Jibu la Swali
Ukweli wa Migogoro Kati ya Nchi Zinazotegemea Dola Kubwa Moja
Swali:
Assalamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh,
Je, inawezekana kwa nchi tegemezi (tabi’a) au nchi zinazozunguka kwenye mhimili (taduru fi al-falak) kupigana zenyewe kwa zenyewe ikiwa dola kubwa inayofuatwa ni moja kwa nchi hizo zote? Ikiwa hilo linawezekana, basi tunawezaje kufafanua jambo hili maadamu dola inayofuatwa ni moja? Je, mgogoro huu hauathiri maslahi ya dola hiyo kubwa inayofuatwa? Na ikiwa mgogoro kama huo hautokei, tunawezaje kufafanua, kwa mfano, kile kinachoendelea kati ya Iraq na Uturuki, au kati ya Iran na Saudi Arabia, au kati ya Uturuki na Iran? Shukrani kwako.
Jibu:
Waalaykum Salam Warahmatullahi Wabarakatuh,
Miongozo mikuu katika mada hii ni kama ifuatavyo:
1- Haifikiriki kwa nchi zinazotegemea (tabi’a) dola kubwa kufanya vitendo ambavyo vingeiumiza dola hiyo kubwa. Hii ni kwa sababu maana ya kuwa nchi tegemezi katika sera za kigeni ni kwamba nchi hizo hufuata mipango inayochorwa na dola kubwa au sera inayozitekeleza, na hazitoki nje ya sera hiyo hata kwa sehemu ndogo. Vitendo vyao vya nje vimefungwa na matakwa ya dola kubwa, na haziwezi kufanya kitendo chochote kabla ya kushauriana na dola kubwa na kufuata amri zake, kama ilivyo Jordan na Uingereza. Watawala wake hutekeleza amri zake na hawafanyi jambo lolote katika sera za kigeni kabla ya kuitaarifu dola kubwa inayofuatwa, isipokuwa ikiwa ni sera inayojulikana na kufuatwa hapo awali na wanafanya kazi ndani yake, kama vile Jordan kuwasiliana na Qatar inayotegemea Uingereza ili kufanya kazi inayotumikia sera ya Uingereza.
2- Ama nchi inayozunguka kwenye mhimili (dawla al-falak), yenyewe inaunganishwa na dola kubwa kwa maslahi na si kwa ufuasi kamili (taba'iyyah). Hivyo, huenda ikatoka nje ya mhimili wake katika sehemu fulani ya sera za kigeni kwa sababu inatafuta maslahi yake huku ikiwa bado inazunguka kwenye mhimili wa dola kubwa. Kutoka huku kunalingana moja kwa moja na kiwango cha ushawishi wa dola kubwa katika kuwafikisha watawala wa nchi hiyo madarakani, kama ilivyoelezwa katika Jibu la Swali la tarehe 30/07/2013: "Ni lazima kuzingatia mambo ya ushawishi na shinikizo la dola kubwa kwa nchi ya mhimili ambayo huizuia kutoka nje katika sehemu fulani, na nguvu au udhaifu wa uzuiaji huu unategemea kiwango cha ushawishi wa dola kubwa katika kuifikisha tabaka tawala madarakani. Ikiwa ushawishi wa dola kubwa ni mkuvu, basi itakuwa vigumu sana kwa nchi inayozunguka kwenye mhimili kujitenga na sehemu yoyote ile. Na kadiri ushawishi wa dola kubwa unavyopungua, ndivyo nchi inayozunguka kwenye mhimili inavyoweza kujitenga katika sehemu moja au zaidi za sera za kigeni za dola kubwa." Kwa mfano: Canada inazunguka kwenye mhimili wa Marekani kama inavyozunguka kwenye mhimili wa Uingereza kulingana na maslahi yake yanavyohitaji. Lakini Canada ilitangaza mnamo tarehe 29/09/2015 kuwa Iran ni nchi inayofadhili ugaidi na ikafunga ubalozi wa Iran nchini humo; bali iliichukulia Iran kuwa "inawakilisha tishio kubwa zaidi kwa amani na usalama wa ulimwengu leo," kama ilivyosemwa na Waziri wake wa Mambo ya Nje, John Baird. Hii ilikuja baada ya makubaliano ya nyuklia yaliyopikwa na Marekani ili kuifanya Iran ishirikiane nayo waziwazi katika kile kinachoitwa kufikia amani na usalama katika eneo hilo. Hivyo, kitendo hiki cha Canada – ambayo inazunguka kwenye mhimili wa Marekani – kinatofautiana na Marekani katika sehemu hii, na hakiungi mkono sera ya Marekani. Ni kwa maslahi ya Marekani kwamba Canada ikubali Iran kama nchi inayotafuta amani na usalama na si kuvunja nayo mahusiano na kuitangaza kuwa nchi ya kigaidi inayotishia amani na usalama. Hivyo basi, nchi inayozunguka kwenye mhimili inaweza kutofautiana katika sehemu fulani ikiwa ushawishi wa dola kubwa uko mbali na kuwafikisha watawala wa nchi hiyo madarakani.
