Home About Articles Ask the Sheikh
Siasa

Jibu la Swali: Shambulio la Ndege Zisizo na Rubani Juu ya Kremlin

May 09, 2023
70

Jibu la Swali

Shambulio la Ndege Zisizo na Rubani Juu ya Kremlin

Swali:

Wataalamu wa ndege zisizo na rubani (droni) nchini Marekani wameeleza kuwa (droni mbili zilizopata ajali juu ya Kremlin Jumatano iliyopita, zilifanikiwa kukwepa mifumo mingi ya ulinzi ndani na nje ya Moscow, jambo linaloashiria uwezekano wa kurushwa kutokea ndani ya Urusi. Al Jazeera, Reuters 6/5/2023). Shambulio hilo la droni dhidi ya Ikulu ya Kremlin katikati mwa Moscow lilifanyika usiku wa tarehe 3/5/2023. Katibu wa Kamati ya Masuala ya Nje katika Bunge la Ukraine amesema kuwa (shambulio dhidi ya Kremlin lilipangwa na Moscow... Al Jazeera 3/5/2023). Swali ni: Je, shambulio hili limepangwa na upande wa nje "Ukraine" kama Urusi inavyoituhumu? Au ni mpango wa ndani "Moscow" kama walivyosema wataalamu wa Marekani na Ukraine? Kwa maneno mengine: Nani yuko nyuma ya shambulio hili baada ya matamshi haya yanayokinzana?

Jibu:

Ndiyo, utawala wa Urusi ulitangaza kuzuia shambulio la droni mbili dhidi ya Kremlin, ukilitaja kama "la kigaidi". Mara moja, Ukraine ilikanusha kuhusika na shambulio hilo, ikituhumu Moscow kuwa imelikuza makusudi katika vyombo vya habari ili kuhalalisha uwezekano wowote wa kuongeza ukali wa mapigano. Kremlin ilisema kuwa Rais wa Urusi Vladimir Putin hakudhurika... Ili kuelewa malengo ya shambulio hili, ni lazima kuzingatia yafuatayo:

Kwanza: Baada ya zaidi ya mwaka mmoja tangu kuanza kwa vita nchini Ukraine vilivyoanzishwa na Urusi mnamo Februari 2022, kumekuwa na hali ya kudorora katika nyanja za mapigano. Isipokuwa kwa mapigano yanayoendelea katika mji wa Bakhmut kwa muda wa miezi minane sasa na baadhi ya mashambulizi ya makombora ya Urusi ndani ya Ukraine, maeneo mengine ya mapigano yanashuhudia utulivu. Kudorora huku kuna sababu mbili; ya kwanza ni ya kimaumbile kutokana na msimu wa baridi, na ya pili ni upungufu wa zana za kijeshi kwa pande zote mbili. Huku kukiwa na mazungumzo ya mara kwa mara kuhusu shambulio tarajiwa la Ukraine, shambulio dhidi ya Kremlin linahitimisha hali ya kudorora kwa mapigano na kuna uwezekano mkubwa wa kuongezeka kwa ukali wa vita.

Pili: Magharibi, ikiongozwa na Marekani, kupitia msaada endelevu na wa hatua kwa hatua kwa Ukraine, imefanikiwa kuidhoofisha Urusi. Mkuu wa kundi la Wagner la Urusi, linalopigana hasa katika mji wa Bakhmut, analalamika kila mara kuhusu upungufu wa risasi na zana, akivishutumu baadhi ya vyombo ndani ya jeshi la Urusi kwa kufanya hivyo makusudi, hasa kwa kuwa maeneo mengine ya mapigano yalikuwa karibu kusimama wakati wa msimu wa baridi. Aidha, mashambulizi ya Urusi ndani ya Ukraine mara nyingi huchukua mfumo wa mawimbi, ikimaanisha kuwa Urusi inaweza kuwa haina makombora na droni za kutosha kufanya mashambulizi ya mfululizo. Inaonekana kana kwamba inakusanya kiasi inachozalisha kwa mwezi mmoja, kisha inakirusha ndani ya Ukraine. Huu ni udhihirisho mwingine wa hali ya kudhoofika kwa Urusi, achilia mbali upungufu wa vipuri muhimu katika sekta ya kijeshi ya Urusi kutokana na vikwazo vya Magharibi. Ingawa habari pia zinazungumzia kupungua kwa zana za kijeshi kwa upande wa Magharibi, ukweli ni kwamba viwanda vya kijeshi vya Magharibi vina uwezo mkubwa kuliko vya Urusi kuziba pengo hili.

