Jibu la Swali
Swali: Mnamo tarehe 07/04/2022, nchini Saudi Arabia, kiliundwa Baraza la Uongozi wa Rais nchini Yemen kuchukua nafasi ya Rais Hadi, ambapo alikabidhi mamlaka yake yote kwa baraza hili. Kabla ya hapo, mnamo tarehe 02/04/2022, pande zinazozozana zilikubaliana kusitisha vita nchini Yemen kwa muda wa miezi miwili...
Swali ni: Je, sitisho hilo la vita lilikuwa ni maandalizi kwa ajili ya baraza hili? Na nini dhumuni lake? Kisha kwa nini Wahouthi wanakataa kuliunga mkono baraza hilo ilhali walikubali sitisho la vita na Iran pia ikalikubali?!
Jibu: Ili jibu liwe wazi kuhusu maswali haya, tunapitia mambo yafuatayo:
Kwanza: Uhalisia wa sitisho la vita, kuundwa kwa baraza na mamlaka yake:
1- (Mjumbe Maalumu wa Umoja wa Mataifa nchini Yemen, Hans Grundberg, alitangaza kuwa sitisho la vita la miezi miwili linaloweza kuongezwa limeanza kutekelezwa jioni ya Jumamosi, tarehe 02/04/2022, siku ya kwanza ya mwezi wa Ramadhani. Umoja wa Mataifa na Marekani zilikaribisha sitisho hilo la ghafla na kutoa wito wa kuongezwa kwake. Grundberg aliwashukuru Wahouthi na serikali inayotambulika kimataifa kwa kufanya kazi naye "kwa nia njema na kwa kutoa makubaliano ya lazima ili kufikia mkataba huu". Aliona kuwa "sitisho la vita ni hatua ya kwanza iliyochelewa kwa muda mrefu". Grundberg alisisitiza kuwa ataendelea kufanya kazi katika kipindi cha miezi miwili "kwa lengo la kufikia usitishaji wa kudumu wa mapigano"... Kwa upande wake, Rais wa Marekani Joe Biden alikaribisha siku ya Ijumaa sitisho la vita nchini Yemen ambalo alilitaja kama "pumzi ambayo watu wa Yemen wameingojea kwa muda mrefu" lakini akaliona kama "haingatoshi". Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson alikaribisha tangazo la Ijumaa na kuhimiza "kufanya kazi kuelekea suluhu ya kudumu ya kisiasa". Johnson alisema kupitia Twitter: "Sasa tuna fursa adhimu ya kuleta amani hatimaye na kumaliza mateso ya kibinadamu"... France 24/AFP 02/04/2022).
2- Wakati huohuo mazungumzo kuhusu sitisho la vita yakiendelea, mkutano ulifanyika Riyadh mnamo tarehe 30/03/2022 na kudumu kwa wiki moja, ukijumuisha takriban haiba 800 za Kiyemen chini ya udhamini wa nchi za Ghuba na wawakilishi wa kigeni kutoka Umoja wa Mataifa, Marekani, Uingereza na nyinginezo. Mwishoni mwa mkutano huo, Rais wa Yemen Abd Rabbo Mansour Hadi anayeishi Riyadh, alitangaza tarehe 07/04/2022 kuundwa kwa Baraza la Uongozi wa Rais na kulikabidhi mamlaka yake yote, na kumfuta kazi makamu wake Ali Mohsen al-Ahmar. Runinga ya Yemen ilitangaza tamko la Hadi ambapo alisema: ("Kwa mujibu wa tangazo hili, Baraza la Uongozi wa Rais linaundwa ili kukamilisha utekelezaji wa majukumu ya kipindi cha mpito, na ninalikabidhi Baraza la Uongozi wa Rais, kwa mujibu wa tangazo hili, mamlaka yangu yote yasiyoweza kutenguliwa kulingana na katiba, mpango wa Ghuba na utaratibu wake wa utekelezaji". Pia aliliagiza "kufanya mazungumzo na Wahouthi kwa ajili ya usitishaji vita wa kudumu katika maeneo yote ya jamhuri na kuketi kwenye meza ya mazungumzo ili kufikia suluhu ya mwisho na ya kina ya kisiasa inayojumuisha kipindi cha mpito kinachoiondoa Yemen kutoka hali ya vita kwenda hali ya amani"). Hivyo, baraza hilo limepewa jukumu la kufanya mazungumzo na Wahouthi ili kupata suluhu ya mwisho...
