Jibu la Swali
Maendeleo ya Hivi Karibuni katika Mgogoro wa Libya
Swali: Serikali ya umoja wa kitaifa imeundwa nchini Libya, na inaonekana kuwa pande zinazopigana nchini humo zimekubaliana nayo. Je, makubaliano haya ni ya kweli au la? Na yaliwezekanaje baada ya mzozo wa silaha uliodumu kwa miaka kumi ambapo kila upande ulikuwa ukijaribu kuuangamiza mwingine? Na nini ukweli wa misimamo ya Marekani, Uingereza, nchi za Ulaya, Uturuki na nchi nyingine zinazoingilia mgogoro wa Libya kuhusiana na makubaliano haya?
Jibu: Kwa kuangalia maendeleo ya hivi karibuni katika mgogoro wa Libya katika miaka miwili iliyopita, na haswa tangu tarehe 05/02/2021 wakati Jukwaa la Mazungumzo ya Kisiasa chini ya udhamini wa Umoja wa Mataifa lilipochagua mamlaka ya utendaji ya pamoja ambayo ilianza kazi zake tarehe 16/03/2021, maendeleo haya yalisababishwa na mfululizo wa matukio:
Kwanza: Katika robo ya mwisho ya mwaka jana, vita vya mazungumzo kati ya Marekani na Uingereza vilipamba moto katika ulingo wa Libya. Uingereza, kupitia vibaraka wake, ilikuwa ikiandaa mikutano ya mazungumzo nchini Morocco, wakati Marekani, kupitia mjumbe wa kaimu wa Umoja wa Mataifa, mwanadiplomasia wa Marekani Stephanie Williams, ilikuwa ikiandaa mikutano nchini Tunisia na Geneva. Tulielezea hili kwa kina katika jibu la swali la tarehe 25/11/2020, na baada ya hapo mambo yalifuata kama ifuatavyo:
1- Uingereza ilifanya mkutano kupitia vibaraka wake, kwa ushiriki wa wajumbe 13 + 13 kutoka Tripoli na Tobruk, huko Bouznika nchini Morocco mnamo tarehe 24/01/2021 ili kuchagua mamlaka za utendaji na kugawa nafasi kuu za uongozi... hadi pale Marekani ilipofanikiwa kuitisha mkutano wa Geneva kati ya tarehe 01 na 05/02/2021 ambao ulishirikisha haiba za kisiasa 75 ilizozichagua kwa ajili ya mazungumzo na kuchagua viongozi wapya. Shinikizo lilikuwa likitolewa kwao kutoka pande nyingi ili wapigie kura uchaguzi wa Baraza jipya la Urais na mkuu wa serikali. Ilitangazwa mnamo tarehe 05/02/2021 kuwa Mohammad Menfi amechaguliwa kuwa Rais wa Baraza la Urais na Abdul Hamid Dbeibeh kuwa Waziri Mkuu, na Musa al-Koni na Abdullah al-Lafi walichaguliwa kuwa wanachama wa Baraza la Urais. Hivyo, Marekani iliweza kuchagua mamlaka za utendaji nchini Libya na kushinda duru hii katika mzozo na Uingereza. Hivyo basi, Uingereza ilipoteza duru hiyo na haikuweza kuchagua viongozi wapya katika mkutano wa mazungumzo wa mwisho huko Bouznika nchini Morocco. Hii inachukuliwa kuwa hasara kubwa kwa Uingereza baada ya mafanikio yake ya awali katika mkutano wa Skhirat nchini Morocco mwaka 2015 ambapo ilimchagua waziri mkuu na rais wa baraza la urais na kuunda serikali nchini Tunisia iliyoongozwa na Fayez al-Sarraj...
2- Kwa kuchaguliwa kwa mamlaka ya utendaji ya pamoja (Rais wa Baraza la Urais na Waziri Mkuu) na Jukwaa la Mazungumzo ya Kisiasa la Libya lililoanzishwa na mwanadiplomasia wa Marekani na kaimu mjumbe wa Umoja wa Mataifa Stephanie Williams mnamo Septemba 2019 na kuanza mikutano yake katika miezi ya mwisho ya mwaka 2020, Marekani kwa vitendo imechukua uongozi wa mchakato wa kisiasa nchini Libya. Kwa kufanya hivyo, imefanikiwa kwa masharti kunyakua usukani wa Libya kutoka mikononi mwa Waingereza na Wazungu, ingawa hiyo haimaanishi kuwa imedhibiti karata zote za ulingo wa Libya.