Tatu: Matokeo yake, jeshi la Urusi, licha ya kampeni za kuandikisha askari wapya, linaonekana kupoteza uwezo wa mashambulizi ya nchi kavu hasa. Wanajenga mitaro kando ya mstari wa mbele kama ishara ya hofu yao dhidi ya shambulio la Ukraine linalotarajiwa kwa kutumia silaha za kisasa za Magharibi. Hata kiongozi wa kundi la Wagner amelitaja shambulio hilo tarajiwa la Ukraine kama "maafa kwa Urusi". Hali hii inapoambatana na kutokuwepo kwa nguvu za anga za Urusi — nguvu ambazo zimeshindwa kabisa kutawala anga ya Ukraine na kutosheka tu na mashambulizi ya mbali — udhaifu huu wa Urusi uko wazi kwa Magharibi na Marekani ambayo inaongoza vita vya Ukraine kutokea nyuma ya pazia. Kwa sababu hiyo, mipango ya vita sasa inachukua sura mpya dhidi ya Urusi ambayo haikutarajiwa wakati vita vilipoanza. Hasa kwa kuwa Marekani na Magharibi bado wanafanikiwa kuepuka tishio la vita vya nyuklia, kwani ishara zote za Urusi zilizofikia kiwango cha kutishia kutumia silaha za nyuklia zimekutana na ukosoaji mkubwa na hata kuitia hofu Urusi kuhusu hatua ya kukurupuka na majibu ya Marekani.

Nne: Katika mazingira haya yote, msimu huu wa joto unaonekana kuwa wa joto kali na usio na vizuizi vingi. Mojawapo ya vizuizi hivyo ni kwamba vita vilikuwa vikiendelea ndani ya Ukraine pekee. Lakini mashambulizi kadhaa yameshatokea ndani ya Urusi bila Ukraine kukiri kuhusika, bali kumevumbuliwa "upinzani wa Kirusi" unaopinga utawala wa Putin kana kwamba ndio unaohusika na mashambulizi dhidi ya Urusi. Shambulio hili dhidi ya Ikulu ya Kremlin katikati ya mji mkuu wa Moscow linajeruhi vibaya heshima ya Urusi. Urusi imelitaja shambulio hilo kama jaribio la kumuua Rais Putin. Popote pale droni hizo zilipotokea, kufika kwake juu ya majengo ya Kremlin na kulipuka moja kwa moja juu ya Kremlin kunaonyesha udhaifu wa Urusi.

Tano: Kutokana na mshtuko huko Moscow na Urusi kwa ujumla kufuatia ujasiri wa shambulio hilo, ambalo Urusi iliituhumu Ukraine kulitekeleza, matamshi makali yametolewa yanayoashiria kiwango cha mshtuko miongoni mwa maafisa wa Urusi:

1- Makamu wa Rais wa Baraza la Usalama la Urusi, Dmitry Medvedev, alitangaza: (Chaguo pekee lililosalia baada ya shambulio la utawala wa Kyiv dhidi ya Kremlin ni kumuangamiza Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky na washirika wake. Medvedev aliandika kupitia akaunti yake ya Telegram, Jumatano: "Baada ya shambulio la kigaidi la leo 'dhidi ya Kremlin', hakuna chaguo jingine lililosalia isipokuwa kumuondoa kimwili Zelensky na genge lake... Sputnik ya Urusi, 3/5/2023).