3- Mamlaka ya baraza la rais yanajumuisha ("kusimamia dola kisiasa, kijeshi na kiusalama katika kipindi chote cha mpito na kufuata sera ya nje yenye usawa inayolinda mamlaka ya dola na mipaka yake". Mamlaka ya mwenyekiti wa baraza hilo, Rashad al-Alimi, yanajumuisha "uamiri mkuu wa vikosi vya ulinzi, kuiwakilisha jamhuri ndani na nje ya nchi, kuteua magavana wa mikoa, wakurugenzi wa usalama, majaji wa mahakama kuu, gavana wa benki kuu, kuanzisha ujumbe wa kidiplomasia, na kutangaza hali ya hatari na uhamasishaji mkuu"... Al-Ain News 11/04/2022). Baraza hili linajumuisha wajumbe 8 wakiwemo mwenyekiti wake Rashad al-Alimi, ambaye ni waziri wa zamani wa mambo ya ndani na mshauri wa Rais wa Yemen, na wajumbe ambao ni Aidarus al-Zoubaidi (mwenyekiti wa Baraza la Mpito la Kusini anayekaribiana na Imarati), Tariq Saleh (mpwa wa rais wa zamani Ali Abdullah Saleh), Sultan Ali al-Arada (Gavana wa Marib anayefuata chama cha Islah), Abdullah al-Alimi Bawazir (mshirika wa chama cha Islah na mkurugenzi wa ofisi ya Hadi), Abdulrahman Abu Zara'a al-Mahrami (Kamanda wa Brigedi za Giant), Faraj al-Bahsani (Gavana wa Hadramaut), na Othman Majli. Inaonekana kuwa wajumbe wote wa Baraza la Uongozi wa Rais ni wale wanaoungwa mkono na Imarati na kundi la Rais Hadi mwenyewe, hivyo uamuzi wenye nguvu ndani ya baraza hilo utakuwa unafuata Uingereza. Baraza limekusanya wawakilishi wa nguvu za Kusini ili wawe washirika katika mazungumzo na katika kutia saini makubaliano yoyote yatakayofikiwa na Wahouthi, ili kusiwe na yeyote anayeweza kupinga siku zijazo. Pia ilitangazwa kuendelea kwa mamlaka ya bunge na kuhuisha imani kwa serikali. Inaonekana kuwa lengo ni pande zote kutia saini makubaliano yoyote yajayo ili kuyapa kundi la Houthi uhalali na kulifanya kuwa sehemu ya muundo wa kisiasa na usalama nchini.
Pili: Miitikio ya kimataifa na kikanda:
1- Saudi Arabia ilikaribisha sitisho la vita na uamuzi huu na kutangaza kutoa msaada wa kiuchumi wa dola bilioni 3, zikiwemo dola bilioni mbili kwa ushirikiano na Imarati kusaidia benki kuu. Baada ya hapo, mnamo tarehe 07/04/2022, Mrithi wa Kiti cha Ufalme wa Saudi, Mohammed bin Salman ("alimpokea Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Rais Rashad al-Alimi na wajumbe wa baraza hilo na kuelezea uungaji mkono wake na matumaini yake kwamba kuundwa kwake kutachangia kuanza kwa ukurasa mpya nchini Yemen utakaoindoa katika vita kuelekea amani na maendeleo"... Al-Arabiya 07/04/2022). Khalid bin Salman, Naibu Waziri wa Ulinzi, alisema kupitia akaunti yake ya Twitter mnamo tarehe 09/04/2022: ("Hatua ya kishujaa na ya kihistoria iliyochukuliwa na Rais wa Yemen Abd Rabbo Mansour Hadi katika kukabidhi mamlaka kwa Baraza la Uongozi wa Rais, ambayo imeungwa mkono na wasomi na makundi ya kisiasa na kijamii ya Yemen na kuungwa mkono na jamii ya kimataifa, inaweka msingi wa hatua muhimu na ya maamuzi ya kufikia amani, usalama na utulivu kwa Yemen na eneo hili". Alisema: "Tunasisitiza kuendelea kwa muungano wa kuunga mkono uhalali nchini Yemen kusaidia baraza katika nyanja zote ikiwemo msaada wa kijeshi hadi kufikia suluhu ya kisiasa itakayomaliza mgogoro"). Saudi Arabia inataka kujiondoa kwenye mizigo ya vita ambayo imeigharimu sana na kuionyesha kuwa dhaifu na isiyoweza kufikia malengo yake. Baraza hili lililoundwa na Hadi, ingawa ni la wafuasi wa Uingereza, lakini lengo la kuanzishwa kwake ni kufanya mazungumzo na Wahouthi na kutoa makubaliano ili kufanikisha mazungumzo hayo.