3- Mamlaka mpya ya utendaji nchini Libya iliyochaguliwa na jukwaa la mjumbe wa Marekani Williams (Jukwaa la Mazungumzo ya Kisiasa la Libya) ilipata kwa urahisi kura za Bunge la Libya, (Bunge la Libya mnamo Machi 10 lilitoa imani kwa serikali ya umoja wa kitaifa inayoongozwa na Dbeibeh kwa kura 132 kati ya jumla ya 188... BBC, 14/03/2021), kadhalika mchakato wa kukabidhi madaraka kutoka kwa serikali ya Sarraj mjini Tripoli inayounga mkono Wazungu ulienda kwa urahisi: (Libya ilishuhudia serikali mpya ikichukua majukumu yake kwa njia ya amani na bila vikwazo. Fayez al-Sarraj, mkuu wa Baraza la Urais na serikali ya zamani ya mwafaka wa kitaifa mjini Tripoli, alimkumbatia Abdul Hamid Dbeibeh, mkuu wa serikali mpya wakati akimkabidhi madaraka... Na Dbeibeh alikula kiapo cha kikatiba jana Jumatatu katika mji wa Tobruk upande wa mashariki wa nchi, ambapo utawala uliopo mashariki ulikaribisha uteuzi wake. Deutsche Welle ya Ujerumani... 16/03/2021). Kwa haya yote, vibaraka wa Uingereza na Ulaya nchini Libya wamekwenda na suluhisho la Marekani, na hii haitokei isipokuwa kwa ridhaa ya Uingereza na Ulaya kwa suluhisho hili hata kama ni kwa muda.
4- Ili kukamilisha taswira hiyo, kulikuwa na urahisi wa kukabidhi madaraka kutoka kwa serikali ya mashariki mwa Libya ambayo haitambuliki kimataifa na inayoungwa mkono na Misri na Marekani, (Serikali sambamba upande wa mashariki mwa Libya siku ya Jumanne ilikabidhi mamlaka yake kwa serikali mpya ya umoja wa kitaifa inayoongozwa na Abdul Hamid Dbeibeh, wiki moja baada ya serikali hiyo kuanza kazi zake rasmi kutoka mji mkuu Tripoli. Mchakato wa makabidhiano ulifanyika katika makao makuu ya serikali sambamba isiyotambulika kimataifa mjini Benghazi, mji wa pili kwa ukubwa nchini Libya, mbele ya mkuu wake Abdullah al-Thani. Ujumbe wa serikali ya umoja wa kitaifa uliwakilishwa na Naibu Waziri Mkuu Hussein al-Qatrani, Waziri wa Mambo ya Ndani Khaled Mazen na idadi ya mawaziri. Al-Qatrani alisisitiza kuwa hatua ya mgawanyiko "imeisha". Alisema katika taarifa kwa vyombo vya habari "Serikali ya umoja wa kitaifa imekuja kwa ajili ya kuwatumikia wananchi wote". France 24, 23/03/2021).
Pili: Kwa kuangalia misimamo ya kimataifa na kikanda kuhusu maendeleo ya sasa ya mgogoro nchini Libya, tunakuta yafuatayo:
Marekani na Umoja wa Mataifa: Kwa kuzingatia kuwa mkondo wa suluhisho hili la kisiasa ulichorwa na kusimamiwa moja kwa moja na mjumbe wa Marekani katika Umoja wa Mataifa nchini Libya, basi Marekani na Umoja wa Mataifa zinaunga mkono mkondo huu bila shaka. Stephanie Williams, mwanadiplomasia wa Marekani anayefanya kazi kwa niaba ya Umoja wa Mataifa, alisherehekea mafanikio yake baada ya kuchaguliwa kwa viongozi wapya akisema ("Ninafuraha kushuhudia wakati huu wa kihistoria" na aliwaambia pande za Libya "Huu ni ahadi rasmi na ni lazima mamlaka ya utendaji iliyochaguliwa itekeleze"... Al Arabiya 05/02/2021). Hivyo kazi aliyoifanya imekuwa kazi rasmi yenye lazima kwa pande hizo iliyowekwa juu yao na hawana haki ya kuikiuka vinginevyo watakabiliwa na vikwazo vya Marekani ambavyo alikuwa amevitishia hapo awali, kwa njia ya kiburi na ujeuri wa Marekani unaolazimisha masuluhisho na kutishia wanaopinga. Balozi wa Marekani nchini Libya Richard Norland alisisitiza wakati wa mazungumzo ya simu na Mkuu wa Baraza la Urais la Libya Mohammad Menfi ("uungaji mkono wa Marekani kwa Baraza na serikali" na aliwapongeza washiriki wote katika mazungumzo ya Libya na viongozi wa Libya. Alisema "Kuna muingiliano unaokuja kutoka Washington"... Bawabat Al-Wasat ya Libya 12/02/2021).
