kuimarisha ushawishi wake Kusini, hasa kwa kuwa haikuwa ikimtegemea Hadi kikamilifu kwa kuzingatia kuwa Saudi Arabia inamdhibiti. Hivyo ilishughulikia jambo hili kupitia Imarati, pamoja na kuanza kwa vikosi vya Rais wa zamani wa Yemen Ali Saleh – aliyeuawa na Wahouthi mwishoni mwa mwaka uliopita tarehe 2017/12/4 – kurejea Kusini na kupanga safu pamoja na vikosi vya Imarati katika kupambana na Wahouthi. Chanzo kimoja cha serikali ya Yemen "kilithibitisha kuwa Tariq Saleh, mpwa wa Ali Saleh, yuko mjini Aden chini ya ulinzi wa vikosi vya Imarati. Vyanzo vya kidiplomasia vilieleza kuwa Imarati inafanya juhudi kubwa ili kuondoa vikwazo vilivyowekwa kwa Ahmad mwana wa Ali Saleh ili acheze nafasi ya kisiasa katika siku zijazo"... (Tovuti ya Nass Times ya Yemen 2018/2/5). Kamanda wa vikosi vya Baraza la Mpito la Kusini, Aidarus al-Zubaidi, alitangaza akisema: "Sisi tutamuunga mkono Tariq Saleh na tutasimama naye Kaskazini na katika ardhi zote hadi Sana'a itakapokombolewa kikamilifu... 2018/1/30 France 24"). Hii ina maana kwamba Uingereza inacheza mchezo Kusini na kuimarisha ushawishi wake kupitia vibaraka wake miongoni mwa jamaa wa Ali Saleh wenye ushawishi katika vikosi vya Walinzi wa Jamhuri ya Yemen (Republican Guard) na chama cha General People's Congress. Vikosi vya wanaotaka kujitenga vilikuwa vinaungwa mkono na Imarati, ikumbukwe kuwa Imarati inashiriki kwa vikosi vya anga na nchi kavu, huku Saudi Arabia ikishiriki kwa vikosi vya anga pekee.
4- Hivyo Uingereza ilianza kufanya kazi Kusini kupitia Imarati ili kupenya Vuguvugu la Kusini la asili au kulidhoofisha kwa kuunda vuguvugu jipya linaloongoza uwanjani... Imarati ilianza na mrengo wa Ali Salem al-Beidh, licha ya kwamba Uingereza ilikuwa inatambua ukubwa wa majaribio ya Marekani ya kumuunga mkono Ali Salem al-Beidh na Ali Nasir. Miongoni mwa majaribio hayo ya Marekani ni kutoa uungaji mkono wa Iran, na pia msaada wa Misri kama mkutano wa Vuguvugu la Kusini mjini Cairo chini ya uongozi wa Ali Nasir Muhammad mwaka 2014. Pia, msaada wa Lebanon ambapo Beirut ilimpa Ali Salem al-Beidh hifadhi na jukwaa la habari ambalo alikuwa amenyimwa nchini Oman tangu alipokimbilia huko mwaka 1994. Kisha, kufuatia kuanza kwa operesheni ya Asifat al-Hazm ya Saudi Arabia mwaka 2014, alihamia Riyadh iliyompa fedha nyingi... Licha ya hayo, kama tulivyosema hapo awali, Imarati ilianza kujaribu kumshawishi al-Beidh na Nasir... Sababu ya kuanza na mrengo huu ni kwa sababu mbili: Kwanza: Inafuata vurugu. Pili: Historia yake ya zamani ya utii kwa Waingereza, kwani wao ndio waliohusika na kuundwa kwa Mstari wake wa mbele wa Kitaifa na kumkabidhi utawala wa Yemen Kusini. Walitaka kufufua kumbukumbu za kipindi hicho ili kumrejesha au kumvuta karibu nayo, hivyo wakamtendea wema... Baada ya kuanza kwa operesheni za Muungano wa Kiarabu nchini Yemen mwaka 2015, walimhamisha kutoka Saudi Arabia