2- Kuhusu Imarati, yenyewe (ilikaribisha uamuzi wa rais wa zamani wa Yemen Abd Rabbo Mansour Hadi wa kuunda Baraza la Uongozi wa Rais ili kukamilisha majukumu ya kipindi cha mpito... ikielezea matumaini yake kuwa hatua hii itachangia kufikia suluhu ya kina ya kisiasa kati ya pande za Yemen... Imarati ilikaribisha wito wa Saudi Arabia kwa Baraza la Uongozi wa Rais kuanza mazungumzo na Wahouthi chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa ili kufikia suluhu ya mwisho na ya kina ya kisiasa... Al-Arabiya 08/04/2022).
3- Ama kundi la Houthi, msimamo wao ulikuwa wa kijanja! Walikubaliana na sitisho la vita na walikuwa sehemu muhimu yake, na walimpokea mjumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Yemen, Hans Grundberg huko Sana'a kwa muda wa siku 3 ambapo alikutana na uongozi wa Baraza la Kisiasa la kundi la Ansar Allah (Houthi) na kujadili utekelezaji na uimarishaji wa sitisho la vita. Hata hivyo, msimamo wao kuhusu Baraza la Uongozi la Yemen ulikuwa tofauti! Kundi la Houthi lilitangaza kukataa maamuzi ya hivi karibuni ya Hadi. Msemaji wao, Mohammed Abdul Salam, alisema kupitia akaunti yake ya Telegram baada ya hapo: (Hatua hizi zilizochukuliwa na muungano wa uchokozi hazina uhusiano na Yemen wala maslahi yake wala amani, bali zinasukuma kuelekea mapigano kwa kuunganisha tena wanamgambo waliotawanyika na wanaozuana katika muundo mmoja unaotumikia maslahi ya nje na nchi za uchokozi). Kundi la Houthi lilialikwa kushiriki katika mkutano huo lakini likakataa kuhudhuria kwa sababu ulifanyika Saudi Arabia, na likataka ufanyike katika nchi isiyofungamana na upande wowote. Hii ina maana kwamba kundi la Houthi litashiriki katika mikutano ijayo na kufanya mazungumzo na baraza hilo hata kama sasa wanakataa uamuzi wa kuundwa kwa baraza na wajumbe wake. Kukataa kwao huku kunaonekana kuwa na lengo la kuimarisha msimamo wao katika mazungumzo yajayo. Wao wameunganishwa moja kwa moja na Iran ambayo inafuata mzunguko wa Marekani. Na walikubali sitisho la vita mwanzoni mwa mwezi wa Ramadhani kwa muda wa miezi miwili linaloweza kuongezwa, na sitisho hili liliandaliwa kama maandalizi ya baraza hilo na utangulizi wa mazungumzo!
