Jibu la Swali
Maendeleo ya Kisiasa nchini Chad
Swali: Jeshi la Chad lilitangaza mnamo 20/04/2021 kuuawa kwa Rais wa Chad, Idriss Déby, katika mapigano na waasi kaskazini mwa nchi hiyo waliotokea kusini mwa Libya. Lilitangaza pia kuundwa kwa baraza la kijeshi litakaloongozwa na mtoto wa Rais aliyeuawa, mkuu wa walinzi wa rais, Mahamat Déby, kwa kipindi cha mpito cha miezi 18. Lilitangaza kuvunjwa kwa bunge na serikali, amri ya kutotoka nje usiku, na kufungwa kwa mipaka ya anga na nchi kavu, huku likivialika vikosi vyote vya upinzani kwenye mazungumzo. Ni nini hasa ukweli wa yaliyotokea na yanayoendelea nchini Chad, na hali inaelekea wapi? Ni nini mafungamano ya vikosi vya waasi? Na nini uhusiano wa haya yote na mzozo wa kimataifa?
Jibu: Ili jibu liwe wazi, tunapitia mambo yafuatayo:
Uchaguzi wa rais ulifanyika nchini Chad mnamo 11/04/2021, ambapo makundi ya upinzani uliususia huku wakimshutumu Rais Déby kwa udanganyifu, kukandamiza uhuru wa kusema, na kuwazuia viongozi wake kugombea. Mnamo 19/04/2021, ilitangazwa kuwa Rais Idriss Déby ameshinda kwa 79.32% ili kuiongoza nchi kwa miaka sita mingine, saa chache kabla ya kujeruhiwa katika mapigano na waasi. Mnamo 12/04/2021, kundi la Front for Change and Concord in Chad (FACT) lilitangaza kukataa uchaguzi huo na kuhamisha vikosi vyake vilivyokuwa kusini mwa Libya kuelekea mji mkuu wa Chad, N'Djamena. Kiongozi wa kundi hilo, Mahamat Mahdi Ali, alitangaza kuanza kwa harakati hiyo, na vikosi vyake vinakadiriwa kuwa na watu 1,500 walioingia kwa mamia ya magari ya four-wheel drive. Waliingia Chad kutokea mji wa Al-Jufra kusini mwa Libya kuelekea kaskazini mwa Chad mnamo 12/04/2021, wakapita jimbo la Tibesti kisha jimbo la Kanem, ambalo liko umbali wa kilomita 400 kutoka N'Djamena. Walitangaza kwenye ukurasa wao wa Facebook kuwa "uchaguzi uliofanyika ulikuwa ni kiini macho na wakawataka wananchi kuwaunga mkono ili kuikomboa nchi yao ya Chad na kushinikiza udikteta," na wakatangaza kuteka kambi za kijeshi karibu na mpaka wa Libya bila upinzani.
Msemaji wa jeshi la Chad, Jenerali Azem Bermandoa Agouna, alisema kupitia televisheni ya taifa mnamo 20/04/2021: "Rais wa Jamhuri Idriss Déby Itno amepumua pumzi yake ya mwisho akitetea umoja na usalama wa ardhi katika uwanja wa vita... Tunatangaza kwa masikitiko makubwa kwa watu wa Chad habari za kifo cha Marsha wa Chad Jumanne, Aprili 20, 2021." Pia alitangaza kuundwa kwa baraza la kijeshi na kuteuliwa kwa Mahamat Déby, mwana wa rais aliyeuawa, kuwa mwenyekiti wa baraza hilo, na kutangaza kuvunjwa kwa bunge na serikali. Msemaji huyo aliongeza kuwa "Baraza la Kijeshi la Mpito (CMT) chini ya uenyekiti wa Mahamat Idriss Déby linahakikisha uhuru wa kitaifa, usalama wa ardhi, umoja wa kitaifa, kuheshimiwa kwa mikataba ya kimataifa, na linahakikisha kipindi cha mpito cha miezi 18 ambapo baada ya hapo uchaguzi huru, wa kidemokrasia na wa