Ama kuhusu Uturuki, ilielezwa katika Jibu la Swali lililotajwa hapo juu la tarehe 30/07/2013 yafuatayo: "Ushawishi wa Marekani katika kuifikisha tabaka tawala madarakani ni mkubwa; Erdogan anahisi kuwa hakuweza kufika madarakani na kuimarisha ushawishi wake ndani ya nchi isipokuwa kwa msaada wa Marekani. Hivyo, anaona kuwa hatima yake imefungamana na Marekani ambayo sasa ina udhibiti mkubwa nchini Uturuki kiasi kwamba inaweza kudhibiti utawala, watawala, mahakama, uchumi, jeshi, na vyombo vya usalama... Kwa hiyo, ushawishi wa Marekani ni mkubwa kwa utawala wa Uturuki, na hivyo basi, kutoka kwa Uturuki katika sehemu yoyote ya sera za kigeni za Marekani ni jambo gumu sana." Jibu la Swali lilihitimishwa kwa kusema: "Yaani kwa sasa Uturuki inazunguka kwenye mhimili wa Marekani, na ushawishi wa Marekani ni mkubwa katika masuala ya Uturuki. Ikiwa hali itaendelea hivi kwa Uturuki kufungamana sana na Marekani, Uturuki inaweza kukaribia ufuasi kamili (taba'iyyah) kwa Marekani na mzunguko wake kwenye mhimili ukaanza kutiliwa shaka!" Kwa sababu hiyo, Uturuki haiko katika kiwango cha Canada; bali ushawishi wa Marekani kwake ni mkubwa sana kiasi kwamba Uturuki haikuweza kutoka katika sehemu yoyote dhidi ya Marekani. Badala yake, iliimarisha uhusiano wake na Marekani na ikakubaliana nayo katika kila jambo, dogo na kubwa. Wakati Uturuki iliposema kupitia kwa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, Feridun Sinirlioglu, kwa kituo cha CNN cha Marekani mnamo tarehe 11/08/2015: "Nchi hizi mbili (Uturuki na Marekani) zimekubaliana kuanzisha eneo (salama) lenye urefu wa kilomita 100 na upana wa takriban kilomita 50." Na taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki ilisema kuwa "vikosi vya upinzani vya Syria vitachukua udhibiti wa eneo hili wakati Marekani na Uturuki zitatoa ulinzi wa anga," Marekani ilijitokeza na kukanusha hilo kupitia kwa msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, Mark Toner, siku iliyofuata yaani tarehe 12/08/2015, akisema: "Hakuna makubaliano juu ya eneo salama... na kwamba hajaona matamshi ya Uturuki na hawezi kushughulika nayo." Akasema: "Tumekuwa wazi kutoka hapa na katika nyakati nyingine kadhaa, hakuna eneo salama...". Hivyo Uturuki haikuweza kutoka nje ya Marekani katika jambo hili, na ilipotaka kuanzisha maeneo salama ilisema kuwa imekubaliana na Marekani, ikimaanisha kuwa haiwezi kufanya jambo lolote katika sera za kigeni kabla ya kuratibu na Marekani na kupata idhini yake, na ikiwa Marekani haitakubali, jambo hilo halifanyiki. Kwa mfano, suala la mafunzo kwa wapinzani wenye msimamo wa wastani ambalo Marekani ilianza mwaka mmoja uliopita, Uturuki ilikubali bila kupinga, pamoja na suala la kufungua kambi ya Marekani inayotumikia maslahi ya Marekani. Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki ilitangaza mnamo tarehe 29/07/2015 kuhusu kusainiwa kwa makubaliano na Marekani yanayofungua kambi ya Incirlik ya Uturuki kwa ndege za Marekani kufanya mashambulizi nchini Syria. Na matukio mengine mengi. Kwa hivyo, haiwezi kufikirika kuwa Uturuki katika enzi ya Erdogan itatofautiana na Marekani hata katika sehemu ndogo, nayo inatenda katika sera za kigeni na Marekani kana kwamba ni nchi tegemezi kwake, na haijatofautiana nayo tangu Erdogan alipoingia madarakani miaka 13 iliyopita. Hivi karibuni, Erdogan alitembelea Saudi Arabia ya Salman inayotegemea Marekani, na nchi hizo mbili zilitangaza mnamo tarehe 30/12/2015 kuundwa kwa baraza la kimkakati la pamoja ili kuimarisha uhusiano kati yao. Uturuki ilikuwa imekubaliana na Saudi Arabia kuanzisha muungano wa kijeshi wa kupambana na ugaidi kama ilivyotangazwa na Naibu Mrithi wa Kiti cha Ufalme wa Saudi, Muhammad bin Salman.
