Mfululizo wa Majibu ya Mwanachuoni Mtukufu Ata Bin Khalil Abu al-Rashta, Amir wa Hizb ut-Tahrir, kwa Maswali ya Wageni kwenye Ukurasa Wake wa Facebook "Feqhi"
Kwa Pipit Meidawati na Фатиме Сулиманова
Swali: Pipit Meidawati
assalamu'alaikum wa rahmatullahi wa baarakaatuh
Namuomba Allah azidi kukulinda na kukunusuru. La'ala Allahu yusahhil umuuraka.
Ningependa kuuliza kuhusu tabarruj. Tunaitafsiri vipi na kuitekeleza vipi? Ninachojua ni kwamba tabarruj inamaanisha kuonyesha urembo mbele ya mwanamume mgeni (isiyo mahram). Kisha kuwavutia watazame, au hata kutukodolea macho. Pia inategemea na mazoea/mila/ada (urf).
Ninaishi Indonesia, tunavutana kuhusu utekelezaji wa tabarruj. Kwa hakika, mtindo wa maisha wa Magharibi umeathiri jinsi tunavyovaa na kujiremba. Wanawake wanatumia vipodozi kama poda ya uso, lipstick, eyeshadow n.k. Wakati mwingine, ni vipodozi vya asili tu au vya kila siku. Wanafanya kazi, wanasoma vyuoni, wanahudhuria majlisi za ta'lim, wanatembeleana n.k. wakiwa na aina hii ya vipodozi. Wakati mwingine wanataka kuonyesha urembo zaidi ya kawaida katika hafla fulani kama vile siku ya harusi, au kuhudhuria sherehe ya harusi, hawatumii vipodozi vya kila siku, bali hujiremba zaidi kwa namna inayovutia (bold/glam makeup). Baadhi ya wanawake wanafanya kazi kama watumbuizaji, mastaa, waimbaji, kisha wanavaa na kujipaka vipodozi vilivyokithiri sana.
Je, ni lazima tuache vipodozi hivyo vyote kwa sababu vimeundwa na mtindo wa maisha wa Magharibi? Je, hatuna ruhusa ya kupaka chochote kwenye nyuso zetu, au ni sawa ikiwa tutapaka tu vipodozi vya kila siku/vya asili?
Wakati huo huo, baadhi ya wanawake wanapaka itsmid (wanja wa Kiajemi) kwenye macho yao, kwa sababu Rasulullah SAW aliamrisha na pia alifanya hivyo. Lakini wao ni wachache tu na hata wakati mwingine wanavuta hisia za watu wanaowazunguka.
Natamani wewe, Syeikh Ata Abu al-Rashta, usijali kunielezea utekelezaji wa tabarruj.
Asante sana, jazakallahu khairan katsiran.
Wassalamu'alaikum wa rahmatullahi wa baarakaatuh
Pipit Meidawati, kutoka Indonesia.
Swali: Фатиме Сулиманова
Assalamu Alaikum wa Rahmatullahi wa Barakatuh. Mpendwa Sheikh, nina swali kwako; ikiwa wanawake wataenda sehemu za umma na kupaka make-up kwenye nyuso zao, je, wanaingia chini ya neno tabarruj? Ni nini maana ya uananamke (femininity) katika Sharia?
Jibu:
Wa Alaikum Salaam wa Rahmatullahi wa Barakatuh,
Maswali haya mawili yako kwenye mada moja, kwa hiyo tutayajibu kwa pamoja:
Tumeshatoa majibu ya maswali huko nyuma kuhusiana na mada ya tabarruj... na ninanukuu moja ya majibu ya tarehe 09/10/2016 kwani yanatosheleza, In Shaa Allah:
Jibu lililotajwa:
(Kabla ya kuingia katika maelezo ya maswali yako, nitakutajia baadhi ya mambo katika mada hii ambayo yamefafanuliwa katika kitabu cha Nidhamu ya Kijamii katika mlango wa "Kumtazama Mwanamke", na nitakutajia baadhi ya mambo ya msingi:
1- Kutoka kwa mwanamke katika maisha ya kijamii ni lazima kuwe kwa vazi la kisheria linalojumuisha: Jilbab, kusitiri uchi (awrah), na kutoonyesha mapambo (kutofanya tabarruj).
2- Uchi ni mwili mzima wa mwanamke isipokuwa uso na vitanga vya mikono viwili, na mwanamke kufunua uchi wake ni haramu, na hapa haisemwi "kuvutia macho", yaani iwe amevutia macho au hakuvutia, kufunua uchi ni haramu...
