Home About Articles Ask the Sheikh
Maswali na Majibu

JIBU LA SWALI: MASHARTI YA KUOMBA NUSRA HAYAKUPATIKANA NDANI YA MAQURAISHI KABLA YA USHINDI WA MAKKA

September 13, 2021
2950

Mfululizo wa Majibu ya Mwanachuoni Mtukufu Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah, Amir wa Hizb ut Tahrir, kwa Maswali ya Wageni wa Ukurasa Wake wa Facebook "Fiqhi"

Kwa: Ghaith Ghaith

Swali:

Assalamu Alaikum Wa Rahmatullahi Wa Barakatuh,

Sheikh wetu, nina swali kama utaruhusu. Inafahamika kuwa Mtume ﷺ aliomba nusra (msaada wa mamlaka) kutoka kwa makabila, lakini je, Maquraishi walikuwa miongoni mwa makabila ambayo Mtume ﷺ aliomba nusra kutoka kwao?

Jazakumullah Khairan.

Jibu:

Wa Alaikum Salam Wa Rahmatullahi Wa Barakatuh,

Kuomba nusra (Talab an-Nusrah) hufanywa kwa yule anayeitikia Uislamu na kusilimu... na lazima awe miongoni mwa watu wenye nguvu na ulinzi (As-hab al-Quwwah wal-Man’ah) kiasi kwamba anaweza kuunusuru Uislamu na kusimamisha hukmu kwa yale aliyoteremsha Allah... Masharti haya mawili ni lazima yapatikane kwa yule anayeombwa nusra... Ikiwa hataitikia Uislamu na kusilimu, au ikiwa si miongoni mwa watu wenye nguvu na ulinzi wenye uwezo wa kuleta mabadiliko — awe peke yake na kabila lake au pamoja na wengine — basi hawi miongoni mwa watu wa nusra (Ahl an-Nusrah).

Maquraishi hawakuwa na sifa hizo kabla ya ushindi wa Makka (Al-Fat-h); watu wenye nguvu na ulinzi miongoni mwao ambao walikuwa na uwezo wa kuleta mabadiliko hawakusilimu wakati huo. Hivyo basi, Mtume ﷺ hakuomba nusra kutoka kwao. Badala yake, alikuwa akilingania Uislamu kule Makka, ambapo waliosilimu walikuwa ni watu dhaifu na baadhi ya watu wenye nguvu mmoja mmoja bila makabila yao, hivyo hawakuwa na uwezo wa kuleta mabadiliko, kama vile Umar na Hamza... Kwa sababu hiyo, hakukuwa na kuomba nusra kutoka kwa watu wa Makka kutokana na kutopatikana kwa masharti hayo mawili. Badala yake, kule Makka kulikuwa na da’wah ya kuingia katika Uislamu, na hapakuwa na kuitikia Uislamu kutoka kwa watu wenye nguvu na ulinzi waliokuwa na uwezo wa kuleta mabadiliko. Kwa hivyo, hakukuwa na kuomba nusra Makka, bali ilifunguliwa kwa ushindi (Fat-han).

Ndiyo maana Mtume ﷺ alikuwa akijitokeza kwa makabila yenye nguvu na ulinzi, akiwalingania katika Uislamu kwanza, kisha akiomba nusra yao ikiwa watasilimu. Na hapa kuna baadhi ya yale yaliyokuja kuhusu hilo katika Sira:

Kwanza: Kutoka Sira ya Ibn Hisham:

1- Kuomba nusra kutoka kwa Thaqif:

[Ibn Ishaq amesema: Abu Talib alipofariki, Maquraishi walimfanyia Mtume wa Allah ﷺ maudhi ambayo hawakuwahi kuyafanya wakati wa uhai wa ami yake Abu Talib. Hivyo, Mtume wa Allah ﷺ alitoka kwenda Taif akitafuta nusra kutoka kwa Thaqif na ulinzi kupitia kwao dhidi ya watu wake (Maquraishi), na kwa matumaini kuwa wangekubali yale aliyowaletea kutoka kwa Allah Aliyebarikiwa na kutukuka. Alitoka kwao akiwa peke yake.

