Jibu la Swali
Mkutano wa Kilele wa Marekani na Ghuba
Swali:
Rais wa Marekani, Obama, aliwasili nchini Saudi Arabia tarehe 20/04/2016 katika ziara yake ya nne tangu aliposhika urais mwaka 2009. Alifanya kikao chake cha kwanza na mfalme wake, Salman Al Saud, kabla ya Mkutano wa Kilele wa Marekani na Ghuba uliofanyika siku iliyofuata ya ziara hiyo mjini Riyadh. Ziara hii imezungukwa na kelele nyingi katika vyombo vya habari kwamba itajadili matatizo ya eneo hili na ufumbuzi wake! Matatizo haya yalitokea katika taarifa ya mwisho kama vile Syria, Yemen, Iraq, Libya, na Palestina... yote haya yanatokea huku Obama akiwa katika mwaka wake wa mwisho na uwezo wake wa kutatua matatizo ukiwa dhaifu, na hali yake inatajwa kwao kama "bata mlemavu" (lame duck)! Hivyo basi, malengo ya ziara hii yanawezaje kueleweka? Na Mwenyezi Mungu akulipe kheri.
Jibu:
Hakika malengo ya ziara hiyo hayakuwa ya kutatua matatizo ya eneo hili, kwani Marekani iliweka miradi ya suluhu kabla ya ziara ya Obama; iliiweka kwa ajili ya Syria na kuithibitisha tangu kuanzishwa kwa "Kamati ya Riyadh" ya mazungumzo, na iliiweka kwa ajili ya Yemen na kuithibitisha tangu operesheni ya Asifat al-Hazm (Dhoruba ya Maamuzi) ambayo iliwatoa Wahouthi ili washindanie ushiriki katika utawala baada ya kuwa wametengwa huko Saada na viunga vyake, na iliiweka kwa ajili ya Palestina kwa kuitambua dola ya Kiyahudi, na kadhalika Iraq na Libya... Miradi ya Marekani imewekwa kabla ya Obama kuwa "bata mlemavu"! Na kutajwa kwa masuala haya katika taarifa ya mwisho haikuwa ila ni kwa ajili ya kuongeza mistari ya taarifa hiyo!
Haya siyo malengo makuu yaliyokusudiwa katika ziara hiyo, bali kwa kuangalia kwa kina yaliyotokea katika ziara hiyo na matamshi yaliyoambatana nayo, kisha kile kilichotolewa katika taarifa ya mwisho... na baada ya kupita yaliyomo katika taarifa hiyo ya dibaji, maneno ya kujaza nafasi, na masuala yasiyokusudiwa ambayo taarifa hiyo iliyapitia ili tu kujaza nafasi! Baada ya hapo, inabainika kuwa malengo ya ziara hiyo yalikuwa ni kufanikisha maslahi ya Marekani na kuimarisha ushawishi wake katika eneo hilo na kisha kupanga mambo ya vibaraka wake humo... Na mambo haya hayawaachi maraisi wa Marekani iwe miguu yao ni mizima au ni mlemavu, na hasa wanapopata vibaraka wanaowatandikia njia chini ya miguu yao ile mlemavu! Malengo haya yanaweza kufupishwa katika malengo makuu mawili kama ifuatavyo:
1- Kuhakikisha udhibiti wa Marekani juu ya eneo la Ghuba na kuzuia kuimarika kwa ushawishi mwingine, hasa ule wa Uingereza. Na yeyote anayetafakari taarifa ya mwisho iliyochapishwa na gazeti la Al-Riyadh mnamo 22/04/2016 ataikuta ikizungumza hayo, na tutagusia baadhi ya mambo yanayohusiana na taarifa hii na kuyatolea maelezo.... Ilitajwa katika taarifa hiyo: (... "Viongozi wa nchi za Baraza la Ushirikiano la Ghuba (GCC) na Marekani walifanya mkutano wao jana mjini Riyadh ili kusisitiza tena ushirika wa kimkakati kati ya pande hizo mbili, wenye lengo la kufikia utulivu, usalama na ustawi wa eneo hilo. Ambapo viongozi walipitia maendeleo ya wazi yaliyopatikana tangu mkutano wa kwanza wa kilele uliofanyika Camp David mnamo Mei 2015...") Taarifa hiyo iliongeza: "Pia nchi za GCC ziliahidi kufanya utafiti wa kina wa ofa za Marekani za ushirikiano katika nyanja ya usalama wa baharini, na kufikia haraka makubaliano juu ya hatua muhimu za kutekeleza