3- Tabarruj kilugha ni mwanamke kuonyesha mapambo yake na uzuri wake kwa wanaume. Imetajwa katika Lisan al-Arab: Na at-tabarruj: ni kuonyesha mapambo kwa watu wageni (wasio mahram), na hilo ndilo lenye kulaumiwa, ama kwa mume hapana... Na imetajwa katika Al-Qamus al-Muhit: Na tabarrajat: ameonyesha mapambo yake kwa wanaume... Na imetajwa katika Mukhtar al-Sahih: Na at-tabarruj ni mwanamke kuonyesha mapambo yake na uzuri wake kwa wanaume... Na imetajwa katika Maqayis al-Lugha: Baraja: herufi Ba, Ra, na Jim ni asili mbili: mojawapo ni kuchomoza na kudhihiri... na kutokana na hiyo kuna at-tabarruj, nayo ni mwanamke kudhihirisha uzuri wake, na inaeleweka kutokana na neno "kudhihirisha" na neno "kuchomoza na kudhihiri" kuwa mapambo hayo yanavutia macho kana kwamba anajitokeza kwa wanaume... Na maana ya kisheria haitofautiani na hilo, kwani Mwenyezi Mungu Subhanahu amesema:
وَلَا يَضْرِبْنَ بِأَرْجُلِهِنَّ لِيُعْلَمَ مَا يُخْفِينَ مِنْ زِينَتِهِنَّ
"Wala wasipige chini miguu yao ili yajulikane mapambo waliyoyaficha." (QS. An-Nur [24]: 31)
Hivyo mwanamke asitingishe mguu wake kwa nguvu chini anapotembea ili kutoa sauti ya kikuku (pingu za miguuni) na mwanamume ajue kuwa mwanamke huyo amevaa pambo kwenye mguu wake chini ya nguo. Haya yote yanamaanisha kuwa tabarruj kilugha na kisheria ni mapambo yanayovutia macho, na si mapambo tu peke yake.
Hivyo basi, tabarruj ni mapambo yanayovutia macho bila ya kufunuka kwa uchi. Ama kufunuka kwa uchi, hilo ni haramu iwe limevutia macho au la... Kwa hiyo tabarruj si mapambo yenyewe, kwani kuna mapambo ya kawaida yasiyovutia macho ambayo yanaruhusiwa kwa wanawake, na kuna mapambo yanayovutia macho ambayo yanaitwa tabarruj, na tabarruj ni haramu. Tabarruj hutokea katika mambo mawili:
Mapambo ya mwanamke kwenye sehemu inayoruhusiwa katika mwili wake, yaani kwenye vitanga vya mikono na uso wake, na kwenye mavazi yake ikiwa yanavutia macho.
Mapambo ya mwanamke kwenye sehemu isiyoruhusiwa (uchi) bila ya kufunuka kwa uchi wenyewe, yaani kama vile kujipamba kwenye mguu wake kwa kuvaa kikuku, au kujipamba kwenye mikono yake kwa kuvaa bangili fulani, huku mguu au mkono ukiwa umefunikwa, kisha mwanamke akionyesha harakati kwa mguu wake au mkono wake inayomfanya mwanamume ajue kuwa kuna mapambo kwenye mguu wake au mkono wake, basi huko ni tabarruj hata kama mguu au mkono umefunikwa.
4- Ama mapambo kwenye sehemu inayoruhusiwa katika mwili wa mwanamke, au kwenye vazi lake, ikiwa yanavutia macho basi ni tabarruj na ni haramu. Maana ya kuvutia macho ni kuwa mapambo haya katika eneo hilo si ya kawaida, yaani anapopita mbele ya wanaume akiwa na mapambo hayo yanavuta macho yao kwenye uananamke wa mwanamke huyo. Na maana ya kutovutia macho, ni kuwa mwanamke akipita mbele ya wanaume, basi fikra za kivutio cha uanamke haziji kichwani mwao... Jambo hili linaingia katika tahqiq al-manat (uhakiki wa uhalisia), na sidhani kama ni gumu, kwani uanaume na uananamke upo kwa mwanamume na mwanamke, na ni rahisi kwake yeye (mwanamume) au kwake yeye (mwanamke) kutambua kama mapambo hayo yanavutia macho au hayavutii, hasa mwanamke kwa sababu anajua mapambo yake ikiwa ni ya kawaida au ikiwa yanavutia macho ya wanaume...