kwenda Imarati ambako anaishi Abu Dhabi sasa. Hii ni kwa sababu al-Beidh alikuwa akihama kati ya nchi zinazotii Marekani; alikaa takriban miaka miwili (2012 na 2013) nchini Lebanon akisaidiwa na Iran na kwa ulinzi wa chama chake huko. Kisha akahamia Saudi Arabia na baadaye Imarati ikamvuta kwa kuwa iko katika muungano huo na kumhamishia kwake huko Abu Dhabi na kumfanyia heshima kubwa... Inajulikana kuwa Salem al-Beidh ni mtu wa kugeuka-geuka; utii wake ulikuwa kwa Waingereza alipokuwa Rais wa Yemen Kusini, kisha mapema miaka ya tisini Marekani ikamvuta na akabaki kwenye utii huo huku akihama kati ya nchi zinazotii Marekani. Sasa yuko Imarati wanajaribu kumvuta na haiepukiki kuwa anaweza kugeuka tena, na ikitokea, mambo yanaweza kuwa na mvutano kati yake na Imarati... Kwa vyovyote vile, msimamo wake uko karibu zaidi na Baraza la Mpito kwani alilisifu: ("Makamu wa zamani wa Rais wa Yemen, Ali Salem al-Beidh, ametangaza kuunga mkono na kubariki wito wa kuundwa kwa 'chombo cha kisiasa cha Kusini', siku moja baada ya magavana watatu katika mikoa ya kusini kuunga mkono wito wa gavana wa Aden, Aidarus al-Zubaidi, wa kuunda chombo hicho. Al-Beidh alisisitiza katika taarifa ambayo 'Al-Arabi Al-Jadeed' ilipata nakala yake, kwamba ataunga mkono wito huu 'kwa kila linalowezekana', na akahimiza nguvu mbalimbali za kisiasa za Kusini na watu huru 'kuitikia vyema wito huu na kutoka katika hali ya kusubiri, kutojali, na utegemezi kuelekea awamu mpya'... Taarifa ya al-Beidh ilikuja siku moja baada ya kujiunga kwa magavana watatu: Gavana wa Abyan al-Khader al-Saeedi, Gavana wa Lahij Nasser al-Khobaji, na Gavana wa Ad-Dali' Fadhl al-Jaadi kwenye wito wa Gavana wa Aden Aidarus al-Zubaidi wa kuunda 'chombo cha Kusini'.... Al-Arabi Al-Jadeed 2016/9/16"). Mwenzake Ali Nasir Muhammad naye anafanana naye katika hilo; wakati mwingine anaunga mkono kujitenga na wakati mwingine anataka serikali moja nchini Yemen lakini kwa masharti anayoyaona! Alipoulizwa kuhusu suluhisho nchini Yemen 2017/10/4, yaani kabla ya uasi wa Ali Saleh dhidi ya Wahouthi mwishoni mwa 2017, alisema ("Kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa ya makubaliano. Kuondolewa kwa wahusika wakuu waliosababisha vita kutoka pande zote mbili 'Wahouthi na serikali ya Hadi' kutoka katika nafasi zote rasmi wakati wa kipindi cha mpito. Kunyang'anywa silaha kutoka kwa pande zote na vyama na kukabidhiwa kwa Wizara ya Ulinzi, kwa sababu Yemen inahitaji rais mmoja, serikali moja, na waziri wa ulinzi mmoja na kuheshimu sanduku la kura katika kipindi kijacho... Al-Ahram Al-Arabi 2017/10/4"). Ni wazi kutokana na haya yote kwamba Waingereza wamefanikiwa kupitia Imarati kupenya na kuwa na ushawishi kwa watu hao wawili na mirengo yao; hawakuchukua utengano kama itikadi thabiti wasiyoiacha kama ilivyokuwa asili ya Vuguvugu la Kusini, bali kulingana na mazingira yanayowazunguka.