2- Spika wa Bunge la Urusi (Duma), Vyacheslav Volodin, alidai (kutumika kwa "silaha zenye uwezo wa kuzuia na kuangamiza utawala wa kigaidi wa Kyiv" kama jibu la shambulio la droni mbili dhidi ya Kremlin. Volodin aliongeza - katika taarifa kwenye programu ya Telegram - kwamba Urusi haipaswi kufanya mazungumzo na Rais wa Ukraine baada ya shambulio hilo "linalodaiwa" ambalo Kyiv imekanusha kuhusika nalo, akibainisha kuwa mazungumzo na utawala wa Zelensky "hayawezekani, kwani yanatishia usalama wa Urusi, Ulaya, na ulimwengu mzima". Al Jazeera Net, 3/5/2023).

Hivyo, inabainika ukubwa wa mshtuko uliotanda nchini Urusi kutokana na shambulio la droni mbili dhidi ya Kremlin.

Sita: Kuhusu uwezekano kuwa Urusi ndiyo iliyopanga shambulio hilo ili kuongeza ukali wa vita nchini Ukraine, jambo hili halina mashiko kwa upande mmoja kwa sababu ni jeraha kwa heshima yake na pigo kwa ukubwa wake, na ni ishara kwamba hakuna anayemuogopa tena wala kumuogopa Rais wake. Kwa upande mwingine, Urusi haina uwezo wa kuongeza ukali wa vita nchini Ukraine kwa njia madhubuti isipokuwa kwa silaha za nyuklia, na haina uthubutu wa kuzitumia ndani ya Ukraine kwa hofu ya majibu kutoka kwa Marekani. Kinachokanusha pia uwezekano wa Urusi kujishambulia yenyewe ni kwamba imetoa tuhuma za moja kwa moja dhidi ya Marekani kuhusika na shambulio hilo. Hili pia halijawahi kutokea na linaashiria ukubwa wa mshtuko huko Moscow kutokana na ujasiri wa shambulio hilo, na matamshi yanayohusiana na hilo yanabainisha hili:

1- Msemaji wa Kremlin, Dmitry Peskov, alitangaza (kuwa Marekani iko nyuma ya shambulio la Ukraine dhidi ya Kremlin kwa msaada wa droni, na ndiyo iliyochagua shabaha za Kyiv. Haya yalikuja katika mkutano na waandishi wa habari wa Peskov leo Alhamisi "4/5/2023", ambapo aliendelea kusema: "Majaribio kama haya ya kujitenga na hili huko Kyiv na Washington ni ya kipuuzi kabisa. Tunajua vyema kuwa maamuzi kuhusu vitendo kama hivi na mashambulizi ya kigaidi kama haya hayachukuliwi Kyiv, bali Washington. Kyiv inafanya kile inachoamriwa, na amri hiyo imeshatolewa". Marekani ilikanusha hili kupitia mratibu wa mawasiliano ya kimkakati katika Baraza la Usalama la Taifa katika Ikulu ya Marekani, John Kirby, akizungumza na kituo cha MSNBC, ambapo alisema: "Hatujui bado nini kilitokea, na hatujafanya tathmini yoyote. Nimeona tu maoni ya Dmitry Peskov asubuhi, na madai kuhusu kuhusika kwetu kwa namna fulani katika jambo hili.

Naweza kuwahakikishia kuwa hakukuwa na ushiriki wowote kutoka upande wa Marekani, na vyovyote itakavyokuwa, Marekani haikuhusika". RT, 4/5/2023).

2- Kwa sababu hiyo yote, inaweza kusemwa kuwa Marekani imeanza kuyapeleka vita vya Ukraine mbali zaidi na bila vizuizi dhidi ya Urusi kutokana na udhaifu na kudhoofika inakoshuhudia nchini Urusi. Bali shambulio dhidi ya Kremlin linawakilisha tishio la kibinafsi kwa Rais wa Urusi. Kutokana na matamshi ya Peskov, msemaji wa Kremlin, inaonekana Urusi imeelewa ujumbe huo, ndiyo maana ilitaka kuiambia Marekani kuwa inajua Marekani iko nyuma ya shambulio hilo, lakini yenyewe "Urusi" inajizuia kuitishia Marekani moja kwa moja kwa sababu ya hofu kubwa kwake, na inatosheka tu kuitishia Ukraine na kutishia kumuua rais wake, Zelensky.

