Home About Articles Ask the Sheikh
Uchambuzi

JIBU LA SWALI: UHUSIANO KATI YA MAREKANI NA UCHINA

December 19, 2010
2734

Swali:

Vyombo vya habari vilichapisha hapo jana 16/12/2010 habari mbili zenye kuvutia: Kwanza, ziara ya Waziri Mkuu wa Uchina nchini India akiwa na ujumbe mkubwa wa kibiashara (takriban wafanyabiashara 300), ambapo ziara na mapokezi hayo yaliambatana na hali fulani ya uchangamfu isiyo ya kawaida. Pili, makubaliano ya pande tatu kati ya Korea Kusini, Uchina, na Japani ya kuanzisha sekretarieti ya jumla kati ya nchi hizo tatu; yote haya yakitokea wakati joto la mvutano kati ya Korea mbili likiwa bado halijapoa, kutokana na vitisho vya pande zote kati ya Marekani na Korea Kusini kwa upande mmoja, na Korea Kaskazini kwa upande mwingine, huku kukiwa na uungaji mkono wa kimyakimya wa Uchina kwa Korea Kaskazini. Je, nini maana ya yanayoendelea?

Jibu:

Ili kujibu swali hili, tunapitia yafuatayo:

1- Tangu muongo wa sita wa karne iliyopita, Marekani imekuwa ikihofia kuibuka kwa Uchina kama nguvu ya kimataifa, na imejitahidi kupunguza matamanio ya Uchina katika masuala ya kikanda. Marekani imetumia msururu wa masuala mbalimbali ili kudhibiti ushawishi wa Uchina katika ulingo wa kikanda na kuifanya uongozi wake uendelee kujishughulisha na matatizo madogo madogo ya kikanda. Marekani imetumia mara kwa mara suala la Taiwan na Korea Kaskazini, unyanyasaji wa Uchina dhidi ya makundi ya wachache hususan mamlaka ya ndani ya Tibet, na kuingilia mizozo ya pande mbili kati ya Uchina na Japani kuhusu visiwa vinavyozozaniwa kati ya nchi hizo mbili kama njia ya kuchochea moto katika mazingira ya Uchina. Aidha, Marekani imeizingira Uchina kwa msururu wa kambi zinazoanzia Afghanistan, Asia ya Kati, Pakistan hadi Bahari ya Pasifiki, ikiwemo rasi ya Korea na Japani... Lengo la kambi hizi za kijeshi ni kuizingira Uchina na kuizuia isiibuke kama nguvu ya kijeshi.

2- Pamoja na juhudi za Marekani za kuzuia upanuzi wa kijeshi wa Uchina, Marekani imejitahidi kwa nguvu kujenga uwezo wa kiraia na kijeshi wa India ili kukabiliana na Uchina. Sera hii ilikuwa ikitumiwa na serikali zote nchini India, hata zile zilizokuwa tiifu kwa Uingereza na siyo kwake tu kama serikali ya Chama cha Congress. Obama alisema akizungumza mbele ya kikao cha pamoja cha Bunge la India: "Nimesimama mbele yenu leo kwa sababu nina imani kuwa maslahi ya Marekani na maslahi tunayoshiriki na India ndiyo sababu bora zaidi ya ushirikiano... Marekani haikaribishi tu India kama nguvu ya kimataifa, bali tunaunga mkono hilo kwa dhati, na tunaunga mkono ustawi wa pamoja, kudumisha amani na usalama, na kuimarisha utawala wa kidemokrasia na haki za binadamu; huu ndio wajibu wa uongozi. Ushirikiano huu wa kimataifa kati ya Marekani na India unaweza kuleta maendeleo katika karne ya 21, na sasa tuko tayari kuanza utekelezaji wa makubaliano ya nyuklia ya kiraia... Tunahitaji kuanzisha ushirikiano katika sekta za teknolojia ya hali ya juu kama vile ulinzi na anga ya kiraia." (Marekani yaunga mkono India kama nguvu ya kimataifa, mtandaoni tarehe 8 Novemba 2010).

Inafaa kuashiria kuwa India ilikuwa imetuma mnamo tarehe 29 Septemba 2010 makundi manne ya jeshi la nchi kavu, anga, na majini la India kufanya mazoezi na Marekani katika vitengo 31 vya watembea kwa miguu na majini katika kambi ya Marekani huko Okinawa katika Bahari ya Uchina Mashariki. Uchina ilikuwa na majibu makali dhidi ya mazoezi hayo ya kijeshi. Mwishoni mwa Septemba, Adimiral wa Uchina, Zhu Yin, alionya kuwa "msururu wa mazoezi ya kijeshi yaliyoanzishwa na Marekani na nchi jirani na Uchina ulionyesha kuwa Marekani inataka kuongeza uwepo wake wa kijeshi barani Asia, na lengo la mazoezi haya ya kijeshi yaliyoanzishwa na Marekani ni kuzilenga nchi kadhaa zikiwemo Uchina, Urusi, na Korea Kaskazini, na kuimarisha uhusiano wa kimkakati na nchi washirika wa Marekani kama Japani na Korea Kusini." (Global Times 26 Septemba 2010).