Msimamo wa Uturuki: (Rais wa Uturuki Erdogan alifanya mawasiliano na mamlaka mpya ya utendaji "Mkuu wa Baraza la Urais Mohammad Menfi na Mkuu wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Abdul Hamid Dbeibeh" akiashiria - yaani Erdogan - kuwepo kwa dalili za matumaini kuhusu kupata suluhisho la kudumu nchini Libya... Al Jazeera Net, 20/03/2021). Kisha Mohammad Menfi alitembelea Uturuki tarehe 26/03/2021 (Menfi alidai wakati wa mkutano wake na Erdogan umuhimu wa kushikamana na mahitaji ya hatua ya mpito nchini Libya ambayo inaishia na kufanyika kwa uchaguzi tarehe 24 Desemba mwaka huu, Al Arabiya Net... 27/03/2021). Kisha, kama inavyoonekana, kulikuwa na ombi la Uturuki la kuondoa wapiganaji wa Syria kutoka Libya, (Vyanzo vya Shirika la Uangalizi wa Haki za Binadamu nchini Syria vilieleza kuwa "amri zilitolewa kwa wapiganaji wa Syria wanaoiunga mkono Ankara nchini Libya kuanza kuandaa mizigo yao na nafsi zao kwa ajili ya maandalizi ya kurejea kwao Syria... Independent Arabia, 20/03/2021). Haya yote yanaashiria mwitikio mkubwa wa Uturuki kwa mkondo wa suluhisho la kisiasa unaoongozwa na mjumbe Williams.
Vyanzo vya habari vilitaja kuwa Abdul Hamid Dbeibeh alielekea Uturuki mara moja baada ya kuchaguliwa huko Geneva kama mkuu wa serikali ya Libya, na matamshi haya pamoja na matamshi ya Yasin Aktay, mshauri wa Rais wa Uturuki yanathibitisha hilo, kwani Aktay alisema "Mikataba ambayo Uturuki ilikuwa imeingia na serikali ya zamani ya mwafaka wa kitaifa nchini Libya iliyoongozwa na Sarraj na uwepo wa kijeshi wa Uturuki nchini Libya hautatahirika na uchaguzi wa serikali mpya. Na serikali mpya ya mpito haipingi mikataba hiyo wala uwepo wa Uturuki nchini humo." Gazeti la Le Monde la Ufaransa lilisema mnamo tarehe 08/02/2021: "Maslahi ya kibiashara ya waziri mkuu mpya yanamfanya kuwa karibu sana na Uturuki, kwani yeye ni mwakilishi nchini Libya wa taasisi rasmi za serikali ya Uturuki zinazovutiwa na soko la Libya...".
Msimamo wa Misri: Rais wa Misri Sisi mwenyewe alimpokea mjini Cairo Mohammad Menfi, Mkuu wa Baraza jipya la Urais siku ya Alhamisi tarehe 25/03/2021 (Sky News Arabic, 25/03/2021) katika ishara ya wazi ya uungaji mkono wa Misri kwa mkondo huu wa kisiasa nchini Libya, na kwamba Misri nayo msimamo wake umegeuka kuhusu mgogoro wa Libya kufuatia maendeleo yaliyokuwa yakifanywa na diplomasia ya Marekani na mjumbe wa Umoja wa Mataifa Williams. Huenda kuoana kwa mabadiliko ya misimamo ya nchi hizi mbili "Uturuki na Misri" kukawa na ishara ya wazi kuwa nchi hizi mbili zinachota kutoka chanzo kimoja. Viongozi wapya wa Libya walikuwa na hamu ya kutembelea nchi mbili za kikanda zenye ushawishi katika ulingo wa Libya ambazo ni Misri na Uturuki ambazo zinatekeleza sera ya Marekani huko kila moja kulingana na dhima yake. Rais wa Misri Sisi alimpokea mkuu wa serikali mpya ya Libya Abdul Hamid Dbeibeh mnamo tarehe 18/02/2021 ("akampongeza tena uongozi mpya wa Libya na kueleza utayari wake wa kutoa uungaji mkono kamili kwake, na kukubaliwa kubadilishana ziara katika ngazi ya viongozi wa utendaji na kushauriana kuhusu sekta zote". Dbeibeh alisema "Libya ikiwa ni serikali na wananchi inatazamia kuanzisha ushirikiano mpana na Misri kwa lengo la kuiga mifano ya mafanikio kutoka katika uzoefu wake wa kimaendeleo uliopatikana katika miaka iliyopita chini ya uongozi wa Rais"... Alhurra 18/02/2021).
Msimamo wa nchi tatu za Maghreb "Morocco, Algeria na Tunisia" ambazo ni miongoni mwa nchi za kikanda zenye ushawishi nchini Libya, zilitangaza kuunga mkono mamlaka mpya ya utendaji nchini Libya. Mfalme wa Morocco alituma uthibitisho wake kwa mkuu wa Baraza jipya la Urais ("msaada wa kawaida wa Morocco kwa hatua na juhudi zote mnavyofanya ili kukabiliana na changamoto zinazoikabili Libya ili kufanikisha hatua hii nyeti.. na alimpongeza Mohammad Menfi kwa imani aliyoipata ili kuitumikia nchi yake katika hatua hii muhimu ya mpito"... Anadolu 31/03/2021). Waziri wa mambo ya nje wa Tunisia Othman Jerandi na mwenzake wa Algeria Sabri Boukadoum walikutana tarehe 01/04/2021 nchini Tunisia na kujadili masuala kadhaa ya kimataifa na kikanda haswa faili la Libya na kusisitiza ("umuhimu wa kuunga mkono mamlaka mpya ya utendaji ili kufanikisha mkondo wa kisiasa wa Libya kuelekea uchaguzi ujao kwa namna itakayohifadhi umoja wa nchi hii ndugu na ulinzi wake"... Anadolu 02/04/2021). Waziri wa mambo ya nje wa Algeria alikuwa amesisitiza upinzani wa nchi yake dhidi ya "uwepo wa vikosi vyovyote vya kigeni kwenye ardhi ya Libya". Alisisitiza katika taarifa kwa vyombo vya habari "umuhimu wa kuhakikisha usalama nchini Libya kupitia kuunganisha taasisi za usalama"... Independent Arabia, 20/03/2021).