3- Kinachoashiria pia kuwa shambulio hilo ni changamoto kwa Urusi iliyopangwa na Marekani, ni kumuondoa Rais wa Ukraine nje ya nchi. Alionekana ghafla asubuhi ya siku ya shambulio akiwa katika ziara huko Helsinki, Finland, kisha ndege yake ikaonekana ikitua Amsterdam, Uholanzi, na kufuatiwa na ratiba ya Kansela wa Ujerumani iliyoonyesha kumpokea Rais wa Ukraine Zelensky. Haya yote ni kwa ajili ya kumuepusha Rais wa Ukraine Zelensky na hasira za Urusi, yaani kuizuia Urusi kumuua kama alivyotaka Medvedev.

4- Kuhusu Marekani yenyewe, ilionekana kana kwamba haitaki kutoa maoni juu ya tukio hili, bali ilionyesha shaka juu ya simulizi ya Urusi. (Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Antony Blinken, alisema ameuona ripoti kutoka Moscow kuhusu shambulio linalodaiwa la droni kutoka Ukraine dhidi ya Kremlin, lakini "hawezi kuthibitisha ukweli wake kwa namna yoyote ile". Alisema: "Sisi hatujui tu". Blinken aliongeza: "Tutaona ukweli ni upi. Na ni vigumu sana kutoa maoni au kukisia jambo hili bila kujua ukweli". CNN Arabic, 3/5/2023).

5- Kinachoashiria mchango wa Marekani katika jaribio la kumuua Rais wa Urusi Putin ni nyaraka za Marekani zilizovuja katika miezi iliyopita na kufichuliwa mnamo Aprili 2023, ambazo zilizungumzia kifo cha Rais wa Urusi Putin kama mojawapo ya mazingira ya vita. (Inaonekana kuwa mchakato wa kuvuja kwa nyaraka za siri za Wizara ya Ulinzi ya Marekani "Pentagon" umebeba siri nyingi, ikiwa ni pamoja na kile kilichofichuliwa na gazeti la "New York Times" kuhusu hati ya siri ya kijasusi iliyoipata yenye maelezo ya mipango iliyowekwa kushughulikia dharura baada ya mwaka mmoja wa vita nchini Ukraine. Hati hiyo inajumuisha uchambuzi uliofanywa na Shirika la Kijasusi la Ulinzi la Marekani unaobainisha mazingira manne tarajiwa, na jinsi yanavyoweza kuathiri mkundo wa mzozo nchini Ukraine yakitokea. Mazingira hayo ni pamoja na: "Kifo cha Rais wa Urusi Vladimir Putin... na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky... na mabadiliko ya uongozi wa vikosi vya jeshi la Urusi... na mashambulizi ya Ukraine dhidi ya Kremlin". Gazeti la Al Sharq, 12/4/2023).

Saba: Kwa muhtasari, shambulio la droni mbili dhidi ya Ikulu ya Kremlin huko Moscow ni ongezeko kubwa la hatari katika vita vya Ukraine.

Linaashiria kuwa Marekani pamoja na Ukraine wanamiliki mawakala wa kutosha ndani ya Urusi kufanya mashambulizi makali yanayoweza kubadilisha mkundo wa vita. Milipuko imeshaanza na inashika kasi ndani ya Urusi ikilenga reli, vituo vya mafuta na umeme na vinginevyo. Yaani mchakato wa kuhamisha vita kutoka Ukraine kwenda ndani ya Urusi unaendelea sasa, tena kwa ujasiri mkubwa hasa kwa kuwa jeshi la Urusi limedhoofika kwa kiwango kikubwa nchini Ukraine na ni vigumu kwake kufanya mashambulizi madhubuti ya kubadilisha mkundo wa vita. Aidha, Magharibi ikiongozwa na Marekani inaendelea kuipa Ukraine silaha za kisasa zaidi ili kubadilisha mkundo wa vita kwa faida ya Ukraine. Ikumbukwe kuwa mkundo wa sasa wa vita si kwa faida ya Urusi baada ya Ukraine kukomboa mji wa Kherson na maeneo ya Kharkiv, pamoja na hasira ya hasara za Urusi katika shambulio lake linaloendelea kwa miezi minane katika mji wa Bakhmut bila kuutawala.