mfumo jumuishi wa ulinzi wa onyo la mapema dhidi ya makombora ya balestiki..." Ni kana kwamba Marekani inachukua hili kama kisingizio cha kuweka ngao ya makombora katika eneo hilo kwa ufadhili wa nchi za Ghuba ili kuimarisha udhibiti wake katika eneo hilo na kuzuia kujikomboa kwake kutoka kwenye mtego wake... Taarifa hiyo iliongeza: "Hakika sera ya Marekani inayojikita katika kutumia mbinu zote za nguvu ili kuhakikisha maslahi yake ya kimsingi katika eneo la Ghuba na kuzuia na kukabiliana na uchokozi wowote wa nje dhidi ya washirika wake kama ilivyofanya katika vita vya Ghuba ni jambo lisilo na shaka." Huu ni unyenyekevu na utiifu wa kudhalilisha kutoka kwa nchi za Ghuba kwa Marekani, ambapo nchi hizi zinairuhusu Marekani kwa mujibu wa maandishi ya taarifa hiyo kutumia nguvu ili kulinda maslahi yake na kueneza ushawishi wake, na katika hilo kuna tishio kwao wenyewe ikiwa watatoka nje ya utiifu wa Marekani, na taarifa hiyo ilitoa mfano wa hilo kuwa ni vita vya Ghuba, yaani kuikalia Iraq kwa mabavu...! Taarifa hiyo iliongeza: "Pia viongozi wa nchi za GCC wanatoa ahadi yao ya kukamilisha utafiti wa ofa za Marekani katika nyanja ya ushirikiano wa kijeshi na mafunzo yenye lengo la kuimarisha uwezo wa nchi za Ghuba katika kuchukua jukumu kubwa zaidi katika kukabiliana na changamoto za kikanda." Yaani kwamba nchi za Ghuba zinatekeleza maombi ya Marekani bila upinzani, na hili ndilo lililothibitishwa na taarifa hiyo kwa kusema: "Viongozi walisikiliza ripoti ya mkutano wa pamoja wa mawaziri wa ulinzi wa nchi za Baraza hilo na Marekani, ambayo ilisisitiza umuhimu wa mazoezi ya kijeshi kati ya GCC na Marekani, na viongozi walitangaza kuwa nchi za Baraza na Marekani zitaanza mara moja kupanga kufanya zoezi la pamoja la kijeshi mnamo Machi 2017 ili kuonyesha uwezo wa pamoja wa kijeshi wa pande zote mbili... Pia nchi za Baraza ziliunga mkono upanuzi wa upeo wa ushirikiano na Marekani katika nyanja ya usalama wa mtandaoni (cybersecurity) na kufuata vigezo vya usimbaji wa kielektroniki vilivyowekwa na Saudi Arabia, Marekani na nchi za G20... Pia viongozi walielekeza kuwa makundi yote ya kazi ya pamoja yakutane angalau mara mbili kwa mwaka, kwa lengo la kuharakisha kasi ya ushirika kuhusu kupambana na ugaidi na kurahisisha uhamishaji wa uwezo wa ulinzi nyeti, ulinzi dhidi ya makombora ya balestiki, utayari wa kijeshi na usalama wa kielektroniki (cybersecurity)." Inabainika kutokana na yote haya kiasi gani taarifa hii ilitoa utawala kwa Marekani katika Ghuba, na taarifa hiyo haikuishia hapo bali ilihitimisha kwa kuhakikisha utekelezaji wake! ("Na ili kuhakikisha mwendelezo wa shughuli hizo na utekelezaji wa haraka wa maamuzi yaliyomo katika taarifa ya pamoja ya Camp David ya tarehe 14 Mei 2015, na nyongeza yake, na taarifa hii, viongozi walielekeza vyombo husika vya pande zote mbili kuimarisha mifumo ya ushirika kati yao, ikiwa ni pamoja na 'Jukwaa la Ushirikiano wa Kimkakati la Ghuba na Marekani.' Riyadh 22/04/2016 )... Kwa hiyo, Obama alitangaza ushindi wake katika mkutano wake na waandishi wa habari baada ya mkutano huo kwa kusema: "Mkutano huu umesisitiza tena sera ya Marekani inayotaka kutumia mbinu zetu za nguvu ili kulinda maslahi yetu ya msingi katika eneo la Ghuba na kuzuia na kukabiliana na uchokozi wowote wa nje dhidi ya washirika wetu na washirika wetu." (Reuters 21/04/2016).