Nchi hizi tatu zenye ushawishi katika ulingo wa Libya kwa niaba ya Wazungu na haswa Uingereza zililazimika kuitambua mamlaka ya utendaji iliyoundwa na Marekani nchini Libya kama zilivyofanya nchi zinazofanya kazi kwa niaba yake, na ili kujipa nafasi katika hatua hii ya mpito kufanya kazi ya kuunga mkono vibaraka wa Ulaya. Hii ni kwa sababu mafanikio ya Marekani nchini Libya na kujikita kwake humo inamaanisha upanuzi wake kuelekea Afrika Kaskazini kufikia nchi hizo na kutishia vibaraka wanaofuata Wazungu na haswa Uingereza. Hii ni mara ya kwanza kwa Marekani kuingia katika nchi mojawapo ya Afrika Kaskazini tangu miongo mingi...
Misimamo ya nchi za Ulaya: Hakuna nchi yoyote ya Ulaya iliyoonyesha misimamo hasi dhidi ya mamlaka mpya ya utendaji nchini Libya, na misimamo yao ni kama ifuatavyo:
1- Rais wa Baraza la Ulaya Charles Michel alitembelea Tripoli na kukutana na Menfi na Dbeibeh tarehe 04/04/2021. Alitangaza kwenye akaunti yake ya Twitter ("kusimama kwa Umoja wa Ulaya upande wa serikali mpya ya Libya na kuipatia uungaji mkono ili kuhifadhi umoja wake, mamlaka yake na kufikia ustawi". Hii inachukuliwa kuwa ziara ya kwanza ya afisa wa Ulaya baada ya kuundwa kwa serikali mpya ya umoja wa kitaifa. Alisema katika mkutano na waandishi wa habari "Tunataka kuwaunga mkono ili mjenge nchi yenu lakini kwa masharti, ni lazima mamluki na askari 'wa kigeni' wote waondoke nchini, tunahamasisha uchaguzi katika wakati wake uliopangwa na tunataka kuwaunga mkono zaidi. Utulivu, usalama na uhamiaji ni mada muhimu"... Anadolu 04/04/2021). Mwakilishi mkuu wa sera za kigeni na usalama katika Umoja wa Ulaya, Josep Borrell, alisema ("Uwepo wa kijeshi na mtiririko wa mamluki kwenye ardhi ya Libya uliongezeka mwaka uliopita", akiona kuwa "misheni ya Irini ilipata matokeo dhahiri katika kufuatilia ukiukwaji wa vikwazo vilivyowekwa kwa Libya, jambo lililochangia hatua chanya zilizofikiwa na Walibya kwa kuunda serikali ya umoja wa kitaifa". Umoja wa Ulaya uliongeza siku chache zilizopita muda wa operesheni ya baharini ya "Irini" ya kufuatilia pwani ya Libya kwa miaka miwili zaidi hadi mwaka 2023. Independent Arabia, 20/03/2021).
2- (Mawaziri wa mambo ya nje wa Italia, Ufaransa na Ujerumani waliwasili leo Alhamisi katika mji mkuu wa Libya, Tripoli, kama sehemu ya misheni ya Ulaya inayolenga kufungua njia za mazungumzo na serikali mpya... Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Heiko Maas alisema alipowasili Tripoli "Maendeleo yaliyoshuhudiwa nchini Libya ni mojawapo ya nukta chache angavu katika sera za kigeni wakati wa mwaka uliopita. Aliongeza kuwa Walibya wanapoendesha mustakabali wao kwa mikono yao wenyewe mara nyingine tena, hapo ndipo usitishaji vita utageuka kuwa amani na maridhiano ya kweli", akisisitiza juu ya "ufuatiliaji wa mchakato wa kuzuia silaha kwa pande zote". Alisisitiza kuwa "kuondolewa kwa vikosi vya kigeni na mamluki ni sharti la msingi kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi ujao"... Al Jazeera Net, 25/03/2021).
Kwa misimamo hii yote ya Ulaya ambayo Uingereza haikuwepo, inaonekana wazi kuwa Ulaya inakubali kwa sharti suluhisho hili la Marekani nalo ni kuhakikisha kuondoka kwa vikosi vya kigeni kutoka Libya, na haswa vile vya Uturuki na Urusi. Hasa ikizingatiwa kuwa Ulaya ilikuwa inatambua ukubwa wa mvurugano wa sera zake unaosababishwa na uwepo wa Uturuki na Urusi nchini Libya na utata unaotokana na hilo, na misheni yake ya baharini "Irini" ilikuwa ikifuatilia ndani na nje ya Libya.