5- Ama mrengo wa Hassan Baoum ulikuwa wa kisiasa, kiitikadi na wa kujitenga hadi mifupani... Waingereza wakatambua kuwa suluhisho lolote la kuridhisha, ushawishi au udhibiti halitafanya kazi, hivyo wakajaribu kumzingira nchini Oman kwa kifungo cha nyumbani kwa njia ya ujanja, yaani bila uamuzi rasmi. Yeye alikuwa amekimbilia huko kwa sababu Oman ilikuwa ikijionyesha kuwa upande wowote, kana kwamba hakujua kuwa inafuata Uingereza kulingana na jukumu ililopangiwa! Kupitia vibaraka wake nchini Oman, Hassan Baoum alibanwa na kuwekwa chini ya kifungo cha nyumbani katika mji wa Salalah kwa muda mrefu... Kutokana na kutokuwepo huku kwa muda mrefu kwa mtu nambari moja wa Marekani katika Vuguvugu la Kusini, makundi yanayotii Marekani katika vuguvugu hilo yalidhoofika kwa kiasi fulani. Waingereza kupitia Imarati wakatumia fursa hiyo na kuelekeza juhudi za kuunda vuguvugu la kusini linalofanana na la mrengo wa Baoum lakini lenye nguvu zaidi katika suala la Kusini. Wakampata Aidarus al-Zubaidi, ambaye ni mmoja wa viongozi wanaojulikana katika Vuguvugu la Kusini, na mwanzilishi wa harakati ya kujitenga ya "Hatm" mwaka 1996. Kutokana na ukaribu wake na kundi la Waingereza, Rais Hadi alimteua 2015/12/7 kuwa Gavana wa Aden, miezi kadhaa baada ya kuanza kwa operesheni ya Asifat al-Hazm (Machi 2015). Hiyo ilikuwa ishara tosha ya imani ya vibaraka wa Waingereza kwake. Aidarus al-Zubaidi alipewa sifa kubwa mjini Aden; alionekana kama gavana aliyefanikiwa mjini humo, akarudisha umeme, akafukuza magenge ya wahalifu, akapambana na Wahouthi, na akapinga mapendekezo ya mjumbe wa Marekani wa Umoja wa Mataifa, Ould Cheikh. Haya yote yalifanyika kwa uungaji mkono wa kifedha na kijeshi wa wazi na wa moja kwa moja kutoka Imarati. Kwa kuwa alikuwa mpiganaji katika vita vya wenyewe kwa wenyewe vya 1994 na kiongozi aliyehusika katika harakati ya kujitenga tangu mapema, na kusakwa na utawala wa Ali Saleh mjini Sana'a tangu alipokimbilia Djibouti mwaka 1994, na kwa kuwa ni mtoto wa eneo la Ad-Dali' (kitovu na uzito wa Vuguvugu la Kusini), pamoja na mafanikio yake kama gavana wa Aden na vita vyake dhidi ya Wahouthi, macho yote Kusini yakamwelekea kama kiongozi wa kisiasa anayechipukia na kushindana na uongozi wa kihistoria wa Hassan Baoum katika Vuguvugu la Kusini... Kijeshi, Aidarus al-Zubaidi anamtegemea Hani bin Breik, mwanzilishi wa vikosi vya "Mkanda wa Kusini" (Security Belt), ambaye anaelezewa kwa upana kama mtu wa Imarati Kusini (Hani bin Breik ambaye alitokea kwenye uwanja wa Yemen kama mpiganaji anayekabiliana na Wahouthi, kisha kwenye uwanja wa kisiasa kama waziri anayelazimishwa na nguvu ya Imarati, kutokana na ushawishi wake uliothibitika kwa uungaji mkono mkubwa kutoka Abu Dhabi, na kuanzisha kile kinachoitwa vikosi vya "Mkanda wa Usalama", ambavyo ni wanamgambo wanaoungwa mkono waziwazi na nchi ya Imarati kusini mwa Yemen... Sasa Post 2017/11/2). Hivyo, Zubaidi na Breik walikuwa na nafasi Kusini. Lakini kwa sababu walikuwa katika serikali ya Hadi na utii wao ulikuwa wazi kwa Waingereza, jambo ambalo lisingewapa umaarufu katika wito wa Vuguvugu la Kusini, hatua ya kwanza ilikuwa ni kuwaondoa katika serikali ya Hadi kwa njia inayowaonyesha, hasa Zubaidi, kuwa katika hitilafu kubwa na upande wa Hadi, na kisha watu wa Kusini wakusanyike karibu naye kuunda Vuguvugu jipya. Na ndivyo ilivyokuwa...