Hizi ndizo sura za shambulio hili dhidi ya Kremlin nchini Urusi, na huo ndio ulikuwa msingi wake. Haya yote yanaonyesha kutetereka kwa uwezo wa kijeshi na usalama wa Urusi kiasi kwamba imeshindwa kulinda kituo chake cha kisiasa katikati mwa Moscow! Ni kweli kwamba mapigano si kati ya Urusi na Ukraine pekee, bali Marekani na Magharibi zinaisaidia Ukraine kimali na kimaadili. Pamoja na hayo, kuendelea kwa shambulio la Urusi dhidi ya Ukraine kwa zaidi ya mwaka mmoja huku utulivu wa Urusi ukiwa umeretereka vibaya katika maeneo iliyoyakalia nchini Ukraine pamoja na hasara kubwa za mali na watu, yote hayo yanaonyesha kuwa Urusi inazidi kupoteza hadhi ya kuitwa dola kuu. Inaonekana Urusi inatambua hili, na ndio maana imefanya kila juhudi kurejesha heshima ya jina hili kwa kuuteka mji wote wa Bakhmut kabla ya sherehe za Urusi mnamo 9/5/2023, lakini imeshindwa hadi leo licha ya kuongeza mashambulizi na kukusanya kundi la Wagner.

Ama Marekani na Magharibi, zinapigana hadi askari wa mwisho wa Ukraine! Hazitaki kuingilia kati mapigano hayo, bali nchi hizo zinafikia maslahi yake kupitia damu za wengine.

Kwa kuhitimisha, narejea yale niliyoyataja hapo awali katika jibu la swali la tarehe 1/3/2023: [...Nchi hizi za kikafiri za kikoloni zinazoitwa kubwa katika ulimwengu wa leo zinapigana zenyewe kwa zenyewe si kwa ajili ya kheri ya ulimwengu bali kwa ajili ya shari na madhara. Urusi inaivamia Ukraine ili kumuua kila Mkraine anayejaribu kujitetea, na Marekani na Magharibi wanapigana dhidi ya uvamizi huo kwa kutumia kila Mkraine na si kwa askari wao! Pande zote mbili zinapigana nchini Ukraine ili kumuua kila Mkraine... Hivi ndivyo zilivyo nchi hizi zinazofanya ufisadi duniani, hazithamini wingi wa damu inayomwagika mradi tu zinafikia maslahi yake, bali hata sehemu ndogo ya maslahi yake... Ni kana kwamba historia inajirudia wakati dola za Uajemi na Roma zilipokuwa zikipigana, huyu anashinda na huyu anashindwa na kadhalika... Na kila mmoja wao anafanya kazi kama mashine ya kunyonya damu za watu ili kufikia maslahi yake mwenewe... Hali hiyo iliendelea hadi Mwenyezi Mungu alipowakirimu watu wa haki na uadilifu, Ummah wa Kiislamu, kwa ushindi na ufunguzi ulio wazi, Uislamu na Waislamu wakapata utukufu, na ukafiri na makafiri wakadhalilika. Na hili litatokea tena kwa idhini ya Mwenyezi Mungu:]

وَيَوْمَئِذٍ يَفْرَحُ الْمُؤْمِنُونَ * بِنَصْرِ اللَّهِ يَنْصُرُ مَنْ يَشَاءُ وَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ

"Na siku hiyo waumini watafurahi. Kwa nusura ya Mwenyezi Mungu. Yeye humnusuru amtakaye, Naye ni Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu." (QS Ar-Rum [30]: 4-5)

Na hilo litafikiwa kwa kusimamisha Khilafah ya Rashida.

وَيَقُولُونَ مَتَى هُوَ قُلْ عَسَى أَنْ يَكُونَ قَرِيباً

"Na husema: Lini hayo? Sema: Huenda yakawa karibu." (QS Al-Isra [17]: 51)

19 Shawwal 1444 H

09/05/2023 M

Share Article

Share this article with your network