Swali: Rais wa Amerika amesema (kwamba utiaji saini wa awamu ya kwanza ya makubaliano ya biashara na China unaweza kufanyika "muda mfupi baada ya" Januari 15, tarehe ambayo ilitangazwa mwezi uliopita kuwa ndiyo siku ya kutia saini. Trump aliongeza: Natamani kukamilisha makubaliano ya awamu ya pili na China baada ya uchaguzi wa rais kama sehemu ya juhudi za kumaliza vita vya kibiashara vinavyoendelea kati ya chumi mbili kubwa zaidi duniani kwa miezi kadhaa sasa, ambavyo vimesababisha msukosuko sokoni na kuathiri ukuaji wa uchumi wa kimataifa... Al-Ain Portal, 10/01/2020). Wizara ya Biashara ya China ilikuwa imethibitisha rasmi (kwamba Naibu Waziri Mkuu Liu He ataenda Washington kutia saini awamu ya kwanza ya makubaliano ya biashara. Hii inachukuliwa kuwa taarifa ya kwanza rasmi ya uthibitisho iliyotolewa na China kuhusu utiaji saini huo, ambapo awali Trump alisema kuwa ataenda Beijing baada ya utiaji saini wa makubaliano hayo kuanza mazungumzo ya awamu ya pili... Trade Captain, 10/01/2020). Je, hii inamaanisha kuwa mvutano wa kibiashara kati ya Amerika na China umekwisha?
Jibu: Ili kujibu maswali haya na kuelewa asili ya vita vya kibiashara kati ya Amerika na China, tunapitia mambo yafuatayo:
Kwanza: Historia ya suala hili:
1- Mfuatiliaji wa sera za Amerika kuelekea China anaona kuwa Amerika daima inatafuta kuwa juu katika Eurasia (Ulaya na Asia), na hairuhusu China kuipita. Hii ni kwa sababu Eurasia ni eneo muhimu ambapo Marekani imeweka sera thabiti ya kigeni ili kuhakikisha utawala wake, ambao unaendelea kutumikia maslahi ya taasisi za Amerika hadi leo... Tangu kusambaratika kwa Umoja wa Kisovieti mwaka 1991, tabaka la kisiasa nchini Amerika limegawanyika katika sehemu kuu mbili kuhusu muundo wa sera ya Amerika kuelekea China:
Kwanza: Inahusu kuishirikisha China au kushirikiana nayo ili iwe mdau na mhusika mwenye dhamana katika mfumo wa kimataifa unaoongozwa na Amerika.
Pili: Inasisitiza kuwa nia ya China haiwezi kuaminiwa, na kwamba mwishowe ni nguvu pinzani inayopinga mfumo wa kimataifa wa Magharibi unaoongozwa na Amerika.
Katikati ya miaka ya tisini, taasisi ya sera za kigeni ya Amerika iliamua kuainisha China kama nguvu inayochuana nayo na sera zikapitishwa ili kudhibiti kuinuka kwa China. Wakati wa utawala wa kisiasa wa Clinton na Obama, sera ya kudhibiti (containment) ilichukuliwa kuelekea sera ya China, na wakati wa tawala za Republican za Bush Mdogo na Trump, sera ya kishari zaidi ilichukuliwa katika kuidhibiti China. Trump alihamasisha vita vya kibiashara vya wazi dhidi ya China. (Financial Times)
2- Sera ya kudhibiti ya Amerika ilikuwa na malengo makuu mawili: Kwanza, kuepuka kujitokeza kwa China kama nguvu ya kikanda, na pili, kuizuia kubadilisha kipengele chochote cha mfumo wa kimataifa unaoegemea Magharibi. Ili kufikia malengo haya, Marekani ilichukua hatua kadhaa, ikiwa ni pamoja na [kuibua ukiukaji wa China wa haki za binadamu huko Tibet, Turkistan Mashariki na Hong Kong... kuifanya China iendelee kushughulishwa na mgogoro wa nyuklia wa Korea Kaskazini na migogoro ya kikanda katika Bahari ya China Kusini... kuitumia India, Japan na Australia kuzuia matamanio ya kijeshi ya China na ukuaji wake katika eneo la Asia-Pasifiki... kuzuia China kupata teknolojia za kisasa... na kurudisha nyuma mpango wa China wa Belt and Road Initiative]. Taasisi ya kisiasa ya Amerika imefungamana na sera ya kudhibiti huku kukiwa na mabadiliko kidogo katika baadhi ya hatua za kuzuia matamanio ya nguvu nchini China. Hata hivyo, baada ya mgogoro wa kifedha wa kimataifa mwaka 2008, na vita vya maafa vya Amerika nchini Afghanistan na Iraq, Marekani iligundua kuwa sera ya kuidhibiti China haikutosha na ikaamua kuiimarisha. Lengo la mkakati wa Obama katika kile kinachojulikana kama (mkakati wa Asia) lilikuwa kuhamisha zana za kijeshi na askari kutoka Ulaya kwenda Asia-Pasifiki, na kukabiliana na uwezo wa kijeshi wa China. Kisha Trump alianza kuilenga sekta ya uchumi wa China moja kwa moja, na utawala wake uliitaja China kuwa "inachezea sarafu" na kuanzisha vita vya kibiashara na Beijing, na jambo hili lilichukua kipaumbele kuliko juhudi za kuidhibiti China ndani ya mfumo unaozingatia sheria za kimataifa. (BBC).