3- Ama kuhusu Iran, yenyewe inazunguka kwenye mhimili wa Marekani na haijatoka katika sehemu yoyote, na inakaribia kuwa nchi tegemezi (tabi'a), hasa katika enzi ya Rais wa sasa Hassan Rouhani na timu yake katika Wizara ya Mambo ya Nje inayoongozwa na Javad Zarif, ambaye anachukuliwa kuwa kibaraka wa Marekani. Iran imeratibu na Uturuki katika suala la Syria, kwani msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki, Levent Gumrukcu, alifunua mnamo tarehe 28/11/2013 kuhusu kuwepo kwa: "Makubaliano kamili juu ya kuendeleza uhusiano wa pande mbili kati ya nchi hizo mbili" na kuhusu kuwepo kwa "mazungumzo chanya kuhusu Syria," na kuhusu "makubaliano kamili juu ya ahadi ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili ili kutatua mgogoro wa Syria na kusitisha umwagaji damu nchini humo." Erdogan alitembelea Iran tarehe 07/04/2015 ili kuimarisha uhusiano kati ya nchi zao, ikimaanisha kuwa tofauti za kifikra kati yao hazikuzuia makubaliano yao katika sera za kigeni na kufuata mkondo wa Marekani. Uturuki pia iliiunga mkono Iran katika suala la mazungumzo ya mpango wa nyuklia.
4- Haitarajiwi kutokea mgogoro kwa maana ya vita kati ya nchi tegemezi au nchi zinazozunguka kwenye mhimili ikiwa dola kubwa inayofuatwa ni ile ile moja. Hii ni kwa sababu yenyewe ndiyo inayosimamia sera za kigeni kwa ujumla, na sera hii ndiyo inayodhibiti mgogoro huo... Hii ni kwa upande wa mgogoro. Ama kutofautiana bila ya kufikia hatua ya kupigana – jambo ambalo liko wazi zaidi kati ya nchi za mhimili – hilo linawezekana kutokea katika hali tatu:
Hali ya kwanza: Ikiwa ni kwa ajili ya kugawa majukumu ili kutumikia maslahi ya dola kubwa.
Hali ya pili: Ikiwa tofauti hizo zinatokana na sababu za ndani bila ya athari za nje zinazoathiri sera za kigeni za dola kubwa ambayo nchi hizo zinazunguka kwenye mhimili wake.
Hali ya tatu: Ikiwa ni kwa ajili ya kumuunga mkono mmoja wa vibaraka kwa kupasha moto tukio ambalo "lilikuwa limetulia" kati yake na kibaraka mwingine, kisha hali inarudi kuwa shwari baada ya kumalizika kwa mahitaji ya msaada huo.
