Alhamdu Lillahi, na swala na salamu zimwendee Mtume wa Mwenyezi Mungu, jamaa zake, maswahaba zake na waliomfuta, na baada ya hayo:
Kwa wale wanaofunga safari kuelekea kwenye mwamko na nasaha, Kwa wale wanaotafuta kuufikia ukweli, Kwa wale wanaotafuta neno la kweli na jema, Kwa hawa na wale wote wanaoipokea redio hii, Kwao ninasoma neno la Mwenyezi Mungu (swt):
أَلَمْ تَرَ كَيْفَ ضَرَبَ اللّهُ مَثَلاً كَلِمَةً طَيِّبَةً كَشَجَرةٍ طَيِّبَةٍ أَصْلُهَا ثَابِتٌ وَفَرْعُهَا فِي السَّمَاءِ. تُؤْتِي أُكُلَهَا كُلَّ حِينٍ بِإِذْنِ رَبِّهَا وَيَضْرِبُ اللّهُ الأَمْثَالَ لِلنَّاسِ لَعَلَّهُمْ يَتَذَكَّرُونَ
"Je! Huoni jinsi Mwenyezi Mungu alivyopiga mfano wa neno jema? Ni kama mti mwema, mizizi yake ni imara, na matawi yake yako mbinguni. Hutoa matunda yake kila wakati kwa idhini ya Mola wake. Na Mwenyezi Mungu huwapigia watu mifano ili wapate kukumbuka." (Ibrahim [14]: 24-25)
Enyi ndugu wasikilizaji,
Hakika neno jema ni neno la haki la kweli na la uchamungu, lenye ujasiri na nguvu. Nalo ni msingi katika Uislamu mtukufu, likitamkwa na kuamrishwa na aya za Mwenyezi Mungu (swt):
يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ اتَّقُواْ اللّهَ وَكُونُواْ معَ الصَّادِقِينَ
"Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu na kuweni pamoja na wakweli." (At-Tawbah [9]: 119)
Na hadithi za Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw):
ألا إنَّ أفضل الجهاد كلمةُ حق عند سلطان جائر
"Hakika jihadi bora zaidi ni neno la haki mbele ya mtawala dhalimu." (Imepokewa na Ahmad)
Na neno hili jema, lenye matawi mawili: ukweli wa uchamungu na nguvu ya ujasiri, litakuwa—kwa idhini ya Mwenyezi Mungu—ndio msingi wa redio hii hai, ili kuitangaza haki kwa sauti kuu katika wakati ambapo idhaa nyingine—isipokuwa alizozirehemu Mola wako—zimeitupa haki nyuma ya migongo yao, na zikashindana katika hadaa na upotoshaji, uzushi na uongo, ghilba na udanganyifu. Zimefanya lengo kuwa ni kisingizio cha njia yoyote ile, iweje njia hiyo, na hata kama itaporomoka kiasi gani na kufikia kiwango cha chini kabisa cha anguko, zikipindua haki kuwa batili na batili kuwa haki. Mwenyezi Mungu awaangamize; ni vipi wanavyogeuzwa!
Enyi ndugu, Katika zama hizi ngumu ambapo neno la haki lenye nguvu ni adimu na la thamani, likipigwa vita na madhalimu ili lisiwaangamize kwa kufichua dhuluma na uasi wao; katika zama hizi ngumu, enyi ndugu, redio yenu hii itafanya—kwa msaada wa Mwenyezi Mungu—neno la haki lenye nguvu kuwa anwani yake bila ya kuogopa lawama ya mwenye kulaumu kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Redio hii itakuwa, kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, ni uhai na maangamizi kwa wakati mmoja:
Uhai kwa yule anayependa heri na kuitafuta, kwani kwake itakuwa ni nuru juu ya nuru, mwongozo juu ya mwongozo, mwamko na ufahamu. Na redio yetu kwa hawa: masikio hufurahia kuisikia, nafsi hutulia kwayo, na nyoyo hutulia. Na matangazo yake yatakuwa ni bishara kwao, na ni bishara njema iliyoje!
Na itakuwa ni maangamizi kwa kila dhalimu muasi, mpotevu mwenye kupoteza, kipofu wa macho na wa busara, kwani itamdhalilisha na kumfedhehesha, na kumfichua mbele ya wale waliofanywa wahadaike naye. Itadhihirisha upotovu wake, kufichua njama zake, na kubainisha njia ya kumuondosha na namna ya kumwangusha. Na redio yetu kwa hawa: ni upofu juu ya macho yao, na uzito katika masikio yao, na matangazo yake yatakuwa ni onyo kwao, na ni onyo kali lililoje!
Hayo yote, enyi ndugu, ni ili mambo yawe wazi na yenye kung’ara kama jua la mchana, yasiyofunikwa na wingu, wala kugubikwa na giza:
لِّيَهْلِكَ مَنْ هَلَكَ عَن بَيِّنَةٍ وَيَحْيَى مَنْ حَيَّ عَن بَيِّنَةٍ
"...ili aangamie wa kuangamia kwa dalili wazi, na apone wa kupona kwa dalili wazi." (Al-Anfal [8]: 42)
Enyi ndugu, Katika siku hii, na saa hii, naifungua redio hii kwa jina la Mwenyezi Mungu, ili itoe neno jema, la kweli na lenye nguvu, huenda ikawa, enyi ndugu:
Kwanza: Inawathibitisha wale walioamini katika maisha ya dunia na akhera, na kuangaza njia kwa wanaotafuta nuru, na kuondoa ujinga na kuchanganyikiwa kwa wanafunzi wa elimu na uongofu.
Pili: Na wakati huo huo, huenda ikamshtua msaliti, au kumwamsha aliyelala, au kumrudishia akili aliyepumbazwa.
Mwisho, lakini si kwa umuhimu, nawapongeza nyinyi enyi wasikilizaji, kwa mwana huyu mbarikiwa, ambaye anawaita sasa hivi kwa jina la Hizb ut-Tahrir ili mjibu na muitikie wito wa haki anaoulingania, na ili mumnusuru na kumsaidia. Na mwana huyu hatachelewa—kwa idhini ya Mwenyezi Mungu—kukua kwa haraka, kisha awe mkubwa anayewaita wakati huo kwa ulimi wa Kiarabu ulio wazi:
Hapa ni Sauti ya Khilafah, hapa ni Redio ya Dar al-Islam, hapa ni Neno la Haki, Neno Jema:
أَصْلُهَا ثَابِتٌ وَفَرْعُهَا فِي السَّمَاءِ
"Mizizi yake ni imara, na matawi yake yako mbinguni." (Ibrahim [14]: 24)
Na hilo kwa Mwenyezi Mungu si gumu.
Wassalamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh.
Alhamisi, 15 Rabi’ al-Akhir 1425 H Sawa na 03/06/2004 M
Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah Amir wa Hizb ut-Tahrir