2- Kusawazisha jukumu la Saudi Arabia na jukumu la Iran, ili Iran iwe upande wa mashariki wa Ghuba na Saudi Arabia iwe upande wa magharibi wa Ghuba, kisha wagawane majukumu katika nchi nyingine za eneo hilo kwa ushindani wa kirafiki bila kuzingatia ushawishi wa kijadi wa Uingereza katika Ghuba au vibaraka wake, bali kwa kumkabidhi mfalme wa Saudi Arabia, Salman, jukumu la kudhibiti usumbufu wa vibaraka wa Waingereza katika Ghuba, hasa Qatar, dhidi ya mipango ya Marekani, na kumpa Salman umuhimu maalum katika jambo hili... Na hili lilikuwa wazi wakati Obama alipokutana na Salman kabla ya kufanyika kwa Mkutano wa Kilele wa Marekani na Ghuba, jambo ambalo linaashiria uhusiano maalum kati ya Marekani na Salman wa Saudi Arabia, na kwamba Salman ana jukumu maalum katika mipango ya Marekani, la sivyo Rais wa Marekani angeingia moja kwa moja kwenye mkutano wa kilele kama wengine bila mkutano maalum kabla ya mkutano mkuu. Kwa hiyo, msemaji wa Ikulu ya White House, Ben Rhodes, alisema "kwamba mkutano uliodumu kwa saa mbili na Mfalme Salman siku ya Jumatano 21/04/2016 ulikuwa mkutano mrefu zaidi kati ya viongozi hao wawili..." (Reuters 21/04/2016), na jukumu hili maalum haliathiriwi na kitendo cha Mfalme Salman kutomlaki Obama yeye mwenyewe binafsi, kwani huo ulikuwa ni ujumbe kwa Congress na kwa Warepublican hasa ambao kwa madhumuni ya uchaguzi waliibua suala la dhima ya Saudi Arabia kwa vifo vya Wamarekani vilivyosababishwa na Al-Qaeda, wakichukulia kuwa kuibuka kwa Al-Qaeda kulikuwa kwa fedha za raia wa Saudia na hivyo wanadai fidia, na waliwasilisha mradi wa uamuzi kwa Congress... Na kwa ajili ya ushindani wa uchaguzi, baadhi ya wabunge wa chama cha Democratic waliungana nao... Licha ya shinikizo la utawala wa Marekani kuzuia mradi huo usipitishwe, lakini hasira ya Saudia ilikuwa ni lazima ili kufeli kwa majaribio ya Congress, hasa Warepublican ambao walitaka kupitia jambo hili kujionyesha kuwa wanajali familia za waliouawa ili wapate kura katika uchaguzi, na hivyo Saudi Arabia ilichukua hatua ya kuonyesha hasira kama ujumbe kwa Congress ili iache mradi wa dhima na fidia, bali hata walitishia kuondoa mabilioni ya Saudia kutoka kwenye benki zao, na kuondoa mabilioni kuna athari kubwa kwa watu wa mfumo wa kirasimali... Tovuti ya Huffington Post Arabi iliripoti "... Na kwa mujibu wa maafisa wa urais na wasaidizi katika Congress kutoka vyama vyote viwili, utawala wa Obama uliishinikiza Congress kuzuia kupitishwa kwa mswada huo. Maafisa wamewaonya wanachama wa Seneti dhidi ya athari za kidiplomasia na kiuchumi zinazoweza kutokana na kupitishwa kwa sheria hii, kwa mujibu wa ripoti iliyochapishwa na New York Times. Na waziri wa mambo ya nje wa Saudia, Adel al-Jubeir, wakati wa ziara yake mjini Washington mwezi uliopita, alikuwa amewaambia baadhi ya wabunge kuwa Saudi Arabia italazimika kuuza hadi thamani ya dola bilioni 750 za dhamana za hazina ya Marekani zinazomilikiwa na Saudi Arabia, pamoja na mali nyingine nchini Marekani..." (Huffington Post Arabi: 18/04/2016).