Pili: Vita vya kibiashara kati ya Amerika na China:
1- Kama tulivyotaja hapo awali, Amerika ilianzisha vita vya kibiashara na China ili kuzuia kuinuka kwa China. Vita hivi kati ya mataifa hayo mawili makubwa kiuchumi viliongezeka kasi kutokana na usawa mbaya katika biashara, ambapo Amerika inaingiza bidhaa na huduma zenye thamani ya dola bilioni 558 kutoka China, na kwa upande mwingine, China inaingiza bidhaa na huduma zenye thamani ya dola bilioni 179 kutoka Marekani (Ofisi ya Mwakilishi wa Biashara wa Marekani). Lakini hivi karibuni pameonekana kukaribiana kati yao ili kila mmoja afikie maslahi yake kwanza!
2- Marekani na China zimefikia makubaliano ya sehemu ya biashara katika miezi ya hivi karibuni, (ambayo yataweka ukomo wa vita vya kibiashara vinavyozidi kuongezeka kati ya mataifa mawili yenye uchumi mkubwa duniani tangu mwaka jana. Trump alisema awali kuwa awamu ya kwanza ya makubaliano ya biashara itahusisha takriban 60% ya makubaliano ya jumla, na inatakiwa kuhusisha ahadi ya China kununua bidhaa zaidi za kilimo za Amerika, mkabala wa Marekani kupunguza ushuru wake uliowekwa kwenye bidhaa za China... Al-Araby Al-Jadeed, 05/01/2020). Al-Arabiya Net ilikuwa imechapisha mnamo 15/12/2019 yafuatayo: (Baada ya miezi 21 tangu kuanza kwa vita vya kibiashara kati ya chumi mbili kubwa zaidi duniani, Marekani imefikia makubaliano ya awamu ya kwanza na China lakini hayatatiwa saini kabla ya Januari ijayo. Chini ya makubaliano hayo, Marekani ilithibitisha kuwa itapunguza ushuru kwa asilimia 15 hadi nusu kwenye bidhaa za China zenye thamani ya dola bilioni 120, lakini itabakisha ushuru wa 25% kwenye bidhaa za China zenye thamani ya dola bilioni 250. Pia Marekani iliahirisha utekelezaji wa ushuru mpya wa asilimia 15 kwenye bidhaa za China zenye thamani ya dola bilioni 160 ambazo zilipaswa kuanza kutekelezwa leo, zikijumuisha vichezeo na simu janja... Aidha Beijing ilikubali kuagiza bidhaa na huduma za ziada za Amerika zenye thamani ya angalau dola bilioni 200 katika kipindi cha miaka miwili ijayo. Vilevile China itasitisha utekelezaji wa ushuru wa ziada kwa baadhi ya bidhaa zinazoingizwa kutoka Amerika ambazo zilipaswa kuanza leo, ambapo itasitisha utozaji wa ushuru wa ziada wa 25% kwenye magari na 5% kwenye vipuri vya Amerika. China ilifafanua kuwa itaendelea kusitisha ushuru kwa takriban dola bilioni 126 za bidhaa za Amerika, mbali na ahadi yake ya kuongeza ununuzi wa bidhaa za kilimo kutoka Marekani kufikia dola bilioni 50 kwa mwaka). Trump alikuwa na hamu ya kutengeneza soko linalokua la mauzo ya nje ya kilimo kwa sababu anashiriki katika uchaguzi mkuu mwaka huu wa 2020 na hataki kupoteza kura za wakulima waliolemewa na madeni kwa kukosa masoko ya kutosha ya kuuza bidhaa zao... Kabla ya hapo, tovuti ya Al-Bayan News ilichapisha (na Wizara ya Biashara ya China ilisema - katika taarifa yake Ijumaa jioni - kwamba makubaliano hayo yalikuja kulingana na kanuni ya usawa na kuheshimiana, na yanajumuisha sura tisa: utangulizi, haki miliki ya kiakili, uhamishaji wa teknolojia, bidhaa za chakula na kilimo, huduma za kifedha, kiwango cha ubadilishaji na uwazi, upanuzi wa biashara, tathmini ya pande mbili na utatuzi wa migogoro, na vifungu vya mwisho... Al-Bayan News, 13/12/2019).