4- Msimamo wa Iran: (Tehran ilisisitiza kukaribisha kwake sitisho la vita na umuhimu wa kufanya mazungumzo ya Kiyemen mbali na uingiliaji wa nje. Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Hossein Amir-Abdollahian alisema kuwa nchi yake inakaribisha usitishaji vita nchini Yemen na inasisitiza ulazima wa kuondoa mzingiro dhidi ya Wayemen na kuanzisha mazungumzo ya Kiyemen kwa Kiyemen mbali na uingiliaji wa kigeni... Al Jazeera 14/04/2022) na Wahouthi waliwafuata katika hilo.
5- Msimamo wa Marekani: Marekani ilikaribisha tangazo la kuundwa kwa Baraza la Uongozi wa Rais nchini Yemen:
a- (Taarifa ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken ilisema: "Marekani inaunga mkono matamanio ya watu wa Yemen kuelekea serikali yenye ufanisi, kidemokrasia na uwazi inayojumuisha sauti tofauti kutoka kwa wanasiasa na asasi za kiraia", akiongeza kuwa jambo muhimu zaidi ni kwamba Wayemen wanastahili serikali inayolinda haki na uhuru, sambamba na kuimarisha haki, uwajibikaji na upatanisho... 08/04/2022 sabq.org)
b- Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani Ned Price aliandika kupitia Twitter mnamo tarehe 08/04/2022 taarifa akisema: "Marekani inakaribisha tangazo la kuundwa kwa Baraza la Uongozi wa Rais nchini Yemen".
c- Mjumbe wa Marekani nchini Yemen, Tim Lenderking alitoa hotuba ya ufunguzi katika mkutano wa Riyadh kuhusu Yemen akisema: ("Marekani inaunga mkono pande za Yemen kufikia suluhu ya amani ya kina. Mazungumzo ya Yemen yanawakilisha ahadi ya kimataifa ya kufanya hali kuwa thabiti zaidi"... DPA 30/03/2022). Mjumbe wa Marekani alisema mwishoni mwa mkutano huo: ("Marekani inatarajia Iran kuchukua nafasi nzuri na kubadili mbinu yake nchini Yemen". Alisema "Labda wakati huu muhimu tuliofikia ndio hatua ambayo Iran inaweza kuonyesha sura bora kwa jamii ya kimataifa"... CNN ya Marekani 06/04/2022).
Hivyo basi, Marekani imeunga mkono hatua ya Hadi ya kuachia mamlaka yake kwa baraza hilo, na inasisitiza kuwa Iran ichukue nafasi muhimu nchini Yemen na kisha kuwashirikisha Wahouthi katika utawala, kwani Wahouthi hawawezi kustahimili bila msaada wa Iran.
6- Msimamo wa Uingereza: (Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza Liz Truss alikaribisha siku ya Ijumaa tangazo la Rais wa Yemen Abd Rabbo Hadi la kuunda Baraza la Uongozi wa Rais linalojumuisha wawakilishi wa nguvu mbalimbali za kijamii na kisiasa. Truss, kama ilivyoripotiwa na kanali ya Al-Yaman, alikaribisha tangazo la Saudi Arabia na Imarati la msaada wa dola bilioni 3 kusaidia uchumi wa Yemen... 08/04/2022 alwafd.news). (Richard Oppenheim – Balozi wa Uingereza nchini Yemen – alieleza katika mahojiano maalum na gazeti la Asharq Al-Awsat la London yaliyochapishwa Alhamisi hii, kwamba matokeo ya mazungumzo ya Kiyemen kwa Kiyemen yanayomalizika leo katika makao makuu ya Baraza la Ushirikiano wa Ghuba huko Riyadh, yanaweza kutumika katika mazungumzo ya baadaye chini ya udhamini wa mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa... akibainisha wakati huohuo kwamba mafanikio ya sitisho la vita yapo mikononi mwa pande husika na sio waangalizi. Oppenheim alisisitiza kuwa nchi yake inahimiza mazungumzo yoyote yatakayopelekea kutatua tatizo la Yemen, akionyesha kuwa makubaliano yoyote kati ya Saudi Arabia na Wahouthi yatakuwa msingi wa suluhu ya mwisho ya kisiasa... 07/04/2022 dw.com).