Ibn Ishaq amesema: Yazid bin Ziyad alinihadithia kutoka kwa Muhammad bin Ka’b al-Quradhi, akisema: Mtume wa Allah ﷺ alipofika Taif, aliwaelekea watu fulani wa Thaqif, ambao wakati huo walikuwa viongozi na waheshimiwa wa Thaqif. Walikuwa ndugu watatu: Abd Yalil bin Amr bin Umair, Mas’ud bin Amr bin Umair, na Habib bin Amr bin Umair... Na kwa mmoja wao kulikuwa na mwanamke wa Kiquraishi kutoka Bani Jumah. Mtume wa Allah ﷺ aliketi nao na kuwalingania kwa Allah, akazungumza nao kuhusu lengo la kuwajia la kumuunga mkono katika Uislamu na kusimama naye dhidi ya wale waliompinga miongoni mwa watu wake. Mmoja wao akamwambia: "Yeye anapasua mavazi ya Al-Kaaba ikiwa Allah amekutuma wewe!" Mwingine akasema: "Je, Allah hakupata mwingine wa kumtuma isipokuwa wewe?" Na wa tatu akasema: "Wallahi, sitazungumza nawe abadan! Ikiwa wewe ni Mjumbe wa Allah kama unavyosema, basi wewe una hatari kubwa mno kiasi cha mimi kukujibu. Na ikiwa unamzulia Allah uongo, basi haunipasi mimi kuzungumza nawe." Mtume wa Allah ﷺ akasimama kutoka kwao akiwa amekata tamaa na kheri ya Thaqif...]

2- Mtume kujitokeza kwa Bani Amir:

[Ibn Ishaq amesema: Al-Zuhri alinihadithia kuwa yeye (Mtume) aliwaendea Bani Amir bin Sa’sa’ah, akawalingania kwa Allah Aliyetukuka na akajitambulisha kwao. Mtu mmoja miongoni mwao — anayeitwa Bayhara bin Firas — akasema: "Wallahi, lau ningemchukua kijana huyu kutoka kwa Maquraishi, ningewala Waarabu kupitia kwake." Kisha akasema: "Je, unaonaje, ikiwa tutakupa baia (kiapo cha utii) juu ya jambo lako hili, kisha Allah akakuwezesha kuwashinda waliokupinga, je, mamlaka yatakuwa yetu baada yako?" Akasema: "Mamlaka ni ya Allah, huyaweka pale anapotaka." Yule mtu akamwambia: "Je, tuyatoe koo zetu (tupigane) kwa Waarabu kwa ajili yako, kisha Allah akikupa ushindi mamlaka yaende kwa wengine? Hatuna haja na jambo lako." Basi wakakataa kumuunga mkono...]

Pili: Kutoka kitabu cha al-Bidayah wa an-Nihayah cha Ibn Kathir ad-Dimashqi:

[Amesema: Kisha tuliishia kwenye baraza lenye utulivu na heshima, na kukawa na masheikh wenye hadhi na haiba. Abu Bakr akatangulia na kutoa salamu — Ali amesema: Abu Bakr alikuwa mstari wa mbele katika kila kheri — Abu Bakr akawauliza: "Watu hawa ni akina nani?" Wakasema: "Kutoka Bani Shayban bin Tha’labah."

Basi akageuka kwa Mtume wa Allah ﷺ na kusema: "Baba yangu na mama yangu wawe fidia kwako, hakuna utukufu zaidi katika watu wao baada ya hawa."

Na katika riwaya nyingine: "Hawa ndio viongozi wa watu wao, na hawa ndio watu bora kabisa."

Na katika watu hao walikuwemo Mafruq bin Amr, Hani bin Qabisah, Al-Muthanna bin Harithah, na Al-Nu’man bin Sharik. Na aliyekuwa karibu zaidi na Abu Bakr alikuwa Mafruq bin Amr. Mafruq bin Amr alikuwa amewashinda kwa ufasaha na usemi...

Abu Bakr akamuuliza: "Idadi yenu ikoje?" Akamwambia: "Sisi tunazidi elfu moja, na elfu moja haishindwi kwa uchache." Akamuuliza: "Vipi kuhusu ulinzi (uwezo wenu wa kujilinda)?"

Akasema: "Jitihada ni juu yetu na kila watu wana juhudi zao." Abu Bakr akauliza: "Vipi kuhusu vita kati yenu na adui yenu?" Mafruq akasema: "Sisi tunakuwa wakali zaidi wakati tunapokasirika, na tunapendelea farasi bora kuliko watoto, na silaha kuliko ngamia, na ushindi unatoka kwa Allah; hutupa ushindi mara moja na mara nyingine hutushinda. Labda wewe ni ndugu wa Kikuraishi?" Abu Bakr akasema: "Ikiwa imewafikia habari kuwa yeye ni Mjumbe wa Allah, basi huyu hapa..."