3- Lakini hii haina maana kwamba makubaliano haya kuhusu vita vya kibiashara yatashatisha hali ya mvutano wa kiuchumi kati ya pande hizo mbili. Hii ni kwa sababu vita vya kibiashara siyo kichocheo halisi cha kudhibiti China, bali kuna jambo nyuma yake ambalo ni la ndani zaidi na hatari zaidi kwa uchumi wa Amerika na kipaumbele chake cha kimataifa. China ndiyo nchi inayoongoza katika teknolojia ya 5G, ambayo ni kizazi kijacho cha mawasiliano ya wireless, na muhimu zaidi ni mlango wa udhibiti wa Akili Bandia (Artificial Intelligence). Baraza la Ulinzi la Ubunifu, na aliyekuwa mwenyekiti wa Alphabet (Eric Schmidt), mwanzilishi wa LinkedIn (Reid Hoffman), na Walter Isaacson, mwandishi na aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Aspen, waliandika: "Inatarajiwa kwamba anayedhibiti 5G atapata mamia ya mabilioni ya dola katika mapato katika muongo ujao, huku akitengeneza fursa nyingi za kazi katika sekta ya teknolojia ya wireless. Nchi itakayomiliki 5G itapata uvumbuzi mwingi na itaweza kuweka viwango kwa ulimwengu mzima, na kwa sasa haiwezekani kwamba nchi hiyo itakuwa Amerika"... (Tovuti ya ZDNet).
4- Kwa taarifa, teknolojia ya 5G ina kasi ya ajabu, (watafiti walitangaza kuwa majaribio ya kasi ya muunganisho kupitia teknolojia ya 5G yalifikia kasi ya rekodi ya terabyte kwa sekunde, ikijulikana kuwa kasi hii ni kubwa mara 200 kuliko kasi ya sasa. Kulingana na majaribio yaliyofanywa na timu ya utafiti kutoka kituo cha maendeleo cha mitandao ya 5G katika Chuo Kikuu cha Surrey nchini Uingereza, faili yenye ukubwa wa mara 100 ya faili za filamu ndefu inaweza kupakuliwa kwa takriban sekunde 3 pekee. Pia, kasi hiyo mpya ni kubwa mara 65,000 kuliko wastani wa kasi ya kupakua katika mitandao ya 4G. Inatarajiwa kwamba idadi ya vifaa vilivyounganishwa kwenye intaneti itakuwa kati ya vifaa bilioni 50 hadi 100 mwaka huu, kwa hivyo ni lazima kuwe na mitandao yenye masafa mapya na tofauti ili kutosheleza hitaji hili kubwa la muunganisho wa intaneti. Kuhusu jinsi 5G inavyofanya kazi kiufundi, kuna teknolojia inayojulikana kwa kifupi kama MIMO, yaani "milio mingi na matokeo mengi", ambayo itachukua nafasi kuu katika kuendesha mitandao ya 5G na viwango vyake vya ufanisi. Teknolojia ya MIMO inatumia antena nyingi ndogo kuhudumia mtiririko wa data mbalimbali, na Samsung imetegemea teknolojia hii kutoa kasi ya kushangaza ya kupakua data, na kuna uwezekano kuwa mitandao ya 5G itatumia idadi kubwa zaidi ya vituo vya kurushia matangazo... Al-Arab, 13/08/2017).
5- Mnamo mwaka 2017, Schmidt alifichua katika Jukwaa la Kiuchumi la Dunia (WEF) kwamba "haitachukua muda mrefu kabla ya China kuipita Marekani katika kukuza Akili Bandia ya juu (AI)" (Jukwaa la Kiuchumi la Dunia). Akili Bandia inajidhihirisha katika:
Matumizi ya roboti za mazungumzo (chatbots) zinazotumia akili bandia kuelewa matatizo ya wateja kwa haraka na kutoa majibu yenye ufanisi zaidi.
Matumizi ya wasimamizi wa akili bandia kuchambua taarifa muhimu kutoka kwa kundi kubwa la data za maandishi ili kuboresha upangaji ratiba.