Tatu: Kwa kuzingatia yaliyotangulia, inabainika yafuatayo:
1- Kwamba uingiliaji wa kijeshi wa Saudi Arabia ulioanza mwaka 2015 ulikuwa na lengo – kama Marekani ilivyopanga – la kuwaimarisha Wahouthi na sio kuwaangamiza. Vivyo hivyo, mkutano wa Stockholm uliofanyika kwa shinikizo la Marekani mwaka 2018 uliizuia Imarati na nguvu za Kiyemen zinazoiunga mkono kudhibiti Hudaydah, na kuwalazimisha kurudi nyuma kutoka kusonga mbele kuelekea Sana'a na kuikomboa kutoka kwa Wahouthi kama Uingereza ilivyokuwa ikipanga... Hivyo Uingereza ikaanza kufikiria suluhu ya (muda) pamoja na Marekani, ikamsukuma kibaraka wake Hadi kuchukua hatua hii. Hii inaonekana kutokana na maneno ya balozi wa Uingereza nchini Yemen, Richard Oppenheim, aliyeshiriki katika mkutano huo ambapo alisema: ("Kwamba Wahouthi wanakaribishwa kushiriki katika mijadala na mazungumzo chini ya udhamini wa Baraza la Ghuba, na ni juu yao kuchukua fursa hii... Wahouthi lazima wawe sehemu ya mazungumzo kwa sababu ni sehemu muhimu ya ulingo wa kisiasa wa Yemen"... Asharq Al-Awsat 07/04/2022). Balozi wa Uingereza aliyeiwakilisha nchi yake katika mkutano uliofanyika Riyadh anatangaza mabadiliko yaliyotokea katika msimamo wa Uingereza tangu mwaka 2016. Inaonekana kuwa imeelekea kuwashirikisha Wahouthi kwani haikuweza kuwaangamiza au kuwaondoa Sana'a kupitia vibaraka wake Imarati na nguvu za Kiyemen inayozifadhili.
2- Mjumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Yemen, Hans Grundberg aliwasili tarehe 11/04/2022 kwa mara ya kwanza huko Sana'a tangu achukue nafasi yake miezi 8 iliyopita na kukutana na maafisa wa kundi la Houthi. Taarifa kutoka ofisi yake ilisema ("Ndege ya Grundberg ilitua Sana'a kwa lengo la kuhimiza uongozi wa Houthi kutekeleza na kuimarisha usitishaji vita wa siku 60 katika nchi iliyoharibiwa na vita"... AP 11/04/2022). Katika mwisho wa ziara yake alisema: ("Alijadili na viongozi wa kisiasa (Houthi) huko Sana'a maendeleo ya utekelezaji wa sitisho la vita kwa vipengele vyake vyote na njia za kujenga juu yake kama hatua kuelekea suluhu ya kina ya kisiasa ya mgogoro"... Anadolu 13/04/2022). Hivyo basi mjumbe wa Umoja wa Mataifa atakuwa amewapelekea Wahouthi maamuzi ya mkutano wa mwisho ili kuwaandaa kwa mazungumzo baada ya kuyaondoa mamlaka kutoka kwa Rais Hadi na kuyatoa kwa baraza la rais. (Baraza la Usalama, katika taarifa iliyoitoa kwa kauli moja (nchi 15), lilielezea matumaini yake kwamba kuundwa kwa baraza hilo "kutawakilisha hatua muhimu kuelekea utulivu na suluhu ya kina ya kisiasa inayoongozwa na Wayemen chini ya udhamini wa Umoja wa Mataifa". Na likaliita kundi la Houthi "kushirikiana na kufanya kazi na mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa (Hans Grundberg) katika juhudi zake za kufikia usitishaji wa kina wa mapigano na kufanya mazungumzo ya suluhu ya kina ya kisiasa"... aa.com.tr).