Ama msimamo wa Uingereza ulichanganyikana na mvurugano na ujanja kwa wakati mmoja:
1- (Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson, siku ya Ijumaa, alifanya mazungumzo ya simu na mwenzake wa Libya Abdul Hamid Dbeibeh, akimpongeza kwa uteuzi wake, na alisisitiza uungaji mkono wa Uingereza kwa mchakato wa kisiasa nchini Libya, kulingana na kile kilichoripotiwa na shirika la Anadolu... Aliongeza "Walikubaliana kubaki katika mawasiliano ya karibu katika miezi ijayo wakati serikali ya mpito ikijiandaa kwa uchaguzi wa kitaifa mwishoni mwa mwaka huu"... Middle East Monitor, 12/02/2021). Hii ilikuwa baada ya zaidi ya wiki moja tangu kuchaguliwa kwa Dbeibeh, jambo linaloashiria mvurugano wake...
2- Katika maoni ya Johnson kuhusu pendekezo la Jordan kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa la kuondoa vikwazo vya uuzaji wa silaha nchini Libya, (Waziri wa mambo ya nje wa Uingereza, Philip Hammond, wakati wa ziara yake mjini Madrid alisema: "Tatizo ni kwamba hakuna serikali nchini Libya inayofanya kazi vizuri na inayodhibiti ardhi yake. Hakuna jeshi la Libya ambalo jumuiya ya kimataifa inaweza kuliunga mkono kwa ufanisi". Hammond aliongeza: "Sharti la kwanza lazima liwe kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa, kisha jumuiya ya kimataifa lazima iungane haraka karibu na serikali hiyo na kuhakikisha kuwa ina njia za kukabiliana na ugaidi unaosababishwa na wanamgambo". Sky News Arabic, 20/02/2021). Ni wazi kutokana na maneno yake kuwa Uingereza haikuwa katika picha ya mipango ya Marekani ambayo ilikuwa imeshazalisha uchaguzi wa rais wa Baraza la Urais na mkuu wa serikali ya umoja wa kitaifa... na huu ni mvurugano mwingine!
3- Kufuata kwake Marekani baada ya kuhisi kushindwa kuishinda Marekani nchini Libya kwa wakati huu. Kwa hivyo, katikati ya mkondo mkubwa unaounga mkono mchakato wa kisiasa ambao sasa unaongozwa na Marekani na haraka ya Marekani katika utekelezaji, (Balozi wa Marekani Richard Norland aliona katika tweet yake kupitia Twitter kuwa kura ya Bunge ya kutoa imani kwa serikali mpya ya mpito "imekuwa ikitakiwa kwa haraka ili iweze kuanza majukumu yake", akiashiria kuwa "kuna haja ya kuchukuliwa kwa hatua za haraka na viongozi wa Libya kufadhili mageuzi yanayohitajika katika sekta ya umeme, na nyanja nyingine kuu". Asharq Al-Awsat 07/03/2021). Balozi wa Uingereza katikati ya mkondo huu, kulingana na chanzo hicho hicho, alilazimika kutweet kuelekea kwenye tamko la Marekani (Nicholas Hopton, balozi wa Uingereza nchini Libya, alijiunga na orodha ya wanaotaka kufanyika kwa kikao cha kutoa imani kwa serikali ya Dbeibeh, na alisema katika taarifa yake fupi kupitia Twitter, jioni ya juzi, kwamba ni muhimu kikao cha Bunge kifanyike hivi karibuni kupigia kura ya imani matokeo ya Jukwaa la Mazungumzo ya Kisiasa la Libya huko Geneva, na kuunga mkono Libya katika njia ya kuelekea mustakabali bora).
4- Kutokana na haya yote inabainika kuwa Uingereza imekuwa katika dhiki kubwa mbele ya maendeleo yaliyofanywa na diplomasia ya Marekani na mjumbe wa Umoja wa Mataifa Williams na kwamba hakuwa na lingine isipokuwa kwenda na mkondo. Hivyo iliwaagiza wafuasi wake mjini Tripoli kukabidhi madaraka kwa serikali ya Dbeibeh kwa amani. Hii inawakilisha kushindwa kwa kisiasa kwa Uingereza nchini Libya ambayo haikuweza yeye wala wafuasi wake kurekebisha hali hiyo si kupitia mazungumzo ya Bouznika nchini Morocco wala kupitia kuzuia upigaji kura na kile mjumbe wa Umoja wa Mataifa Stephanie Williams alichokiita "fedha chafu za kisiasa". Alisema: ("Wale wanaojaribu kutoa fedha kwa washiriki katika mazungumzo wataorodheshwa kama wahujumu wake kadhalika uchunguzi utafunguliwa kuhusu taarifa za kutoa rushwa na kununua kura" na akaashiria kuwa "kuna mwongozo wa maadili kuhusu uingiliaji wa fedha chafu za kisiasa"... Asharq Al-Awsat 17/11/2020) na mashaka haya ya fedha chafu ni ishara ya nafasi ya nchi ya Imarati na majaribio yake ya kushawishi uchaguzi wa wajumbe wa jukwaa la mazungumzo la Libya (Al Jazeera Net, 16/11/2020).