6- Rais wa Yemen alitoa uamuzi tarehe 27 Aprili 2017 wa kumfuta kazi Aidarus al-Zubaidi, Gavana wa Aden, na Waziri wa Nchi Hani bin Breik, huku akimpeleka huyu wa pili kwenye uchunguzi. Maelfu ya Wayemen walitoka katika maandamano mjini Aden kupinga maamuzi ya Hadi. Makundi ya Vuguvugu la Kusini katika "Azimio la Aden" tarehe 4 Mei 2017 yalitangaza kuwa yameamua kumpa Aidarus al-Zubaidi mamlaka ya kuunda na kuongoza kundi la kisiasa litakalosimamia na kuwakilisha Kusini ili kufikia malengo na matarajio yake, pamoja na kumpa mamlaka kamili ya kuchukua hatua muhimu kutekeleza vipengele vya azimio hilo... Baada ya wiki moja tangu Vuguvugu la Kusini kumteua Zubaidi kuunda uongozi wa kisiasa, Zubaidi alitangaza uenyekiti wake wa Baraza la Mpito la Kusini mjini Aden tarehe 11 Mei 2017, na kumteua Bin Breik kama naibu wake, pamoja na wanachama wengine 26. Kwa ajili ya kuonekana ana nguvu zaidi ya Baoum, alikuwa akihutubia akiwa ameweka bendera ya zamani ya Yemen Kusini pembeni yake ("Zubaidi alisema katika hotuba ya televisheni siku ya Alhamisi, akiwa ameweka bendera ya dola ya zamani ya Yemen Kusini, kwamba kulingana na 'Azimio la Kihistoria la Aden', uongozi wa juu wa kisiasa wa kusini umeundwa uitwao Baraza la Mpito la Kusini. Aliongeza kuwa Hani bin Breik atakuwa naibu mwenyekiti wa baraza hilo pamoja na wanachama 26. Alieleza kuwa 'Baraza la Mpito la Kusini litasimamia kukamilisha taratibu za kuanzisha idara za baraza hilo, na kusimamia na kuwakilisha kusini ndani na nje ya nchi'... CNN kwa Kiarabu 2017/5/11"). Kwa hili, Zubaidi na Bin Breik na nyuma yao Imarati/Waingereza wakawa na mamlaka ya kuunda uongozi wa Kusini kikamilifu. Magavana wa mikoa ni wale walioteuliwa na Rais wa Yemen, yaani wamo katika mzunguko wa Waingereza nchini Yemen, vilevile viongozi wengine wa Baraza la Mpito ni wafuasi wake. Hata ameweza kujumuisha katika baraza lake baadhi ya watu wa mrengo wa Baoum kama Ali al-Saadi na Nasser al-Khobaji hata kama ni kwa muda; ukweli ukibainika watatoka au watatolewa, au inaweza kuwa njia ya kuwavuta. Nasser al-Khobaji, kutokana na kutokuwepo kwa Baoum, amekuwa muungaji mkono wa mapema wa Zubaidi!
Kutokana na udhibiti huu wa karibu wa Baraza la Mpito likiongozwa na Aidarus al-Zubaidi mjini Aden, na kuwa na vikosi vya kijeshi vikubwa kiasi vikiongozwa na Bin Breik katika mikoa mingine ya kusini, na hata Marib, na kutokana na magavana wa mikoa kuungana na uongozi wa Aidarus al-Zubaidi, vilevile uungaji mkono wa wanachama wa zamani wa "Dola ya Kusini" kama "wasoshalisti" mfano Ali Salem al-Beidh, na Tariq al-Fadhli na mkondo wake wenye mwelekeo wa Kiislamu ulioongezwa kwenye nafasi yake ya kikabila Abyan, na kusimama kwa Imarati upande wake kifedha, kisiasa, na kijeshi, Waingereza watakuwa wamemaliza suala la Vuguvugu la Kusini kupitia kibaraka wao Aidarus al-Zubaidi kwa kiwango kikubwa. Ikiwa hali ya kisiasa itaendelea hivi, hasa kuwepo kwa uzito wa Imarati Kusini, basi udhibiti huu una uwezekano wa kuendelea.