Mafruq akasema: "Imetufikia kuwa anataja hilo. Basi unalingania nini ewe ndugu wa Kikuraishi?" Kisha akamgeukia Mtume wa Allah ﷺ, naye (Mtume) akaketi na Abu Bakr akasimama akimfunika kwa vazi lake, akasema ﷺ:

أَدْعُوكُمْ إِلَى شَهَادَةِ أَنْ لَا إِلَهَ إِلَّا اللَّهُ وَحْدَهُ لَا شَرِيكَ لَهُ، وَأَنِّي رَسُولُ اللَّهِ، وَأَنْ تؤوونى وَتَنْصُرُونِي حَتَّى أُؤَدِّيَ عَنِ اللَّهِ الَّذِي أَمَرَنِي بِهِ، فَإِنَّ قُرَيْشًا قَدْ تَظَاهَرَتْ عَلَى أَمْرِ اللَّهِ، وَكَذَّبَتْ رَسُولَهُ، وَاسْتَغْنَتْ بِالْبَاطِلِ عَنِ الْحَقِّ، وَاللَّهُ هُوَ الْغَنِيُّ الْحَمِيدُ

"Ninakualikeni kwenye shahada ya kwamba hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Allah peke yake, hana mshirika, na mimi ni Mjumbe wa Allah, na kwamba mnipokee na mninusuru mpaka nifikishe kutoka kwa Allah yale aliyoniamrisha, kwani hakika Maquraishi wamepingana na amri ya Allah, na wakamkadhibisha Mjumbe Wake, na wakajitosheleza kwa batili badala ya haki, na Allah ni Mkwasi, Msifiwa."

Akasema: "Na huyu hapa Muthanna, ni sheikh wetu na kiongozi wetu wa vita." Muthanna akasema: "Nimesikia maneno yako na nimeyapenda ewe ndugu wa Kikuraishi, na nimevutiwa na yale uliyoyasema. Jibu ni kama alivyojibu Hani bin Qabisah; na kuacha dini yetu na kukufuata wewe kwa ajili ya kikao kimoja tu ulichoketi nasi... na sisi tumepiga kambi kati ya mipaka miwili, mmoja ni Yamamah na mwingine ni Samawah."

Mtume wa Allah ﷺ akamuuliza:

وَمَا هَذَانِ الصَّرَيَانِ؟

"Ni ipi mipaka hii miwili?"

Akamwambia: "Mmoja ni upande wa jangwa na ardhi ya Waarabu, na mwingine ni ardhi ya Uajemi na mito ya Kisra. Na sisi tumeweka ahadi na Kisra kuwa tusianzishe jambo jipya wala tusimpe hifadhi yeyote anayeanzisha jambo jipya. Na huenda jambo hili unaloitisha likawa ni miongoni mwa mambo ambayo wafalme wanayachukia. Ama kwa yale yanayopakana na nchi za Waarabu, basi kosa la mwenye nalo husamehewa na udhuru wake hukubaliwa. Lakini kwa yale yanayopakana na nchi za Uajemi, kosa la mwenye nalo halisamehewi na udhuru wake haukubaliwi. Ikiwa unataka tukunusuru na kukulinda kwa yale yanayopakana na Waarabu, tutafanya hivyo."

Mtume wa Allah ﷺ akasema:

مَا أَسَأْتُمُ الرَّدَّ إِذْ أَفْصَحْتُمْ بِالصِّدْقِ، إِنَّهُ لَا يَقُومُ بِدِينِ اللَّهِ إِلَّا مَنْ حَاطَهُ مِنْ جَمِيعِ جَوَانِبِهِ

"Hamkukosea katika jibu lenu mlipoeleza ukweli waziwazi. Hakika hawezi kuisimamisha dini ya Allah isipokuwa yule anayeizingira (anayeitekeleza) kwa pande zake zote."]

Kisha ikafuata Baia ya kwanza na ya pili ya Aqaba, kisha Hijra na kusimamishwa kwa serikali... Mukhtasari ni kwamba watu wenye nguvu na ulinzi kule Makka hawakuwa na sifa hizo katika miaka ya kwanza ya Mtume ﷺ kule Makka; hawakuwa wameingia katika Uislamu wala kuwa na utayari wa kumnusuru Mtume wa Allah ﷺ. Kwa hivyo, Mtume wa Allah ﷺ hakuomba nusra yao kwa ajili ya kusimamisha serikali kule Makka kwa njia ya nusra, bali aliiomba kwa wale waliokuwa na sifa hizo kwa kuitikia Uislamu na kuwa ni miongoni mwa watu wenye nguvu na ulinzi wenye uwezo wa kuleta mabadiliko... Hivyo Maansari walipata heshima hii kubwa duniani na Akhera na huo ndio ushindi mkuu. Na baada ya hapo, serikali ya Kiislamu ikafungua Makka kwa ushindi...

Natumai hili linatosheleza, na Allah ni Mjuzi zaidi na Mwenye Hikma zaidi.

Ndugu yenu, Ata bin Khalil Abu Al-Rashtah

06 Safar 1443 Hijria Inayoambatana na 13/09/2021 Miladia

Kiungo cha jibu kutoka ukurasa wa Amir (Allah amhifadhi) kwenye Facebook

Kiungo cha jibu kutoka ukurasa wa Amir (Allah amhifadhi) kwenye Wovuti

Share Article

Share this article with your network