Wataalamu wanaashiria nia kubwa na uwekezaji katika nyanja ya Akili Bandia katika kipindi cha miaka michache ijayo. Deloitte inakadiria kuwa dola bilioni 57.6 za Marekani zitatumika katika Akili Bandia na ujifunzaji wa mashine (machine learning) ifikapo mwaka 2021, ikiwa ni mara tano zaidi ya ilivyokuwa mwaka 2017.
6- Haikuwa jambo la kushangaza kwa Trump kuipinga waziwazi kampuni ya Huawei inayozalisha 5G, na ametoa kauli mara kadhaa kuhusu hatari inayowakilishwa na kampuni hiyo ya China. Trump alisema katika mkutano wa kilele wa hivi karibuni wa NATO: "Nadhani ni hatari ya kiusalama, ni hatari ya kiusalama" (Business Insider). Kwa sababu hii, Marekani ilizishinikiza nchi nyingi za Magharibi (Italia, Uingereza, Ujerumani n.k.) kuiondoa kampuni ya Huawei katika kutoa zabuni au kuwasha teknolojia ya 5G katika nchi zao, yote hayo kwa kisingizio cha uongo cha ukiukaji wa usalama. Marekani pia iliiomba Kanada kumkamata Meng Wanzhou, Mkurugenzi wa Fedha wa kampuni ya Huawei, kwa tuhuma za kukiuka vikwazo vya Marekani vilivyowekwa dhidi ya Iran. Amerika ina nia ya kupiga marufuku mtandao wa 5G wa China, kama vile Trump alivyopiga marufuku uuzaji wa vidonge vya silicon (silicon chips) kwenda China.
7- Wachina wamefanya kazi kwa muda mrefu ili waweze kujitegemea kiteknolojia chini ya mpango wa China 2025, lakini jinsi Wamarekani walivyoshughulika na kampuni ya Huawei na kampuni nyingine za China kuliharakisha juhudi za China kupata uhuru kamili katika teknolojia muhimu. Wachina wametangaza mipango ya kuunda mfumo wao wa uendeshaji (operating system), ifikapo mwaka 2022, jambo ambalo limefunga mlango kwa kampuni za IBM, Microsoft, Dell na kampuni nyingine za Amerika. Zaidi ya hayo, China inapanga kutengeneza vidonge vyake vya silicon. Imewalipa mishahara mara mbili maelfu ya wahandisi wa vidonge wa Taiwan na kuwahamishia China katika kipindi cha miaka michache iliyopita. Wachambuzi wa Amerika wanatarajia kuwa China itafikia uhuru katika tasnia ya vidonge ndani ya miaka mitano hadi saba. Kwa kufuata hatua hizi, Beijing itapata faida kubwa kutoka kwa uchumi mpya wa Akili Bandia.
8- Amerika inafanya kila iwezalo kuzuia uwezo wa China wa kuchukua uongozi katika mfumo wa 5G na Akili Bandia, kwa sababu teknolojia hii ni muhimu kama ilivyokuwa injini ya mvuke, umeme, na kidonge cha silicon. Teknolojia hizi ndizo injini za uzalishaji na ukuaji wa kiuchumi. Hivyo, vita vya sasa vya kibiashara ni zaidi ya vita tu vya kukabiliana na urari wa biashara kati ya Amerika na China; ni vita vya teknolojia, haswa 5G. Inatarajiwa, kulingana na data za sasa, kwamba ulimwengu utakuwa na mfumo wa kiteknolojia wa ncha mbili: Magharibi inayoongozwa na Amerika, na ulimwengu mwingine unaoongozwa na China. Ikiwa mfumo wa kiteknolojia wa China utatawala katika Eurasia, basi uwezekano wa China kutishia vipaumbele vya Amerika katika nyanja hii utaongezeka.
Kwa hivyo, makubaliano ya biashara kati ya Amerika na China, hata kama yatafikiwa na kisha kutiwa saini katika awamu zake zote baada ya mwaka mmoja kama alivyosema Trump: (kwamba utawala wake utaanza kujadili makubaliano ya awamu ya 2 kati ya Marekani na China hivi karibuni lakini unaweza kusubiri kukamilisha makubaliano yoyote baada ya uchaguzi wa rais wa Marekani mwezi Novemba ujao... Al-Ain Portal, 10/01/2020), hata kama yatatiwa saini katika awamu zake za mwisho, inatarajiwa kuwa hayatakuwa zaidi ya "mapumziko ya mpiganaji", hususan katika upande wa teknolojia ya 5G. Hii ni kwa sababu Amerika haikubali kuwa na mshindani kama China hata kama China itakubali, kwani kiburi na uonevu wa Amerika unaizuia kukubali hilo!
17 Jumada al-Ula 1441 H 12/01/2020 M