Kwa hivyo, hasira hiyo ya kidhahiri ya Saudia na tishio la kuondoa mabilioni ni ujumbe kwa Congress na siyo kwa Obama, bali haiondolewi uwezekano kuwa kuonyesha hasira ya kidhahiri kwa kutomlaki mfalme binafsi, na pia tamko la Al-Jubeir la kuondoa mabilioni, haiondolewi uwezekano kuwa ni kwa makubaliano fulani na Obama ili kufeli lengo la Warepublican, kwa sababu tishio la kuondoa mabilioni ni kichocheo chenye nguvu kinachopunguza kasi ya msukumo wao katika mradi wao. La sivyo, kama hasira ingekuwa ya kweli, Obama asingehusishwa na mkutano maalum kabla ya mkutano mkuu, bali angehudhuria mkutano huo kama wengine bila mkutano maalum wa awali. Kisha, vipi kwa Al-Jubeir ambaye alikulia na kulelewa katika mikono ya Marekani kutishia kuondoa mabilioni ya dhamana za hazina ya Marekani?! Na utawala wa Obama bila shaka unatambua hilo, kwani CNN Arabi iliripoti mnamo 20/04/2016 yafuatayo: (Wakati huo huo, afisa mmoja wa Marekani alisema kuwa "kutokuwepo kwa Mfalme Salman katika mapokezi mara tu baada ya kuwasili hakukuchukuliwa kama tusi", akibainisha kuwa Rais wa Marekani mara chache huwalaki viongozi wa kigeni kwenye uwanja wa ndege mara tu wanapowasili Marekani... Kwa upande wake, Bruce Riedel, mtaalam katika taasisi ya "Brookings" ya utafiti na afisa wa zamani katika Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA), alisema kuwa "licha ya tofauti zote, Saudi Arabia na Marekani hazitatengana"...) Kwa hivyo, uhusiano ni imara kati ya Marekani na Mfalme Salman...
Ama kuhusu uhusiano kati ya Saudi Arabia na Iran, hakika Marekani inataka kutatua mzozo huu na kurudisha uhusiano kati ya pande mbili, kwa sababu Marekani inajihisi sana kufanya eneo hilo likubali jukumu la Iran ambalo lina maslahi kwa Marekani. Obama alishawahi kusema katika mahojiano yake na jarida la The Atlantic la Marekani mnamo 10/03/2016 kuwa anazipendekeza Saudi Arabia na Iran ziishi pamoja kwa amani katika eneo hilo: (Rais wa Marekani, Barack Obama, alisema kuwa "Saudi Arabia na Iran zinapaswa kujifunza kanuni ya kuishi pamoja na kutafuta njia ya kufikia aina fulani ya amani..." Obama aliongeza katika mahojiano na jarida la The Atlantic la Marekani kuwa "ushindani kati ya Wasaudia na Wairani ambao ulisaidia kuchochea vita vya wakala na machafuko nchini Syria, Iraq, na Yemen unahitaji sisi kuwaambia marafiki zetu Wasaudia na pia Wairani kuwa wanahitaji kutafuta njia bora ya kuishi pamoja"). (Chanzo: BBC, Reuters 10/03/2016)... Ni kana kwamba Obama ndiye msimamizi wa nchi hizo mbili anayezipangia mambo yao na kuziusia jinsi ya kutenda katika eneo hilo! Na inaonekana kuwa usia wa Obama umetekelezwa, kwani ilitajwa katika taarifa ya mwisho ya mkutano wa kilele: "Marekani na nchi za GCC zimesisitiza uungaji mkono wao kwa mpango wa kina wa utekelezaji wa pamoja na Iran, wakibainisha kuwa utekelezaji wa mpango huo hadi sasa umezizuia jitihada za Iran za kumiliki silaha za nyuklia, jambo linaloimarisha usalama na utulivu katika eneo hilo... Na nchi za GCC zimesisitiza utayari wao wa kujenga uaminifu na kutatua migogoro ya muda mrefu na Iran, kwa sharti la Iran kujitolea katika kanuni za ujirani mwema, kutoingilia masuala ya ndani, na kuheshimu usalama wa maeneo kwa mujibu wa sheria za kimataifa..." (Riyadh 22/04/2016).
Mwishoni, hakika inasikitisha sana Marekani kunyoosha mikono yake kuvuka bahari ili kudhibiti ardhi yetu na bahari yetu, na vyanzo vya nguvu zetu na utajiri wetu... Lakini Marekani haipati mbele yake ila ni viongozi ruwaibidhah wanaofanya jitihada za kulinda viti vyao na utajiri wao na kudumisha utawala wa familia zao, hivyo wanainyenyekea na kutekeleza matakwa yake; wanaiogopa na hawamuogopi Mwenyezi Mungu, na kwa njia hiyo inafanikiwa kupitisha malengo yake kupitia kwao katika nchi za Waislamu! Lakini hali hii haitaendelea kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, kwani Mwenyezi Mungu Mtukufu Mwenye Hikma ametuahidi na Mtume Wake (saw) ametubashiria kurejea kwa Khilafah ya Kidini inayofuata njia ya Utume, ambapo Uislamu na Waislamu watatukuka na makafiri wakoloni watadhalilika.
وَسَيَعْلَمُ الَّذِينَ ظَلَمُوا أَيَّ مُنْقَلَبٍ يَنْقَلِبُونَ
"Na walio dhulumu watakuja jua ni mgeuko gani watakao geuka." (QS. Ash-Shu'ara [26]: 227)
20 Rajab 1437 H 27/04/2016 M