7- Ama Marekani imetambua kuchelewa kwake na kuonyesha kufadhaika kwake. Kinachoashiria kufadhaika kwa Marekani kutokana na kuundwa kwa Baraza la Mpito ni upinzani wa mjumbe wake wa kimataifa Ould Cheikh kwa baraza hilo ("Mjumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Yemen, Ismail Ould Cheikh, alimtumia gavana aliyefutwa kazi wa Aden, Aidarus al-Zubaidi, ujumbe wa 'tishio la wazi' kufuatia kutangaza kwake kuunda baraza la mpito kwa ajili ya kujitenga kwa Kusini, kwa mujibu wa chanzo kilicho karibu na mambo hayo. Tovuti ya Al-Mashhad al-Yemeni ilinukuu chanzo hicho kikitaja kuwa Ould Cheikh alikutana na Zubaidi na kumpa tishio la wazi ikiwa atashikilia baraza alilotangaza, ambalo lilikataa na serikali ya Yemen, Baraza la Ushirikiano la Ghuba, Wahouthi, na wengi ndani ya Vuguvugu la Kusini. Na kwamba akishikilia hilo, Umoja wa Mataifa na Baraza la Usalama litamjumuisha miongoni mwa wanaokwamisha mchakato wa amani nchini Yemen na utekelezaji wa Azimio 2216 lililotolewa chini ya Sura ya Saba, na watashughulikiwa kama Wahouthi na Saleh kama 'waasi'... Russia Today 2017/5/14"). Inaonekana Marekani ilirekebisha mambo kwa kuishinikiza Oman kumwachilia Baoum. Baada ya kuachiliwa kwake, Hassan Baoum alianza mienendo mikali inayopinga Baraza la Mpito inayoungwa mkono na Imarati, katika picha kubwa ya mapambano ya Kiingereza na Marekani nchini Yemen. Ilionekana kuwa mienendo yake ina uungaji mkono wa wazi wa Saudi Arabia; mkutano wa kwanza wa Baraza la Mapinduzi la Vuguvugu (Revolutionary Movement Council) ulifanyika chini ya uangalizi wao mjini Aden tarehe 2017/8/17 ukijumuisha wafuasi wake mia sita, akishutumu nchi ya Imarati kwa kuikalia kwa mabavu Yemen Kusini... Taarifa ya mkutano huo ilisema: ("Tunakataa katakata kutumia shauku ya watu wetu wa Kusini na kusambaza uongo na kuwaathiri kihisia ili kupata uungaji mkono wa watu kisha kwenda kinyume na matakwa ya watu wa Kusini... Tunasisitiza kuwa kiongozi Hassan Baoum, mwenyekiti wa Baraza Kuu la Vuguvugu la Mapinduzi, anachukuliwa kuwa kiongozi na alama ya Kusini tunayemuenzi na kujivunia... Kinachoendelea leo Kusini ni mbio za kasi kati ya nguvu za nje kama nchi ya Imarati ambayo imekuwa ikihodhi milango ya Kusini na mali zake na kudhibiti hatima ya watu wetu, kisha inakuja kuwapa kundi la wale iliowafanya wafuasi wake makombo madogo ya kudunisha... Aden al-Ghad 2017/8/17"). Yaani kundi la Baoum linaonyesha uadui wa wazi kwa Imarati na kuitaka iondoke Yemen, na mkutano wa Baoum uliwaita kundi la Zubaidi kama "wafuasi wa Imarati ambao inawapa makombo madogo"...
Kisha kukawa na mkutano wa pili wa kundi la Baoum uliofanyika tarehe 2017/11/11. Taarifa ya mwisho ya mkutano huo iliyofanyika Aden ilisema: "Tunatoa wito kwa nchi zinazojiita Muungano wa Kiarabu kwa ajili ya mazungumzo ya moja kwa moja na Baraza Kuu la Vuguvugu baada ya kuondoa vikosi vyake vyote katika ardhi yetu, tukisisitiza nia yetu juu ya mafungamano ya kijamii na kidini yaliyopo kati yetu"... Baraza linaloongozwa na Baoum liliuelezea muungano huo kama "nchi zinazokalia kwa mabavu" na kuongeza: "Tunasisitiza haki yetu kamili ya kushughulika na uvamizi kwa njia na vyombo vyote halali kwa wakati na mahali mwafaka kulingana na maslahi yetu ya kitaifa". Taarifa hiyo ilisisitiza kuwa "mazungumzo yoyote au suluhisho yanayopuuza suala la Kusini na mwakilishi wake wa kisheria hayatafanikiwa kwa sababu wawakilishi wa kisheria ndio walioongoza vuguvugu tangu siku ya kwanza na si wale waliotokea kwa bahati mbaya au waliotengenezwa na pesa au walionakiliwa na uvamizi wa kigeni"... (Al-Arabi Al-Jadeed 2017/11/11). Ingawa taarifa hiyo ilizungumzia Muungano wa Kiarabu, kimsingi ilimlenga Imarati kwa sababu mkutano huo ulifanyika kwa ulinzi wa Saudi Arabia!