Tatu: Na ama kuhusu jinsi Marekani ilivyofanikiwa kunyakua usukani wa Libya kutoka mikononi mwa Uingereza, hilo haliwezi kueleweka isipokuwa kulingana na ukweli ufuatao:
1- Ushawishi ndani ya Libya: Kwa kuisha kwa kibaraka wa Uingereza Gaddafi mnamo mwaka 2011, vizuizi vilivunjika mbele ya Marekani na ikapata ushawishi nchini Libya. Ushawishi huu uliendelea kukua ambapo udhibiti wa kibaraka wa Marekani Haftar upande wa mashariki mwa Libya ulikuwa ishara kuwa Marekani inamiliki nusu ya Libya. Kisha John Bolton, mshauri wa usalama wa taifa katika utawala wa Trump, aliruhusu shambulio la Haftar dhidi ya Tripoli mwaka 2019, kwa uungaji mkono wa Rais wa Marekani wakati wa mazungumzo yake na Haftar. Marekani ilitangaza kukataa kwake mswada wa azimio uliowasilishwa na Uingereza tarehe hiyo wa kusitisha kampeni ya Haftar dhidi ya Tripoli. Hata hivyo, kampeni hii ilifeli na aliondolewa mbali na Tripoli na alikuwa karibu kuanguka kama si Uturuki, ambayo ilitangaza uungaji mkono wake kwa serikali ya Tripoli inayoongozwa na Sarraj, kusitisha uungaji mkono wake kwa ajili ya kuingia Sirte na Jufra, ngome za kimkakati za Haftar ambazo kama zingeanguka mikononi mwa serikali ya Sarraj basi Haftar angeanguka. Uturuki ilimtaka Sarraj kusimama na kufanya mazungumzo...
Marekani ilitaka kuifanya serikali ya Sarraj iwe kati ya machaguo mawili: Kwanza ni kuifanya iwe mateka wa uungaji mkono wa Uturuki ili ijiangukie mikononi mwa Erdogan ambapo Uturuki itaiungulia kamba zake za Ulaya. Pili ni Uturuki kuweza kupenya katika makundi ya "Kiislamu yenye msimamo wa kati" ambayo yanaunda uti wa mgongo wa nguvu mjini Tripoli na Misrata na kuwafanyia senario ya Syria kwa kuzifanya milisheni hizo kuwa mawakala wake zinazofuata amri zake. Jambo hili linapelekea kuondoa nguvu katika uti huu mgongo imara wa serikali ya Sarraj na hivyo kuzuia Uingereza kufaidika na uti huo, hasa kwa kuwa makundi hayo mioyo yao imejawa na mapenzi kwa Erdogan! Inavyoonekana mambo yote mawili yamefanikiwa kwa Marekani kwa pamoja kwa kiasi kinachokubalika ingawa si kwa ukamilifu. Kinachoashiria hilo ni urahisi wa mawasiliano yaliyokuwa yakifanywa na mjumbe wa Umoja wa Mataifa Williams na wakuu wa manispaa, taasisi za vijana na kijeshi bila tofauti kati ya mashariki mwa Libya inayofuata Marekani na magharibi yake inayofuata Uingereza hadi siku hizo. Yaani, juhudi za Marekani za kuchukua uongozi katika mchakato wa kisiasa zilikwenda kwa vikwazo vichache kwa sababu Uturuki ilikuwa ikiitengenezea mazingira zaidi upande wa magharibi mwa Libya, na matokeo yake ni kwamba ushawishi wa Marekani nchini Libya ulikuwa ukiongezeka kwa gharama ya kupenya upande wa magharibi wakati ushawishi wa Uingereza na Ulaya ulikuwa ukipungua hata katika eneo la magharibi.
Sasa Marekani imetimiza inachotaka kwa kutoa kundi jipya la uongozi wa Baraza jipya la Urais na serikali mpya. Kwa hivyo, si jambo la ajabu kupungua kwa utegemezi wa Marekani kwa Haftar isipokuwa kwa kiasi kinachohitajika kumtumia kama chombo cha shinikizo kwa wanasiasa kutekeleza amri zake, na labda jambo lake litaisha ikiwa mafanikio yake ya kisiasa yataendelea, hasa kwa kuwa hajapewa kazi yoyote katika serikali mpya ya mpito naye alikuwa akitamani kuwa waziri wa ulinzi humo au mkuu wa jeshi, lakini mkuu wa serikali mpya amebaki na nafasi ya ulinzi kwake na Baraza la Urais limebaki na nafasi ya amiri jeshi mkuu.