3- Tangu kuanza kwa mazungumzo ya pande sita mwaka wa 2003 ili kuzuia matamanio ya nyuklia ya Korea Kaskazini, Marekani imekuwa ikitoa madai fulani, na kila mara Korea Kaskazini inapokaribia kuyatekeleza, Marekani huvunja ahadi zake kuhusu majukumu yake. Isitoshe, Marekani imefanikiwa kuionyesha Korea Kaskazini na mshirika wake mkuu Uchina kuwa ndio upande wenye makosa katika kufeli kwa mazungumzo hayo mara kwa mara. Kwa mfano, mwaka wa 2007, Marekani ilitangaza kuwa ingeachia dola milioni 25 za fedha za Korea Kaskazini zilizokuwa zimezuiliwa mkabala na Pyongyang kusitisha kinu chake cha nyuklia cha Yongbyon na kuruhusu kurudi kwa wakaguzi wa wakala wa kimataifa wa nyuklia. Hata hivyo, Marekani ilirudi nyuma katika ahadi yake ambapo iliachia fedha hizo kwa kuchelewa sana kiasi kwamba dili hiyo haikuweza kukamilika kwa wakati uliopangwa. Korea Kaskazini ilijiondoa kwenye mazungumzo ya pande sita kutokana na kufadhaika kufuatia vikwazo vingi vilivyowekwa na Marekani mwaka wa 2009. Hii ilifuatiwa na mivutano kuanzia kufukuzwa kwa wakaguzi wa wakala wa kimataifa wa nyuklia, kutangazwa kwa mipango ya kuanza tena urutubishaji wa urani, mlipuko wa nyuklia chini ya ardhi mnamo Mei 2009, mapigano na vikosi vya majini vya Korea Kusini, na shambulio la hivi karibuni kwenye kisiwa cha Korea Kusini.

4- Kwa upande mwingine, jibu la Marekani lilikuwa ni kupeleka meli ya kubeba ndege za kivita na kufanya mazoezi ya kijeshi na kufanya mazungumzo, bila kujumuisha Uchina na Korea Kaskazini, ili kuishinikiza Uchina kuchukua msimamo mkali zaidi dhidi ya mshirika wake Korea Kaskazini. Adimiral Mike Mullen, Mwenyekiti wa Wakuu wa Vikosi vya Pamoja vya Marekani, aliashiria mnamo tarehe 8 Desemba 2010 hamu yake ya kutaka Uchina ichukue jukumu la manufaa zaidi ambapo alisema: "Wachina wana ushawishi mkubwa kwa Korea Kaskazini, na hakuna taifa duniani lenye ushawishi zaidi kwa Korea Kaskazini kuliko Uchina, lakini licha ya kuwa na maslahi ya pamoja katika kupunguza mivutano, bado haiko tayari kutumia ushawishi huo." Inashangaza kuwa kufuatia shambulio la hivi karibuni, Uchina ilitoe wito kwa haraka wa kuanza tena mazungumzo ya pande sita, jambo ambalo Marekani ililikataa. Baada ya hapo, Uchina ilisimama hadharani kuilinda Korea Kaskazini dhidi ya uingiliaji kati wa Marekani katika eneo hilo! Hii inamaanisha kuwa Marekani inataka mvutano uendelee kuwa wa juu, na kuionyesha Uchina na Korea Kaskazini kana kwamba ndizo chanzo cha mvutano na hivyo kuzifanya nchi za eneo hilo kuwa na uadui nazo. Lakini bila kufikia ukingo wa vita, kwa sababu hali ya kimataifa na kikanda haimruhusu kufanya hivyo kwani imejishughulisha huko Iraq na Afghanistan.

5- Kutokana na hayo, tunaweza kusema kwamba hatua za sasa za Uchina, iwe ni zile zilizochapishwa na mtandao wa Uchina (Arabic.china.org.cn) ikinukuu shirika la habari la Xinhua kuhusu kutia saini kwa Uchina, Japani na Korea Kusini mnamo 16/12/2010 makubaliano ya kuanzisha sekretarieti ya ushirikiano wa pande tatu mjini Seoul mwaka ujao, au yale yaliyochapishwa na vyombo mbalimbali vya habari ikiwemo tovuti hii kuhusu ziara ya Waziri Mkuu wa Uchina nchini India... hatua hizi zote ni za kufelisha juhudi za Marekani za kuitenga Uchina na majirani zake na kuionyesha kama nchi ya kichokozi. Korea Kusini na Japani ni miongoni mwa washirika watiifu zaidi wa Marekani, ambapo kukaribiana kwa Uchina nazo kunachukuliwa kuwa ni kufelisha unyonyaji wa Marekani kuzitumia dhidi ya Uchina. Kadhalika, India ni miongoni mwa silaha ambazo Marekani ilikuwa ikizitumia, na bado inazitumia, kuchochea mvutano wa kudumu kati yake na Uchina kwa kuibua matatizo ya kila mara kati yao. Hivyo, kukaribiana kwa Uchina na India ni kuzima moto wa mvutano ambao Marekani inajaribu kuuchochea kati ya Uchina na India.

Inatarajiwa kuwa Uchina itakuwa imejipatia alama kwa upande wake katika kukabiliana na Marekani, iwapo Uchina itatumia vyema ziara yake nchini India na makubaliano yake na Japani na Korea Kusini, na kutoanguka katika mtego wa udanganyifu kutoka kwa Japani na Korea Kusini kwa uchochezi wa Marekani.

Share Article

Share this article with your network