Mfano wa hali ya kwanza:
Uturuki na Iran zinatekeleza sera ya Marekani katika eneo la Kurdistan ya Iraq lakini kwa majukumu tofauti ambayo kidhahiri yanaonekana kugongana lakini ukweli ni tofauti. Kila moja ina jukumu kwa ajili ya Marekani linaloifaa:
Iran inawaunga mkono vibaraka wa Marekani katika eneo hili, kwani Masoud Barzani ni mmoja wa vibaraka wa Waingereza. Hivyo Iran inawaunga mkono vibaraka wa Marekani huko dhidi yake, miongoni mwao ni harakati ya Gorran, ambacho ni chama cha kisiasa cha kisekula kinachofanya kazi katika eneo la Kurdistan kilichoanzishwa na mwanasiasa wa Kikurdi, Nawshirwan Mustafa mwaka 2009 baada ya kujiuzulu kutoka chama cha Patriotic Union of Kurdistan (PUK) kinachounga mkono Marekani, baada ya chama hicho kudhoofika Kurdistan tangu mwanzilishi wake, Jalal Talabani, alipokuwa Rais wa Iraq. Chama hicho kilihusika katika vitendo vya ufisadi kama ilivyo kwa chama cha Barzani. Marekani ikaona umuhimu wa kuanzisha chama kingine chenye sura mpya, hivyo kikaibuka chama cha harakati ya Gorran ili kunyanyua kaulimbiu ya kupambana na ufisadi na kufanya kazi katika upinzani dhidi ya Barzani na kufanya kazi ya kumdhoofisha au kumwangusha. Kilitaka uchaguzi wa urais wa eneo hilo ufanyike kupitia bunge na si kwa njia ya uchaguzi wa watu wote, na kikataka kupunguza mamlaka ya Rais wa eneo hilo na kuyapa bunge. Kiliingia katika uchaguzi wa bunge uliofanyika katika eneo hilo mwaka 2013 na kikapata viti 24 kati ya viti 111, na kikawa chama cha pili baada ya chama cha Barzani kilichopata viti 38. Chama cha Talabani kilishuka hadi nafasi ya tatu kwa kupata viti 18.
Ama Uturuki, yenyewe inafanya kazi ya kumfanya Barzani awe chini ya ushawishi wake na kufanya kazi ya kumdhibiti kwa maslahi ya Marekani. Hivyo, inafanya miradi mingi ya kiuchumi katika eneo hilo, na wakati huo huo inamshinikiza ili akate msaada wowote kwa vibaraka wa Waingereza ndani ya chama cha PKK ambao wamejichimbia katika mlima wa Qandil kaskazini mwa Iraq na kufanya operesheni za kijeshi dhidi ya Uturuki. Ndege za Uturuki zinawashambulia katika eneo hilo bila ya Barzani kupinga kwa sababu sasa anaihitaji Uturuki, nayo inampokea kama Rais wa nchi na imeanzisha ubalozi mdogo wa Uturuki katika eneo hilo na inanunua mafuta kutoka kwake.
Hivyo, hizi nchi mbili zinaonekana kuwa na migongano lakini zinafanya kazi kwa kupatana na sera ya Marekani.
Mfano wa hali ya pili:
- Mvutano uliotokea hivi karibuni kati ya Saudi Arabia na Iran kutokana na kuuawa kwa Nimr. Nimr alikuwa amehukumiwa kifo zaidi ya mwaka mmoja uliopita tarehe 16/10/2014 wakati wa enzi ya Mfalme aliyepita Abdullah aliyekuwa anawaunga mkono Waingereza, naye alikufa kabla ya kutekelezwa kwa hukumu ya kifo... Sheikh huyu alikuwa anatoa wito wa kujitenga kwa Qatif na Al-Ahsa na kuzirudisha Bahrain ili kuunda jimbo moja huru, na inajulikana kuwa Iran inadai kuwa Bahrain ni sehemu yake na inaichukulia kama mkoa wake wa kumi na nne. Kutotekelezwa kwa hukumu ya kifo dhidi yake kungeweza kusababisha aibu ya ndani kwa Mfalme wa sasa Salman anayewaunga mkono Wamarekani. Kwa hiyo, ilitangazwa kunyongwa kwa watu wengine 46 bila yeye, na miongoni mwao watu 43 ambao utawala uliwachukulia kuwa ni matakfiri, makhawariji na wanachama wa mashirika ya kigaidi.
Hii ni kwa upande wa Saudi Arabia. Ama kwa upande wa Iran, hali yake ya kimadhehebu na kikaumu inailazimu kupinga sheikh kama huyo kwa sababu ya hali ya ndani iliyojaa chuki za kimadhehebu...