3- Wajumbe wa Baraza la Rais kwa ujumla ni wafuasi wa Uingereza, na mkutano wa kuidhinisha baraza hilo ulidhaminiwa na Saudi Arabia inayofuata Marekani na ulifanyika Riyadh. Licha ya kwamba Wahouthi hawakuhudhuria, lakini Iran na Wahouthi wanaofuata nyayo zake walikubali sitisho la vita ambalo lilikuwa utangulizi wa kuidhinisha baraza hilo. Kisha Marekani na Uingereza zimekubali sitisho hilo na baraza hilo ingawa zilikuwa zikiendesha vita ili kila mmoja afanye mambo ya Yemen peke yake, lakini sasa wao na zana zao za kikanda na mitaa wamekubali sitisho hilo na baraza hilo! Haya yote yanaonyesha kuwa kuna sababu muhimu zilizotokea katika hali ya mambo zilizozifanya Marekani na Uingereza kuacha ukinzani wao wa kila mmoja kutaka kuwa peke yake nchini Yemen, na kisha kuelekea kwenye suluhu ya makubaliano hata kama ni ya "muda" katika hatua hii... Ama kuhusu sababu hizi zinaweza kueleweka kutokana na mabadiliko yaliyotokea katika wiki au miezi ya hivi karibuni ambayo ni kama ifuatavyo:
a- Vita nchini Ukraine na athari zake kwa Marekani na nchi za Ulaya hasa Uingereza, ambapo nchi hizi zimeelekeza umakini wao mkubwa kwenye vita hivyo.
b- Kushambuliwa kwa miundombinu ya sekta ya mafuta ya Saudi Arabia na vikosi vya Sana'a kwa makombora ya masafa marefu (cruise), na athari zake kwa usambazaji wa mafuta duniani, wakati ambao Marekani iliziahidi nchi za Ulaya kufuatia vita vya Urusi nchini Ukraine, kutoa mbadala wa Urusi kwa vyanzo vya nishati barani Ulaya. Na kwa kuwa Saudi Arabia inaweza kusukuma kiasi kikubwa cha mafuta, basi inaweza kuziba sehemu kubwa ya mahitaji ya Ulaya ya mafuta kama mbadala wa mafuta ya Urusi. Kwa upande mwingine ambao sio mdogo, kuongezeka kwa usukumaji wa mafuta wa Saudi Arabia kunafanya kazi ya kudhibiti bei zake sokoni jambo ambalo linaongeza nafasi za kuchaguliwa kwa Chama cha Kidemokrasia katika uchaguzi wa katikati ya muhula wa Bunge mnamo Novemba 2022: (Chanzo rasmi katika Wizara ya Mambo ya Nje kilisema kuwa Riyadh "haitawajibika kwa upungufu wowote wa usambazaji wa mafuta katika masoko ya kimataifa kutokana na mashambulizi inayokumbana nayo". France 24, 25/03/2022). Haya yote yalikuwa yakiisukuma Marekani kutuliza hali kati ya Wahouthi na Saudi Arabia...
c- Marekani kushughulishwa na mzozo na China huko Mashariki ya Mbali na Bahari ya China Mashariki...
d- Kushindwa kwa Hadi kuweka mamlaka yake nchini Yemen ambayo inapitia migogoro mfululizo tangu kuchaguliwa kwake mwaka 2012, jambo ambalo liliathiri utendaji wake...
e- Kisha kuendelea kwa vita hivi kwa takriban miaka saba bila yoyote kati ya pande zinazozozana zinazoongozwa na Marekani na Uingereza kuweza kufikia malengo yake...
f- Hatimaye, mazingira ya sasa ya Marekani na pia mazingira ya Uingereza yamezipelekea kwenye makubaliano haya:
Marekani kwa upande wake inatambua nguvu ya ushawishi wa Waingereza katika tabaka la kisiasa nchini Yemen, na inatambua ushawishi wake kwa baadhi ya makabila ya Kaskazini ambayo yamekusanyika na kupigana na Wahouthi kwa ukali mkubwa huko Marib na kuwazuia kudhibiti kikamilifu Kaskazini mwa Yemen. Na kwamba wanamgambo wanaoungwa mkono na Imarati wamefanikiwa kudhibiti takriban Kusini yote, ikimaanisha kwamba Marekani inaona kuwa Wahouthi hawawezi kudhibiti Yemen yote. Hii inaifanya Marekani ikubali kugawana ushawishi nchini Yemen na Uingereza baada ya kuwa haina kitu cha maana katika ushawishi kabla ya mwaka 2014.