5- Ama mapambo kwenye sehemu isiyoruhusiwa bila ya kufunuka kwa uchi, kama vile mwanamke kujipamba mguuni kwa kikuku kisha akapiga miguu yake chini anapotembea ili kutoa sauti mwanamume ajue kuwa kuna mapambo mguuni mwake, basi huu ni tabarruj na ni haramu... Au kama vile kujipamba mkononi na kuvaa bangili kisha akatikisa mkono wake ili mwanamume ajue kuwa kuna mapambo mkononi mwake... basi huu ni tabarruj, na ni haramu hata kama mguu au mkono umefunikwa.
6- Baada ya hapo nitaanza na maelezo ya maswali yako na kukujibu:
a- Kuhusu mapambo ya wanawake kwa pete kwenye vidole vya mikono yake, ikiwa ni pete za kawaida basi hazivutii macho... isipokuwa kwa mfano akivaa pete inayotoa mwanga au inayotoa sauti, au yenye ukubwa wa kusisimua, au mfano wa hayo... basi hii inavutia macho na ni tabarruj... Na mfano wa hili ni kama kuvaa kiatu kinachotoa mwanga au mfano wake...
Ama kuvaa mkufu juu ya Jilbab, hili iwe limevutia macho au halikuvutia halijuzu kwa sababu asili ya Jilbab ni kuficha mapambo ya ndani juu ya uchi wake, na mkufu huu ni pambo la shingo, na shingo ni sehemu ya uchi na ni lazima iwe imefichwa chini ya Jilbab, hivyo akitaka kuvaa mkufu shingoni mwake basi auweke chini ya Jilbab. Ama bangili kwenye mkono, ikiwa atatikisa mkono wake na sauti za bangili ikatoka na ikajulikana kuwa mkononi mwake kuna mapambo, basi huu ni tabarruj na haijuzu.
b- Hakika Jilbab ni vazi pana linalofunika mapambo ya ndani na nguo za ndani, yaani Jilbab lenyewe si mahali pa mapambo, na kwa sababu hiyo, mapambo na nakshi juu yake hazijuzu...
c- Mwanamke kupaka wanja (kohl) kwenye macho yake, hilo halivutii macho kwa sababu liko ndani ya jicho, ilhali ikiwa atapaka kwenye kope za macho yake au juu ya ngozi ya jicho rangi fulani, basi hizo zinavutia macho...
d- Kadhalika ikiwa atasafisha ngozi ya uso wake na kuondoa madoa, au baadhi ya chunusi usoni na uso ukaonekana mzuri zaidi kuliko awali lakini unafanana na uso wa kawaida, basi hauvutii macho. Lakini ikiwa ataweka rangi (vipodozi) usoni kwa rangi zinazojitokeza, basi inavutia macho. Na bila shaka, eneo ambalo mwanamke anaishi lina nafasi katika kuvutia macho kama vile kuishi kijijini au kuishi mjini... Jambo la muhimu katika mada hii ni kwamba mapambo yanayokuwa kwa namna isiyo ya kawaida katika eneo hilo na yakavutia macho, mapambo haya yanakuwa ni tabarruj) - Mwisho wa jibu la awali.
Mwishoni, kwa kawaida mwanamke anajua ikiwa mapambo anayojipamba yanavutia macho ya wanaume au la, yaani si vigumu kujua mapambo yanayovutia macho na yale yasiyovutia macho, na wanawake wanajua hilo kupitia hisia zao... Na kwa vyovyote vile, mwanamke Muislamu mchamungu hujiepusha si na haramu tu, bali hata na yale yenye shaka, na baadhi ya Maswahaba walikuwa wakijiepusha na aina fulani za mambo ya halali kwa sababu yako karibu na maeneo ya haramu... Kwani imethibiti kutoka kwa Mtume wa Allah ﷺ kwamba amesema:
لَا يَبْلُغُ العَبْدُ أَنْ يَكُونَ مِنَ المُتَّقِينَ حَتَّى يَدَعَ مَا لَا بَأْسَ بِهِ حَذَراً لِمَا بِهِ البَأْسُ
"Mja hafikii kuwa miongoni mwa wachamungu mpaka aache yale yasiyo na neno (halali) kwa kuhofia yale yenye neno (haramu)." (Imepokelewa na Tirmidhi na akasema: Hii ni Hadithi Hasan)
Natumai katika jibu hili kuna utoshelevu, na Allah ndiye Mjuzi zaidi na mwenye Hekima zaidi.
Ndugu yenu, Ata bin Khalil Abu al-Rashta
30 Shawwal 1441 H Sawia na 21/06/2020 M
Kiungo cha jibu kutoka kwa ukurasa wa Amir (Allah amhifadhi) kwenye Facebook Kiungo cha jibu kutoka ukurasa wa Amir (Allah amhifadhi) kwenye Tovuti