Lakini mvutano huu hauathiri utekelezaji wa pande zote mbili kwa mipango ya Marekani. Marekani imechukua hatua ya kuondoa mvutano huo, ambapo msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, John Kirby, alisema: "Tunaamini kwamba mazungumzo ya kidiplomasia na mazungumzo ya moja kwa moja yanabaki kuwa zana muhimu za kutatua tofauti na tutaendelea kuwahimiza viongozi wa eneo hilo kuchukua hatua chanya ili kutuliza mivutano." (Al-Quds Al-Arabi 04/01/2016). John Kerry, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, aliwasiliana na mwenzake wa Iran Javad Zarif na kusoma naye hali hii, na kufuatia hayo Kerry alitangaza akisema: "Tunataka kupunguza mvutano na kuanza mazungumzo kati yao ili kufikia suluhu ya amani na kidiplomasia kati yao" (CNN 04/01/2016)... Kisha Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudi Arabia, Adel al-Jubeir, aliliambia shirika la Reuters mnamo 04/01/2016 kuwa "Tehran lazima ifanye kazi kama nchi ya kawaida ili kurejesha mahusiano ya kidiplomasia yaliyokatika," na Abdullah Al-Mouallimi, mwakilishi wa Saudi Arabia katika Umoja wa Mataifa, alisema: "Mgogoro na Iran hautakuwa na athari kwa juhudi za amani nchini Syria na Yemen. Tutashiriki katika mazungumzo yajayo kuhusu Syria yaliyopangwa kuanza Januari 25 mjini Geneva chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa"... Na mwakilishi wa kimataifa wa Syria, De Mistura, baada ya ziara yake Saudi Arabia na kukutana na Waziri wake wa Mambo ya Nje Al-Jubeir, alisema: "Saudi Arabia imethibitisha kuwa mivutano na Iran haitazuia mazungumzo maalum ya mchakato wa kisiasa nchini Syria yaliyopangwa kufanyika Geneva mwezi huu" (Al-Jazeera 05/01/2016). Yaani mivutano hii kati ya nchi hizo mbili ni katika masuala ya ndani ambayo hayaathiri mwenendo wa nchi hizo mbili kutekeleza mradi wa Marekani unaohusiana na kumaliza mapinduzi ya Syria, kuharibu mradi wake wa Kiislamu na kulinda mfumo wa kisekula wa kijasusi nchini Syria...
Hivyo basi, sababu za ndani zinaweza kuibua tofauti za muda mfupi hadi kutoweka kwa sababu hizo au kutulia kwake, lakini tofauti hizo zinakuwa ndani ya udhibiti na haziathiri maslahi ya Marekani.
Mfano wa hali ya tatu:
- Suala la Abadi kupinga kuwepo kwa majeshi ya Uturuki. Jambo hili lilikuja ili kuimarisha msimamo wake na msimamo wa serikali yake ambayo imani kwayo na kwake ilikuwa imeshuka hadi chini kabisa. Marekani ilitaka kusafisha picha ya kibaraka wake Abadi na serikali yake kwa kuibua mada hii ili kumuunga mkono kisaikolojia kwa kumwonesha kama mlinzi wa nchi! Uturuki ilimjibu kuwa iliingia kwa ombi lake mwaka mmoja uliopita ili kuwafundisha askari wake, na pamoja na hayo Uturuki ilikubaliana naye na ikafanya operesheni ya kuondoa sehemu ya majeshi yake na kuyapanga upya. Kisha Jumuiya ya nchi za Kiarabu ikatoa taarifa inayounga mkono maombi ya serikali ya Abadi na kuitaka Uturuki iondoke. Inajulikana kuwa Jumuiya hii ya nchi za Kiarabu inaongozwa na Marekani. Hivyo jambo hilo liliisha bila ya kuwepo mgogoro!
Na kwa taarifa, Marekani haimuungi mkono Abadi kisaikolojia pekee, bali zaidi ya hapo, haitaki serikali ya Abadi ianguke katika mazingira haya, hasa baada ya Abadi kuonekana kutetereka baada ya kuahidi kuikomboa Ramadi na kushindwa, akahitaji dozi ya msaada inayomhakikishia msaada wa Marekani. Hivyo, Marekani ilifanya mashambulizi ya anga mfululizo huko Ramadi yaliyofikia mashambulizi 630 kama ilivyotangazwa na Ikulu ya Marekani mnamo tarehe 30/12/2015, na kufuatia hayo ikatangazwa jeshi la Iraq kudhibiti majengo ya serikali huko Ramadi.
Muhtasari ni kwamba ni vigumu kutokea mgogoro kwa maana ya vita kati ya nchi tegemezi au zile zinazozunguka kwenye mhimili ikiwa dola kubwa inayofuatwa ni hiyo hiyo moja. Isipokuwa tu inaweza kutokea tofauti inayodhibitiwa kwa ajili ya kugawa majukumu, au kwa sababu za ndani, au kumuunga mkono mmoja wa vibaraka; na katika hali zote bila ya kudhuru maslahi ya dola kubwa inayofuatwa.