wazi utafanyika." Alibainisha pia "kuwekwa kwa amri ya kutotoka nje kuanzia saa kumi na mbili jioni hadi saa kumi na moja alfajiri na kufungwa kwa mipaka ya nchi kavu na anga," na akatangaza "mkataba wa mpito unaompa rais wa mpito mamlaka makubwa na kufuta katiba." Hivyo, serikali, bunge, na katiba ya utawala huo vilifutwa na taasisi ya kijeshi ya utawala uleule na watu walewale waliokuwa madarakani, isipokuwa Déby aliyeuawa. Hii ni kwa sababu idadi kubwa ya maafisa wa juu wanatoka katika familia na jamaa wa rais aliyeuawa kutoka kabila la Zaghawa, ambalo lina matawi nchini Chad, Libya, na Sudan. Hata hivyo, kabila hili limegawanyika, kwani wapo baadhi ya waasi wanaotoka kabila hili. Inasemekana kuwa binamu zake ndio walioongoza shambulio mwanzoni mwa mwaka 2019 wakiongozwa na Timane Erdimi chini ya jina la Union of Resistance Forces. Walikaribia kufanikiwa katika uasi wao lau si kuingilia kati kwa Ufaransa. Ikumbukwe kuwa baraza jipya la kijeshi lililoundwa chini ya uenyekiti wa Mahamat Déby lina maafisa 15, wakiwemo 8 kutoka kabila la Zaghawa. Waasi wametangaza kukataa kwao katakata baraza hilo la kijeshi, na msemaji wa waasi akasema, "Vikosi vyetu viko njiani kuelekea N'Djamena, lakini tutawapa watoto wa Déby kati ya saa 15 hadi 28 ili wamzike baba yao kulingana na mila." Wameahidi kuendeleza uasi wao hadi wafike mji mkuu.
Idriss Déby mwenyewe aliongoza harakati ya uasi mwaka 1990 hadi akanyakua madaraka nchini Chad na kumuangusha Hissène Habré (1982-1990) ambaye aliigeuka Ufaransa na kuwa kibaraka wa Marekani. Déby alikuwa mkuu wa jeshi akaongoza uasi kwa msaada wa Ufaransa hadi akaingia madarakani, na alifungamana na Ufaransa kwa ukaribu ili ilinde kiti chake na abaki mamlakani. Ufaransa ilikuwa na mchango mkubwa zaidi katika kumsaidia Déby kushinda uasi ambao haukuwahi kukoma. Mnamo Februari 2008, shambulio la waasi lilizuiwa kutokana na msaada wa Ufaransa walipofika milangoni mwa ikulu ya rais huko N'Djamena. Déby mwenyewe alikuwa akishirikiana na askari wake kupambana na uasi tangu mwaka 2006. Lakini Ufaransa ilikuwa na jukumu kubwa katika kuzima harakati za awali za uasi. Inaonekana safari hii Ufaransa haikuchukua hatua mara moja kuzuia uasi wa hivi karibuni, na jukumu lake lilikuwa ni kusaidia vikosi vya Déby. Hii ni kwa sababu kundi la Front for Change and Concord in Chad (FACT) lilieleza katika taarifa yake iliyochapishwa kwenye ukurasa wa Africa Post mnamo 15/04/2021 kuwa "kundi hilo liliitaka Ufaransa kutoingilia upande wowote, likibainisha kuwa ndege za Ufaransa kuruka juu ya maeneo yao inaweza kutafsiriwa kama msaada kwa Rais wa Chad, kwani inazingatiwa kuwa baada ya kila ndege za Ufaransa kupita, hufuatiwa na mashambulizi ya anga kutoka kwa serikali." Inaonekana Ufaransa iliona kuwa vikosi vya Déby vilitosha kuzuia shambulio hilo, lakini ilishtushwa na kifo chake ambacho kilikuwa pigo kubwa kwake.