2- Mabadiliko ya utawala nchini Marekani: Kuja kwa utawala wa Biden na kushindwa kwa utawala wa Trump kulikuwa na athari kubwa katika kuharakisha Marekani kunyakua usukani wa Libya kutoka mikononi mwa Uingereza. Licha ya kuwa utawala wa Biden umechuma matunda ya kile ambacho utawala wa Trump ulipanda ndani ya Libya, lakini kubadilika kwa utawala nchini Marekani kulikuwa na maamuzi katika kuharakisha mabadiliko nchini Libya. Hivyo, uchaguzi wa jukwaa la mazungumzo la Libya kwa wakuu wa Baraza la Urais na serikali ya umoja wa kitaifa ulikuja baada ya takriban wiki mbili za Biden kuchukua urais mjini Washington, na kuundwa kwa serikali ya Libya kulikuja baada ya takriban miezi miwili ya kuchukua kwake urais. Athari ya mabadiliko katika utawala wa Marekani ilikuwa kama ifuatavyo:
a- Kurejea kwa washirika na kuwatumia dhidi ya China na Urusi:
Utawala wa Biden ulitangaza kuwa umerejea kwa washirika wake wa Ulaya baada ya mivutano ya utawala wa Trump, (Biden akiwa na makamu wake Kamala Harris alisema wakati wa hotuba fupi katika makao makuu ya wizara ya mambo ya nje kuwa "Amerika imerejea na diplomasia imerejea. Sputnik ya Urusi, 04/02/2021), na kauli mbiu ya Biden "Amerika imerejea" ikawa mbadala wa kauli mbiu ya Trump "Amerika kwanza". Jambo ambalo waziri wa mambo ya nje wa Marekani alikariri mjini Brussels, akisema: (Tulitaka kuja hapa tukiwa na dhamira kuu nayo ni: kuthibitisha tena ahadi yetu kwa muungano wa NATO, miungano yetu, na ushirikiano wetu na Umoja wa Ulaya na washirika wetu wakuu... Nakariri: kwamba Amerika imerejea kwa upande wa kushikamana na miungano yake na ushirikiano wake. Euronews Arabic, 26/03/2021). Marekani inarejea kwa washirika wake wa Ulaya kwa ajili ya kuwatumia dhidi ya China na dhidi ya Urusi, na hii ina mwangwi mkubwa katika mgogoro wa Libya. Kwa upande mmoja, suluhisho la kisiasa la Marekani kwa mgogoro wa Libya litawaacha Wazungu na ushawishi fulani mkabala wa lengo kubwa zaidi ambalo ni kuwaweka upande wake dhidi ya China na Urusi. Jambo ambalo matamshi ya Marekani yanaliweka wazi: (Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken alijadili na mwenzake wa Italia Luigi Di Maio leo Jumanne mafaili ya China, Afghanistan na Libya, wakati wa mkutano wa mawaziri wa mambo ya nje wa nchi za NATO mjini Brussels. Mwishoni mwa mkutano huo, msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Marekani, Ned Price, alieleza kuwa "pande hizo mbili zilibadilishana maoni kuhusu matatizo yanayowakilishwa na China na mustakabali wa NATO nchini Afghanistan na njia bora zaidi za kuunga mkono mageuzi ya kisiasa nchini Libya". Kulingana na msemaji huyo, mawaziri wa ulinzi wa nchi hizo mbili walikubaliana kuendelea kufanya kazi kati ya Washington na Roma kuhusu matatizo ya kimataifa na kueleza kuunga mkono kwao kuendeleza "ushirikiano wa karibu zaidi kati ya Marekani na Umoja wa Ulaya". RT, 23/03/2021).
Kwa haya yote inabainika kuwa mabadiliko ya utawala nchini Marekani yalikuwa sababu ya maamuzi katika kuharakisha mabadiliko ya kisiasa nchini Libya kwa manufaa ya Marekani...
b- Kuzorota kwa mahusiano ya Ulaya na Uingereza baada ya kutekelezwa kwa "Brexit": Mazungumzo magumu ya Uingereza kujiondoa katika Umoja wa Ulaya kwa makubaliano yalikuwa sababu ya kupanda chuki kati ya Uingereza na nchi za Ulaya. Ubinafsi wa Waingereza ulionekana kwa njia mbaya wakati wa mazungumzo hayo na ukazalisha ukaidi wa Ulaya ambao uko karibu na faini na adhabu. Chuki kati yao imekuwa ndio sifa kuu ya mahusiano ya baada ya Brexit. Hilo lilidhihirika katika kubembeleza kwa Uingereza kwa Uturuki wakati ikipingana na Ufaransa na Ulaya mashariki mwa Mediterania, na lilionekana zaidi katika mgogoro wa chanjo ya korona "AstraZeneca" ya Uingereza na Ulaya. Hii ilipelekea mahusiano ya Uingereza na nchi za Umoja wa Ulaya kuwa katika hali iliyo karibu na mgogoro na mvutano. Kwa hiyo mawaziri wa mambo ya nje wa Ufaransa na Ujerumani walitembelea Libya baada ya kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa wakiwa wameongozana na waziri wa mambo ya nje wa Italia na si waziri wa mambo ya nje wa Uingereza kama ilivyokuwa desturi katika harakati za Ulaya za kimataifa kabla ya Brexit. Hiyo inamaanisha kuwa kuzorota kwa mahusiano ya Uingereza na nchi za Umoja wa Ulaya kumezipelekea hizi za mwisho kufuata Marekani katika mkondo wa suluhisho nchini Libya, hivyo kukosekana kwa uratibu wa Ulaya na Uingereza. Na Ulaya haikusimama na Uingereza ili kuunda kizuizi nchini Libya mbele ya harakati za Marekani, jambo ambalo lilipelekea mwishowe Uingereza kujikuta peke yake mbele ya mkondo mkubwa wa Marekani, hivyo Uingereza ikainama mbele ya wimbi la Marekani na kuwaomba vibaraka wake kukabidhi madaraka mjini Tripoli.