Ama Uingereza, ambayo ilipoteza ushawishi nchini Saudi Arabia kwa kuja kwa Salman na mwanawe madarakani mwaka 2015, na Saudi Arabia ikaanza kufanya kazi kwa maslahi ya Marekani, hivyo zana za Uingereza za kikanda zikawa dhaifu. Uhalisia huu mpya unaifanya Uingereza mbele ya mabadiliko haya makubwa ya kikanda, hasa ikiongezwa na Marekani kupanua nafasi ya Iran katika eneo, kushindwa kurudisha hali ya Yemen chini ya udhibiti wake. Hivyo basi, nayo pia inakubali kugawana ushawishi na Wamarekani nchini Yemen. Kusadiki huku kutoka kwa pande zote mbili (Marekani na Uingereza) kunatengeneza mazingira yanayofaa kwa suluhu ya kisiasa nchini Yemen.
4- Hivyo basi, sitisho la vita na uamuzi huu na kuundwa kwa baraza, yote hayo yamefanyika kwa makubaliano ya Marekani na Uingereza, na vibaraka wanaofuata mkumbo wamefuata makubaliano haya... Isipokuwa kuna jambo ambalo halipaswi kusahaulika: nchi za kikoloni kwa kawaida kila moja hupenda kuwa na ushawishi peke yake katika nchi iliyokoloniwa, na hazikubali makubaliano isipokuwa zikilazimika, hivyo hukubaliana kwa muda kisha kila moja hufanya kazi kwa njia zake za hila kuvuta zulia chini ya mwenzake... Kwa hiyo makubaliano haya kuendelea kwake kutalingana na sababu zilizotajwa hapo juu. Katika hali zote, makubaliano haya sio ya kudumu ambayo Marekani na Uingereza zitafuata, bali mzozo utaendelea kati yao hata kama ni kwa njia zisizoonekana, mpaka mazingira yaliyopelekea makubaliano haya yabadilike na sauti ya mzozo kupanda tena. Mkakati mkuu kwa nchi za kikoloni ni kwamba zinacheza mchezo wa wakati; ikiwa haziwezi kufikia malengo yake ya kuwa na ushawishi peke yake kwa sasa, basi huacha jambo hilo kwa wakati ili kufanya majaribio ya kufikia malengo yake...
5- Yemen ni mahali pa mzozo wa kimataifa kati ya Marekani na Uingereza na zana zao za kikanda na mitaa. Na wanaoumia ni watu wa Yemen kwani wao ndio kuni za mzozo huu na waathirika wake, ambapo umesababisha njaa, umaskini na kuzorota kwa hali katika nyanja zote. Na hakuna mwokozi kwao isipokuwa kumrudia Mwenyezi Mungu na kumtegemea Yeye na kukataa zana hizi zote na mabwana zao, na kufanya kazi na watu wenye ikhlasi ili kusimamisha hukumu ya Mwenyezi Mungu inayodhihirika katika Khilafah ya Rashidah kwa njia ya Utume.
وَمَنْ يَتَّقِ اللَّهَ يَجْعَلْ لَهُ مَخْرَجاً * وَيَرْزُقْهُ مِنْ حَيْثُ لَا يَحْتَسِبُ وَمَنْ يَتَوَكَّلْ عَلَى اللَّهِ فَهُوَ حَسْبُهُ إِنَّ اللَّهَ بَالِغُ أَمْرِهِ قَدْ جَعَلَ اللَّهُ لِكُلِّ شَيْءٍ قَدْراً
"Na anayemcha Mwenyezi Mungu humfanyia njia ya kutokea, na humruzuku kwa namna asiyoitarajia. Na anayemtegemea Mwenyezi Mungu, basi Yeye humtosheleza. Hakika Mwenyezi Mungu anatimiza amri yake. Mwenyezi Mungu amekwisha kiwekea kila kitu kipimo chake." (QS. At-Talaq [65]: 2-3)
19 Ramadhani Mubarak 1443 H 20/04/2022 M