Kifo cha Déby ni hasara kubwa kwa mkoloni Mfaransa. Taarifa kutoka Ikulu ya Elysee saa chache baada ya kifo chake ilisema: "Ufaransa imepoteza rafiki shujaa... Ufaransa inasisitiza umuhimu wa kipindi cha mpito kufanyika katika mazingira ya amani na kwa ari ya mazungumzo na pande zote za kisiasa na asasi za kiraia, na kuruhusu kurejea kwa haraka kwa serikali shirikishi inayotegemea taasisi za kiraia. Inaonyesha kushikamana kwake thabiti na utulivu wa Chad na umoja wa ardhi yake. Ufaransa inatoa rambirambi kwa familia ya Rais Déby na watu wote wa Chad." Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa, Jean-Yves Le Drian, alitoa wito wa "kipindi cha mpito cha kijeshi kilicho na mpaka kitakachopelekea serikali ya kiraia na shirikishi," na hapa Ufaransa inatangaza kuunga mkono kipindi cha mpito na hivyo mamlaka yaliyoshika hatamu. Msemaji wa serikali ya Ufaransa, Gabriel Attal, alitangaza kuwa "Rais Macron atashiriki katika mazishi ya aliyekuwa Rais wa Chad, Déby." (AFP 21/04/2021), jambo ambalo linaonyesha kiwango cha umuhimu wake katika kulinda ushawishi wake au tuseme ukoloni wake nchini Chad. Vilevile, ushiriki wake katika mazishi ni kwa ajili ya kuzungumza na mtoto wa rais aliyeuawa na viongozi wengine wapya ili kusisitiza utiifu wao kwa Ufaransa.
Magazeti ya Ufaransa yalishughulika sana na kifo cha Déby katika kurasa zao zilizotoka siku iliyofuata; gazeti la La Croix lilitaja kuwa "kifo cha Déby kinachukuliwa kuwa pigo kali kwa diplomasia ya Ufaransa," na gazeti la Libération likasema "Ufaransa sasa imenyimwa Déby baada ya kifo chake jana. Alikuwa zao la usimamizi wa kijeshi wa Ufaransa na mshirika wa Ufaransa katika eneo hilo," na likaongeza "Lakini kilicho hakika ni kwamba operesheni ya kijeshi ya Ufaransa ya Barkhane, ambayo imekuwa ikikabiliwa na udhaifu mkubwa hivi karibuni, leo ipo katika hali ngumu." Likauliza ikiwa kuna nguvu za nje nyuma ya waasi. Wafaransa wanatambua kuwa kuna mataifa makubwa nyuma ya harakati za uasi. Hii ni kwa sababu nchi yao iko katika hali mbaya katika eneo hilo na ilikaribia kuondoa vikosi vyake huko kutokana na hasara inayopata bila kupata ushindi tangu kuingilia kwake moja kwa moja katika eneo hilo mwaka 2014 baada ya mapinduzi yaliyotokea Mali mwaka 2012 na maafisa vibaraka wa Marekani. Kisha maafisa wanaoiunga mkono Marekani mwaka jana, 2020, walifanya mapinduzi. Na kaskazini mwa Chad kuna Libya, ambapo Marekani inafanya kazi kupanua ushawishi wake. Hivyo hali ya Ufaransa imekuwa ya wasiwasi katika eneo hilo.
Chad na nchi nyingine za Afrika kwa mtazamo wa kimataifa zinachukuliwa kuwa nchi huru, lakini kiuhalisia ni makoloni ya Ufaransa kama zilivyokuwa kabla ya kupata uhuru wa kijuujuu mwaka 1960 kutoka kwa Ufaransa. Vikosi vya mkoloni Mfaransa vimepiga kambi humo na askari wa jeshi la Chad wanapigana kwa ajili ya Ufaransa na maslahi yake ya kikoloni katika eneo la Sahel, na utajiri na mali zao huenda Ufaransa, kwani sarafu yao pamoja na sarafu za nchi nyingine 13 za Afrika zimefungamanishwa na Euro ya Afrika ambayo hapo