Nne: Kutokana na hapa inabainika kuwa Marekani imeshinda duru ya sasa katika mzozo na Wazungu juu ya nchi ya Kiislamu inayochukuliwa kuwa nchi tajiri zaidi kwa mafuta barani Afrika. Na tamaa yake inazidi katika kupata uwekezaji humo na kupora utajiri wake. Ilikuwa imetangaza kuunga mkono Haftar kwa matumaini kuwa angemhakikishia mtiririko wa mafuta ikiwa angetwaa madaraka katika jaribio lake la kuiteka Tripoli mnamo Aprili 2019, kama alivyotaja rais wake wa zamani Trump ambaye alifanya mazungumzo ya simu naye yaliyotangazwa tarehe 19/04/2019 ambapo ilikuwa wazi (Trump anasisitiza nafasi "muhimu" ya Haftar katika kupambana na ugaidi na kuhakikisha mafuta... Deutsche Welle 19/04/2019), kisha hatua zake zikafuata hadi ikawa inadhibiti Baraza la Urais na mkuu wa serikali... Pamoja na hayo, mzozo wa Marekani na Ulaya utabaki bila kusimama katika mustakabali unaoonekana, kwani Uingereza ina uzoefu wa kisiasa wa zamani nchini humo, na nchi nyingine za Ulaya kama Ufaransa na Italia zina maslahi na uwepo kupitia kampuni zinazowekeza...
Na ni jambo la kuumiza kwa nchi hii ya Kiislamu kuwa kama nchi nyingine za Kiislamu uwanja wa mzozo kati ya wakoloni kwa ajili ya kupanua ushawishi na kupora utajiri! Wakati ambao watawala katika nchi za Waislamu wamefungamana na mkoloni huyu au yule, na hawafikirii kujikwamua kutoka katika fungamano hili la udhalili! Hakika ni wajibu kwa Umma na haswa waaminifu miongoni mwa wanawe kuwa mstari wa mbele katika kazi ya kisiasa na kutoa juhudi zote katika kuwabadilisha hawa watawala, na kuziangusha nchi za kigeni zinazowaunga mkono, na kuanzisha nchi inayotekeleza sheria ya Mwenyezi Mungu na kuibeba kwa ulimwengu na kurejesha utajiri kwa wenyewe na kuugawanya kwa wana wa Umma ili asibaki ndani yake maskini wala mhitaji... Hiyo ni dola ya Khilafah Rashidah kwa njia ya Utume ambayo Mwenyezi Mungu Subhanahu wa Ta’ala ameahidi:
وَعَدَ اللَّهُ الَّذِينَ آمَنُوا مِنْكُمْ وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ لَيَسْتَخْلِفَنَّهُمْ فِي الْأَرْضِ كَمَا اسْتَخْلَفَ الَّذِينَ مِنْ قَبْلِهِمْ
"Mwenyezi Mungu amewaahidi wale walioamini miongoni mwenu na wakatenda mema, kwamba atawafanya makhalifa katika ardhi kama alivyowafanya makhalifa wale waliokuwa kabla yao." (QS. An-Nur [24]: 55)
Na akaitolea bishara Mtume wa Mwenyezi Mungu ﷺ baada ya huu utawala wa kidikteta ambao tunaishi ndani yake kwa kusema kwake Swala na salamu za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake:
ثُمَّ تَكُونُ مُلْكاً جَبْرِيَّةً فَتَكُونُ مَا شَاءَ اللَّهُ أَنْ تَكُونَ ثُمَّ يَرْفَعُهَا إِذَا شَاءَ أَنْ يَرْفَعَهَا ثُمَّ تَكُونُ خِلَافَةً عَلَى مِنْهَاجِ النُّبُوَّةِ ثُمَّ سَكَتَ
"Kisha utakuwepo utawala wa kidikteta (wa kulazimisha), na utakuwepo kwa muda anaotaka Mwenyezi Mungu uwepo, kisha Atauondoa Atakapotaka kuuondoa, kisha itakuwepo Khilafah kwa kufuata njia ya Utume, kisha akanyamaza." (Imepokelewa na Ahmad kutoka kwa Nu’man bin Bashir)
Mnamo tarehe ishirini na tano ya Sha'ban 1442 H 07/04/2021 M