8- Muhtasari: Baada ya kushindwa kwa Ali Salem al-Beidh na Ali Nasir Muhammad mwaka 1994, na Ali Saleh kudhibiti rasilimali za Yemen Kusini na kutengwa kwa watu wa Kusini na kukandamizwa kwa wanajeshi wengi wa Kusini... haya yote yalisababisha kuibuka kwa harakati nyingi za upinzani tangu wakati huo hadi leo... Zinazojitokeza zaidi ni harakati tatu:
Vuguvugu la Kusini mrengo wa Ali Salem al-Beidh: Huyu ni kigeugeu; mara yuko na Marekani na vibaraka wake, mara anakubaliana na Uingereza na vibaraka wake...
Vuguvugu la Kusini mrengo wa Hassan Baoum: Anaungwa mkono na Marekani na vibaraka wake hasa Iran...
Vuguvugu la Kusini mrengo wa Zubaidi: Anaungwa mkono na Uingereza na vibaraka wake hasa Imarati...
Kama tulivyoeleza hapo juu, tumeangazia mienendo yake muhimu kuelekea masuala ya sasa ya Yemen... Na ni jambo la kusikitisha kwamba masuala yetu yanachezewa na makafiri wakoloni kwa kutumia zana mbovu kutoka miongoni mwetu! Damu zetu zinamwagika Yemen na kwingineko kwa maslahi ya makafiri kupitia zana za ndani... Watu hawa wamesahau au wamejisahaulisha mambo ambayo kama wangeyafanyia akili wangelia damu kwa ubaya wa kile walichokifanya:
Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu na Mtukufu, amekataza kwa mkatazo mkali Mwislamu kuwategemea makafiri madhalimu:
وَلَا تَرْكَنُوا إِلَى الَّذِينَ ظَلَمُوا فَتَمَسَّكُمُ النَّارُ وَمَا لَكُمْ مِنْ دُونِ اللَّهِ مِنْ أَوْلِيَاءَ ثُمَّ لَا تُنْصَرُونَ
"Wala msiwategemee wale walio dhulumu, isije ikakuguseni Moto. Wala nyinyi hamna walinzi badala ya Mwenyezi Mungu, kisha hamtanusuriwa." (Hud: 113)
Na Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) anasema kuhusu umwagaji wa damu unaofanyika bila haki kuwa ni jambo kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu kuliko kutoweka kwa dunia. At-Tirmidhi ametoa kutoka kwa Abdullah bin Amr kwamba Mtume (saw) amesema:
لَزَوَالُ الدُّنْيَا أَهْوَنُ عَلَى اللَّهِ مِنْ قَتْلِ رَجُلٍ مُسْلِمٍ
"Hakika kuondoka kwa dunia ni jambo jepesi mbele ya Mwenyezi Mungu kuliko kuuawa kwa mtu Mwislamu." (Imetolewa na Ibn Asakir katika kamusi yake na kusema hii ni hadithi nzuri).
Basi iweje wakati damu inamwagika kwa maslahi ya makafiri wakoloni?! Hakika ni jinai juu ya jinai:
سَيُصِيبُ الَّذِينَ أَجْرَمُوا صَغَارٌ عِنْدَ اللَّهِ وَعَذَابٌ شَدِيدٌ بِمَا كَانُوا يَمْكُرُونَ
"Wale waliofanya jinai itawafika udhalili mbele ya Mwenyezi Mungu na adhabu kali kwa sababu ya vitimbi walivyokuwa wakivifanya." (Al-An'am: 124)
Pamoja na hayo, Yemen ambayo Mtume (saw) aliielezea kama nchi ya imani na hekima, haikosi watu waumini wakweli na wenye ikhlasi ambao watasimama kidete dhidi ya wale wanaowategemea makafiri wakoloni... Na watairudisha Yemen kwa idhini ya Mwenyezi Mungu kuwa Nyumba ya Uislamu (Dar al-Islam) inayofunika kwa bendera ya Uislamu katika Khilafah ya Rashidah itakayoirudishia utukufu wake, ili iwe kama alivyosema Mtume (saw) katika kile alichokitoa Al-Bukhari katika sahihi yake kutoka kwa Abu Hurayrah (ra) kutoka kwa Mtume (saw):
أَتَاكُمْ أَهْلُ الْيَمَنِ هُمْ أَرَقُّ أَفْئِدَةً وَأَلْيَنُ قُلُوبًا الْإِيمَانُ يَمَانٍ وَالْحِكْمَةُ يَمَانِيَةٌ
"Wamewajia watu wa Yemen, wao wana nyoyo laini na za huruma zaidi. Imani ni ya Kiyemen na hekima ni ya Kiyemen."
8 Jumada al-Akhirah 1439 Hijria 24/02/2018 Miladi