awali ilikuwa CFA Franc, ambapo nusu ya fedha za Chad huenda katika Benki Kuu ya Ufaransa. Ufaransa imeweka askari 5,100 baada ya kuwa askari 4,500 mwaka mmoja uliopita nchini Chad katika mfumo wa operesheni inayoitwa Barkhane kupambana na kile kinachoitwa ugaidi. Chad inashiriki upande wake katika kikosi kikubwa zaidi cha kijeshi cha nchi za Sahel kinachoundwa na yenyewe, Mauritania, Mali, Burkina Faso, na Niger chini ya usimamizi wa Ufaransa ili kuhifadhi ushawishi wa Ufaransa Magharibi na Kati mwa Afrika, hususan nchini Mali. Pamoja na hayo, Ufaransa iko kati ya matumaini na kukata tamaa ya kupata ushindi au hata kubaki katika eneo hilo, kwani kuwepo kwake kunatishiwa kwa dhati, kwa sababu Marekani inaiandama katika eneo zima. Sauti zimeanza kupazwa zikitaka kuondolewa kwa kikosi hiki kutokana na hasara ya maisha miongoni mwa askari wa Ufaransa, ambapo idadi imefikia vifo 50 kulingana na takwimu rasmi. Ufaransa inafanya kazi kuimarisha kile kinachoitwa vikosi vya Sahel ili vipigane kwa niaba yake na inaomba msaada kutoka nchi za Ulaya, na pia inatumia Imarati (UAE) kuifadhili. Lakini kumpoteza Déby kunachukuliwa kuwa hasara kubwa kwa kikosi hiki. Sekretarieti ya nchi za Sahel imetangaza kuwa "inaunga mkono kikamilifu kipindi cha mpito kilichotangazwa nchini Chad kufuatia kifo cha Rais Idriss Déby, aliyekuwa mwenyekiti wa zamu wa kundi hilo..." (Al Jazeera 22/04/2021). Hivyo Chad inatarajiwa kukumbwa na ushindani mkali wa kimataifa. Marekani iliweza katika miaka ya themanini ya karne iliyopita kumnunua Hissène Habré, hivyo Chad ikaingia chini ya ushawishi wa Marekani, kisha ikapoteza ushawishi huo wakati Déby alipompindua, lakini Marekani haiachi majaribio yake ya kurejea...
Marekani ilikuwa ikifuatilia harakati za uasi tangu zilipoanza nchini Libya, na ilitangaza mnamo 18/04/2021 kuwa "makundi ya kijeshi yasiyo ya kiserikali kaskazini mwa Chad yameelekea kusini kuelekea N'Djamena, na kutokana na ukaribu wake na mji mkuu na uwezekano wa kuzuka kwa vurugu mjini humo, amri imetolewa kwa wafanyakazi wasio wa lazima wa Marekani kuondoka Chad kwa safari ya ndege ya kibiashara..." (Al Jazeera 18/04/2021). Baada ya kifo cha Rais wa Chad, ilitangaza kupitia msemaji wa wizara yake ya mambo ya nje, Ned Price, mnamo 20/04/2021 kuwa "Washington inataka kuona mpito wa mamlaka nchini Chad unaoendana na katiba yake baada ya kuuawa kwa Rais Déby Jumatatu," na akasema "ubalozi wa Marekani nchini Chad bado upo katika hali ya kuondoka kwa lazima kuanzia Aprili 17" (Reuters 20/04/2021). Siku iliyofuata, msemaji wa wizara ya mambo ya nje alisema: "Washington imefadhaishwa sana na vurugu nchini Chad kufuatia kifo cha Rais Déby na ina wasiwasi na chochote kinachozuia mpito wa kidemokrasia wa mamlaka huko... na Washington inafuatilia kwa karibu hali ya kisiasa nchini Chad" (AFP 21/04/2021). Hivyo, Marekani inafanya kazi kusogeza mbele tarehe ya uchaguzi na kuuita huo kuwa ni mpito wa kidemokrasia ili kuandaa mazingira ya kuifikisha upinzani madarakani na kukomesha ushawishi wa Ufaransa.
Vyombo vingi vya habari vimeashiria uhusiano kati ya waasi wa Chad na vikosi vya Haftar, kibaraka wa Marekani, na huu si uhusiano mpya bali umekuwepo tangu awali. Reuters iliripoti mnamo 12/02/2019 ikimnukuu Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa Jean-Yves Le Drian akisema: "Kufuatia ombi la Déby, ndege za kivita za Ufaransa zilishambulia msafara wenye silaha kali wa waasi uliovuka wiki iliyopita kutokea Libya na kuingia ndani ya ardhi ya Chad. Le Drian aliwaambia wabunge: 'Rais Déby alituomba kwa maandishi tuiingilie kati ili kuzuia mapinduzi na kuilinda nchi yake'." Kwa sababu hatari hizi ambazo Haftar, kibaraka wa Marekani, anazisukuma kuelekea Chad ni za kweli, Ufaransa inatuma kikosi kikubwa katika mji mkuu wa Chad ili kumlinda kibaraka wake Idriss Déby, idadi iliyofikia takriban elfu tano! Al Jazeera iliripoti mnamo 22/04/2021 kutoka kwa chanzo kimoja kuwa "upinzani wenye silaha umehamisha kambi zake nyingi kutoka mpakani na Libya hadi ndani ya Chad na kwamba makundi ya upinzani ikiwemo Baraza la Uongozi la Kuikomboa Jamhuri ya Chad yanajiandaa kuondoka katika maeneo yao nchini Libya na kuingia ndani ya ardhi ya Chad baada ya saa chache."
Kutokana na hapa, inabainika kuwa Chad iko katika hatari ya kuongezeka kwa mzozo kati ya vikosi vya utawala na vikosi vya waasi, kwani pande zote mbili zimefungamana na mataifa ya kigeni ya kikoloni yanayoshindana, ambayo ni Ufaransa na Marekani. Walioshika madaraka si rahisi kwao kusalimu amri huku wakiona hatima yao inatishiwa na kwamba nyuma yao kuna dola ya kikoloni kama Ufaransa inayowaunga mkono ili kudumisha ushawishi wake na ukoloni wake katika nchi yao. Ufaransa ni sababu inayowasaidia kuwalinda ili waendelee kutumikia maslahi yake ya kikoloni katika Afrika ya Kati na Magharibi. Wakati huo huo, waasi wenye tamaa ya kufika madarakani wanaungwa mkono na dola ya kikoloni kama Marekani inayotafuta kupanua ushawishi wake nchini Chad na eneo hilo. Hivyo, nchi za Waislamu ni uwanja wa mapambano kati ya wakoloni, na watoto wao ni kuni za moto wa mzozo huu, huku utajiri wao ukienda kwa mkoloni, nao wakibaki wakiteseka kwa umaskini, kunyimwa haki, na kuenea kwa magonjwa. Hakuna wokovu kwa Waislamu nchini Chad ambao wanachomwa na moto wa mzozo wa kimataifa juu ya nchi yao, isipokuwa kwa Waislamu wa Afrika Kaskazini na Sudan kuchukua hatua ya kusimamisha utawala wa Kiislamu katika nchi zao na kuziunganisha, na kisha kuelekea katika nchi nyingine za Afrika ili kuzikomboa nchi baada ya nchi kutoka katika nira ya mkoloni. Hivyo ni wajibu kwa Waislamu kuwanusuru watendaji miongoni mwa watoto wao wanyofu, wenye uelewa, na wanaofanya jitihada za kusimamisha Khilafah ya Rashidah kwa njia ya Utume.
وَعَدَ اللَّهُ الَّذِينَ آمَنُوا مِنكُمْ وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ لَيَسْتَخْلِفَنَّهُم فِي الْأَرْضِ كَمَا اسْتَخْلَفَ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ وَلَيُمَكِّنَنَّ لَهُمْ دِينَهُمُ الَّذِي ارْتَضَى لَهُمْ وَلَيُبَدِّلَنَّهُم مِّن بَعْدِ خَوْفِهِمْ أَمْنًا يَعْبُدُونَنِي لَا يُشْرِكُونَ بِي شَيْئًا وَمَن كَفَرَ بَعْدَ ذَلِكَ فَأُوْلَئِكَ هُمُ الْفَاسِقُونَ
"Mwenyezi Mungu amewaahidi wale walio amini miongoni mwenu na wakatenda mema, ya kwamba atawafanya makhalifa katika ardhi kama alivyo wafanya makhalifa wale wa kabla yao, na kwa yakini atawaidhinishia dini yao aliyo wapendelea, na atawabadilishia amani baada ya hofu yao. Wawe wananiabudu Mimi, wala wasinishirikishe na chochote. Na watakao kufuru baada ya hayo, basi hao ndio mafaasiki." (QS. An-Nur [24]: 55)
13 Ramadhani 1442 H
25/04/2021 M